Showing posts with label Chacha Wangwe. Show all posts
Showing posts with label Chacha Wangwe. Show all posts

Friday, September 26, 2008

Mchungaji Christopher Mtikila alazwa baada ya kupigwa Mawe Tarime


Nimesikitika sana kusikia kuwa Mchungungaji Christopher Mtikila, kapigwa huko Tarime leo. Sisi waTanzania si tulikuwa tunajivunia ni watu wa amani? Sioni sababu ya mtu yeyote hata awe mwanasiasa kutoka chama gani kupigwa.
*******************************************************************

Kutoka Lukwangule Blog (Beda Msimbe):


Mtikila apigwa mawe Tarime

MCHUNGAJI Christopher Mtikila amelazwa katika Zahanati ya Tarime mjini hapa baada ya kupigwa jiwe la kichwani wakati akihutubia kumnadi mgombea wake.

Kwa mujibu wa maelezo ya daktari anayemtibu Mchungaji Mtikila, Philemon Hungiro, kiongozi huyo ameumizwa vibaya na jiwe hilo kisogoni kiasi cha kushonwa nyuzi tatu.

Mtikila alisema alipigwa jiwe hilo na mtu asiyemfahamu wakati akimnadi mgombea ubunge kupitia chama chake cha DP, Denson Makanya, kwenye Uwanja wa Shule ya Sabasaba mjini Tarime.

Jiwe hilo alipigwa majira ya saa 11 jioni leo wakati akitoa ufafanuzi wa taarifa zake kuhusu kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Tarime, Chacha Wangwe.

Wakati akiishambulia Chadema kuhusika na kupanga mauaji hayo, ndipo mtu huyo alipochoropoka kutoka nyuma na kumpiga jiwe la kisogoni.

Hata hivyo, Mchungaji Mtikila alidai kipigo alichokipata ni matokeo ya ahadi ya Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbrod Slaa, kwamba damu itamwagika na kwamba kiongozi huyo akifika Tarime atapigwa mawe.

Awali akihutubia mamia ya wananchi waliofurika katika uwanja huo wa mkutano, Mchungaji aliwataka wananchi kumchagua mbunge anayemnadi kwani yeye hana ufisadi wala mipango ya mauaji.


*****************************************************

Kutoka ippmedia.com

Tarime ni soo!

2008-09-26 16:35:51
Na Mwandishi Wetu, Tarime

Wakati siku za kuelekea uchaguzi mdogo wa kumsaka mbunge wa Jimbo la Tarime zikizidi kukaribia, hali ya kisiasa mjini hapa imeanza kuwa tete baada ya wafuasi wa vyama vinavyoshiriki uchaguzi huo kuendelea kufanyiana visa mfululizo, vikiwemo vile vya kumwagiana pilipili na kuwatwangana mawe mikutanoni.

Uchaguzi huo mdogo, unatarajiwa kufanyika Oktoba 12, ili kujaza nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Marehemu Chacha Wangwe, aliyefariki mjini Dodoma Julai 28 mwaka huu baada ya kupata ajali ya gari.

Jana, muendelezo wa visa vya baadhi ya wafuasi wa vyama hivyo vya CCM, CHADEMA, NCCR-Mageuzi na DP ulifikia pabaya baada ya Mwenyekiti wa UDP, mchungaji Christopher Mtikila kupigwa jiwe la kichwa wakati akiwa kwenye mkutano wa kampeni kwenye viwanja vya Sabasaba.

Mtikila alijeruhiwa vibaya na kukukimbiziwa hospitali mjini hapa ambako inadaiwa alishonwa nyuzi saba.

Kutokana na vibweka vinavyoendelea katika kampeni za kuelekea siku ya uchaguzi huo, , viongozi mbalimbali wa vyama vilivyosimamisha wagombea wamekuwa wakitoa kauli tofauti kuhusiana na yanayojiri.

Dk. Sengondo Mvungi (NCCR-Mageuzi)
Yeye aliripotiwa kuwa kiongozi wa kwanza kufanyiwa vurugu wakati wa kampeni jimboni humo.

Mvungi alikumbana na kadhia ya kutimuliwa kwa mawe wakati akimnadi mgombea wa chama chake cha NCCR.

Baada ya hapo, Dk. Mvungi ambaye pia ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alilaani tukio hilo na kueleza kuwa ni la hatari, kwani hakuna chama chenye hakimiliki ya jimbo hilo.

Pius Msekwa (CCM)
Makamu huyu Mwenyekiti wa CCM, naye alionja ya joto ya jiwe ya kufanyiwa vituko vya kampeni hizo wakati alipokuwa akimnadi mgombea wa chama chake, Bw. Ryoba Kangoba.

Msekwa alifanyiwa fujo na kuzomewa na watu wanaodaiwa kuwa ni wafuasi wa vyama pinzani.

Aidha, wafuasi wawili wa chama chake wameripotiwa kuumizwa baada ya mmoja kupigwa jiwe na mwingine kumwagiwa pilipili.

Kutokana na hali hiyo, bosi huyo namba mbili wa CCM akailalamikia hali hiyo na kuripotiwa akitishia kulifikisha suala hilo kwa Rais Jakaya Kikwete ili hatimaye zifanyike taratibu za kudhibiti hali ya namna hiyo ambayo ni ya hatari.

Christopher Mtikila (DP)
Baada ya kasheshe la jana la kupigwa mawe kwenye uwanja wa Sabasaba, amekaririwa akilalamikia hali hiyo aliyodai kuwa imetokana na njama za wapinzani wake.
Akizungumza na waandishi wa habari, Mtikila amekaririwa leo asubuhi akisema: ``Nilitoa taarifa mapema kwa Msimamizi wa Uchaguzi na OCD.. niliwaeleza juu ya agizo la mimi kupigwa mawe...``

Freeman Mbowe (CHADEMA):Mbowe na chama chake cha CHADEMA wamekuwa nao wakilalama kuonewa na askari polisi walio katika operesheni kali ya kulinda amani katika jimbo hili.

Aidha, kwa nyakati tofauti, yeye, Katibu Mkuu wake Dk. Wilbroad Slaa na Mbunge wa Viti Maalum wa chama hicho, Halima Mdee, wamekuwa wakitoa madai ya kuonewa kwa kunyimwa viwanja vya kufanyia kampeni za mgombea ubunge wa chama chao, Bw. Charles Mwera.
Prof. Ibrahim Lipumba (CUF)

Baada ya kutosimamisha mgombea jimboni humo ili kuwapa fursa wenzao wa upinzani jimboni humo, Prof. Lipumba na chama chake wamekuwa katika wakati mgumu wa kuamua wamuunge mkono mgombea yupi baada ya wenzao kuwasaliti kwa kusimamisha mgombea zaidi ya mmoja, kinyume cha makubaliano.

Mkanganyiko huo unadaiwa kutokea baada ya vyama vinavyoungana nacho katika umoja wao wa vyama vikiwemo vya CHADEMA, TLP na NCCR-Mageuzi kushindwa kumsimamaisha mgombea mmoja, hasa baada ya NCCR na CHADEMA kusimamisha wagombea wawili tofauti.

Hata hivyo, ingawa CUF Tarime wameamua kumuunga mkono Bw. Charles Mwera wa CHADEMA, Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, Bw. Wilfred Lwakatare, amekaririwa asubuhi ya leo akisema kuwa wamemtuma jimboni humo kiongozi wao Mustafa Wandwi ili kuangalia ni mgombea yupi anayeelekea kukubalika zaidi ili hatimaye wamuunge mkono.

Wakati huohuo, Jeshi la Polisi jimboni humo limesema liko makini katika kudhibiti vitendo vyote vinavyoashiria kuvunja amani.

Akizungumza na Alasiri juzi, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mara, Liberatus Barlow, amesema FFU na polisi wengine kibao waliomwagwa jimboni humo wamejipanga vilivyo katika kuhakikisha kuwa uvunjifu wa amani unadhibitiwa ipasavyo.

Wakati huohuo, katika kuthibitisha kuwa Polisi wako makini, tayari wameshawanasa watu wanne wanaotuhumiwa kumvurumishia mawe Mchungahji Mtikila jana na kuwawezesha kuburuzwa kortini.

Walionaswa na polisi katika tukio hilo la jana na ambao leo wamepandishwa kizimbani ili kujibu mashtaka.

Kamanda Barlow amewataja watuhumiwa hao kuwa ni Mussa Peter, Mwita Chacha, Hafidh Stanslaus na Mwita Kilongo.

Amesema watuhumumiwa hao, mmoja alikamatwa wakati wa tukio la kupigwa kwa Bw. Mtikila na wengine watatu walikamatwa jana katika msako wa Polisi uliofuatia kujiri kwa tukio hilo la kupigwa kwa Mtikila.

SOURCE: Alasiri

Friday, August 15, 2008

Chacha Wangwe aibuka toka Kuzimu

Wadau, niliona hii huko World Press. Kwa kweli maneno ni mazito si mchezo:

*********************************************************************
Kutoka
http://tarishi.wordpress.com/2008/08/

Chacha Wangwe aibuka toka kuzimu

Filed under: habari ndio hiyo — tarishi @ 12:15 pm

JARIDA LA CHACHA ZAKAYO WANGWE MBUNGE WA TARIME CHADEMA

Utangulizi:

Jarida hili la Mheshimiwa Chacha Zakayo Wangwe lina sehemu tatu. Sehemu ya kwanza litaweka bayana na kufafanua sababu za mimi kuchafuliwa kisiasa na baadhai ya viongozi wa ngazi za juu za Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA, na sehemu ya pili itaonyesha baadhi ya maswali ya msingi niliyopata kuuliza Bungeni na majibu yake na sehemu ya tatu itakuwa na michango mbalimbali niliyopata kuchangia kwa muda wa miezi miaka miwili na nusu.

Lengo hasa la Jarida hili ni kumwelewesha Mtanzania na hususan MWANADEMOKRASIA juu ya tuhuma zilizoelekezwa kwangu kwa lengo la kunichafua kisiasa huku viongozi wa CHADEMA wakidai kukisafisha chama jambo ambalo si kweli na ni kampeni chafu zilizoandaliwa na baadhi ya viongozi wa Chama na kuwarubuni wajumbe 31 wasiokuwa wanademokrasia na kunipaka matope ya siasa zao zisizo na hata chembe ya Demokrasia.

Nasema hivi nikijua wazi kwamba, CHADEMA kama chama kinaendeshwa kwa katiba na kwa wakati huo huo kikiwa kinaendeshwa kidikteta na kauli za NDIYO MZEE. Ninajua wazi kwamba, viongozi wa sasa wa chama changu wanatofautiana sana na viongozi wa mwanzo wakati CHADEMA ikianzishwa kwani wanatofautiana kiitikadi, kisera na hata kimtazamo. Kwa mfano, mzee Mtei alikuwa akikieneza chama hasa vijijini miaka ya 95 kwa kutumia magari chakavu na alifanikiwa kwa kiasi kikubwa kuwashawishi wananchi na wakijua kuwa CHADEMA si chama cha mjini, na hapa ndipo mwanzo wa CHADEMA kuwa Chama Tawala kule Tarime hadi sasa. Ila katika uongozi huu wa kizazi kipya basi kila kitu kinaenda kwa kauli za “Mheshimiwa Mwenyekiti kasema” na matumizi mabaya huku ufisadi ukikitafuna chama kwa matumizi hewa na kwa kigezo kuwa eti wanajilipa madeni ya Kampeni. Nililia sana juu ya matumizi ya helkopta katika kampeni lakini nikaanza kuonekana kuwa mini ni mbaya. Binafsi sikuona sababu za Chama kutumia helkopta ilhali bado wanachama wa vijijini hawakijui chama wala sera zake huku viongozi wa wilaya na mikoa wakishindwa hata kutoa durufu (photocopy) za viepeperushi vya chama kwa kukosa ruzuku. Hii si sawa.

SEHEMU YA KWANZA

Sababu za baadhi ya Viongozi wa CHADEMA kuamua kunichafua kisiasa.

Baadhi ya Kampeni za chini chini dhidi yangu, tarehe 28 na 29 Juni 2008 katika kikao cha Kamati Kuu kilichofanyika Dodoma ambacho kiluhudhuriwa na wajumbe 31 kiliridhia mimi kuondolewa kwenye wadhifa niliokuwa nao ndani ya chama kama Makamu Mwenyekiti kwa sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutuhumiwa kuwa navujisha siri za chama kwa CCM. Binafsi kwangu kama mwanasiasa wa kiwango cha juu ni pigo kubwa sana kisiasa kuchafuliwa na watu 31 tu ndani ya chama. Ninachokiamini hapa ni kwamba, kutokana na msimamo wangu wa siku nyingi hata kabla sijawa makamu mwenyekiti CHADEMA, ndiyo sababu rasmi ya kupigiwa kampeni na baadaye kura za kutokuwa na imani na mimi kwa taarifa nilizo nazo ni kwamba anaandaliwa Dr. Slaa kushika nafasi hiyo. Hapa ikumbukwe kuwa Mke wa Dr. Slaa ni diwani kupitia CCM hivyo kuna uwezekano wa sera za chama zikavuja kupitia Mama huyu katika njia mbalimbali.

Ofisi ya Katibu Mkuu (Ofisi ya Slaa) ndiyo ya kwanza kunituhumu kuwa nawaingilia majukumu yao katika suala zima la matumizi mabovu ya fedha za ruzuku ya chama. Chama hupata zaidi ya milioni 60 kila mwezi. Ni fedha nyingi sana kukijenga chama kama zikipata mipango mizuri na kuachana na matumizi mabovu kama matumizi ya helkopta kwenye kampeni kama ilivyotokea kwenye chaguzi zetu pamoja na baadhiya viongozi kudai kuwa wanajilipa madeni waliokikopesha chama wakati wa kampeni za 2005.

Mhe. Philemon Ndesamburo Mbunge wa Moshi Mjini inadaiwa kuwa anakidai chama milioni 100 alizokopesha wakati wa kampeni za 2005.

Mhe. Philemon Ndesamburo Mbunge wa Moshi Mjini inadaiwa kuwa anakidai chama milioni 100 alizokopesha wakati wa kampeni za 2005, Freeman Mboe ambaye hadi sasa ni Mwenyekiti wa chama changu katika ngazi ya Taifa naye kwa taarifa nilizo nazo ni kwamba kila mwezi hulipwa shilingi milioni 10 ili kufidia fedha anazodai kukikopesha chama ambazo ni zaidi ya milioni 500 katika kampeni hizo hizo na hadi sasa anaendelea kukidai chama mamilioni ya shilingi.

Mimi nilipoonyesha wasiwasi juu ya madeni haya yasiyoisha, ikaundwa tume ya kampeni za kutokuwa na imani na mimi. Binafsi sijui kama viongozi wanaojiita makini kama kina Dr. Slaa na Kabwe Zitto wangeweza kuusimamia ufisadi mkubwa kama huu ndani ya chama huku wakiwa mstari wa mbele kuwafichua mafisadi Serikalini. Au ni kawaida kuwa Mganga hajigangi? CHADEMA kuna ufisadi wa aina nyingi sana kuanzia uchapaji bendera hadi manunuzi ya vifaa vya chama!

Katika ofisi ya Vijana nako kunanuka ufisadi kwani ni vijana wachache sana ambao hupata nafasi ya kwenda nje ilhali mikoani nako kuna vijana wanaohitaji kujifunza. Ofisi hii ina watu maalumu wa kwenda kwenye Semina na Matamasha mbalimbali. Na watu hao hupangwa na John Mnyika.

Pamoja na hayo, Kurugenzi hii inayoendeshwa na John Mnyika imekuwa ikifanya hesabu za “Mbili mara Mbili toa nne”. Nakumbuka matamasha mbalimbali yaliyowahi kuratibiwa na Kurugenzi hii kwa kutumia fedha za chama yamekuwa hayana maslahi yoyote kwa chama ….labda kwake mwenyewe kwani itakumbukwa kwamba Kurugenzi ilizindua mfuko ulioitwa Tumaini jipya Septemba 16, 2007 katika hafla ya wafanyakazi vijana na akaunti ya Tumaini Jipya 01810301 NBC ilifunguliwa. Jumla ya shilingi milioni 6,176,500 zimekusanywa na shilingi milioni 6,064,300 zimetumika kwa shughuli mbalimbali za vijana ikiwemo gharama za hafla yenyewe. Hafla nyingine kama hiyo ilifanyika Arusha.

Hafla hii ilifanyika tarehe 29 Machi, 2008 The New Polygon Triangel Arusha na kuhudhuriwa na washiriki 67 mgeni rasmi akiwa Mhe. Mzee Edwin Mtei. Jumla ya shilingi milioni 2,300,700 zilikusanywa na shilingi milioni 1,885,000. Zimetumika kwa shughuli mbalimbali za vijana ikiwemo gharama za hafla yenyewe. Sasa najiuliza, kulikua na mantiki gani ya kutumia fedha za chama kiasi cha shilingi 6,064,300 na kukusanya shilingi 6,176,500/=? Ni faida ya shilingi ngapi ilipatikana kama ameamua kukiingiza chama katika kufanya biashara ya matamasha?

Jingine, tangu nimekuwa mbunge Chadema na Baadaye Makamu Mwenyekiti sijawahi kuandaliwa safari za kibunge ama za kukiwakilisha chama ilhali kuna watu wasio na uwezo kiakili, kifikra na hata nafasi za uongozi lakini waliandaliwa safari za nje. Chama kimefikia hatua ya kuwakilishwa kimataifa na watu wasio na vigezo kwa ajili ya utawala mbovu! Siandiki haya kwa kuwa nimeondolewa katika uongozi, hapana! Hizi ni harakati zangu za muda mrefu juu ya utawala bora. Tazama, wafuatao wamewahi kusafiri katika mataifa mbalimbali kwa shughuli mbalimbali kukiwakilisha chama. Mhe. Suzan Lymo (Mb. Viti maalumu) Cape Towan, Afrika Kusini kwa Mkutano wa Interparliamentary Union. Susan pia amesafiri kwenda USA kwa High Level meeting ya HIV/AIDs mwezi June, 2008. Mhe. Zitto Kabwe, (Mb) alisafiri kwenda Berlin mara mbili – Mhe. Zitto pia alisafiri kwenda Marekeani kwa wiki 3 kwa mwaliko wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani pamoja na Wabunge vijana toka dunia nzima ambako walipata nafasi ya kutembelea majimbo mbalimbali ya Marekani. Mhe. Mhonga Said (Mb – Viti maalum) alisafiri kwenda Burundi kwa Mkutano wa Nchi za Maziwa Makuu. Mhe. Dr. Slaa amesafiri kwenda Johannesburg, Windhoek na Manzini Swaziland kwa vikao vya Kamati na Bunge la SADC. Dr. Slaa ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya InterParliamentary Cooperation Committee ya Bunge la SADC. Mhe. Maulida Komu (Mb. Viti Maalumu) alisafiri kwenda Nairobi na pia Finland. Mhe. Ndesamburo (Mb) alisafiri kwenda Australia kama Commissioner wa Bunge.

Wafuatao walisafiri kichama; Mhe. Mhonga Said (Mb – Viti Maalum), Maulida Komu (Mb – Viti Maalum), Suzan Kiwanga (Afisa Msaifizi Idara ya Uchaguzi na Kampeni) na John Mnyika Mkurugenzi wa Idara ya Vijana) walisafiri kwenda Norway na Sweden. Anthony Komu (Mkurugenzi wa Fedha na Utawala) alisafiri kwenda Norway kwa mwaliko wa Centre Party, Mhe. Balozi Ngaiza (Mjumbe wa heshma wa kamati kuu wa kuteuliwa na Mwenyekiti), John Mnyika (Mkurugenzi katika Ofisi ya Vijana), John Mrema (Afisa katika Kurugenzi ya Halmashauri na Bunge), walisafiri kwenda Windhoek Namibia kwa Mkutano wa Dua, na Mhe. Kimesera (Katibu Mtendaji wa kuteuliwa na Mwenyekiti), Suzan Lymo (Mb) Viti maalum, na John Mrema walisafiri kwenda Kampala, Uganda kwa Mkutano wa Dua.

Ndugu Regia Mtema (Afisa katika Kurugenzi ya Vijana) alisafiri kwenda Malawi kwa Mkutano wa NIMD. Mama Naomi Kaihula (Mkurugenzi katika Idara ya Wanawake) na Regia Mtema walisafiri kwenda Finland kwa mwaliko wa Shirika la Demo Finland. Johna Mrema, Msafiri Mtemelwa na Happiness Mwaipopo (Sina hakika kama ni Mwanachama) walisafiri kwenda London/Uingereza kwa mwaliko wa Conservative Party/WFD wakati wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Mhe. Benson Kigaila (Mkurugenzi wa Oganaizesheni na Mafunzo) alienda Zimbabwe katika uchaguzi uliofanyika 27 June, 2008 kupita Ofisi ya Msajili wa Vyama.

Suala la ukabila ni jambo ambalo halihitaji kupingwa kwani asilimia karibu 85 ya viongozi wa CHADEMA wametoka katika mikoa ya Kilimanjaro na Arusha pamoja na kwamba baada ya mimi kulishupalia jambo hili wameanza kubadilisha majina.

Wapo wanachama kama mimi ambao nao wakipewa nafasi za uongozi ndani ya chama hiki watafanya vizuri zaidi ya hawa na wengine ambao ni Jobless! Pengine niweke wazi hapa kuwa, mimi ni kiongozi shupavu nisiye kuwa na hata chembe ya woga katika kuteta na kusimamia haki za mwanachama wa CHADEMA tena nisiyependa siasa za kisanii. Ukweli huu ndio uliowafanya kina Mbowe, Slaa kuwa mstari wa mbele katika kupiga kampeni na baadaye kura ya kutokuwa na Imani na mimi. Binafsi naamini katika chama cha siasa mtu muhimu ni Mwanachama na si Mwenyekiti au Katibu. Hapa mimi siandiki maneneo haya kukufanya udhani kuwa nataka kuwa king’ang’anizi kwenye wadhifa niliovuliwa, la hasha bali napenda upate picha halilisi ya uendeshwaji wa Siasa ya CHADEMA na kisha uweze kugundua uhalisia wa mgogoro ulivyo. Viongozi wa CHADEMA Makao Makuu wamening’oa kutoka katika wadhifa niliokuwa nao kwa sababu zao binafsi na si sababu za chama kama chama, na wanajitahidi kuzunguka mikoani kwa siri kuendelea kunichafua kisiasa kuwa sifai. Kweli sifai kwa wafuja ruzuku ya chama, kweli sifai kwa mafisadi ndani ya chama ila nafaa kukiendesha chama katika ngazi ya taifa katika nafasi yoyote na siku zote. Nafaa kwa sababu nimefukuzwa kwa kusema ukweli hivyo nikageuka mwiba kati kati ya majipu, nikatolewa. Ndiyo, nafaa kwa sababu siko tayari kufanya kazi na watu waliozoea kukaa ofisini kama mafaili! Nafaa kwa sababu mimi ni mpambanaji, kamanda shujaa niliye tayari kuwajibishwa kwa ajili ya kuwatetea WANADEMOKRASIA hususan WANACHADEMA nchi nzima.

Kuliendesha Taifa kama Tanzania hakuhitaji siasa za kisanii, fitina, na chuki. Kinachotakiwa ni nani abadilike alete mabadiliko katika siasa ili aweze kukabidhiwa dola na alete mabadiliko. Wananchi wamechoshwa na siasa zetu ndio maana wanaziita siasa za kisanii. Wanahitaji mabadiliko. CHADEMA maana yake ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo, lakini huku wanakoelekea tayari uongozi wa Mbowe na Slaa wameiondosha Demokrasia kwa kunitoa katika wadhifa wa umakamu Mwenyekiti kwa kupiga kampeni ndogo ya wajumbe 31 tu! Tena huku wakinituhumu kuwa navujisha siri za chama!!. Dhahama kama hii siwezi kuivumilia hata kidogo na ni wazi kuwa hata wanachama wetu hawajafurahishwa na jambo hili. Mimi nilipokuwa kwenye ngazi hiyo ndipo fedha zilipoanza kupelekwa mikoani kwa viwango halali, ndipo ukarabati wa Makao Makuu ulifanyika. Niweke wazi hapa kuwa, jambo lililonifanya niandike jarida hili si kuwashawishi Freeman Mbowe na Slaa kunirudisha kwenye nafasi waliyonitoa kwa matusi, la hasha! Lengo ni kuweka wazi kwa wanachama wajue aina ya uongozi uliopo Makao Makuu ya Chama. Kama ni suala la mimi kurudi katika nafasi hiyo ni mimi mwenyewe nikiamua na kwa kutumia Demokrasia. Ikumbukwe kuwa, Freeman ndiye aliyesema kuwa hataki kufanya kazi na mimi na kutokana na UMANGIMEZA na Kauli za NDIYO MZEE akapata kuungwa mkono na wajumbe 31 tu! Baada tu ya mimi kutangazwa kuwa nimetolewa kwenye wadhifa niliokuwa nao nilipata simu nyingi sana za wanachama na hata baadhi ya watendaji Makao Makuu wakiniambia kuwa kama Mbowe hayuko tayari kufanya kazi na mimi, wao bado wananihitaji katika Uongozi Taifa. Kuna mila ya kichagga kuwa, katika eneo la kazi/biashara, ukimuona anayekusababisha ukose maslahi Fulani unatakiwa kumuondoa kwa gharama yoyote! Na hili ndilo lililojiri kwangu na mwenyekiti wangu.

Aluta Continue…………………..

Wangwe Chacha Zakayo,
Mbunge wa Tarime-CHADEMA


KAULI YANGU KWA MSOMAJI

Awali ya yote, nasikitika sana kwa maamuzi yaliyofikiwa na wajumbe 31 kule Dodoma aidha, kwa hasira, chuki au majungu na kuamua kuniondoa katika wadhifa niliokuwa nao wa Makamu Mwenyekiti Tanzania Bara wakitumia kivuli cha Katiba ya Chama. Pili nimezidi kuumia zaidi pale nilipotuhumiwa kuwa eti navujisha siri za Chama kwa CCM! Niliwapa siku Arobaini (40) kuwaza kuthibitisha juu ya tuhuma hizo lakini wameshindwa hadi leo! Inamaanisha kuwa walitumia tuhuma hizo ili kunitoa kati yao ili nisiendelee kutetea ahadi za wanachama wa CHADEMA na nisiendelee kupinga ubadhirifu wa fedha za chama. Pengine kutokana na hasira, chuki na majungu hayo hayo wakaamua kuzidi kunichafualia jina katika mkutano uliofanyika Tanga kwa kunisema kuwa mimi ni mhuni. Hapa sintakuwa na huruma wala urafiki na yeyote aliye mstari wa mbele kunichafua kisiasa nitahakikisha nawafungulia mashtaka na waweze kuthibitisha tuhuma hizo. Mpendwa msomaji, pamoja na hayo ni vyema ukumbuke kuwa, uongozi wa CHADEMA Taifa umeshindwa kukieneza chama hadi vijijini. Ni kwa ajili ya majungu haya haya!.

Kimsingi, tusiposhikamana kwa sauti moja, lengo moja na kwa msimamo, ni dhahiri kuwa chama cha mapinduzi kitaendelea kushika Dola hadi Ukamilifu wa Dahari! Chama kisipokuwa madhubuti hakitaweza kushika Dola hakiwezi kuaminika na Wananchi. CHADEMA tufike mahali tugeuke, tujue tuna lengo la kuiongoza Tanzania na si vinginevyo. Badala ya kulewa katika kuwafichua mafisadi. Tumejisahau!.

Naamini kuwa, nguvu za umma ndiyo nguvu inayoweza kuleta mabadiliko ya kweli.

Naamini kuwa, katika chama chochote cha siasa, mwanachama ndiye bora kuliko Kiongozi.

Naamini kuwa msingi bora wa chama hujengwa na watu makini.

Naamini pia baada ya kusoma Jarida hili ukiwa kama mwanachama au Mwanademokrasia utaungana nami katika kupiga vita UFISADI ndani ya CHADEMA.

Monday, August 04, 2008

Vigogo Wahaha! - Kifo cha Wangwe

Naona hata mwandishi wa hii stori kahofia maisha yake, wameandika 'mwandishi wetu' . Sasa kilichobaki ni kuita Scotland Yard wachunguze.

*******************************************************

Kutoka ippmedia.com

Kifo cha Wangwe: Vigogo BP juu!

2008-08-04

Na Mwandishi Wetu, Jijini

Mazingira tata ya kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Tarime, Mhe. Chacha Wangwe (CHADEMA), yamewafanya baadhi ya vigogo kuingiwa na hofu kubwa ya maisha yao na sasa wengine wamedai kuwa wana data ambazo hata kuzianika hadharani wanaogopa kwa sababu za kiusalama.

``Uchunguzi umethibitisha wazi kuwa Wangwe hakuuawa kwa risasi... lakini pamoja na ukweli huo, bado baadhi ya vigogo katika siasa, hasa wale wa upinzani, wamekuwa na hofu kutokana na mazingira tata ya ajali yenyewe na kile kilichomtokea (Wangwe) hadi kufa,`` kimesema chanzo chetu kimoja kilicho jirani na vigogo maarufu wa upinzani nchini.

``Hivi sasa kuna data nyingi zilizopatikana na kuibua maswali mengi kuhusiana na kile kilichotokea. Kijana aliyekuwa na Wangwe wakati wa ajali ndiye anayeelekezewa kidole zaidi kutokana na maelezo yake kila alipohojiwa... hili limeongeza hofu zaidi kwa vigogo hao, wakiamini kuwa wao wako hatarini na taifa pia liko hatarini,`` kimeongeza chanzo hicho.

Taarifa hizo za kuwepo kwa hofu miongoni mwa baadhi ya vigogo zimetiwa nguvu na yale yaliyosemwa jana Wenyeviti wa Umoja wa Vyama vinne vya upinzani nchini jana na kunukuliwa na vyombo vya habari leo asubuhi, kuhusiana na shaka iliyopo katika ajali iliyomuua Mheshimiwa Wangwe.

Wakizungumza hiyo jana, wenyeviti wa vyama hivyo vya CUF, CHADEMA, TLP na NCCR, wamesema wanazo taarifa zinazoibua maswali mengi kuhusiana na kifo cha Wangwe, hasa juu ya kijana anayedaiwa kuwa naye ndani ya gari, Bw. Deus Mallya.

Wakasema maelezo ya kijana huyo juu ya tukio hilo, namna Wangwe alivyopata majeraha yaliyomuua na ziada ya taarifa walizopata toka kwa watu wanaomfahamu kijana huyo (Mallya), ni baadhi ya mambo yanayowafanya wawe na hofu kuwa kuna ujasusi umefanyika.

Wakasema viongozi hao ambao ni Prof. Ibrahim Lipumba wa CUF, Augustino Mrema (TLP) na James Mbatia (CHADEMA), kuwa kwa taarifa walizo nazo, wanaamini vilevile kuwa upo mtandao hatari unaotishia usalama wa taifa.

Akizungumzia hofu hiyo, Prof. Lipumba akasema waliyemuona Mallya kabla ya tukio, wanasema alikuwa ni mtaalam wa kompyuta, alikuwa na vitambulisho vingi na vingine vimeandikwa kiarabu na pia, wanahisi kuwa amepata mafunzo ya kijasusi nchini Libya.

``Imekuwaje akawa karibu na marehemu kwa muda mfupi?`` Akahoji Profesa Lipumba wakati wakizungumza na waandishi wa habari. Akautaja utata mmojawapo juu ya kifo cha Wangwe kuwa ni kuonekana kuwa kichwa cha marehemu kimepondeka na hakuna maelezo dhahiri ya suala hilo. ``...mle ndani ya gari hakuna hakukuwa na vyuma wala mabati yaliyopondeka.

Kweli hakufa kwa kupigwa risasi... lakini ile ajali ilitokeaje mpaka lochwa kikapondeka?`` akasema Prof. Lipumba. Aidha, Mbatia naye akasema.

Aidha, Mbatia naye akasema kutokana na utata mwingi juu ya kifo hicho ikiwa ni pamoja na maelezo ya kujikanyaga ya kijana Mallya, wao wameamua kumuona IGP Said Mwema ili wampe taarifa za siri kuhusiana na ukweli wa kifo hicho, kwa maslahi ya taifa.

``Inaonekana kuna mtandao unaohatarisha usalama wa nchi.... kijana huyo (Mallya) ana mafunzo ya Kimafia,`` akasema Mbatia.

SOURCE: Alasiri

Thursday, July 31, 2008

Fujo kwenye Mazishi ya Wangwe - FFU waingilia!

Mdau Jacob Mugini kamletea Kaka Michuzi picha hizi sasa hivi kuonesha hali ilivyokuwa huko tarime kwenye mazishi ya hayti chacha wangwe. Juu ni meza kuu ambapo viongozi wa vyama vya siasa wakiwa wameketi, na chini ni baadhi ya waombolezaji. Duh, naona walikuwa roho juu juu hapo!

Na Mwandishi wa Globu ya Jamii, Tarime

Mazishi ya Mh. Chacha Wangwe, aliyekuwa Mbunge wa Tarime aliyefariki dunia kwa ajali ya gari majuzi huko Dodoma, yameshindwa kufanyika leo kijijini kwake Kamokorere baada ya kufumuka kwa vurugu kubwa ambapo wabunge na viongozi wa serikali na vyama vya siasa walohudhurian ilibidi watoke bomba kusalimisha maisha yao.

Vurugu hiyo ilianza dakika chache baada ya kuwasili kilioni hapo kwa Mwenyekiti wa Taifa wa CHADEMA, Mh. Freeman Mbowe, katika kijiji cha Kemokorere kiasi cha kilomita 20 hivi toka mjini Tarime.

Hali ilipokuwa mbaya, ilibidi Mh. Mbowe na viongozi wote waliohudhuria mazishini waondolewe kilioni chini ya ulinzi mkali wa FFU ukiongozwa na Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Mara Afande Leberatus Barlow ambao walifanya kazi ya ziada kuepusha balaa.
Viongozi wengine waliohudhuria walikuwa ni pamoja na wenyeviti wa vyama vya upinzani Profesa Ibrahim Lipumba (CUF), Augustino Lyatonga Mrema (TLP), John Cheyo (UDP) James Mbatia (NCCR-Mageuzi) na Mbunge wa Karatu Mh. Wilbroad Slaa pamoja na kiongozi wa upinzani bungeni, Mh. Hamad Rashid.

Wote hao walisindikizwa chini ya ulinzi mkali wa FFU kuondoka mahali hapo na kuelekea Musoma. Waziri wa Kilimo na Umwagiliaji, Mh. Steven Wassira, na Manaibu Mawaziri ambao ni wabunge wa Kanda ya Ziwa, Dr. James Wanyacha na Gaudensia Kabaka nao ilibidi waondoke.
Ujumbe toka Kenya ulioongozwa na Dr Wilfred Machage ambaye ni mbunge wa jimbo la Kurya na pia Naibu Waziri katika serikali ya mseto ya Kenya pamoja na wakuu wa wilaya wawili nao walikuwepo na ilibidi waondoke kwa kuruka ukuta.

Tofauti na walivyoingia, itifaki haikuweza kufuata kama walipowasili wabunge 20 wakiongozwa na mbunge wa Bumburi Mh. William Lukindo vurugu hilo lilipoanza na ilibidi kila mmoja aondoke chini ya ulinzi mkali.

Maelfu ya waombolezaji, wengi wao wakiwa vijana waliobeba mabango yenye ujumbe mbalimbali unaohoji kifo cha Mh. Wangwe, walitawala hapo kilioni. Juhudi za Mkuu wa mkoa wa Mara Mh. Issa Machibya kuwatuliza hazikuzaa matunda.

Hata juhudi za kututuliza ghasia hizo za Wah. Zitto Kabwe na mmoja wa wanafamilia waandamizi kama vile Profesa Samwel Wangwe na Mkuu wa zamani wa Halmashauri ya Tarime Mh. Peter Wangwe pia hazikuambulia kitu.

Prof Wangwe aliwaambia waombolezaji hao wenye hasira kwamba familia ya Wangwe imeamua kumtafuta mtaalamu huru kuifanyia upya uchunguzi maiti ya hayati Chacha Wangwe ili kubaini alifariki kwa njia ipi.

Wengi ya waombolezaji wanatuhumu kwamba Mh. Wangwe hakufa kwa ajali ya gari. Mtu moja aliyekuwa na marehemu wakati wa ajali, Bw. Mallya, anahojiwa na polisi na uchunguzi wa kina unaendelea.
****************************************************
VURUGU zilizuka katika maziko ya Mbunge wa Tarime, Chacha Wangwe, pichani,baada ya ndugu wa marehemu kugoma kuzika mwili wake wakidai hawajaridhika na maiti yao ambayo wanadai kuwa ina tundu la risasi.

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, alinusura kujeruhiwa kwa kumrushia mawe na wengine wakitaka kumkata kwa mapanga na aliokolewa kwa juhudi za ziada za polisi. Kabla ya tafrani hiyo kuzuka, ndugu wa marehemu waliigomea Serikali kumzika Mbunge huyo wakisema hadi uchunguzi mpya ufanyike waweze kujiridhisha kuhusu chanzo cha kifo hicho.

Ratiba ya maziko hayo ilikuwa ianze saa 7 mchana, lakini kuanzia saa tatu asubuhi, ukoo wa Wangwe ulikaa chini ya mwenyekiti wake Profesa Samwel Wangwe na kutoa uamuzi wa kutozikwa marehemu hadi daktari wa familia kutoka Dar es Salaam atakapofika na kuufanyia uchunguzi upya.

Mwenyekiti wa Chadema, Mbowe alifika katika msiba huo saa nane mchana akiwa amefuatana na viongozi wengine wa vyama vya siasa ndipo ghafla vijana walipotoa mabango yaliyokuwa yamebeba ujumbe mbalimbali wakipinga kuwa kifo cha Wangwe ni mipango ya Mungu.
“Hatutaki sura ya Mbowe tunataka mbunge wetu,” walisikika wakisema vijana hao ambao walikuwa tayari kutaka kumpiga mwenyekiti huyo wa Chadema, wakidai kuwa chama chake kimehusika katika kifo cha Wangwe,baadaye wengine walitoa mapanga na mikuki, hali iliyowalazimu polisi kumchukua Mbowe na kumwingiza ndani ya nyumba ambako walikuwa wamekaa wabunge wengine 20.

Kuona hivyo vijana wengine walianza kurusha mawe kuwaelekezea viongozi hao. Viongozi hao kuona hivyo walitimua mbio wakihofia maisha yao. Baadhi ya viongozi waliotimua mbio pamoja na Mbowe ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Salehe Ramadhan Feruzi, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbrod Slaa, Zitto Kabwe ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Mwenyekiti wa CCM Mkoani Mara, Makongoro Nyerere na Mjumbe wa NEC wa CCM wa mkoa wa Mara, Christopher Gachuma.

Wednesday, July 30, 2008

Conspiracy Theories - Kifo cha Chacha Wangwe!

Gari aliokuwa anaendesha marehemu Chacha Wangwe katika eneo la ajali (picha za ajali kwa hisani ya Mpoki Bukuku)

Rais Jakaya Kikwete akimwaga marehemu Chacha Wangwe (picha kutoka Lukwangule blog)
**********************************************

Tangu tupate habari ya kifo cha mwana mpinzani, Chacha Wangwe, tumekuwa tukisikia maneno hapa na pale. Mara kajiua, mara kauliwa na Chadema, mara kauliwa na CCM....jamani! Rest in Peace Chacha Wangwe. Politics is a dirty game!

Soma habari zaidi kwa Dr. Faustine:

Spika wa Bunge amlilia Wangwe!

Kutoka ippmedia.com

Spika amlilia Wangwe

2008-07-30

Na Waandishi Wetu Dar es Salaam , Dodoma

Spika wa Bunge, Bw. Samuel Sitta, jana aliangua kilio kwa sauti ya juu wakati akitangaza kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Tarime kupitia CHADEMA, Bw. Chacha Wangwe.

Kilio cha Spika, kilisababisha baadhi ya Mawaziri na Wabunge kuangua vilio huku nyuso za wengine zikiwa zimejaa huzuni. Spika Sitta alilia baada ya kumalizia kutoa matangazo kuhusu kifo hicho. Alisema ajali iliyomuua Mbunge huyo ilitokea juzi saa 2:55 usiku wakati akiendesha gari lake aina ya Toyota Corolla akitokea Dodoma kuelekea Dar es Salaam.

Alisema Bw. Wangwe, alikuwa ameongozana na rafiki yake, Bw. Deus Mallya, ambaye alinusurika na sasa amelazwa katika hospitali ya Mkoa wa Dodoma kwa matibabu. Kwa mujibu wa Spika, ajali hiyo ilitokea katika kijiji cha Pandambili, kilomita 100 kutoka mjini Dodoma.

Alisema gari hilo liliacha njia na kugonga miti kadhaa iliyopo pembeni mwa barabara kabla halijabingirika na kuanguka. Kufuatia kifo hicho, Spika Sitta aliahirisha Bunge jana saa 3:10 asubuhi hadi saa 6:00 mchana ili Kamati ya Uongozi wa Bunge na Tume ya Maadili iweze kuwasiliana na familia na kuweka mipango ya mazishi. Saa 6:00 mchana, Spika alitoa matangazo ya ratiba ya kuaga mwili wa marehemu na mazishi yatakayofanyika kesho huko Tarime mkoani Mara.

Spika aliahirisha Bunge kwa siku nzima ya jana kwa kutumia kanuni ya 149 inayosema kama Mbunge akifariki, Bunge linatakiwa kuahirishwa kwa siku nzima. Rais Jakaya Kikwete alifika mjini Dodoma jana na kuongoza Mawaziri na Wabunge kuaga mwili wa marehemu Wangwe Bungeni kuanzia saa 10:15 jana jioni. Leo asubuhi mwili wa marehemu utasafirishwa kwa ndege maalum kuelekea Tarime ukiwa na familia yake na Wabunge wawili.

Spika Sitta alisema kesho asubuhi (Alhamisi) Wabunge 20 wanaowakilisha Bunge kwenye mazishi hayo wataondoka Dodoma asubuhi kuelekea Tarime kwa ndege maalum ili kuhudhuria mazishi na watarejea Dodoma jioni. Kabla ya kifo hicho, Bw. Wangwe alikuwa awasilishe Bungeni hoja binafsi kuhusu mapigano ya kikabila na wizi wa mifugo lakini alishindwa kufanya hivyo kutokana ratiba kutoruhusu kufanya hivyo.

Nipashe ilipotembelea nyumbani kwa marehemu eneo la Kisasa nje kidogo ya mji wa Dodoma saa 4:00 asubuhi ilikuta Mawaziri, Wabunge na majirani wakiwa wanaomboleza.

Mmoja wa watoto wa marehemu, Zakayo Chacha (18), alisema tangu juzi baba yake alikuwa akisumbuliwa na malaria. Alisema baba yake alilazimika kusafiri kwenda Dar es Salaam ili kuhudhuria mazishi ya mwanasiasa wa zamani, marehemu Bhoke Mnanka aliyefariki dunia mwishoni wa wiki iliyopita.

``Ingawa alisafiri, lakini alikwenda hospitali kupima na kukutwa na malaria, siku moja kabla ya safari hiyo, alimeza dawa mseto za malaria hali iliyosababisha aamke kwa taabu na uchovu kabla ya safari hiyo,`` alisema.

Alisema awali walipoanza safari, gari hilo liliharibika nje kidogo ya mji wa Dodoma na kulazimika kurudi mjini kwa matengenezo. Alisema hali hiyo ilisababisha wachelewe kuanza safari na ilipofika saa 3:00 juzi usiku, ndipo wakapokea taarifa za kifo hicho.

Kwa mujibu wa Bw. Zakayo, marehemu ameacha wake wawili na watoto 10. Wakati huo huo, Rais Jakaya Kikwete, jana aliwaoongoza Mawaziri, Wabunge na viongozi mbalimbali wa serikali kuuaga mwili wa marehemu Chacha Wangwe.

Mwili huo uliwasili katika eneo la Bunge saa 11.00 jioni na kupokewa na Wabunge huku Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA), Bw. Zitto Kabwe akiwa amebeba msalaba. Akitoa salamu za marehemu, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Bw. Hamad Rashid Mohamed alisema tukio hilo ni pigo kubwa mno.

Alisema kambi ya upinzani ina wabunge 45 ambapo wawili kati yao, wamewatoka akiwemo aliyetolewa na Mahakama na mwingine ni marehemu Wangwe. Aliongeza kuwa, enzi za uhai wake wakati akianza Bungeni, Wangwe alikuwa Waziri Kivuli wa Maji na kwamba hadi mwisho wa uhai wake, alikuwa Waziri Kivuli wa Mazingira.

Bw. Hamad alimsifia marehemu kuwa mtetezi mkubwa wa masuala ya wananchi na wapiga kura wake wa Tarime. Hata hivyo, alisema hoja ya Wangwe itashughulikiwa na kambi ya upinzani. Waziri Mkuu, Bw.Mizengo Pinda , akiwasilisha salamu za rambirambi kwa niaba ya serikali alisema hadi sasa Bunge limepoteza wabunge watano tangu kuanza kwa awamu ya nne na kwamba ni dhahiri si jambo ambalo wanalichukulia kwa wepesi.

Alitoa pole kwa ndugu zake akiwemo kaka yake Profesa Samwel Wangwe, familia, Spika na Kamati ya Uongozi ya Bunge . Spika wa Bunge Bw. Samuel Sitta, akiwasilisha salamu za Bunge alimsifu marehemu Wangwe kuwa alikuwa jasiri, aliyetetea hoja zake kwa nguvu kwa kila alichokiamini bila kujali.

Alisema alijiamini na alikuwa hodari wa kusema kwa ujasiri mkubwa kila alichokiamini bila kujali kuwa lile analosema lingeweza kumfanya atofautiane na wenzake. Alisema Bunge limepoteza mtu ambaye anahitajika sana bungeni, jimboni na serikalini na taifa zima.

Kaka yake marehemu, Profesa Samuel Wangwe alitoa salamu za shukurani kwa niaba ya familia na kulishukuru Bunge kwa kugharamia msiba wa ndugu yao. Naye Bw. Deus Malya, ambaye alinusurika, alisema kabla ya ajali hiyo, Wangwe ambaye alikuwa akiendesha gari hilo, alimtaka ahame kiti cha mbele na kukaa cha nyuma.

Akizungumza na PST katika wodi ya wagonjwa daraja la kwanza alikolazwa, Bw. Malya, alisema Wangwe alimwambia asikae kiti cha mbele kwa vile sio salama kwake na kumtaka akae kiti cha nyuma.

Alisema baada ya kuambiwa hivyo, alihamia kiti cha nyuma na baada ya kama kilomita 20, ndipo ajali hiyo ilipotokea na Wangwe kupoteza maisha. Akisimulia mwanzo wa safari hiyo, Bw. Malya, alisema saa 2:00 asubuhi, alimsindikiza Wangwe bungeni lakini alimweleza kwamba, alikuwa akijisikia kuumwa.

Alisema, hata hivyo hakufahamu kama alikunywa dawa yoyote, isipokuwa ilipofika mchana, alirudi naye nyumbani na kupata chakula cha mchana, kisha akapumzika kidogo. Bw. Malya, alisema ilipofika saa 9:00 alasiri, walianza safari ya kuelekea Dar es Salaam, lakini walipofika kama kilomita 20 hivi nati za tairi la kushoto upande wa dereva, zililegea na wakaamua kusimama na kuzikaza.

Alisema baada ya kurudi gereji, walitengeneza gari na ilipofika saa 12:30 jioni, Wangwe alipitia nyumbani kuchukua `chaji` ya simu. Akizungumzia jinsi ajali hiyo ilivyotokea, Bw. Malya alisema, alisikia kishindo kikubwa na baadaye kutimka vumbi nyingi iliyomfanya ashindwe kuona mbele.


Alisema kilichofuatia ni gari hilo kuserereka umbali wa kama mita 50 kutoka barabarani na kisha kubiringika mara kadhaa. ``Baada ya hapo, sikuweza kutambua chochote na niliposhituka nikamkuta Wangwe akiwa amelala pembeni yangu huku kiti chake alichokuwa amekalia kikiwa kimenibana,`` alisema. Bw. Malya, ambaye ameteguka mguu wa kushoto na kuumia kidogo katika paji la uso karibu na jicho la kulia, alisema kila kitu walichokuwa nacho katika gari, yakiwemo mabegi ya nguo, Laptop na vitu vingine, viliibiwa.


Bw. Malya, alisema alifahamiana na marehemu tangu mwaka 2003 walipokutana jijini Dar es Salaam ambapo kuanzia hapo walianza kushirikiana katika mambo mbalimbali. Alisema kwa jinsi gari lilivyopondeka hasa sehemu za mbele alikokuwa amekaa, kama asingehama, bila shaka asingeweza kupona katika ajali hiyo.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk. Godfrey Mtei, alisema hali ya majeruhi huyo inaendelea vizuri na baada ya siku mbili ataruhusiwa. Baadhi ya wabunge ambao walizungumza na marehemu Wangwe juzi kabla ya kufikwa na umauti, walisema alionekana mnyonge wakati wote.

Mbunge wa Muhambwe (CCM), Bw. Felix Kijiko, alisema alimkuta Wangwe katika mgahawa wa Bunge akiwa hana furaha kama siku zote. ``Nilimuuliza mheshimiwa mbona sijakuona siku kadhaa bungeni, akanieleza kuwa, alikuwa na mambo kadhaa yaliyokuwa yakimtatiza, lakini wakati huo, hakuwa anakula chochote,`` alisema.

Alisema baada ya hapo, alimweleza kuwa atamwambia kinachomsumbua muda si mrefu. Kwa upande wake, Mbunge wa Mchinga (CCM) Bw. Mudhihir Mudhihir ambaye alizungumza naye kwa mara ya mwisho kabla ya kuanza safari katika viwanja vya Bunge, alisema alipokutana na Chacha hakuwa na hali ya kawaida ya uchangamfu aliyoizoea siku zote na alipojaribu kumdadisi zaidi, hakuweza kubainisha ni kwa nini yuko katika hali hiyo.


Kwa upande wake mbunge wa Bariadi Mashariki (UDP), Bw. John Cheyo, alisema kambi ya upinzani imempoteza mtu muhimu mno na pengo lake kamwe halitazibika. ``Alikuwa ni mtu mpambanaji, hakuogopa kitu kusema kweli, aliwatetea wananchi wake bila woga...kwa kweli kifo chache sio pigo kwa kambi ya upinzani pekee, bali ni pigo kubwa kwa wananchi wa Tarime,`` alisema.

Mbunge wa Same Mashariki (CCM), alisema Wangwe alikuwa mpiganaji mkubwa wa haki za wananchi wake, pia alikuwa anashirikiana na kila Mbunge bila kujali itikadi za chama.

Naye Waziri Mkuu, Bw. Mizengo Pinda, ambaye alionekana wazi kujawa na simanzi, hakuweza kuzungumza na waandishi wa habari waliokuwa wamemzonga wakitaka kusikia neno kutoka kwake, alizungumza neno moja tu kuwa, ``Chacha alikuwa rafiki yangu.`` Na katika hatua nyingine Rais Kikwete ametuma salamu za rambirambi kwa Spika wa Bunge, kufuatia kifo cha Mbunge wa Tarime (CHADEMA), Bw. Chacha Wangwe, aliyefariki juzi kwa ajali ya gari.

Katika salamu hizo, Rais Kikwete, alisema amepokea habari hizo kwa masikitiko na majonzi makubwa. Aidha, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kimepokea kwa masikitiko makubwa kifo Bw. Wangwe. Taarifa iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam, na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa kituo hicho, Bw. Francis Kiwanga, ilisema inatambua mchango mkubwa uliotolewa na marehemu Wangwe katika kuimarisha demokrasia nchini.

Alisema marehemu Wangwe alikuwa mpigania haki sio tu za wananchi wa jimbo lake bali hata kwa Taifa lote. Alisema marehemu Wangwe alikuwa mstari wa mbele kutetea maslahi ya wananchi bungeni na kuchangia hoja nzito akishirikiana na wabunge wengine na kukifanya chombo hicho cha wananchi kuwa mhimili imara.

Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa CCM, Bw. Yusuf Makamba, amesema chama kimepokea kwa masikitiko makubwa kifo cha mwasisi wa TANU na CCM, Bw. Bhoke Munanka. Taarifa ya Idara ya Itikadi na Uenezi ya CCM, ilisema marehemu Munanka aliyefariki Julai 25 aliwahi kuwa mweka hazina wa TANU pamoja na kushika nyadhifa mbalimbali kama uwaziri katika serikali ya awamu ya kwanza chini ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

SOURCE: Nipashe

Tuesday, July 29, 2008

Tanzia - Chacha Wangwe (Mbunge Chadema)


Mbunge wa Tarime kupitia chama cha CHADEMA Mh. Chacha Wangwe(Pichani) amefariki dunia usiku huu kwa ajali ya gari ilitotokea sehemu ya Kongwa Mkoani Dodoma. Alikuwa analekea Dar es Salaam kwenye msiba wa Mzee Bhoke Munanka.

Mungu ailaze Roho ya Marehemu Mahala Pema Mbinguni. Amen.
***********************************************************
Kutoka Habari Leo (Daily News)

Wasifu wa Wangwe

MAREHEMU Chacha Zakayo Wangwe alizaliwa Julai 15,1956. Nyumbani kwao ni Kijiji cha Kyamakorere,umbali wa kilomita 20 kutoka Tarime Mjini.

Alipata elimu ya msingi katika shule za Rosana na Magoto kati ya mwaka 1962 na 1968 kabla ya kujiunga na elimu ya sekondari katika Shule ya Nyaroha.Baadaye alihamia Dar es Salaam na kujiunga na Sekondari ya Kinondoni Muslim ambako alimaliza kidato cha nne mwaka 1974. Alisoma kidato cha tano na sita katika Sekondari ya Mkwawa kati ya 1975 na 1976.

Alijiunga na masomo ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1978, lakini hakumaliza. Aliwahi kufanya kazi na Benki ya NBC,Shirika la Kujitolea la Ujerumani,Kampuni ya Lacop na Mgodi wa Dhahabu wa Afrika Mashariki.

Kisiasa amewahi kushika nyadhifa mbalimbali ukiwamo uenyekiti wa tawi la vijana wa Tanu katika sekondari ya Mkwawa,Mwenyekiti wa Wilaya wa Chadema,Tarime,kati ya 1994 na 1998 kabla ya kujiunga na NCCR-Mageuzi ambako alikuwa Mwenyekiti wa Mkoa kati ya 1998 hadi 2000,lakini akarejea tena Chadema mwaka 2002 na kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Mkoa wa Mara wa chama hicho.

****************************************************************************

SALAMU ZA RAMBIRAMBI kutoka kwa Rais Kikwete


Mheshimiwa Spika,Nimepokea taarifa ya kifo cha Mbunge wa Tarime, kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo, (CHADEMA) Mheshimiwa Chacha Zakayo Wangwe kwa masikitiko makubwa.

Kupitia kwako, napenda unifikishie rambirambi zangu za dhati kwa wabunge wa Bunge lako Tukufu kwa kumpoteza mbunge mwenzao katika kipindi hiki ambacho wako katika kutekeleza majukumu yao waliyotumwa na Watanzania, ya uwakilishi.

Kwa masikitiko makubwa napenda kutoa salamu zangu za pole kwa wana familia, ndugu, wananchi wa Jimbo la Tarime, wanachama wa Chama cha Maendeleo na Demokrasia (CHADEMA) na Watanzania wote.

Kifo huleta masikitiko na majonzi mengi katika familia na jamii, naungana nanyi ndugu zanguni katika kipindi hiki kigumu cha majonzi na maombolezo, Mwenyezi Mungu awape imani na subira katika kipindi hiki kigumu na huku tukimuombea ndugu yetu, Chacha Wangwe mapumziko mema peponi. Amina.