Friday, May 19, 2006

Wanaoigiza wabaguzi kwenye sinema si wabaguzi kweli!

Watumwa Marekani 1864


Sijui kama umewahi kuona sinema za Roots na Amistad. Hizo sinema zinahusiana na utumwa Marekani. Zilivyotengenezwa nasikia wazungu waigizaji walikuwa wanaowaombea radhi wachezaji wenzao weusi kwa vile ilibidi watukanwe na wateswe kwenye scene. Nasikia mpaka ikabidi watumie crew weusi kufungwa wachezaji weusi pingu kwa ajili ya hizo scenes kwenye films. Halafu baadaye wakawa wanasema, “I’m so sorry, but that’s not me, I’m just acting!” (yaani samahani, siyo mimi naigiza tu). Wiki hii na mimi nilionja hali hiyo.

Nilienda kwenye audition ya sinema (documentary) inayotengenezwa kwa ajili ya History Channel. Hiyo Sinema itahusu kipindi baada ya vita vya wenyewe kwa wenyewe Marekani (Civil War) iliyotokea 1861-1865 na kuangamiza mikoa ya kusini mwa nchi. Hicho kipindi kinaitwa Reconstruction (Kujenga upya).

Nikitazama vijana weusi hapa Marekani najiuliza kama wanajua historia yao na mababu zao walitokea wapi. Kwa kweli waliteswa sana na kuishi maisha iliyojaa woga na wasiwasi. Ingekuwa mimi ningesema kila mtu anayesoma shule ya msingi Marekani lazima atazame ile sinema ya Roots. Asante Civil Rights vijana weusi leo wanasoma shule na wazungu, wanakaa na wazungu, na kuingia kwenye restaurants na wazungu, pia wanaweza kwenda kwenye maduka na wazungu. Lakini wengi wa hao vijana hawajui kuwa si miaka mingi iliyopita mtu mweusi hakuwa na haki Marekani. Walikuwa wanauliwa ovyo na wazungu na hakuna aliyejali. Na hao MaKKK (Ku Klux Klan) walikuwa wanaua weusi ovyo, wakiona mweusi ana nyumba nzuri, shule, wanaichoma moto!. Basi hiyo Sinema niliyofanya audition itahusu MaKKK na jinsi walivyofanya komesha maendeleo ya weusi katika enzi za Reconstruction.

Audition enyewe ilifanyika Arlington, Massachusetts, mji ambayo si mbali na Boston. Nilipanda basi na kufika huko mapema tu. Na nawaambia Mungu ni mwema, maana siku ya kwanza waliponiita niliandika anwani walionipa. Nikapoteza ile karatasi na ikabidi nipige simu kuomba anwani tena. Kumbe ile anwani ya kwanza ilikuwa na kosa. Alisema Park St. kumbe ni Park Avenue sehemu tofauti kabisa. Na watu walipotea na wengine hawakuweza kufika kwenye auditions. Lakini nilifika bila taabu!

Nilipofika kulikuwa na mtu ndani, wanamaudition. Sikuweza kumwona lakini nilimsikia akiongea ‘lines’ kwa nguvu na kuaminika kabisa. Jinsi anayochukia weusi na yuko tayari kuwaua. Jamani msishangae maana ilikuwa script enyewe. Basi, yule baba actor alitoka, mtu mzima labda miaka 50, alionekana kushutuka alivyoniona na kawa mwekundu usoni. Kanisalimia vizuri tu halafu kanishika bega kwa urafiki kabisa na kanitazama kama vile ananiomba msamaha, na mimi nilitabasamu kama ishara kumwonyesha asijali na wala asidhanie namchukia.

Line enyewe ni hii: (landowner): “You have been fooled by the damn Yankee lies till you thought you were free, and you got so you could not obey your master. There is no law against killing ( n-words) and I will kill every damned one I have if they do not obey me and work just as hard as they did before the war.”

Basi kulikuwa na kijana mwingine mzungu, mwembamba. Duh, sijui jamaa alikuwa mwoga. Alivyokuwa anatembea hapa na pale na majasho yanamtoka huko anasubiri zamu yake. Halafu kashindwa hata kutamka maneno. Alisoma sehemu ya kwanza nikamsikia Director akisema hatafaa hiyo part kwa hiyo asome nyingine. Kasoma ile nyingine ya kutumia ile tusi ya n-word, na maskini ilimshinda kabisa. Nikajua hajazoea kutumia hiyo neno na nikashukuru lakini nikasema kama ni actor ni lazima uweke maoni yako pembeni na kufanya kama director anvyotaka.

Basi jamaa katoka, nikamwambia ‘Good Luck” (Ukienda kwenye audition ni mila na desturi kumtakia mwenzako heri )!

Basi Director katoka na hakuona mtu. Yule director alikuwa na mshangao mkubwa kutokuona watu maana karibu watu mia walijiandikisha kufika. Headshots zilipangwa kufuatana na time watu waliopangiwa. Yangu haikuwa chini sana.

Kuingia mle, yule Director akawa anaomba msamaha kwa hiyo ‘sensitive’ topiki. Nikamwambia kuwa ninaelewa kuwa kipindi kile kilikuwa ni kigumu.

Basi niliambiwa niseme line, kwa ajili ya kupima ‘delivery’ yangu, yaani jinsi unavyoongea. Basi nikasema. Haya ikaja sehemu mbaya sasa. Hiyo scene inahusu familia ya weusi kuzungukwa na kupigwa na MaKKK. Basi ikabidi nijifanye kama vile nimepigwa na huko mwanangu mwenye miaka sita kapigwa pia. Loh! Nilianguka kilio. Nilikuwa nimaabiwa audition itachuka dakika 5 lakini yangu ilikuwa kama robo saa na niliweza kufanya mengi. Nilivyomaliza Director na msaidizi walitoka na kunipa mkono na kuniuliza kuhusu schedule yangu. Na amini usiamini nilivyotoka na potential actors wengine wakaanza kuja asante cell phones. Jamaa moja kawa analimika kuwa huko Park St. ilikuwa nyumba ya mtu na karibu anga'twe na mbwa.

Nadhani nilfanya vizuri, lakini mjue katika acting, tuko wengi na si ajabu nyuma yangu walikuja actors wazuri zaidi. Ila najua nilikuwa mwanamke wa kwanza mweusi kufanya audition. Pia yote ilikuwa filmed. Kwa hiyo wataweza kupima kutokana na wanachoona kwenye test film. Ujue kuna kitu kinaitwa ‘stage presence’ kwa hiyo mtu anaweza ku-acti lakini asiwe na presence. Kwa kweli acting, na kutengeneza filamu ni kazi ngumu. Msione hivyo.

Nitawajulisha kama nikichaguliwa kuwa kwenye hiyo sinema!

4 comments:

Chemi Che-Mponda said...

zemarcopolo,

Asante sana! Na wewe pia.

Chemi Che-Mponda said...

zemarcpolo,

Asante sana kwe hiyo linki. Ni kweli unavyosema kuwa sinema nyingi zinatengenezwa Eastern Europe kwa vile ni bei rahisi kuliko ku-shoot USA. Na ni vizuri kujua kuwa wanopenda fani ya sanaa za maonyesho ni wengi.

Simon Kitururu said...

Ilinifurahisha sana pale Dave Chapelle alivyo tengeneza kipande cha Roots kuonyesha behind the scenes. Nasikia Hollywood kuna weusi wengi walipata kazi baada ya Rodney King kupigwa na Mapolisi weupe, kwa maana maajenti wengi walikuwa wanaogopa kuonekana kuwa niwabaguzi wa rangi!Nakutakia kila la heri Chemi!

Anonymous said...

tafadhali tujulishe matokeo.