Showing posts with label Benjamin Mkapa. Show all posts
Showing posts with label Benjamin Mkapa. Show all posts

Wednesday, March 14, 2012

Mkapa Ahusushwa na Kifo Cha Utata cha Mwalimu Nyerere!

Duh!  Hizi tuhuma nzito kweli!  Rest in Peace, Mwalimu Nyerere!

**************************************************************

Kutoka Tanzania Daima

Mkapa Apigwa Kombora
•  Ahusishwa na kifo chenye utata cha Mwalimu Nyerere


na Mwandishi wetu, Arumeru

VITA ya maneno, vijembe na kejeli kati ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), katika kampeni za
uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Arumeru Mashariki, mkoani
Arusha imeanza.

Baada ya juzi Rais mstaafu, Benjamin Mkapa, kufanya uzinduzi wa
kampeni za CCM na kuipiga vijembe CHADEMA, chama hicho jana kilijibu
mapigo kupitia kwa Mbunge wa Msoma Mjini, Vincent Nyerere, ambaye ni
Naibu Meneja wa Kampeni wa CHADEMA.

Akizungumza katika mikutano ya kampeni maeneo mbalimbali, mbunge huyo
alishusha tuhuma nzito juu ya kile alichokiita ‘utata’ wa kifo cha
Mwalimu Nyerere huku akihusisha na maamuzi ya Mkapa kung’ang’ania
Mwalimu aende kutibiwa Uingereza baada ya kuanza kumkosoa juu ya sera
za ubinafsishaji.

Nyerere ambaye ni mmoja wa wanafamilia wa hayati Baba wa Taifa
Mwalimu Nyerere, akiwa amekulia katika familia hiyo, aliwaambia
wananchi wa maeneo hayo kuwa umefika wakati sasa Mkapa atoke hadharani
afafanue alikuwa na nia gani kumlazimisha Mwalimu Nyerere akatibiwe
Uingereza wakati mwenyewe alikuwa amekataa, akisema kuwa ugonjwa
uliokuwa unamsumbua tayari ulikuwa unajulikana na daktari wake,
Profesa David Mwakyusa, alikuwa tayari akimhudumia vizuri bila tatizo.

“Jana katika hotuba yake ametumia muda mwingi sana kuisema CHADEMA na
akanisema mimi kwa jina moja kwa moja, sasa ‘kanibipu’ na mimi
nimeamua kumpigia, tunamtaka kama anaweza arudi hapa Arumeru, aje
ajibu maswali ya msingi juu ya ufisadi unaomwandama. Alianza kwa kuuza
mashirika ya umma, akauza viwanda, ukienda leo miji mikubwa kama Dar
es Salaam na kwingineko, vijana wengi wamegeuka kuwa waokota makopo
kwa sababu hakuna ajira, viwanda viliuawa wakati wa Mkapa.

“Kwa kupitia sera yake ya ubinafsishaji akauza kila kitu, akauza
viwanda, wawekezaji walionunua nao wakafanya ufisadi wamegeuza viwanda
hivyo kuwa maghala ya kutunzia vitu vyao, viwanda ambavyo vingeweza
kuajiri vijana Watanzania vikauzwa kiholela kwa bei ya kutupa, vingine
wakajiuzia wao wenyewe. Misingi iliyowekwa na Mwalimu yote ikabomolewa
badala ya wao kujenga nyumba juu ya misingi hiyo.

“Mashirika yaliyokuwa yakifanya kazi vizuri au ambayo yalihitaji
usimamizi tu mzuri ili yafanye vizuri yakauzwa kiholela, yakauzwa
kifisadi, tena mkumbuke alianza kwa kuuza benki. Mwalimu kuona hivyo
akashtuka, akaanza kumhoji na kumkosoa hadharani juu ya sera yake
hiyo, jamaa (Mkapa) kuona hivyo akaona huu sasa ni usumbufu, akaanza
kumshawishi Mwalimu aende akatibiwe Uingereza, Mwalimu alikataa kabisa
akisema kuwa ugonjwa unaomsumbua tayari daktari wake anamhudumia
vema,” alisema Nyerere na kuongeza:

“Mwalimu alikuwa akihoji inakuwaje reli inakufa, yeye amekazana tu na
ubinafsishaji, Mwalimu akahoji inakuwaje anatoza kodi kibao na kutunza
pesa, kumbe Mkapa tayari alikuwa anaandaa pesa za EPA ambazo baadaye
ndizo mlizisikia kupitia kashfa maarufu ya mabilioni ya EPA. Mkapa
akamng’ang’ania Mwalimua akatibiwe Uingereza, akasema naye ni mmoja wa
wanafamilia yetu, basi tukakubali, lakini mnajua kuwa Mwalimu
alikwenda anatembea akarudi amenyamaza ndani ya jeneza?

“Sasa Mkapa atuambie ukweli juu ya hili, aje ajibu maswali yote haya,
nitakuja na vigongo vingine, lazima tupambane na ufisadi hadi mwisho.
Ilifikia mahali hata taarifa za ugonjwa akawa anatoa yeye Mkapa, oooh
mara Mwalimu amepatwa na mkanda wa jeshi, mara oooh leo imekuwa hivi,
badala ya daktari wake. Baada ya Mwalimu kufariki dunia, wakamwambia
yule daktari wake agombee ubunge watampatia uwaziri, ndivyo
ilivyotokea,” alisema Nyerere.

Aliongeza kusema kuwa pamoja na uhakika wa maisha yake baada ya
kustaafu ambapo anagharimiwa kila kitu kwa kodi za Watanzania, bado
Rais Mkapa alijimilikisha mgodi wa Kiwira ambao baada ya kelele nyingi
za nguvu za umma, zikiongozwa na CHADEMA bungeni na nje ya Bunge,
hatimaye umerudishwa kwa umma.

Alimtaka Rais Mkapa kujibu tuhuma juu ya ufisadi katika ununuaji wa
ndege, wakati tayari serikali ilikuwa na ndege nyingine mbili, moja
ikinunuliwa wakati wa Mwalimu na ina uhakika wa kufanya kazi kwa miaka
100 iwapo ingefanyiwa matengenezo kadiri inavyotakiwa.

Pia akamtaka kujibu hoja za Watanzania juu ya ufisadi wa rada, ambao
hata Waingereza wanaupigia kelele, baada ya yeye na wenzake serikalini
kufanya ‘dili’ kujinufaisha wao badala ya kuongoza wananchi.

Nyerere aliongeza tuhuma kwa Mkapa akisema kuwa pia anatakiwa kujibu
hoja juu ya mauaji ya Zanzibar ya mwaka 2001, ambapo kwa mara ya
kwanza Tanzania mbali ya serikali kuua raia wake kwa risasi,
ilizalisha wakimbizi kwenda nchi za Kenya na Somalia.

Akifafanua tuhuma za ufisadi dhidi ya Rais Mkapa, mbunge huyo alisema
kuwa kama Mkapa anataka kueleweka mbele ya Watanzania wenye uchungu na
nchi yao, anatakiwa kujibu hoja za msingi juu ya tuhuma hizo za
ufisadi zinazomwandama tangu akiwa madarakani hadi anastaafu.

Mbunge huyo ambaye alikuwa akihutubia mamia ya wakazi wa maeneo ya
Lenguruki, Poli, Sing’isia na Nkoaranga, alisema kuwa rais huyo
mstaafu anapaswa kuwa mmoja wa watu wa mwisho kusimama mbele za watu
kwani hali inayolikabili taifa kwa sasa, ikiwamo ufisadi uliotapakaa
ndani ya chama chake na serikali ya CCM, iliasisiwa tangu wakati wa
utawala wake, kwa kuanzia na sera za ubinafsishaji zilizoua misingi ya
viwanda iliyowekwa na Mwalimu Nyerere.

Kwa upande wake, mgombea wa CHADEMA Joshua Nassari, alisema kuwa
amegombea kwa nia ya kubeba ‘mizigo’ ya wana wa Arumeru kwani
anaitambua, hivyo yuko tayari kuibeba kwenda nayo bungeni Dodoma na
katika Halmashauri ya Wilaya ya Meru, kuwasemea na kuiwajibisha
serikali ili iwajibike kwa wananchi.

Joshua alionekana kuwagusa wananchi wa maeneo hayo pale alipokuwa
akizungumzia kero za kila eneo husika, kama vile ardhi, maji, afya na
elimu na namna ambavyo wanaweza kushirikiana pamoja na mbunge wao
katika kuyatatua, iwapo watamchagua yeye ambaye amezaliwa na kukulia
katika maeneo hayo na yuko tayari kuwatumikia akiwa anaishi katika
maeneo ambayo wanaishi wao pia.

Aliwataka watu wa Meru wasidanganyike na maneno ya Mkapa kuwa
atakwenda kumshauri Rais Jakaya Kikwete ashughulikie matatizo ya ardhi
katika wilaya hiyo, kwani alishindwa kufanya hivyo wakati akiwa na
mamlaka ya urais, hawezi kuifanya kazi hiyo kwa sasa kwani rais ana
hiari ya kukubali au kukataa ushauri wa mtu yeyote kwa mujibu wa
katiba yetu mbovu.

“Kwa mujibu wa katiba yetu mbovu ambayo tunataka tuiandike upya, rais
halazimiki kuchukua ushauri wa mtu yeyote, hivyo Kikwete anaweza
kukataa ushauri wake huyo Mkapa, aje ajibu hoja hapa kwa nini
alishindwa kutatua matatizo ya ardhi kwa watu wa Arumeru wakati akiwa
madarakani?” alihoji Nyerere.

CHANZO: Tanzania Daima 14 Machi 2012

Wednesday, November 26, 2008

Kipanya Asema....


Translation:

Kipanya (Rat Character): Is it a grave? No, I don't think so maybe it is a ditch.

Wednesday, May 28, 2008

Mkapa Hajajibu Hoja - Prof. Baregu

Prof. Baregu hachoki! Mwaka jana aliuliza maswali kadhaa kuhusu enzi za Mh. Mkapa. Hakupata majibu. Na jana kaongea tena!

*************************************************************

Kutoka ippmedia.com

Mkapa hujajibu hoja - Baregu

2008-05-28

Na Lucy Lyatuu

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Mwesiga Baregu, amemshangaa rais mstaafu Benjamin Mkapa kwa kutoa majibu ya jumla dhidi ya tuhuma nzito zinazomkabili. Alikuwa anazungumza na Nipashe kwa njia ya simu kuhusu utetezi alioutoa Bw. Mkapa huko Masasi mkoani Mtwara kuwa wanaodai kuwa ni `fisadi` wana chuki binafsi kwa vile aliwanyima madaraka akiwa Ikulu.

Profesa Baregu ambaye ni mtaalamu wa sayansi za siasa alisema tuhuma dhidi ya Rais mstaafu zinajulikana na zinaeleweka, hivyo hakutakiwa kutoa majibu ya jumla na ya juu juu. Alimtaka kiongozi huyo kuweka wazi idadi ya watu aliowanyima vyeo au madaraka wakati akiwa madarakani ili kuipa nguvu hoja yake.

``Kwa mfano mimi sijawahi kutafuta kazi kwake sasa atatoaje majibu ya jumla kuwa wanaotoa madai hayo wana chuki binafsi wakati masuala ya Benki M na mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira unafahamika?`` alihoji Profesa Baregu.

Aliongeza kuwa kama Bw. Mkapa anataka kujibu tuhuma dhidi yake azungumze kwani mambo mengi yameandikwa kwenye vyombo vya habari. Alimtaka asiandame watu kwa ujumbe mbaya na kumkumbusha kuwa ni vyema akafahamu kuwa majibu ya jumla hayamsaidii.
" Asitake kumuua tarishi kwa kuleta ujumbe mbaya,`` alisema Profesa Baregu.

Kwa upande wake, Waziri Mkuu wa awamu wa pili, Jaji Joseph Warioba alipohojiwa hakuwa tayari kutoa maoni na kuongeza kuwa yaliyosemwa dhidi ya kiongozi huyo yanatosha. Rais Mkapa alipochukua madaraka mwishoni mwa 1995 alianza kazi kwa kuunda Tume ya Kuchunguza Kero za Rushwa iliyoongozwa na Jaji Warioba.

Mkapa aliyeingia madarakani kwa jina la aliyetakata (Mr Clean) aliahidi kutumia ripoti ya Jaji Warioba kupambana na rushwa na kuondoa ufisadi serikalini, kitu ambacho hakikuwahi kuonekana waziwazi.

Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Wilbroad Slaa, akizungumzia utetezi huo alisema , Bw. Mkapa hajajibu hoja badala yake ameleta propaganda na poroja za kisiasa. Akitoa maoni yake kwa njia ya simu kufuatia majibu ya Rais mstaafu, alisema Bw. Mkapa alitakiwa kujibu taarifa zilizopo kuwa amesajili makampuni wakati akiwa Ikulu na sio kuleta hoja za kwamba kuna waliokuwa wakitaka madaraka.

``Kama itakumbukwa, mwaka jana Septemba 27. mimi na Bw. Tundu Lissu, tulikuwa watu wa kwanza kutaja orodha ya mafisadi 11 akiwemo Bw. Mkapa,`` alisema. Alisema binafsi hajawahi kupiga magoti akimuomba Bw. Mkapa ampe cheo au madaraka na alichonacho ni uchungu na rasilimali za Watanzania.

Alisema Bw. Mkapa akiwa madarakani alisajili makampuni ya ANBEN na Tanpower Resources Ltd ambayo rais huyo mstaafu na Waziri wa zamani wa Madini na Nishati, Bw. Daniel Yona walitajwa kuwa na hisa ndani ya Tanpower Resources.

Aliongeza kuwa hajawahi kufanya kazi serikalini na hategemei kuwepo na pia hana chuki ya kutokuwa na madaraka kama anavyodai Bw. Mkapa, kwa misingi hiyo anadhani kauli aliyoitoa haina ukweli.

Alisema anachotakiwa kufanya mtuhumiwa huyo ni kujibu hoja ya kwamba ni kweli alisajili kampuni hizo kwa anuani ya biashara ya Luthuli Street namba 15 ambayo ni ya Ikulu.

``Tunataka tu kujua alilipa kiasi gani kama gharama ya pango la kutumia Ikulu?`` alihoji. Dk. Slaa aliongeza kuwa jambo lingine ambalo alitakiwa kujibu ni umiliki wa ANBEN, kampuni iliyokopa Sh. milioni 500 NBC na kushinikiza benki hiyo ibinafsishwe.

Aidha alisema jambo lingine ambalo anatakiwa kujitokeza na kulijibu ni nyaraka zilizoko kwa Wakala wa Kusajili na Kutoa Leseni kwa Kampuni (BRELLA) kwamba anamiliki makampuni hayo akiwa kama mjasiriamali.

Alimtaka kujitokeza hadharani na kujibu hoja hizo ili zionyeshe wazi ukweli wa kauli alizozitoa. Jitihada za kuwapata kwa simu Mwenyekiti wa CHADEMA Bw. Freeman Mbowe na Katibu Mwenezi wa CCM Bw. John Chiligati hazikufanikiwa.

SOURCE: Nipashe

Tuesday, November 06, 2007

Maoni - Falsafa za Watawala wetu na ulinzi wa kikatiba


Falsafa za Watawala wetu na ulinzi wa kikatiba

Imeandikwa na msomaji Ipyana Mwakamela



Ni mambo mengi sana yamejiri tangu Serikali ya awamu ya nne iingie madarakani dhidi ya ile ya awamu tatu juu ya uborongaji uliotawala katika uongozi wa kipindi cha miaka kumi cha Rais Benjamini William Mkapa.

Mengi yamesemwa na tuhuma kedekede dhidi ya Mkapa sasa zimeanikwa wazi juani kwa kila mwenye uchu wa kutaka kuzijua na afanye hivyo. Ninafurahi binanfsi kwamba kila ambacho kiongozi aliye madarakani alidhani amefanya kwa siri huwa kinakuwa peupe peee amalizapo muhula. Labda huo ndio ule tunaita ukomavu wa kisiasa na demokrasia ama uhuru wa kutoa mawazo kwa mujibu wa katiba ya nchi.

Imeandikwa magazetini, imeongolewa katika vyombo vyote vya habari na hata katika vikao vya kahawa juu ya ufisadi uliotawala katika kipindi cha serikali ya awamu ya tatu. Kibaya ama kizuri zaidi, itategemea na kila mtu atakavyotafsiri ni kwamba Mzee Ben ameamua kukaa kimya kitu ambacho ama kinafanya uthibitisho wa tuhuma dhidi yake, kuendeleza tafsiri ya ubabe aliyokwishabatizwa nayo, kudharau vilio vya majeraha aliyotuacha nayo ama ni ujivuni wa kinga ambayo viongozi wakuu wastaafu wamewekewa na katiba yetu.

Mzee Ben aliwambia waandishi wa habari waliomtaka kuthibitisha ukweli wa tuhuma dhidi yake kuwa amestaafu siasa aachwe apumzike. Hii naifananisha kabisa na kauli ya Kikwete mwenyewe pale awali aliposema “Muacheni Mzee Mkapa apumzike”

Nashindwa kutafsiri maana halisi ya kauli hiyo ya Kiongozi aliyeshika dola kwa sasa kama ilimtoka kwa bahati mbaya, woga wa kutekleleza majukumu aliyoaminiwa ama ni kuimarisha ulinzi dhidi yake pale atakapokuwa amestaafu.

Ni mkanganyiko mkubwa maana wao pia wote waliona alichokifanya Fredrick Chiluba wa Zambia dhidi ya muasisi wa taifa hilo Kenneth Kaunda na hatimaye Levy Mwanawasa kumbadilishia kibao pale alipokaa nje ya madaraka.

Pengine ingekuwa vyema na busara zaidi kama Viongozi wetu wa Afrika wangejitahidi kuhakikisha macho yao yote mawili yanafanya kazi sawia kwa kuyazungusha kushoto na kulia huku wakiyapima kwa kutazama vitu vilivyo karibu yao na hata vile vya mbali na pale walipo. Hii ingewasaidia kujua yaliyotokea, yaliyopo kuwazunguka wao na hata yale ya baadaye yanayotazamiwa kuwafika. Wangelitekeleza hili hapana shaka hata utekelezaji wa ahadi zao wanazozitoa kwa waajiri wao zingelitimia.

Ninachojifunza kwa viongozi wetu ni kushindwa kabisa kutekeleza usemi wa “Ukila na kipofu msimshike mkono”. Wanatushika mikono yetu huku wakiendelea kusokomeza chakula chote midomoni mwao tena milo yote ya siku….hii ni kasheshe maana kipofu keshagundua kwamba anadhulumiwa na hatimaye atakufa kwa njaa kama akifanya utani.

Kwa mtazamo wangu Rais Mkapa naye alifanya mengi tu ya kukumbukwa tofauti na tunavyoichukulia kwamba ni mmoja kati ya viongozi waliotawala nchi ambao hawakutakiwa kabisa kuingia madarakani.

Baba yetu wa Taifa hili Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alifanya mengi sana ya kujivunia katika nchi hii na ndio maana anakumbukwa mpaka leo hii na tungependa viongozi wetu wengine wote wanaofuata waige mfano wake. Lakini kama binadam Mwalimu Nyerere pia hakuyatimiza yote kikamilifu na hata yeye mwenyewe alikubali pale alipojikwaa. Hapa pia tukumbuke kwamba ni ngumu sana kwa viongozi waliofuata kufanya kikamilifu kabisa kama Mwalimu alivyotaka iwe. Wanawe tu wa kuwazaa hawajatimiza matakwa hayo sembuse wa urithi?

Baada ya Mwalimu kuachia madaraka alichukua Mzee wetu Ali Hasan Mwinyi ambaye aliongoza nchi kwa kipindi cha miaka kumi ambacho Hayati Baba wa Taifa alikuwa hai na akikemea kila alipodhani hapakua sawa. Tunakumbuka maneno kama ikulu kuwa pango la walanguzi, mtu kuongoza nchi na mkewe na mengine yafananayo na hayo ambazo ni kauli alizitoa Mwalimu kwa kutoridhishwa na uongozi wa Mzee Mwinyi maarufu kama Mzee Ruksa.

Si muafaka kumuongelea Mzee Ruksa kwa kuwa hakuwahi kujibu hata tuhuma moja dhidi yake katika zile alizotwishwa hata kama zilimdharirisha kiasi gani. Pengine ndiye aliyemshauri kijana wake Mkapa kwa kumuasa kukaa kimya kama alivyofanya yeye inaweza kuwa dawa mbadala.

Ninachojiuliza ni kwamba kama amemsihi hivyo aligeuza macho yake pande zote na kuangalia ni mwanga kiasi gani unamulika kwa viongozi kama wao sasa akilinganisha na wakati alioachia ngazi yeye?. Nadhani hapa panahitaji tafakari ya kutosha kabla hatujapandisha mori.

Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Jakaya Mrisho Kikwete yu madarakani sasa, ndiye aliyeshika usukani wa nchi. Kizuri zaidi ni kwamba katika serikali zote mbili kabla yake alikuwamo ndani ya Serikali na hivyo si mgeni sana na mambo yaliyotendeka na pengine yanayoendelea kutendeka.

Labda linalonichanganya mimi sana ni hili: Je Rais atakuwa tayari kuruhusu mabadiliko ya katiba ili vile vipengele vinavyowalinda watu kama yeye waondokapo madarakani vinafutwa ili wakimaliza madaraka yao washitakiwe kwa kila walichotenda kinyume na kiapo walichokula, ama kwa lugha nyingine wahukumiwe sawa na matendo yao?.

Naomba Rais atujibu katika hili ili sasa tuanze kumuona jinsi gani alivyojiandaa kuwa safi katika utawala wake na wala si kufanya mambo kama waliyoyafanya wenziwe waliomtangulia na hivyo kuendeleza Utanzania wa kushupalia mambo wakati muhusika hayupo ama kutoa sifa kwa maiti ambaye hana la kufanya tena kwa wakati huo anapokuwa ndani ya jeneza.

Mheshimiwa Kikwete aliahidi kwamba atafuatailia kwa makini mikataba yote iliyosainiwa ya madini ili kuhakikisha kwamba kila kilichokwenda mrama kinarekebishwa kwa manufaa ya nchi na si kama ilivyofanyika hapo awali. Siwezi kuchimba kiundani kabisa kujua ni kwa kiwango gani mikataba hiyo tayari imekwisha pitiwa na hata kuruhusu kusainiwa kwa mikataba mingine kama ya Buzwagi inayopigiwa kelele kwa sasa na kuiingiza Serikali ya Chama cha Mapinduzi matatani dhidi ya kambi ya upinzani.

Kinacholindwa sana hapa katika mkataba wa Buzwagi hata kupelekea Mh. Zito Kabwe akasimamishwa kuhudhuria vikao vya bunge, Mheshimiwa Lowasa kuiwekea ngao kila anapoulizwa na jeuri ya Karamagi kutojiuzulu kwa kashfa kama alivyofanya Mbilinyi na Mpologomyi enzi za Serikali ya awamu ya tatu ni nini?.

Mheshimiwa Rais alituahidi kwamba Waziri atakayevurunda hataweza kumaliza hata temu ya kwanza ya miaka mitano. Ni nani anathibitisha uvundo wa waziri?, ni mpaka Rais mwenyewe aseme ama kilio cha Wananchi walio wengi ndio chachu ya Rais kujua kiwango ambacho Waziri kavurunda?

Yupo Mheshimiwa Kapuya aliyetumia ndege ya Jeshi kwa safari binafsi na watu wakapiga kelele sana mpaka kwenye vyombo vya habari lakini sisi kama waajiri wakuu wa viongozi hao hatujafahamu hasa nini kilifuata baada ya pale na kelele za vyombo vya habari zilichukuliwa vipi na mkuu wa kaya hii.

Palikuwa na suala la Richmond ambalo lilifukuta na kufuka moshi mzito lakini hatimaye ikaja eksitigwisha ya Dowans ambayo ikauzima moto huo huku na yenyewe ikiwa bado na madhara na inaendelea kutafuna kama kutu inavyokula chuma.

Profesa Maghembe na Wizara yake ya Maliasili, macho yake hayakuzungushwa pande zote na sasa amefanikiwa kupandisha mbao kwa asilimia 700. Hakutazama mlaji mdogo anawezaje kununua ubao mmoja kwa shilingi 9000 kutoka bei ya awali ya shilingi 2000.

Bajeti ya Serikali ya 2007/2008 imepitishwa kwa mabavu pasipo kuzingatia maisha halisi ya Mtanzania na mfumuko wa bei ya vitu wakati tungali na mahubiri ya Maisha bora kwa kila mtanzania. Hakuna asiyejua gharama ya maisha imepanda kwa kiasi gani mpaka hivi sasa na huku mshahara wa kima cha chini wa serikali ukiwa chini ya shilingi laki moja kwa mwezi.

Pamekuja suala la malipo ya wafanyakazi wa majumbani maarufu kama House Girls na House Boys kwamba wanatakiwa kulipwa kima cha chini kabisa shilingi 65000 kutoka katika mfuko wa mfanyakazi anayelipwa shilingi 85000 kwa mwezi. Mahubiri yetu yangali “ maisha bora kwa kila mtanzania.

Kuna mradi wa ugawaji wa viwanja wa Serikali unaitwa viwanja vya bei nafuu lakini unaongelea kwenye malaki kama si mamilioni ya shilingi. Saruji imefikia kiasi cha shilingi 16000 kwenda juu kwa hapa jijini Dar es Salaam kwa mfuko mmoja wa kilogram 50. Tunavyo viwanda vitatu nchini Twiga Cement kilichopo Wazo jijini Dar es Salaam, Tanga Cement kinachozalisha Cement ya Simba na Mbeya Cement kinachozalisha Cement ya Tembo. Nani atajenga hapa ni kila Mtanzania ama tabaka fulani tu la watu?.

Nimeona katika vyombo vya habari matangazo ya Tanga Cement juu ya bei halali ya kununulia Cement yao kwa mikoa yote nchini. Najiuliza utekelezaji wake utakuwa vipi na ni nani atatutetea kuhakikisha bidhaa zinapatikana kwa bei inayotambulika. Sitamani hata kidogo kurudi katika enzi za “Duka la kaya”, nani atakuwa Sokoine wetu wa leo kupambana na uhujumu uchumi unaokuja kwa kasi ya ajabu.

Kikubwa katika haya yote ni kwanini tunawaangalia panya, mende, mchwa, dumizi, nzige na wadudu wengine wanaoingia kwenye boksi la mheshimiwa Kikwete huku wakifanya uharibifu kwa uhuru na viburi tena katika boksi jipya tulilolinunua jana kwa bei ghali zaidi na badala yake tunalishughulikia boksi la Mkapa ambalo tayari limekwisha chanika na hatuna jinsi ya kuliokoa leo.

Ufisadi unaotangazwa leo katika nchi yetu hautaisha kama hatutaacha unafiki wetu kwa wanaokalia madaraka leo ili tuwasubiri kesho watakapokuwa wametoka. Nani atakuwa Raisi wetu jasiri atakayetekeleza kwa dhati kila anayoahidi kuyafanya?.

Wapi Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea na kwa nini imebakia nadharia tu na hakuna ukweli halisi wa kwa nini vitendo vyake vimebaki kuwa ndoto. Cha ajabu na kinachotia kichefuchefu ni kwamba kila panapotajwa jina la muasisi wake Wasomi, Wanadiplomasia, Viongozi mashuhuri hawaishi kutaja Azimio la Arusha na mengine mengi yaliyoasisiwa na Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Kuna sababu gani ya msingi inayofanya kila mtawala aje na falsafa yake ikiwa falsafa zilizotumiwa na watawala waliotangulia hazina matatizo yoyote. Hapana shaka hapa nitapata waliobobea katika tafakari wanisaidie kupata uchambuzi wa hili tena ulio yakinifu.

Najuliza sana ni wapi “Fagio la chuma” lilikopotelea baada ya Mzee Ali Hassan Mwinyi kuondoka madarakani. Ni kwa nini falsafa yake haikutekelezeka kivitendo hata kwake yeye mwenyewe ikaendelea kubaki kinadharia peke yake na hatimaye kuzikwa kabisa baada ya Serikali ya awamu ya tatu kuingia madarakani. Kama ilikuwa ni falsafa nzuri yenye matunda kwanini haikurithiwa ama hata kuzungumziwa katika Serikali zilizofuata.

Kama pangekuwa na “Ukweli na Uwazi” aliotuletea Mzee Benjamin William Mkapa na ukatekelezeka kama ulivyokusudiwa na kupokelewa na umma wa watanzania walio wengi sidhani Mkapa angekuwa na jina baya machoni na masikioni mwa Wananchi aliowaoongoza kwa miaka kumi. Lakini hali kadhalika mazingira ya nadharia katika falsafa za watawala wetu yameendelea kutukuka na hii pia ilimshinda aliyeiasisi. Leo hii amekalia kaa la moto.

Kibaya zaidi ni kwamba kila inapokuwa mchana na usiku jina la tarehe, siku, mwezi na mwaka hubadilika. Sasa leo kuna mashindano ya viongozi bora wa Afrika wanaopata tuzo za heshima na kuvuna donge kubwa la fedha. Mfanyabiashara Mo Ibrahim amejitolea kutoa tuzo hiyo katika kuonyesha ama kutafuta njia mbadala ya kuwafunda watawala wa Afrika jinsi ya kuwatawala Waafrika wenzao.

Mzee Ben akadondoka kama kiongozi wa Tanzania na huku Joaqim Chissano akivuna alichopanda katika utawala wake. Hata hivyo mimi sikushutumu sana kwa hili kwani angalau ulimkaribia Chissano ukilinganisha na wenzio kumi na mmoja. Kumbuka unashutumiwa tu kwa kuwa tulihitaji kuwa na furaha waliyonayo Msumbiji leo hii…..pole sana mzee Ben labda Kikwete atajifunza kutoka kwako ili aje atutoe kimasomaso siku za mbele katika “ishu” kama hiyo.

Imeshika hatamu kubwa sasa “Kasi mpya, Nguvu mpya na Ari mpya” kwa kuwa ndiyo iliyo madarakani sasa. Ewe Mweny-enzi Mungu tunusuru na hili lisije bakia nadharia kama yaliyopita. Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete tunaona utekelezaji hafifu wa falsafa yako hasa ukizingatia kuwa bado upo katika hatua za awali za uongozi wa nchi ambayo ina kiu kubwa kabisa ya kuona mabadiliko ya kimaisha ili kauli mbiu yako “Maisha bora kwa kila Mtanzania” iweze kufikia lengo.

Hii habari ya badilisha huku kwenda kule kwa watendaji wako inakuharibia kabisa na inazidi kutia giza katika juhudi za kutekeleza kwa vitendo falsafa yako. Hii kwa kukuibia siri tu ndio chanzo cha kuanguka kwa falsafa za wenzi wako waliotangulia. Ikiwa huwa mnafanya hayo kwa makusudi yenu binafsi basi lipa fadhila ama ua nyani kwa kumtazama usoni kisha uone haya.

Boksi la uliyempokea kijiti li tafrani kabisa, limeliwa na wale wadudu aliowafuga kwa muda mrefu na kuwaacha wazaliane huko. Tayari boksi lako limeingia wadudu wale wale kwa kuwa hukulichoma moto boksi la Mkapa bali umeliweka karibu na hilo la kwako jipya na wameanza mapema kulitoboa lakini halahala maana sasa hivi madawa ya kuwaangamiza wadudu hao ni mengi tu ni wewe kwenda sokoni na kununua. Ukiwa mvivu dawa yake itakuwa ni kuchoma nyumba nzima ili hata wale walijificha katika kenchi na kona zisizo fikika waweze kuteketea.

Hatuhitaji mbwembwe na ujuvi wa kuibua falsafa zaidi kinachohitajika na Watanzania wote ni “Utekelezaji kwa vitendo wa falsafa zenu”. Nakumbushia tu, tumeyafumbua macho yetu kwa ung`avu kabisa na hatutalala tena.

Ipyana Mwakamela
P.O. Box 17132
Dar es Salaam
Barua pepe: nakumbushia_tu@yahoo.com

Friday, October 26, 2007

Heshima za Mwisho - Mheshimiwa Salome Mbatia



Rais Mstaafu Benjamin Mkapa na Mke wake wakitoa heshima za mwisho.
Baadhi ya waombolezaji.

Picha zote kwa hisani ya Michuzi Blog

Leo watu walitoa heshima za mwisho nyumbani kwa marehemu Mheshimiwa Salome Mbatia, huko Oyster Bay. Marehemu atazikwa kesho kwao Kirua, Moshi.