Showing posts with label Hotuba. Show all posts
Showing posts with label Hotuba. Show all posts

Saturday, February 21, 2015

Wosia wa Baba Wa Taifa Kuhusu Urais - Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya Mei 1, 1995

Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere alialikwa kuwa Mgeni Rasmi kwenye kilele cha Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani iliyofanyika kitaifa Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya Mei 1, 1995. Katika hotuba yake alieleza mengi, leo tunachukua kipengele cha urais, alikuwa na haya ya kusema:
Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere
“Naeleza baadhi ya matatizo ambayo viongozi tutakaowachagua tuwe na hakika iwapo wanayaona hivi kama sisi tunavyoyaona. Yanawauma kama sisi yanavyotuuma na kwamba, watakapofika hapo wanapopataka watusaidie kuyatatua.

“Wanayaona, yanawakera na hata watakapofika hapo, hicho ndicho kitakachowasukuma kutaka kuwa marais wetu na wabunge wetu. “Marekani walikuwa na rais wao kijana mmoja mdogo anaitwa John Kennedy. Walimpiga risasi. Marekani nao ni watu wa ajabu sana! Vijana walilaani tukio hilo kwa kuwa walikuwa wanadhani wamemchagua rais wa umri wa kama miaka arobaini na mitatu au minne hivi.

“Sasa huyo ni kijana, hata kwa hapa Tanzania leo ni kijana. Alipochaguliwa na Marekani akawa rais wao. Katika hotuba yake ya kwanza kabisa aliwambia wananchi wenzake, hasa vijana “Usiulize Marekani itakufanyia nini, jiulize wewe utaifanyia nini Marekani?”.
“Kila anayetaka kuwa mgombea wa urais/ubunge ajiulize ataifanyia nini nchi yake
“Tunataka mtu anayetaka kuwa rais wetu ajiulize anataka kuifanyia nini nchi yetu na sio nchi yetu itamfanyia nini.

“Na tunataka swali hilo ajiulize kila mtu anayetaka kuwa mgombea wa chama cho chote kuwa mbunge/rais: “Kwa nini, kwa dhati kabisa, anaumwa na umasikini wetu na umasikini huo ndiyo unaomsukuma ashughulike na mambo haya ya siasa katika ngazi hiyo ama ya ubunge ama ya urais”. Kama sivyo, hatufai!
“Mtu hapakimbilii Ikulu: Hakuna Biashara Ikulu. Mtu anayetaka kwenda ikulu kutaka faida yo yote ikulu pale, hatufai hata kidogo. Wananchi, mimi nimekaa pale Ikulu kwa muda mrefu zaidi kuliko mwingine ye yote, wala sidhani kuna mtu mwingine anaweza kuzidi muda huo.

“Tayari hapa tumeweka sheria. Kwa mujibu wa sheria, mtu hawezi tena kukaa Ikulu zaidi ya miaka kumi, kipindi ambacho hata hakijafikia nusu ya kipindi nilichokaa. Mimi nimekaa miaka ishirini na tatu!
“Najua, kwa mtu halisi kabisa, Ikulu ni mzigo! Hupakimbilii! Si mahali pa kupakimbilia hata kidogo; huwezi kupakimbilia Ikulu. Unapakimbilia kwenda kutafuta nini?
“Ni mgogoro; ni mzigo mkubwa kabisa! Ukipita barabarani, unakuta watu wana njaa, unaona ni mzigo wako huo. Pazito pale! Huwezi kupakimbilia na watu safi hawapakimbilii.

“Ukiona mtu anapakimbilia, na hasa anapotumia tumia vipesa kwenda Ikulu, huyo ni mtu wa kuogopa kama ukoma!
“Mtu ye yote anayeonekana anapenda sana kwenda Ikulu na hata yupo tayari kununua kura ili kumwezesha kufika Ikulu ni wa kumkwepa kama ukoma. Kwanza, hizo fedha kapata wapi.

“Mtanzania wa leo hawezi kununua watu bila kwanza yeye kununuliwa.
Na kama kanunuliwa, atataka kuzilipaje? Kazipata wapi? Watanzania wote ni masikini tu. Mtanzania anaomba urais wetu kwa hela! Amezipata wapi? “Pili, kama hajanunuliwa, kazipata wapi? Kama kakopa, atarudishaje? Ikulu pana biashara gani mtu akope mamilioni halafu aende ayalipe kwa biashara ya Ikulu? Ikulu mimi nimekaa kwa muda wa miaka ishrini na mitatu.

“Ikulu ni mahali pazito. Kuna biashara gani Ikulu?
“Rushwa na matumizi ya fedha bila utaratiba wakati wa chaguzi: Sisi Waafrika ni watu wa ajabu sana. Unajua ni wadogo, lakini nasema, ni udogo wa mawazo. Umaskini wa mawazo ni umasikini mbaya kupita wote.

“Unaweza ukawa na almasi mfukoni, akaja tapeli na kijiwe kimetengenezwa kama almasi akakuambia “hebu tuone almasi yako. 

Bwana aa! Hii ya kwako sio almasi ni chupa tu, almasi ni hii. Kwanza nipe bwana.” Mkabadilishana. Yeye akachukua almasi yako na akakuachia kichupa na ukatoka hapo unashangilia kama zuzu!
“Sisi hapa Tanzania tulikuwa tumeanza utaratibu ambao ukitumia fedha nje ya fedha za chama na serikali na ukatumia fedha zako mwenywe katika uchaguzi, tunakutoa. Hufai! Huo ndio ulikuwa utaratibu wetu. Tulikuwa tunakuuliza: “hii nchi ya maskini, wewe mwenzetu una mali umeipata wapi?”
“Mali, kwa wakati huo, kwetu sisi ilikuwa ni sifa ya kukunyang’anya uwezo wa kugombea uongozi Tanzania. Tulijua kwamba, kama una mali, utaficha. Leo watu wanasema waziwazi: “Mwalimu uchaguzi wa mwaka huu utapitishwaje?”

“Marekani wanatumia fedha nyingi sana katika uchaguzi. Nyingi sana! Kama Marekani sasa hivi wanazungumza watunge sheria inayofanana na ile mliyoitupa ninyi mnadhani kwa sababu ni mawazo ya masikini, haina maana. “Wakubwa wanayafikiria mawazo hayo sasa hivi. Marekani wanafikiria uwezekano sasa wa kutunga sheria itakayoweka utaratibu wa fedha za ugombeaji kutokana na mfuko mmoja baada ya kugundua kwamba inapokuwa holela na kila mtu akiachiwa lwake, inavuruga.

“Inaleta rushwa kubwa kabisa. Unanunuliwa urais na unaweza kununuliwa na fedha za wauza bangi na wauza baa. Wauza bangi wanaiona hatari hiyo, ninyi haa!“Hapa tulikuwa na utaratibu mzuri kabisa tuliouanzisha mlioutupa, mnafikiri, sisi mwaka huu fedha tu! Uchaguzi wa fedha, mtazipata wapi? Mimi nimetoka juzi tu, mara mmetajirika kiasi hiki!
--

Tuesday, August 05, 2014

Hotuba Ya Mhe Rais Jakaya Kikwete Kwa WaTanzania Washington D.C.



Karibu kusikiliza hotuba ya Mhe. Dk Jakaya M Kikwete alipozungumza na waTanzania usiku wa Agosti 2, 2014 kwenye hotel ya Marriot, jijini Washington DC nchini Marekani.

Wednesday, July 03, 2013

Idi Amin Speech to Queen Elizabeth the II

 
 
Uganda Dictator General Idi Amin Dada called himself Conqueror of the British Empire
IDD AMIN SPEECH TO THE QUEEN

"My majesty Mr. Queen Sir, horrible ministers and members of parliament, invented Guests, ladies under gentlemen. I hereby thank you completely…..Mr. Queen, sir; and also what he has done for me and my fellow Uganda who come with me.

We have really eaten very much. And we are fed up completely:And also very thanks to you keenly open up from all windows: so that those plenty climates can come into lunch. But before I go back to my country with a plane from the Entebbe airport of London I wish to invitation you Mr. Queen, to become home to Uganda so that we can also revenge on you .

You will eat a full cow:and also feel up your stomach and walk with difficult because of full stomach completely. Even when you want to rest at night; I will make sure that you sleep on top of me in the top up stairs of my mansion completely so that you can enjoy all the gravity of fresh air.

"But now am sorry because I have to tell you that I have made a shortcall on you only. But next time I shall make a long call on you to last the whole moon completely. Thank you very much to allow me to undress you completely before these extinguished ladies undergentlemen sir.

Lastly but not list, I ask the band to play our international anthem of the republic of Uganda and also the British international anthem..Your majesty sir, I thank you from the bottom of my heart and from thebottoms of all the people of Uganda .

With this few words I thank you Sir.

Thursday, March 14, 2013

Rais Kikwete Afungua Rasmi Jengo la Kitivo Cha Sayansi MUM

HOTUBA YA MHESHIMIWA RAIS JAKAYA MRISHO KIKWETE KATIKA UFUNGUZI RASMI WA JENGO LA KITIVO CHA SAYANSI KATIKA CHUO KIKUU CHA WAISLAMU CHA MOROGORO (MUM),


TAREHE 14 MACHI, 2013, MOROGORO

Mzee Kitwana Suleiman Kondo, Mwenyekiti wa Taasisi ya Maendeleo ya Waislamu (MDF);
Mheshimiwa Joel Bendera, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro;
Mama Mwantumu Malale, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro;
Profesa Hamza Mustafa Njozi, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro;
Viongozi mbalimbali wa Serikali, vyama vya siasa na Jumuiya mliohudhuria;

Wageni waalikwa;

Mabibi na Mabwana;

Niruhusuni niungane na wenzangu walionitangulia kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma, kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha kukutana hapa. Nakushukuru sana Mama Mwantumu Malale, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro na viongozi wenzako kwa kunialika kuja kujumuika nanyi katika siku hii adhimu ya ufunguzi wa jengo la Kitivo cha Sayansi katika Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro. Mmenipa heshima kubwa ya kuwa sehemu ya historia ya Chuo hiki. Kwa kweli, nimefarijika sana kuona Chuo chetu kinazidi kupata mafanikio ya kutia moyo hasa ukizingatia ukweli kwamba kina muda mfupi tu tangu kuanzishwa kwake.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Natoa pongezi nyingi kwako, Makamu Mkuu wa Chuo na wale wote walioshiriki kubuni wazo la kuwa na jengo la Kitivo cha Sayansi na kufanikisha ujenzi wake. Juhudi zao na moyo wao wa kupenda maendeleo ndio umetufanya sisi kujumuika hapa leo kushuhudia mafanikio haya. Hakika ni jambo la kujivunia. Pia, nawapongeza sana Wajenzi na Mhandisi Mshauri kwa kazi nzuri waliyofanya ya ujenzi wa jengo hili. Sote tunaliona jengo lilivyojengwa vizuri na kwa namna yake linapendezesha mandhari ya Chuo.

Kwa namna ya pekee napenda kwa niaba yenu nitoe shukrani zangu za moyoni kwa taasisi ya Al-Barakah kwa kufadhili ujenzi wa jengo hili. Asanteni sana kwa ukarimu wenu na upendo mkubwa mliouonesha kwa nchi yetu na watu wake. Naomba taasisi nyingine na watu binafsi waige mfano huu mzuri wa kusaidia miradi mbalimbali inayonufaisha jamii. Tukumbuke ule msemo wa wahenga kuwa “kutoa ni moyo, usambe si utajiri”.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Mabibi na Mabwana;

Kwa miaka mingi madhehebu ya dini na mashirika ya dini yamekuwa washirika muhimu sana wa Serikali katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya nchi yetu. Yamekuwa yanajihusisha na kutoa huduma kwa jamii kama vile afya, elimu na nyinginezo. Kwa ajili hiyo watu wengi sana nchini wamenufaika na wanaendelea kunufaika na huduma zinazotolewa na mashirika ya dini.

Kwa miaka mingi mashirika na taasisi za madhehebu ya dini ya Kikristo ndiyo yaliyokuwa yakionekana kutoa huduma hizo. Kwa upande wa Waislamu, ukiacha Mtandao wa Maendeleo wa Aga Khan, mchango umekuwa mdogo sana. Ni jambo la faraja kubwa kuona Taasisi ya Maendeleo ya Waislamu (MDF) ikionyesha njia. Kwa kumiliki na kuendesha Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro kwa ufanisi, MDF inatoa mchango muhimu katika kuendeleza elimu ya juu na maendeleo nchini. Idadi kubwa ya wanafunzi waliofuzu masomo yao na waliopo katika Chuo hiki tangu kilipoanzishwa mwaka 2005 ni ushahidi tosha wa kazi nzuri inayofanywa na MDF. Hongereni sana. Tunawaombea kwa Mola mpate mafanikio makubwa zaidi miaka ya usoni kwa upande wa elimu na huduma nyingine muhimu.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Katika kipindi cha miaka saba sasa, Serikali yetu imeongeza sana uwekezaji katika upanuzi wa elimu tangu ya awali hadi elimu ya juu. Tumeamua kufanya hivyo kwa sababu vijana wengi waliokuwa wanastahili kupata elimu ya awali, msingi, sekondari, ufundi na elimu ya juu walikuwa hawapati. Tanzania ni kubwa kuliko Kenya na Uganda kwa eneo na idadi ya watu lakini ndiyo tuliokuwa na idadi ndogo ya wanafunzi kwa ngazi zote hizo. Kwa mfano, mwaka 2005 idadi ya wanafunzi waliokuwa Chuo Kikuu nchini Kenya ilikuwa 108,407, Uganda 88,360 na kwa baadhi ya nchi za SADC kama vile Afrika Kusini idadi hiyo ilikuwa 717,973. Wakati wenzetu wakiwa na idadi hiyo, sisi tulikuwa na wanafunzi 40,719 tu katika vyuo vikuu nchini. Hali ilikuwa hivyo pia kwa elimu ya sekondari. Kenya ilikuwa na wanafunzi 925,341, Uganda 619,519 na Afrika Kusini 4,186,882 wakati Tanzania ilikuwa na wanafunzi 524,325 tu waliokuwa katika shule za sekondari.

Tuliona hali hii haikubaliki hivyo tukaamua hatuwezi kuiacha iendelee. Tukaamua kudhibiti. Tukachukua hatua tulizochukua za kupanua elimu katika ngazi zote. Matokeo ya uamuzi huo ni kwamba vijana wanaopata fursa ya kupata elimu katika ngazi zote wamekuwa wengi kuliko wakati mwingine wo wote katika historia ya nchi yetu, tumewafikia na kuwapita majirani zetu. Kazi kubwa tunayoendelea nayo sasa ni kuwekeza katika kuimarisha ubora wa elimu waipatayo vijana wetu kwa kuongeza walimu, vifaa vya kufundishia, vitabu na huduma nyinginezo. Inshallah hata kwa dhamira yetu, hii njema Mola atatuwezesha. Mwanzo mgumu lakini hatma itakuwa nzuri.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Kufuatia juhudi hizo, idadi ya wanafunzi waliopo kwenye vyuo vikuu nchini imeongezeka sana, kutoka wanafunzi 40,719 mwaka 2005 hadi wanafunzi 166,484 mwaka 2012. Kwa upande wa sekondari mwaka 2011 tulikuwa na wanafunzi milioni 1.79 na wenzetu wa Kenya walikuwa na wanafunzi milioni 1.77. Haya ni mafanikio makubwa.

Serikali itaendelea kuwekeza kwenye upanuzi wa fursa za elimu na ubora wake. Hata hivyo ushiriki wa wadau wengine kuunga mkono juhudi za serikali ni jambo muhimu sana. Tumeweka mazingira mazuri kwa wadau hao kufanya hivyo na mafanikio yanaonekana wazi. Kama nilivyokwishasema awali, mashirika ya dini yamekuwa wadau wa kutumainiwa na mchango wao uko wazi. Unajieleza wenyewe. Kwa mfano, katika vyuo vikuu 49 vilivyopo nchini, vinavyomilikiwa na umma ni 14 tu. Vyuo vikuu 24 vinamilikiwa na mashirika ya dini na 11 na sekta binafsi.





Ndugu Mkuu wa Chuo;

Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa na muhimu unaotolewa na vyuo vikuu vinavyomilikiwa na mashirika ya dini na sekta binafsi. Ninyi mmekuwa washirika wazuri na wa uhakika katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya elimu katika nchi yetu. Napenda kuwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kuwaunga mkono na kushirikiana nanyi ili kuwawezesha vijana na Watanzania wengi zaidi waweze kupata elimu. Uamuzi wa kufanya utaratibu wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu uhusishe wanafunzi wa vyuo visivyokuwa vya umma ni moja ya mambo mengi muhimu yanayofanywa na Serikali kuthibitisha usemi wangu huo.

Tulipoingia madarakani mwaka 2005 tulifanya mambo mawili muhimu kuhusu mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu. Kwanza uamuzi kwamba, mikopo itolewe kwa wanafunzi wa vyuo vikuu vya umma na vile visivyokuwa vya serikali. Kabla ya hapo ilihusu vyuo vya umma pekee. Pili kwamba, kila mwaka tuongeze fedha zinazotengwa kwa ajili ya Mfuko huo ili idadi ya wanafunzi wanaonufaika iongezeke. Tulikuta Mfuko ukiwa na shillingi billioni 56.1 unanufaisha wanafunzi 16,345 mwaka 2005. Tukaongeza kila mwaka na katika mwaka huu wa fedha (2012/13) tumetenga shillingi bilioni 345 zinazowanufaisha wanafunzi 98,772.

Tutaendelea kuongeza fedha katika Mfuko huo ili wanafunzi wengi zaidi wanufaike na hata ifikie siku moja tuweze kuwakopesha wote bila ya kujali sifa ya uwezo wa wazazi au walezi kulipa ada. Kwa kasi tuliyonayo na kwa jinsi tunavyozidi kufanikiwa katika kukusanya mapato ya serikali, naamini miaka michache ijayo tunaweza kufikia lengo hilo. Nawasihi Bodi ya Mikopo iwekeze katika kuimarisha uwezo wa kuwafuatilia waliokopeshwa kulipa mikopo waliyopewa. Matamanio yangu ni kuwa fedha zilizotolewa zizunguke ili tupunguze kiasi kinachotolewa na bajeti ya serikali kila mwaka.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Mabibi na Mabwana;

Niruhusuni nitumie nafasi hii kukupongeza wewe Mkuu wa Chuo, Makamu Mkuu wa Chuo, Wahadhiri na Jumuiya nzima ya Chuo Kikuu hiki kwa kazi kubwa na nzuri muifanyayo ya kuendeleza na kuboresha Chuo. Tumeshuhudia ujenzi wa jengo nililolifungua leo. Tumeona mafanikio kwa upande wa ongezeko la idadi ya wanafunzi, walimu, wafanyakazi na fani zinazofundishwa katika kipindi hiki kifupi cha uhai wa Chuo hiki.

Nimefurahishwa na kufarijika sana kusikia kuwa ubora wa elimu inayotolewa hapa chuoni ni jambo linalopewa kipaumbele cha kwanza. Jambo hili ni muhimu sana kulisisitiza kwani tunataka wahitimu wa Chuo hiki wafanane na wahitimu wa Chuo chochote kizuri nchini na hata duniani. Ningependa kuona wahitimu wa Chuo hiki wanagombewa katika soko la ajira. Hili ni jambo linalowezekana. Kinachotakiwa ni uamuzi wa Baraza na Seneti kuwa iwe hivyo na kuchukua hatua zipasazo. Sina shaka kuwa mnaweza kufanya hivyo. Hakika mnaweza, na sote kwa umoja wetu tunaweza.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Nimefurahi sana, pia, kusikia kuwa Chuo kinatoa mafunzo ya ualimu. Bila ya shaka mnaelewa kwa nini nafurahi. Tuna uhaba mkubwa wa walimu nchini hivyo Chuo cho chote kinachotoa mafunzo ya ualimu hunifurahisha. Endeleeni kuimarisha mafunzo hayo ili Chuo chenu kitambulike na kukubalika nchini kwa sifa ya kutoa walimu wazuri. Walimu wa kutoka Chuo hiki wawe wale wanaojua vyema masomo wanayofundisha, mahiri kufundisha na waadilifu. Naomba pia mtoe kipaumbele cha juu kwa mafunzo ya ualimu wa masomo ya sayansi na hisabati. Mkifanya hivyo, mtakuwa mnatoa mchango mkubwa katika jitihada za kupunguza uhaba wa walimu wa masomo hayo nchini. Naamini kitendo cha kuzindua Jengo la Kitivo cha Sayansi, kilichofanyika muda mfupi uliopita kinatoa matumaini ya Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro kuchangia katika jitihada za kupunguza pengo la walimu wa sayansi nchini.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Nimewasikia mkieleza kwa ufasaha changamoto kubwa na ndogo ambazo Chuo inakabiliana nazo. Nawapongeza kwa dhati, wewe na viongozi wenzako kwa ubunifu wenu na hatua mnazochukua kuzikabili changamoto hizo. Nawaahidi msaada na ushirikiano wangu na wa serikali kwa yale yaliyoko kwenye uwezo wangu na wa serikali katika kutafuta ufumbuzi kwa changamoto zinazowakabili.

Nawapongeza kwa uamuzi wenu wa kutafuta vyuo vikuu rafiki vilivyoko katika nchi mbalimbali duniani mnavyoweza kushirikiana navyo. Endeleeni kufanya hivyo kwani vyuo vikuu vingi duniani hufanya hivyo. Hamtakuwa wa kwanza na wala hamtakuwa mnafanya jambo la kustaajabisha. Mnaweza, mkipenda, kuwaomba Mabalozi wetu waliopo katika nchi mbalimbali duniani wawasaidie. Ni wajibu wao kufanya hivyo kwani kusaidia kusukuma maendeleo ya hapa nchini kutoka huko waliko ndilo jukumu lao la msingi. Vile vile, nimefurahishwa na mipango yenu ya baadaye ya kuwa na matawi katika mikoa mbalimbali nchini. Hongereni kwa uamuzi wenu wa busara. Lazima Chuo kitanuke kwa maana ya kuwa kikubwa zaidi, makao makuu na kwa kuwa na vyuo vishiriki na shule au vitivo sehemu mbalimbali nchini.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Kazi iliyo mbele yenu ni kubwa, hivyo ni vyema kuweka mikakati mizuri na mipango thabiti ya utekelezaji na ufuatiliaji wa dhamira yenu hiyo njema. Rai yangu kwenu ni kuwaomba muwe wabunifu zaidi hasa katika kutafuta vyanzo vingine vya mapato vitakavyosaidia Chuo kujiendesha bila kutegemea ada peke yake. Chuo kiangalie uwezekano wa kufanya shughuli zitakazowaingizia mapato kama vile kufanya shughuli za kutoa ushauri. Pia muangalie uwezekano wa kuwekeza wenyewe kwenye miradi ya kiuchumi au kwa kushirikiana na wawekezaji katika baadhi ya maeneo.

Kuhusu nafasi mbili za ufadhili nilizopewa na Chuo kikuu cha Tun Abdul Razak cha Malaysia, nitafuatilia kujua kilichoendelea na kinachoendelea. Je, nafasi hizo bado zipo? Zikiwepo, nitawasiliana na wahusika waangalie uwezekano wa kuwapeni. Kama zimeshagawiwa basi tusubiri safari ijayo. Kwa masuala ya ardhi na maombi mengine nimeyasikia, yaleteni tuangalie namna ya kusaidiana.

Ndugu Makamu Mkuu wa Chuo, na

Wafanyakazi wote wa Chuo cha Waislamu cha Morogoro;

Napenda kuwakumbusha kuwa mnayo dhamana kubwa na wajibu mkubwa na wa kihistoria. Ule ukweli kwamba ni mara ya kwanza kwa Taasisi ya Waislamu wazawa kuwa na Chuo Kikuu inawapeni wajibu maalum wa kuhakikisha Chuo kinafanikiwa. Ni mtihani na changamoto ya aina yake kuthibitisha kuwa Waislamu nao wanaweza kuwa na Chuo kizuri na chenye kutoa elimu ya ubora wa hali ya juu. Kwa sababu hiyo hamna budi kuhakikisha kuwa mna mipango mizuri ya kujenga Chuo cha hadhi na ubora wa hali ya juu. Ihakikishwe kuwa mipango hiyo inatekelezwa kwa ukamilifu.

Aidha jumuiya yote inao wajibu wa kufanya kazi kwa bidii, ubunifu, maarifa na weledi ili dhima hiyo ya Chuo iweze kutimizwa kwa ukamilifu. Timizeni wajibu wenu ipasavyo ili jina la Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro likue haraka. Sifa yake isambae na kuvuma kote nchini. Chuo kifanye vizuri ili wanafunzi waone fahari kuwa wahitimu wa Chuo hiki. Chuo ambacho, wazazi wapende kuleta vijana wao kuja kusoma hapa. Kwa jinsi Mkuu wa Chuo alivyoeleza, mimi nina imani mnaweza, fanyeni kweli.





Ndugu Wanafunzi wa Chuo cha Waislamu cha Morogoro;

Naomba wote muone fahari ya kuwa wanafunzi katika Chuo cha kihistoria hapa nchini. Nawasihi mjitume kwa kadri ya uwezo na vipaji mlivyopewa na Mwenyezi Mungu mfanikishe kile kilichowaleta. Jifunzeni kwa bidii mfaulu vizuri ili mkihitimu muwe kielelezo kizuri cha mafanikio na ubora wa Chuo Kikuu Cha Waislamu cha Morogoro. Muwe Mabalozi na kioo cha ufanisi wa Chuo hiki. Nawasihi mjiepushe na mambo yatakayowapunguzia muda au kuwaondoa katika shughuli ya msingi iliyowaleta hapa ya kujifunza mpate digrii katika fani mliyochagua mwenyewe kuisomea. Vishawishi ni vingi na wapo watu wengi wanaopanga kuwashawishi mtumie muda wenu adhimu kufanya wanayoyataka wao ambayo mkishiriki huwatoa kwenye malengo na kutekeleza yao. Mambo ya dunia ya nje ya Chuo ni mengi huna budi kutambua lipi ufanye na lipi usifanye na kwa wakati gani!

Mwanafunzi wa Chuo Kikuu ni mtu mzima, si mtoto. Lazima ujue kuwa unawajibika kwa kila unaloamua na kutenda. Amua kuwajibika vizuri. Fikiri kabla ya kutenda, changanua lipi ni lipi kabla ya kufanya uamuzi wa kile unachotaka kufanya. Wakati wote uongozwe na busara na hekima na siyo jazba na ushabiki wa matakwa ya kundi. Kama ni jema fanya na kama si jema usifanye. Kwanza tambua wewe ni nani na uko hapa kwa ajili gani. Lazima ujue kuwa hatma ya yote uko peke yako. Utafaulu au kufeli wewe. Utapata shahada wewe na si mtu mwingine. Hakuna ubia wa kufaulu au kufeli au kiwango cha kufaulu. It will always remain personal. Katika masomo unanufaika wewe. Shirikiana na wengi lakini usisahau kujali maslahi yako. Maslahi ya wengi yasiyojumuisha yako, yahoji vizuri kabla ya kuamua kushiriki au kufanya. Vinginevyo labda kama umeamua kujitoa muhanga, uwe shujaa. Hata kwa hilo, sijui utakuwa shujaa wa nani.

Mabibi na Mabwana;

Kabla ya kumaliza napenda kutambua na kumshukuru Rais wa Awamu ya Tatu, Mheshimiwa Benjamin Mkapa na viongozi wa MDF kwa juhudi zao za pamoja zilizowezesha Chuo hiki kuwepo. Nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipowashukuru wananchi wanaokizunguka Chuo kwa ujirani mwema na wakazi wa Morogoro kwa ujumla kwa kukipokea vizuri na kuishi na wanajumuiya wa Chuo hiki kwa upendo mkubwa. Naomba muendelee na moyo na ushirikiano huo.

Baada ya kusema hayo, nawashukuru sana kwa kunialika. Nawatakia kila la heri na mafanikio tele.

Asanteni sana kwa kunisikiliza.

Tuesday, February 05, 2013

Ujumbe Kutoka Kwa Rais Obama Kwa WaKenya



Rais Obama katoa ujumbe mzito kwa WaKenya na waafrika kwa ujumla!

Friday, February 01, 2013

Hotuba ya Rais Kikwete Kwa Wananchi Mwisho wa Mwezi Januari 2013

Rais Jakaya Kikwete
Utangulizi
Ndugu Wananchi;
Kama ilivyo ada naomba tuanze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwenye
Rehema, kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha kuzungumza kwa mara
nyingine kwa kutumia utaratibu wetu huu mzuri wa mawasiliano baina ya
Rais na wananchi wa Tanzania kila mwisho wa mwezi.  Siku ya leo
nitazungumzia safari yangu ya Ufaransa, Uswizi na Ethiopia.  Pia
nitazungumzia ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi asili kutoka Mtwara
kuja Dar es Salaam.

Safari za Kikazi Nje ya Nchi


Ndugu Wananchi;
        Safari yangu ya Ufaransa, Uswizi na Ethiopia ilikuwa na
manufaa makubwa kwa nchi yetu.  Nchini Ufaransa licha ya kuimarisha
uhusiano wa kirafiki baina ya nchi zetu, tumepata wawekezaji wengi
wakubwa wenye nia thabiti ya kuja kuwekeza hapa nchini.  Pia
tumekubaliana kuanza mazungumzo ya kuwa na mpango mwingine wa
ushirikiano.  Mpango wetu wa sasa ulioanza mwaka 2006 uliisha mwaka
2010.  Mpango ule ulitusaidia sana kuboresha huduma za maji katika
miji ya Utete mkoani Pwani na Mpwapwa mkoani Dodoma.

        Katika mkutano wa Kongamano la Uchumi wa Dunia uliofanyika
Davos, Uswizi, tumehakikishiwa ushirikiano katika kuendeleza juhudi
zetu za kuleta mapinduzi ya kijani ili tujihakikishie usalama wa
chakula na kupunguza umaskini vijijini na kukuza uchumi wa nchi yetu.
Aidha, tulipata bahati ya kushirikishwa katika mjadala wa kuanzishwa
kwa programu kubwa ya kuzisaidia nchi za Afrika kutatua matatizo ya
upatikanaji wa umeme.  Naamini programu hiyo ikitekelezwa na wakubwa
kuheshimu kauli na ahadi zao itakuwa msaada mkubwa kwa maendeleo ya
nchi za Afrika zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Ndugu Wananchi;
        Nchini Ethiopia tulishiriki katika mkutano wa Wakuu wa Nchi
na Serikali wa Umoja wa Afrika na katika kikao cha African Peer Review
Mechanism (APRM) ambapo taarifa ya tathmini ya utawala bora ya
Tanzania na Zambia iliyofanywa na APRM ilijadiliwa.  Kwa jumla hatuna
mahali tuliponyooshewa kidole kuwa tunafanya vibaya.  Tumepongezwa
katika mambo mengi na tumepewa ushauri kwa baadhi ya maeneo waliyoona
hatuna budi kuyaboresha.  Nilipata nafasi ya kusema ambayo niliitumia
kufafanua baadhi ya mambo yaliyokuwamo kwenye taarifa.  Niliwashukuru
na kuahidi kuufanyia kazi ushauri uliotolewa.  Tathmini ya nchi yetu
ilipitishwa kwa kauli moja.

Vurugu za Kupinga Gesi Kusafirishwa Kutoka Mtwara

Ndugu wananchi;
Kama mtakavyokumbuka tarehe 8 Novemba, 2012 kule Kinyerezi, Wilaya ya
Ilala hapa Dar es Salaam, niliweka jiwe la msingi la ujenzi wa bomba
la kusafirisha gesi asili kutoka Mtwara na Songosongo kuja Dar es
Salaam.  Karibu na mwishoni mwa Desemba, 2012 kukafanyika maandamano
mjini Mtwara kupinga ujenzi wa bomba hilo.  Katika
maandamano yale na baadaye kwenye kauli za wanasiasa na wanaharakati
yakatolewa madai kuwa gesi hiyo itumike kwa maendeleo ya Mtwara na
kwamba yale yanayotakiwa kufanyika Dar es Salaam yafanyike Mtwara.
Pia, zilitolewa shutuma nyingine dhidi ya Serikali eti kuwa kwa miaka
mingi imewasahau na haiwajali wananchi wa Mikoa ya Kusini na ujenzi wa
bomba hilo ni muendelezo wa hayo. Kauli mbalimbali za wanasiasa na
wanaharakati ni kama vile ziliongeza mafuta kwenye kaa la moto na
kuuchochea mpaka kukatokea matukio yaliyotusikitisha na kutshtua
sote.  Baadhi ya ndugu zetu wamepoteza maisha na mali za watu na
Serikali kuharibiwa.

Ndugu Wananchi;
Katika hotuba yangu ya kuaga mwaka 2012 na kuukaribisha mwaka 2013,
tarehe 31 Desemba, 2012, nililisemea jambo hili.  Leo mwezi mmoja
baadae, napenda kusisitiza mambo mawili.  Kwanza kwamba, si kweli kuwa
Serikali inapuuza Mikoa ya Kusini.  Na pili, kwamba kujenga bomba la
kuipeleka gesi Dar es Salaam hakuinyimi Mikoa ya Mtwara na Lindi fursa
ya kunufaika na gesi iliyopo Mtwara.

Ndugu Wananchi;
        Serikali imefanya, inafanya na ina mipango ya kufanya mambo
mengi mazuri kwa ajili ya kuleta maendeleo katika Mikoa ya Mtwara na
Lindi.  Ipo mipango ya kuboresha miundombinu, huduma za kiuchumi na
kijamii pamoja na kukuza uchumi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa viwanda
vikubwa na vidogo.  Serikali ya Awamu ya Tatu chini ya uongozi wa Rais
Mstaafu, Mheshimiwa Benjamin Mkapa, ilijenga daraja katika Mto Rufiji
maarufu kama Daraja la Mkapa.  Hii ilikuwa ni hatua kubwa ya awali
katika safari ya kutatua matatizo ya usafiri ya Mikoa ya Kusini.
Serikali ninayoiongoza mie iliachiwa kazi ya kukamilisha ujenzi wa
barabara za lami kufikia darajani na kuunanisha Mkoa wa Mtwara na Mkoa
wa Ruvuma.  Kazi hiyo, tumeitekeleza vizuri na sasa tunakaribia
kuimaliza.  Tulikamilisha ujenzi wa barabara ya kutoka Mnazi-Mmoja
hadi Nangurukuru.  Mwaka 2009 tukaanza ujenzi wa barabara ya kilomita
56kutoka Somanga hadi Ndundu (darajani).  Ujenzi wakilometa 36 za
mwanzo ulienda vizuri.  Bahati mbaya ujenzi wa kilomieta 20 za mwisho
umechelewa sana kwa sababu ya mmiliki wa kampuni iliyokabidhiwa
kufanya kazi hiyo kufariki.  Kwa sababu hiyo, kampuni ilipata
mtikisiko kiasi na kusababisha kazi kutotekelezwa kwa kasi
tuliyoitarajia.  Sasa mambo yametengemaa na kazi inaendelea kwa kasi
nzuri.  Matumaini yetu ni kuwa ifikapo mwezi Desemba, 2013 kazi hiyo
itakuwa imekamilika.

Hali kadhalika, Rais Mstaafu, Mzee Benjamin Mkapa alituachia jukumu la
kumaliza ujenzi wa Daraja la Umoja katika mto Ruvuma na ujenzi wa
barabara ya lami kuanzia Mikoa ya Mtwara na Ruvuma.  Tumelikamilisha
Daraja hilo na ujenzi wa barabara ya lami kutoka Masasi hadi Mangaka
umekamilika.  Mchakato wa kujenga barabara ya kwenda Songea na kwenda
Darajani umefikia  mahala pazuri.  Tenda ya ujenzi wa barabara kutoka
Tunduru hadi Mangaka mpaka Darajani imeshatangazwa.  Kama mambo
yataenda sawa miezi mitatu ijayo mjenzi atapatikana.  Wakati huo huo
ujenzi wa barabara kutoka Namtumbo hadi Songea – Mbinga na Namtumbo –
Tunduru unaendelea.  Hivyo basi, kwa barabara ya “Mtwara Corridor”
kazi iliyobaki ni kutoka Mbinga kwenda Mbambabay ambayo tutaifanya
wenyewe kama tulivyofanya kwa Mnazi Mmoja – Nangurukuru na Somanga –
Ndudu na Daraja la Umoja.

Ndugu Wananchi;
Ipo pia mipango ya kuipanua na kuijenga upya bandari ya Mtwara ili
iweze kuhudumia mahitaji ya utafutaji na uchimbaji wa gesi baharini,
kuhudumia na kuvifanyia matengenezo vyombo vinavyotumika katika
utafiti, uchimbaji na uendelezaji wa gesi.  Pia iweze kuhudumia
shughuli za kiuchumi zitakazotokana na uchumi wa gesi pamoja na
zilizopo sasa.  Nilipozungumza na makampuni ya utafutaji gesi pale
Mtwara tarehe 25 Julai, 2011 waliomba nikubali bandari ya Mtwara iwe
mahali pa kuhudumia vyombo vyote vinavyofanya shughuli ya utafutaji na
uchimbaji wa gesi na mafuta katika pwani ya Afrika ya Bahari Kuu ya
Hindi.  Pia waliomba kuwa sehemu hiyo ya bandari iwe bandari huru.
Niliwakubalia bila ya kusita na tayari eneo la hekta 110 zimeshatengwa
na kutangazwa rasmi kuwa bandari huru.  Vile vile waliomba wapewe
sehemu ya bandari ya sasa kuendeshea shughuli na eneo la kujenga kituo
cha mitambo ya kuchakata gesi na kusafirisha nje.

Ndugu Wananchi;
Baada ya kuzungumza na makampuni ya utafutaji gesi na mafuta na
kuelezwa mahitaji yao nilibaini kuwa bandari ya Mtwara inahitaji
kupanuliwa na kujengwa upya.  Bahati nzuri viongozi wa Mamlaka ya
Bandari walikuwepo na walinihakikishia kuwa watafanya hivyo.

Tayari eneo la bandari limeongezwa kutoka hekta 70.68 hadi 2,693.68.
Eneo la bandari huru limeshatengwa hivyo hivyo na eneo la kampuni ya
Dangote na makampuni ya gesi yaliyopo.  Aidha, mchakato wa kupanua
bandari iliyopo, kujenga gati mpya na kuendelea na ujenzi hadi maeneo
ya Msanga Mkuu ipo katika hatua mbalimbali za matayarisho na
utekelezaji.

Ndugu Wananchi;
        Kwa upande wa Mkoa wa Lindi mipango ya kupanua na kuijenga
upya bandari ya Lindi imefikia hatua nzuri.  Naibu Waziri wa Uchukuzi,
Mhe. Dkt. Charles Tizeba alithibitisha hayo tarehe 1 Desemba, 2012
nilipotembelea bandari hiyo wakati wa ziara yangu ya Mkoa wa Lindi ya
tarehe 1 mpaka 5 Desemba, 2012.  Hali kadhalika mipango ya kujenga
bandari ya Kilwa iko mbioni.  Tena kwa upande wa Mkoa wa Lindi moja ya
makampuni yaliyogundua gesi baharini wameamua kujenga bandari na kituo
cha kuchakata na kusarifisha gesi nje ya mkoa huo kama ilivyo kwa
Mtwara.  Naambiwa wametambua maeneo matatu, kilichobakia ni kuamua
mojawapo ili ujenzi uanze.

Ndugu Wananchi;
        Nilipotoka bandari ya Mtwara, siku ile nilitembelea Chuo cha
VETA na kuzungumza na viongozi wa VETA taifa na wa Wizara ya Elimu na
Mafunzo ya Ufundi kuhusu kuwa na mitaala ya kutoa mafunzo mahsusi
yanayohitajika na sekta ya gesi na mafuta.  Nilisisitiza kwamba
tuwapatie vijana wetu mafunzo yatakayowawezsha kuajiriwa na makampuni
ya gesi na yale yatakayokuwa yanatoa huduma kwa makampuni hayo.
Nilisema tusipofanya hivyo, makampuni hayo yataajiri watu kutoka nje
na hatutakuwa na sababu ya kuwalaumu wala kulalamika.

Nafurahi kwamba agizo langu hilo limefanyiwa kazi ipasavyo.  Hivi sasa
katika chuo cha VETA Mtwara mafunzo hayo yanatolewa.  Kampuni ya
PetroBrass ya Brazil inaendesha mafunzo ya sekta ya gesi kwa vijana 25
kutoka mkoani Mtwara.  Aidha, chuo cha VETA kwa kushirikiana na
Kampuni ya Gesi ya Uingereza (British Gas) na Volunteers Service
Overseas ya Uingereza, kinatekeleza programu ya miaka mitatu iitwayo
Enhancing Employerbility Through Vocational Training.  Programu hii
inalenga  kutoa kozi zitakazowafanya wahitimu kuweza kuajiriwa katika
sekta ya gesi.  Programu hii ilifunguliwa na Makamu wa Rais,
Mheshimiwa Dkt. Mohamed Gharib Bilal, tarehe 26 Novemba, 2012.

Ndugu Wananchi;
Chini ya programu hii, walimu wa masomo yanayohusiana na gesi
wanaongezewa ujuzi ili waweze kufikia viwango vya kimataifa.  Vile
vile, Wizara ya Nishati na Madini imetoa upendeleo maalum wa
kudhaminiwanafunzi 50 kutoka mkoa wa Mtwara kusoma chuoni hapo ambao
tayari wameshahitimu mafunzo ya msingi ya uunganishaji vyuma
viwandani.  Mchakato wa kuwapatawanafunzi 50 kwa ajili ya mafunzo kama
hayo kutoka mkoa wa Lindi unaendelea.  Nimeambiwa mpaka wameshawapata
vijana 25 bado 25.

        Hali kadhalika, Wizara ya Nishati na Madini inadhamini
wanafunzi 10 kupata mafunzo katika Chuo Kikuu cha Dodoma ambako kozi
za mafuta na gesi zinatolewa.  Kipaumbele kwa udhamini huu unatolewa
kwa wanafunzi wa mikoa ya Mtwara na Lindi wenye sifa za kudahiliwa
katika mafunzo haya.  Wamepatikana watatu.  Wataalamu hawa na wengine
wa fani mbalimbali za gesi na mafuta watafundishwa kwa kiwango cha
shahada ya kwanza na baadae uzamili na uzamivu ili nchi yetu
ijitosheleze kwa wataalamu wa sekta hii.

Kupanga Mji wa Mtwara

Ndugu Wananchi;
        Baada ya kutembelea bandari ya Mtwara na Chuo cha VETA,
nilikaa na kuzungumza na viongozi wa Serikali na Manispaa ya Mtwara.
Katika mazungumzo yangu nao niliwasisitizia umuhimu wa kuwa na mpango
kabambe wa kuendeleza mji wa Mtwara – (Mtwara Masterplan) Mpango ambao
utawezesha kujengwa mji mkubwa wa kisasa unaokidhi mahitaji ya mji wa
uchumi wa gesi.  Niliwataka wahakikishe kuwa kuna maeneo ya viwanda,
biashara, makazi, mahoteli, huduma za afya, elimu, mapumziko na
burudani, viwanja vya michezo na kadhalika.  Kazi ya kutayarisha
Masterplan hiyo imeanza na Manispaa ya Mtwara inashirikiana na Wizara
ya Ardhi, Nyumba na Makazi.
Kwa upande wa uwekezaji nafahamu kuwa mpaka sasa makampuni 51
yameonyesha nia ya kuwekeza Mtwara katika viwanda, hoteli, shughuli za
uchukuzi na huduma hasa kwa sekta ya gesi.  Wanachosubiri ni kutengewa
maeneo ya kujenga, waanze.  Hivyo kukamilika mapema kwa Masterplan ya
mji wa Mtwara kutasaidia kuongeza kasi ya uwekezaji huu kufanyika.
Viwanda hivi vyote vitasaidia kuongeza ajira kwa vijana wa Mtwara na
Watanzania kwa jumla.  Nimeambiwa kwa mfano, wakati wa ujenzi wa
kiwanda cha saruji watu zaidi ya 7,000 wataajiriwa.

Ndugu Wananchi;
        Kabla hata ya ugunduzi wa gesi iliyoko baharini, tulikuwa na
mipango ya kutumia gesi ya Msimbati (Mnazi Bay) kwa ajili ya kuzalisha
umeme, kuzalisha mbolea na kutumika katika kiwanda cha saruji.  Kwa
upande wa umeme kulikuwa na mpango wa kujenga mtambo wa kuzalisha
Megawati 300 kwa kushirikiana na mwekezaji binafsi.  Bahati mbaya
wakati wa matatizo ya kifedha ya dunia mwaka 2009 mwekezaji huyo
akashindwa kupata mkopo, hivyo mradi ukasimama kutekelezwa.  Haukufa
wala haukuhamishiwa Dar es Salaam au Bagamoyo kama ambavyo imekuwa
inapotoshwa kwa makusudi.  Mradi huo bado upo, tena mpango wa sasa ni
kujenga Megawati 600zitumike Mtwara na zingine kuziingiza kwenye gridi
ya taifa kupitia Songea.

NduguWananchi;
Kwa upande wa kiwanda cha mbolea, wawekezaji wengi wameshajitokeza
tangu mwaka 2008 mpaka sasa.  Mchakato umefanyika wa kuchambua
wawekezaji wenye sifa na kutambuliwa.  Mambo mawili yamechelewesha
utekelezaji kuanza.  Jambo la kwanza ni wawekezaji na kampuni ya
Artumas iliyokuwa mbia na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania
(T.P.D.C) wakati ule, kushindwa kukubaliana nao juu ya bei ya kuwauzia
gesi.  Wawekezaji walitaka bei ya gesi ipunguzwe, lakini kampuni ya
Artumas na T.P.D.C. hawakuwa tayari kupunguza zaidi ya kiasi
walichopunguza, ambacho wawekezaji bado waliona hailipi kwa kuzalisha
mbolea.

Sababu ya pili ni matatizo ya kifedha yaliyoikumba kampuni ya Artumas
katika kipindi hicho.  Kufuatia machafuko ya masoko ya fedha na
mdororo wa uchumi wa dunia mwaka 2008/2009 kampuni ya Artumas
iliathirika na kulazimika kuuza hisa zake kwa wawekezaji wengine.
Katika kipindi hicho ilichopitia kampuni, mazungumzo na uwekezaji wa
kiwanda cha mbolea hayakuweza kupewa kipaumbele.  Mtazamo wa sasa wa
wabia wapya na T.P.D.C. ni kuwa wao wenyewe sasa wawekeze katika
ujenzi wa kiwanda cha mbolea. Serikali imekubali rai yao hiyo na
wanaendelea na matayarisho.

Ndugu Wananchi;
        Kwa upande wa kiwanda cha Saruji kitakachojengwa na kampuni
ya Dangote ucheleweshaji ulikuwa kwa sababu mbili.  Kwanza, kampuni ya
Dangote iliomba eneo zaidi ya ililokuwa imeomba na kupewa.  Hoja yao
ilikuwa kwamba eneo la ziada walilokuwa wanaliomba ndilo lenye
malighafi nyingi na bora kwa utengenezaji wa saruji.  Hivyo, waliamua
kusubiri mpaka watakapopewa eneo hilo.

Bahati mbaya eneo hilo lilikuwa linamilikiwa na mtu mwingine na
alikuwa na hati miliki nalo.  Halmashauri ya Mtwara iliomba Serikali
eneo hilo litwaliwe na baadaye ipewe kampuni ya Dangote. Serikali
ilikubali.  Hata hivyo, mchakato ulichukua muda na hata pale
ulipokamilika mwenye eneo aliupinga uamuzi wa Serikali Mahakamani.
Kesi ilichukua muda kusikilizwa na kumalizika.  Bahati nzuri Serikali
ikashinda na mara baada ya uamuzi wa Mahakama ndipo kampuni ya Dangote
ikamilikishwa eneo hilo.

Kampuni nayo ilichukua muda kuanza.  Hivi sasa, timu yake ipo kwenye
eneo na mradi uko tayari kuanza kutekelezwa.  Niliambiwa kuwa katika
magari yaliyopigwa mawe katika fujo za Mtwara ni pamoja na lile la
mradi huu.  Huo ndiyo ukweli kuhusu ujenzi wa kiwanda cha saruji cha
Dangote.  Madai kuwa kiwanda hicho kimehamishiwa Bagamoyo si ya
kweli.  Ni uzushi wa makusudi wa watu wenye nia mbaya na Serikali.
Huwezi kudai kuwa mtetezi wa wananchi wa Mtwara kwa hoja za uongo na
kufanya upotoshaji wa makusudi kabisa.

Ndugu Wananchi;
        Ujenzi wa bomba la gesi ndiyo uliozua mzozo wote huu.
Zilijengwa hisia kuwa gesi yote inapelekwa Dar es Salaam na kwamba
Mtwara itakosa gesi na maendeleo yatayotokana na gesi hiyo.  Na,
wengine wakasema gesi inapalekwa Bagamoyo ili kuzidisha chumvi na
kupandikiza chuki kwa wananchi dhidi ya Serikali kwamba Rais anapeleka
gesi kwao. Kwanza, Kinyerezi iko Ilala na siyo Bagamoyo.  Pili, ukweli
ni kwamba pale Mtwara kuna gesi nyingi ya kutosheleza mahitaji ya
Mtwara, Lindi na Dar es Salaam na kubaki.  Gesi itakayoletwa Dar es
Salaam niasilimia 16 tu ya gesi yote iliyoko Mtwara kwa miaka ishirini
ijayo.  Hivyo asilimia 84 ya gesi itabaki Mtwara kwa ajili ya kuuzwa
nje ya nchi na kupelekwa kwingineko nchini.

        Kwa sababu hiyo, ndugu zetu wa Mtwara hawana sababu ya kuwa
na wasiwasi. Ipo gesi ya kutosha kwa mahitaji ya sasa na ya miaka
mingi ijayo.  Viwanda vinavyotumia gesi kama mali ghafi na vile
vinavyohitaji gesi kama nishati vyote vitapata gesi ya kutosha.  Kwa
upande wa uzalishaji umeme hali kadhalika ipo gesi ya kutosha
kuzalisha umeme mwingi zaidi.  Hivi sasa tunacho kituo kinachozalisha
umeme wa megawati 15 unaotumika Mtwara, Lindi, Tandahimba, Newala,
Masasi, Nachingwea, Ruangwa, na Mtama. Bado umeme huo hautumiki wote
hivi sasa.

Ndugu Wananchi;
        Nayaeleza yote haya kuwathibitishia wananchi wa Mtwara kuwa
tunawathamini sana na kuwajali.  Mimi nitakuwa mtu wa mwisho kuwapuuza
na kuwatupa mkono wananchi wa Mikoa ya Kusini.  Aidha, sitakuwa tayari
kuwaruhusu watu au mtu ye yote Serikalini kuwapuuza wananchi wa Mikoa
ya Kusini au mkoa wo wote hapa nchini.  Hiyo haitakuwa sawa.
Nilishasema siku za nyuma na napenda kurudia tena leo kuwa kwangu mimi
hakuna mkoa ulio bora kuliko mwingine.  Ni kutokana na msimamo wangu
huo ndiyo maana tumeelekeza nguvu na rasilimali nyingi za Serikali
katika mikoa iliyokuwa inadaiwa kuwa imesahauliwa.  Kazi ya ujenzi wa
barabara za lami iliyofanyika na inayoendelea kufanyika katika mikoa
ya Lindi, Mtwara, Ruvuma, Rukwa, Kigoma na Kagera inajieleza yenyewe.
Mipango ya kuboresha Kiwanja cha Ndege cha Mtwara kufikia hadhi ya
kimataifa na uboreshaji wa viwanja vya ndege vya Lindi na Kilwa ni
ushahidi mwingine kati ya mambo mengi tunayoweza kuyataja.

Ndugu Wananchi;
        Haya niliyoyasema ni sehemu ndogo tu ya yale yaliyofafanuliwa
na kuelezwa kwa kina na Mawaziri na Wakuu wa Idara husika  za Serikali
na Mashirika  ya Umma pale Mtwara katika mkutano wa Waziri Mkuu na
viongozi wa Serikali, dini, vyama vya siasa na wazee wa Mkoa wa Mtwara
tarehe 29 Januari, 2013.

Ndugu Wananchi;
Napenda kutumia nafasi hii kutoa pongezi nyingi kwa Waziri Mkuu,
Mheshimiwa Mizengo Pinda, kwa kazi kubwa na nzuri aliyoifanya kule
Mtwara.  Uvumilivu wake, usikivu wake na utulivu wake vimesaidia sana
kulivusha taifa katika moja ya mitihani mikubwa ambayo ingeikuta nchi
yetu tangu Uhuru.  Nawapongeza Mawaziri na Wakuu wa Mashirika ya Umma
na Idara za Serikali kwa mchango wao muhimu walioutoa, uliosaidia
kufafanua masuala ambayo yalikuwa hayaeleweki vizuri.  Kwa wao
nawasisitiza na kuwakumbusha wajibu wao wa kuelimisha jamii kuhusu
shughuli wazifanyazo.  Wakifanya hivyo mara kwa mara migongano
haitakuwepo na wapotoshaji hawatapata nafasi.

Ndugu Wananchi;
        Nitakuwa mwizi wa fadhila kama sitawashukuru viongozi wa
Serikali, vyama vya siasa, madhehebu ya dini, viongozi wa jamii,
wazee, wana-Mtwara na makundi mbalimbali ya jamii, kwa muda waliotumia
kuzungumza na Waziri Mkuu na kuwasikiliza wasaidizi wake wakifafanua
masuala mbalimbali.  Uvumilivu wao na uelewa wao ndivyo vilivyosaidia
kurejesha hali kuwa ya kawaida.  Nawaomba nao sasa, wote kwa pamoja
washirikiane na Serikali kuelimisha umma kuhusu ukweli wa mambo.  Pia
watumie nafasi hiyo kutahadharisha jamii na kuwataka watu kuwa
waangalifu na kupima maneno wanayoambiwa na watu.  Wajiepushe na
maneno au vitendo vinavyofarakanisha, kuchonganisha na kupandikiza
chuki dhidi ya watu au Serikali. Waambieni kuwa ghasia hukimbiza
wawekezaji kwani wakipata hofu kuwa hali ya amani na usalama ni ya
mashaka, watatoka kwenda kuwekeza kwingine.  Vyema iwe hapa hapa
nchini, lakini wanaweza kwenda nchi nyingine na sisi kupoteza kabisa.

Ndugu Wananchi;
        Nawapa pole wananchi wa Mtwara na Masasi kwa usumbufu
walioupata kutokana na ghasia zilizofanywa.  Nawapa pole waliofiwa na
kujeruhiwa.  Nawapa pole waliopoteza au kuharibiwa mali zao.  Kwa
kweli inasikitisha na kufadhaisha kuona watu wanafanya vitendo vya
kuua, kuchoma moto nyumba za watu na majengo ya Serikali pamoja na ,
kuharibu na kuiba mali za watu.  Huu ni uhalifu ambao hauna maelezo na
haukubaliki.  Tunaviachia vyombo husika vya dola na sheria kutimiza
wajibu wao.  Kwa waliohusika iwe fundisho kwao na kwa wengineo
kutokubali kutumika kwa maslahi ya watu wengine siku zijazo.  Sasa
wameachwa pekee yao wakati wenzao wako huru na kufaidi maisha

Ndugu Wananchi;
Hili sakata la bomba la gesi limefika mahali pazuri.  Yaliyopita si
ndwele tugange yajayo.

Mungu Ibariki Afrika!
Mungu Ibariki Tanzania!
Asanteni Sana kwa Kunisikiliza!


Source: http://www.wavuti.com/4/post/2013/02/hotuba-ya-rais-kikwete-ya-mwisho-wa-mwezi-wa-januari-2013.html#ixzz2JkbkOTwJ

Wednesday, November 12, 2008

Hotoba ya Mwalimu Nyeyere

Asante sana Da Subi kwa hii:

****************************************

Karibu kumsikiliza Mwalimu J.K Nyerere katika hotuba aliyoitoa sikuya Jumanne, Machi 14, 1995 katika iliyokuwa hoteli ya Kilimanjaro.

Hotuba ya Mwl. J.K Nyerere siku ya Jumanne Machi 14, 1995 (sehemu ya1/3)

Subi

Thursday, July 31, 2008

Rais Kikwete Aongea na Wananchi Leo!

Rais Jakaya Kikwete



HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO
WA TANZANIA,MHESHIMIWA JAKAYA
MRISHO KIKWETE,KWA WANANCHI,
TAREHE 31 JULAI,2008..

Ndugu Wananchi;Naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uzima na kuniwezesha kuzungumza nanyi leo mwishoni mwa mwezi wa Julai,2008.Nasikitika na nawataka radhi kwamba kwa miezi ya Aprili,Mei na Juni, sikuweza kupata fursa ya kuzungumza nanyi kupitia utaratibu wetu huu mzuri.

Sababu kubwa iliyonifanya nishindwe kuzungumza na Taifa, ni ule ukweli kwamba, tarehe za mwisho wa mwezi katika miezi hiyo zilinikuta nikiwa nje ya nchi kikazi. Safari ambazo nisingeweza kuacha kwenda labda ningekuwa nimepata dharura kubwa.

Huko nyuma katika mazingira ya namna hii nilitumia utaratibu wa kurekodi hotuba yangu kabla ya kuondoka na kuacha itangazwe siku ya mwisho wa mwezi ilipofikia. Utaratibu huo ulikidhi haja, lakini nikaambiwa kuwa haukufurahiwa sana na wengi hasa pale ilipotokea kuwa Rais wao waliyemsikia redioni leo akihutubia,walimsikia jana akiwa nchi ya mbali na wanajua hajarejea.Kwa sababu hiyo basi,nikaona kwamba nizungumze katika utaratibu huu wa mwisho wa mwezi pale tu nitakapokuwa ndani ya nchi.

Hata hivyo, uamuzi huo umezua manung’uniko yake hasa pale ambapo miezi mitatu mfululizo imetokea Rais kutozungumza kwa sababu ya kuwa nje ya nchi kikazi.Maoni ya pande zote nimeyasikia,nipeni muda nitafakari lipi bora tufanye.Ndugu Wananchi;

Ni makusudio yangu leo kuelezea matokeo ya safari zangu hizo.Mwishoni mwa mwezi wa Aprili nilikwenda Ethiopia na Uganda.Kule Addis Ababa,Ethiopia tarehe 28 Aprili,2008 nilitimiza jukumu la kushuhudia makabidhiano ya ofisi ya Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika baina ya Mwenyekiti aliyemaliza muda wake wa uongozi, Mheshimiwa Prof.Alpha Oumar Konare,na Mwenyekiti mpya Mheshimiwa Jean Ping.

Ni utaratibu uliowekwa kuwa shughuli hiyo ya makabidhiano ya ofisi husimamiwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika wa wakati huo.Nilitumia nafasi hiyo kuzungumza na uongozi mpya wa Kamisheni ya Afrika juu ya matarajio yangu na viongozi wenzangu wa Afrika kwao. Aidha,nilizungumza na wafanyakazi wa Umoja wa Afrika pamoja na kuwatambulisha viongozi wapya wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika kwao.

Siku iliyofuata niliitumia kuzungumza na Wajumbe wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika kuhusu hali ya amani na usalama ya Bara letu.Tulitumia muda mwingi kujadili migogoro inayolikabili Bara letu na hatua muafaka za kuchukua kuitafutia ufumbuzi.Tarehe 30 na 31 Aprili,2008 nilikuwa Uganda kwa mazungumzo na Rais Yoweri Museveni wa nchi hiyo.

Pamoja na kuzungumzia masuala yahusuyo nchi zetu za Afrika Mashariki na Afrika tulijadili hali ya usalama na amani ya eneo la Maziwa Makuu.Hususan tulizungumzia Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Jamhuri ya Burundi. Matokeo ya mazungumzo yetu hayo ni mambo mawili muhimu.

Kwanza, ni mkutano uliofanyika Dar es Salaam kati ya Rais Yoweri Museveni wa Uganda na Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo tarehe 11 Mei,2008.Katika mkutano huo nchi hizo mbili jirani zilifanikiwa kuzungumzia tofauti zao na kuafikiana kuhusu namna ya kuzimaliza.

Pili,kuhusu Burundi ni kufanikiwa kumrejesha Burundi Bwana Agathon Rwasa, Kiongozi wa PALIPEHUTU-FNL na viongozi wenzake waandamizi wa chama hicho. Kitendo hicho kimefunga ukurasa wa shughuli za usuluhishi wa mgogoro wa Burundi zilizotuchukua takriban miaka 13 (tangu Disemba, 2005).

Aidha, kitendo hicho sasa kimefungua njia ya kumaliza tatizo la wakimbizi wa Burundi. Wapo waliokuwa wanasita kurejea kwako kwa sababu ya viongozi kuwa nje ya Burundi. Sasa wingu hilo limeondoka. Ni matumaini yangu kuwa kasi ya wakimbizi hao kurudi kwao itaongezeka.
Ndugu Wananchi;

Mwishoni mwa mwezi Mei, 2008 nilikuwa nchini Japan kuongoza ujumbe wa viongozi wa Afrika katika Mkutano wa Nne wa Kimataifa wa Tokyo Kuhusu Maendeleo ya Afrika (TICAD IV) uliofanyika Yokohama kuanzia tarehe 27 hadi 30 Mei, 2008.

Ujumbe wa Afrika niliouongoza nikiwa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, ulikuwa na Wakuu wa Nchi na Serikali wapatao 40.Huu ulikuwa ni moja ya mikusanyiko mikubwa ya viongozi wa Afrika kwa mikutano nje ya Afrika.

Ndugu Wananchi; Mikutano ya TICAD ilianza mwaka 1993 na hufanyika kila baada ya miaka 5. Wazo la kuwa na mikutano hii liliasisiwa na Mheshimiwa Morihiro Hosokawa, aliyekuwa Waziri Mkuu wa Japan wakati ule.Madhumuni ya Mikutano hii ni kusaidia kuongeza kasi ya maendeleo ya Bara la Afrika.

Serikali ya Japan iliamua kutumia mikutano hii kuchangia nguvu zake za kiuchumi na kiteknolojia na zile za nchi rafiki zake pamoja na za mashirika ya kimataifa yanayojihusisha na masuala ya maendeleo kusaidia kukuza uchumi wa Afrika na kuboresha hali ya maisha ya watu wa Bara la Afrika. Katika mkutano uliopita wa TICAD, nchi 34 marafiki wa Japan na Afrika zilishiriki ikiwa ni pamoja na mashirika ya kimataifa 75.

Maamuzi mengi ya msingi yamefanywa na ahadi nyingi za manufaa kwa maendeleo ya nchi za Afrika na watu wake yalifanywa.Kama maamuzi hayo yaliyojumuishwa katika Tamko la Yokohama na Mpango wa Utekelezaji wa Mkutano wa Nne wa TICAD yatatekelezwa, itasaidia sana kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya Afrika kwa kasi zaidi.

Ndugu Wananchi;
Miongoni mwa maamuzi muhimu yenye maslahi kwa Afrika ni haya yafuatayo:(a) Serikali ya Japan itaongeza mara mbili misaada ya maendeleo inayotoa kwa nchi za Afrika.(b) Maeneo ya kipaumbele kwa misaada ya Japan itakuwa ni kuendeleza miundombinu hususan barabara, bandari, reli, usafiri wa anga,maji na umeme.

(c) Japan itasaidia Afrika kuongeza mara mbili uzalishaji wa mpunga.(d) Japan kusaidia Afrika kuendeleza elimu na huduma ya afya.Kwa upande wa huduma ya afya, kipaumbele kimewekwa kwenye kupambana na UKIMWI na kupunguza vifo vya watoto na kina mama kwa matatizo ya uzazi. (e) Japan kuongeza misaada kwa nchi za Afrika kukabili athari za mabadiliko ya hali ya hewa duniani au kwa neno la kitaalam tabia nchi; na(f) Kwa nia ya kukuza uwekezaji wa makampuni ya Kijapani Barani Afrika, serikali ya Japan imetenga dola 2.5 bilioni kwa ajili ya kusaidia wawekezaji wa nchi hiyo watakaowekeza Afrika.Ndugu Wananchi; Hayo ndiyo matokeo ya Mkutano wa Nne wa Tokyo kuhusu Afrika.Ni matokeo yenye matumaini makubwa kwa Afrika kwa maana mbili: Kwanza, tofauti na mikutano iliyopita, safari hii mfumo wa ufuatiliaji umetengenezwa (Follow up mechanism). Hii inatupa imani kuwa yale yaliyokubaliwa yatafuatiliwa kwa dhati.

Pili, kwa maana ya yale yaliyokubaliwa na kuamuliwa kuwa ni mambo yenye maslahi makubwa kwa nchi zetu na watu wake.

Hata hivyo,ndugu wananchi, mambo haya mazuri watayapata wale watakaoyachangamkia. Nchi zitakazopeleka mapendekezo yao ya miradi watanufaika, na wale ambao hawatafanya hivyo watakosa.Kwa kutambua ukweli huo nimeziagiza Wizara husika chini ya uongozi na uratibu wa Wizara ya Fedha na Uchumi watayarishe miradi na kuiwasilisha kwa Serikali ya Japan mapema iwezekanavyo.

Ndugu Wananchi; Wakati wa Mkutano wa TICAD tarehe 29 Mei,2008 kulifanyika mkutano maalum wa kuzungumzia tatizo la bei kubwa za chakula duniani.Nilipewa heshima ya kuwa Mwenyekiti wa mkutano huo ulioitishwa na Benki ya Dunia ikishirikiana na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO),Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo(IFAD)na Shirika la Dunia la Chakula (WFP).

Katika mkutano huo ilibainika kuwa bei za vyakula takriban katika nchi zote duniani imeongezeka mara mbili katika kipindi cha miaka mitano iliyopita na kwamba bei inatarajiwa kuendelea kupanda mwaka huu na hata mwaka ujao.Ilielezwa pia kwamba zipo sababu kadhaa zinazosababisha bei kupanda lakini kubwa zaidi ni:
(a) Chakula kilichopo kuwa kidogo kuliko mahitaji;
(b) Kupanda kwa gharama za uzalishaji kwa sababu ya kupanda sana kwa bei ya mafuta na bei ya mbolea;
(c) Mabadiliko ya hali ya hewa duniani kunakosababisha ukame na mafuriko ya mara kwa mara siku hizi; na
(d) Kupungua kwa kilimo cha nafaka kwa sababu ya kilimo cha mazao ya kuzalisha nishati.
Ndugu Wananchi; Kwa kauli moja mkutano umekubaliana kuwa kwa upande wa Afrika suala la msingi ni kuwasaidia wakulima wa Afrika waongeze tija kwenye kilimo.Hili likifanyika Afrika inao uwezo siyo tu wa kujilisha wenyewe bali pia wa kulisha watu wengi wengine duniani.Mkutano ulipongeza juhudi zinazoendelea kufanywa na mashirika hayo manne ya kimataifa kusaidia nchi za Afrika kuendeleza kilimo.

Aidha, wito ulitolewa kwa nchi zilizoendelea na mashirika ya fedha ya kimataifa kuunga mkono jitihada hizo zikiwemo zile za kuwawezesha wakulima wadogo wadogo kupata mbegu bora, mbolea na mikopo.

Nafurahi kwamba tangu mkutano ule kuna utambuzi mkubwa zaidi na vuguvugu la kuwasaidia wakulima wadogo wa Afrika limeongezeka. Na, sisi kiserikali tumeshaomba Tanzania ijumuishwe katika jitihada hizo.Tunasubiri majibu. Iwapo tutafanikiwa kujumishwa na kupatiwa misaada tuliyoomba, matatizo ya sasa ya upatikanaji wa mbegu, mbolea na mikopo kwa wakulima wadogo yatapungua.

Ndugu Wananchi; Nafurahi pia kwamba tarehe 7 Julai,2008 nchi yetu ilipewa heshima nyingine kubwa ya kuongoza ujumbe wa Marais saba wa Afrika kwenye Mkutano wa Mataifa Manane yenye Viwanda Vingi Duniani (G-8).Mataifa hayo hukutana kila mwaka kujadili hali ya uchumi wa dunia na mwelekeo wake.

Kwa mwaka huu wa 2008, nchi hizo zilikutana huko Hokkaido nchini Japan mwanzoni mwa mwezi huu.Mimi na viongozi wenzangu wa Algeria, Senegal,Ghana,Afrika Kusini,Nigeria na Ethiopia tulitumia fursa hiyo kuelezea matatizo yanayolikabili Bara la Afrika na kusisitiza haja ya wajibu wa nchi zilizoendelea zikiongozwa na Kundi la Nchi Nane zenye viwanda vingi duniani, kuzisaidia nchi za Afrika kuondokana na umaskini uliokithiri na kuwa nyuma kwa kimaendeleo. Tulisisitiza kama tulivyofanya katika mkutano wa Nne wa TICAD haja ya kuongeza misaada ya maendeleo kwa Afrika.

Tuliwakumbusha viongozi wa G-8 kuhusu ahadi yao walioitoa kwenye mkutano wao wa Gleneagles mwaka 2005 kuhusu kuongeza misaada ya maendeleo kwa Afrika. Tumewataka watekeleze.

Aidha, kuhusu vipaumbele,tulisisitiza umuhimu wa kuongeza misaada inayotolewa kuendeleza miundombinu barani Afrika, kwani maendeleo hayatawezekana bila barabara nzuri, bandari, usafiri wa anga,umeme,maji na mawasiliano.Tuliitumia nafasi hiyo kuwasilisha kilio chetu kuhusu matatizo ya kupanda sana kwa bei za chakula na mafuta ya petroli duniani na athari zake kwa watu wa nchi zinazoendelea za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara.Tumeelezea kwa kina athari zake na hasa tishio la kufuta mafanikio kiasi yaliyopatikana na kurudisha nyuma jitihada za kujiletea maendeleo.

Tuliowaomba Wakubwa hao wafanye kila wawezalo kuzuia kupanda holela kwa bei za mafuta na kuzisaidia nchi maskini na zinazoendelea za Afrikakukabili athari za kupanda kwa bei ya mafuta na bei ya chakula. Kama tulivyosema kwenye Mkutano wa TICAD na katika mkutano wa G-8 nako tuliomba kwa upande wa tatizo la upungufu wa chakula,nguvu zielekezwe kwenye kusaidia nchi zetu kufanya mageuzi ya kilimo na siyo kwenye kupewa misaada ya chakula pekee. Ujumbe wetu ulipokelewa vizuri na kuahidiwa kusaidiwa.Tunachosubiri sasa ni kuona vitendo.

Tutaendelea kufuatilia na kukumbushia bila ya kuchoka.Ndugu Wananchi; Mwishoni mwa mwezi wa Sita sikuweza kuzungumza na taifa kwa sababu ya kwenda Misri kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika.Ulikuwa mkutano mgumu kwa kiasi chake, hasa kwa mie niliyekuwa Mwenyekiti.Hata hivyo,nilifurahi kuwa hatimaye mambo yaliisha vizuri hata kuliko tulivyotarajia.

Nilifurahi sana pale rai yangu ya kujipa muda wa kutosha wa kujadili masuala ya maendeleo ya Afrika ilipokubaliwa.Niliomba hivyo kwa sababu tumekuwa na mazoea ya kutumia muda mwingi kujadili masuala ya siasa na migogoro.Watu wan chi zetu hawakuishi kwa siasa pekee. Safari hii tulijipa muda wa kutosha kujadili masuala ya maendeleo ya Afrika. Kuendeleza rasilimali maji na utekelezaji wa malengo ya Milenia barani Afrika yalikuwa ndiyo mambo makubwa yaliyotuchukulia muda mwingi.Kwangu mimi kutoa nafasi stahiki kuzungumzia masuala ya maendeleo ya nchi zetu na watu wake ni hatua kubwa ya maendeleo kwa Umoja wa Afrika. Hili ni jambo la faraja sana na nimeeleza matumaini yangu kuwa utaratibu huu tutaudumisha na kuuendeleza.

Ndugu Wananchi;
Kwa upande wa siasa na migogoro, mambo mawili yalichukua muda mwingi wa mjadala kwenye mkutano wetu. Mambo hayo ni:
(a) Uanzishaji wa Serikali ya Umoja wa Afrika.
(b) Mgogoro wa Zimbabwe. Nafurahi kwamba pamoja na ugumu wa mijadala lakini hatimaye tulielewana vizuri kuhusu nini cha kufanya. Kuhusu Serikali ya Umoja ya Afrika tumekubaliana kuhusu viashiria na vichocheo vya kuwezesha Serikali hiyo kuwepo. Hata hivyo, hatukuweza kuelewana kuhusu lini Serikali hiyo inaweza kuundwa na muundo wake. Bado kuna tofauti kubwa za mawazo miongoni mwetu. Tumekubaliana tuendelee kulizungumza suala hilo kikao kijacho.

Kuhusu Zimbabwe, tulikubaliana kuwa,pamoja na kasoro zilizojitokeza wakati wa mchakato wa uchaguzi na kutia dosari kwa uhalali wake,bado jawabu litapatikana kwa pande husika kukaa chini na kuzungumza.Nafurahi kwamba yale tuliyoamua yafanyike yameanza kutekelezwa. Mchakato huo umeanza.Tuwatakie kila la heri ndugu zetu wa Zimbabwe mazungumzo yakamilike salama na nchi yao irejee katika hali yake ya kawaida na wananchi wa nchi hiyo waanze kazi ngumu ya kujenga upya taifa lao.

Ndugu Wananchi; Katika kipindi cha miezi mitatu hii ambayo sikupata nafasi ya kuzungumza na taifa. Kumekuwepo na matukio kadhaa hapa nchini yaliyogusa maisha,nyoyo na hisia za watu kwa namna mbalimbali.Yalikuwepo mambo mazuri,yalikuwepo mambo magumu na hata ya huzuni na majonzi.
Aidha,yalikuwepo mambo yaliyoleta mtikisiko kwa jamii na hata kwa taifa na utaifa wetu. Kwa vile mambo ni mengi kiasi sitapata nafasi ya kuyazungumzia yote moja baada ya jingine.Napenda kuitumia nafasi hii kuwatoa wasiwasi na kuwahakikishia Watanzania wenzangu kuwa, taifa letu bado ni moja na watu wake bado ni wamoja.

Tofauti za mawazo na fikira miongoni mwetu hazitakosekana.Naomba tuyaone mawazo na fikira hizo kuwa changamoto za kushughulikia katika kuimarisha umoja wa taifa letu na mshikamano wa watu wake.Napenda kuwahakikishia kuwa sisi viongozi wenu tunayatambua hayo na tunayashughulikia. Hakuna kubwa la kutuzidi kimo na kwamba hakuna litakaloharibika. Kwa vile nia yetu ni njema na penye nia pana njia sina shaka mambo yatakuwa sawa.Nawaomba tuwe watulivu kwani utulivu wetu ni sehemu ya jawabu.Ni imani yangu kuwa kila anayeitakia mema nchi yetu atafanya hivyo.

Ndugu Wananchi;

Jambo la mwisho ambalo ningependa kuliongelea leo linahusu msiba uliotukuta wa Mbunge wa Tarime, Marehemu Chacha Wangwe.Kifo chake cha ghafla kimetushtua na kutusikitisha wengi. Marehemu alikuwa mtu muwazi na mkweli.Hakuwa na woga wa kutoa maoni yake kwa jambo analoliamini. Hakika Bunge,Jimbo la Tarime na Taifa limepoteza mwakilishi wa kutumainiwa. Daima atakumbukwa kwa sifa zake hizo na mchango wake huo kwa taifa.

Ndugu Wananchi;
Napenda kuitumia nafasi hii kutoa mkono wa pole na rambirambi kwa familia na ndugu wa marehemu.Naelewa machungu mliyonayo.Mimi na Watanzania wote wenye nia njema tuko pamoja nanyi katika msiba huu mkubwa uliowakuta. Ni msiba wetu sote na ni machungu yetu sote.

Nawapa pole sana Wabunge wote wa Bunge letu tukufu kwa kupoteza mwenzi wenu na rafiki yenu. Nawapa pole viongozi na wanachama wa Chama cha CHADEMA kwa kupoteza kiongozi wenu mahiri.Wananchi wenzangu wa Jimbo la Tarime nao nawapa pole kwa kupoteza mwakilishi na mtetezi wenu shupavu.Tuzidi kumwombea kwa Mwenyezi Mungu ampe mapumziko mema.Hitimisho

Ndugu Wananchi;

Kwa mara nyingine tena nawashukuru tena kwa msaada wenu na ushirikiano wenu. Mimi na wenzangu mliotupa dhamana ya kuliongoza taifa letu tutaendelea kuwatumikia kwa nguvu na uwezo wetu wote ili tufikie kwenye dhamira yetu ya kuharakisha maendeleo ya nchi yetu.
Kwa pamoja tutashinda.Mungu Ibariki TanzaniaMungu Ibariki Afrika.

Asanteni kwa kunisikiliza.