Showing posts with label Mh. John Mnyika. Show all posts
Showing posts with label Mh. John Mnyika. Show all posts

Friday, March 20, 2015

Muswada Binafsi wa Baraza la Vijana la Taifa Kujadiliwa Bungeni

Mh. John Mnyika


MUSWADA BINAFSI WA BARAZA LA VIJANA LA TAIFA KUJADILIWA BUNGENI TAREHE 31 MACHI 2015
Nashukuru wote ambao mmekuwa mkifuatilia hatma ya muswada binafsi wa Baraza la Vijana la Taifa niliouwasilisha tarehe 31 Oktoba 2013.
Vijana na wadau wa maendeleo ya vijana mzingatie kwamba muswada huo hatimaye umepangwa kusomwa kwa mara ya pili na kujadiliwa Bungeni Jumanne tarehe 31 Machi 2015 katika Mkutano wa 19 wa Bunge.
Muswada huo ulisomwa kwa mara ya kwanza katika Mkutano wa 14 wa Bunge tarehe 21 Disemba 2013. Maoni kutoka kwa wadau yalikusanywa Oktoba 2014 na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii.
Baraza la Vijana la Taifa pamoja na malengo mengine litawezesha vijana kuanzia kwenye vijiji/mitaa mpaka taifa kuweza kuwa na vyombo vya kuwaunganisha vijana kwa kike na wa kiume kwa ajili ya maendeleo yao na ya taifa.
Aidha, Baraza hilo litafuatilia pia kwa karibu utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya vijana ikiwemo kuhusu ajira, elimu na sekta zingine katika Halmashauri, Serikali kuu, katika vyombo mbalimbali vya maendeleo na wadau wa maendeleo.
Pia, Muswada huo utawezeshwa kuanzishwa kwa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana na kulipa jukumu Baraza la Vijana kufuatilia kwa karibu utendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana; kuhakikisha kwamba fedha zinatengwa za kutosha na kufika kwa walengwa kuwawezesha vijana kujiajiri, kukuza vipaji vyao na kushughulikia maendeleo yao kwa ujumla.
Kujadiliwa kwa muswada huo ni hatua ya pekee katika historia ya harakati za vijana nchini kwa kuzingatia kuwa Sera ya zamani ya maendeleo ya vijana ya mwaka 1996 ilitamka kwamba kutaanzishwa  Baraza la Vijana na suala hilo kurudiwa katika Sera mpya ya mwaka 2007.
Hata hivyo Serikali imekuwa ikikwepa kuhakikisha kwamba matakwa hayo ya sera tajwa yanatekelezwa kwa wakati pamoja na kuwa suala hilo linahusu mustakabali wa maendeleo ya vijana nchini.

Natambua mchango wa vijana na taasisi zote za vijana mlioshiriki katika maandalizi ya muswada huu, unaitwa binafsi kwa sababu tu ndio neno linalopaswa kutumika kwa mujibu wa Kanuni za Bunge lakini ukweli ni kwamba huu ni muswada wenu; mimi ni mwakilishi.

John Mnyika (Mb)
20 Machi 2015

Tuesday, June 19, 2012

Msimamo wa John Mnyika Juu ya Bajeti!

Msimamo wangu wa sasa juu ya Kauli yangu!


Nitatoa tamko la kina baadae kuhusu kilichotokea lakini kwa ufupi ubovu wa bajeti hii ni matokeo ya udhaifu wa Rais Kikwete, yeye ndiye aliyesaini Mpango wa Taifa wa miaka mitano kama Kiongozi Mkuu wa Nchi tena kwa wino mwekundu kama Amiri Jeshi Mkuu. Na yeye ndiye Mwenyekiti wa baraza la mawaziri, bajeti hii iliyoacha kuzingatia mpango wa Taifa imepita kwenye baraza alilloliongoza, pia kushindwa kutekelezwa kwa bajeti iliyopita ni matokeo pia ya udhaifu wa taasisi ya Urais.

Pia kwa mujibu wa Katiba Rais ndiye ambaye anapeleka bajeti bungeni, Waziri mwenye dhamana anapeleka tu kwa niaba. Rais amepewa mamlaka makubwa juu ya bajeti ibara ya 99 imeweka mipaka kuhusu mambo ambayo bunge lina mamlaka nayo huku ibara ya 90 inasema bunge likikataa bajeti rais ana mamlaka ya kuvunja bunge. Hivyo Rais Kikwete anapaswa kuagiza Waziri wa Fedha bajeti iondolewe irudi kwenye baraza la mawaziri ikafanyiwe marekebisho!

http://mnyika.blogspot.com/2012/06/msimamo-wangu-wa-sasa-juu-ya-kauli.html

John Mnyika
19 Juni 2012