
MAMBAS (Msumbiji) 1- TAIFA STARS - 0Hiyo mechi ilikuwa kali na mlijitahidi sana. Mjipongeze kuwa mliweza kufika mbali safari hii!
WaTanzania na wapenzi wa Kandanda tusikate tamaa. Ni kweli moyo unauma, lakini Taifa Stars wameonyesha kuwa na sisi tumo katika ngazi na kimataifa kwa mchezo wa kandanda.
******************************************************************************
From ippmedia.comLawama sasa zamwandama Maximo
2007-09-10
By Mwandishi Wetu,
Baada ya timu ya taifa, JK Boys, kuchapwa bao 1-0 na timu ya taifa ya Msumbiji `Mambas` (nyoka wakali), baadhi ya wapenzi wa soka wameanza kumuangushia lawama nzito kocha mkuu, Marcio Maximo.
Hata hivyo, kabla ya lawama hizo kuanza kutolewa, Maximo tayari aliwataka Watanzania kuyapokea matokeo yoyote ya mechi hiyo pasipo kumlaumu yeyote. Wakizungumza mara baada ya mechi hiyo iliyochezwa juzi usiku, wapenzi hao akiwemo Shaaban Alexander `Chama`, amesema kitendo cha Maximo kuwakumbatia wachezaji anaowapenda na kuwapanga uwanjani bila msaada, ndicho kimechangia timu kufungwa.
``Kuna wachezaji ambao Maximo huwezi kumweleza kitu, atawapanga tu ingawa hawana msaada wowote...angalia Joseph Kaniki aliyeingizwa dakika chache alivyochangamsha,`` amedai Chama.
Aidha, amesema haungi mkono kitendo cha kocha Maximo kumuacha mshambuliaji Kudra Omari ambaye amekuwa kinara wa ufungaji mabao katika michuano ya ligi ndogo na ile ya Tusker. ``Sijui ni kigezo gani anachotumia huyu kocha kuchagua washambuliaji, inawezekana anashikwa masikio na watu, afanye kazi aliyoijia nchini bila kuelekezwa,`` amesema.
Naye shabiki mwingine, John Edward `Edu`, amelalamikia kitendo cha kocha huyo kushinikiza timu hiyo kwenda `kutalii` Ulaya wakati kulikuwa na timu nyingi za kiafrika zakuweza kupimana ubavu na JK Boys.
``Hakuwa na sababu ya kupeleka timu Ulaya, au timu za Afrika anaziogopa iwapo zingetufunga...hizo timu walizocheza na Stars Ulaya si lolote hazifahamiki kabisa,`` amehoji shabiki huyo. Tanzania imekosa nafasi ya kuingizwa katika `kapu` baada ya kipigo hicho, huku Senegal wakipanda ndege mwakani kuelekea moja kwa moja Ghana baada ya kushika nafasi ya kwanza kwa kuibugiza Burkina faso mabao 5-1.