Tuesday, July 26, 2011

Maoni - Umeme: Mahojiano Ya BBC Na JK

(pichani: Makao Makuu yaTANESCO HQ Ubungo)


Hii imeandikwa na Kaka Maggid Mjengwa. Hivi sasa yuko Sweden.



*****************************************************************

Umeme: Mahojiano Ya BBC Na JK; Tafsiri Yangu

Ndugu zangu,

Kuna mengine yamenipita hapa kati. Leo nimesikiliza mahojiano ya mwandishi wa BBC na Rais Jakaya Kikwete kuhusu tatizo la upatikanaji wa umeme Tanzania.

Nimefuatilia pia maoni ya Watanzania mtandaoni juu ya majibu ya Kikwete. Tafsiri yangu; uongozi wa nchi ni kitu kigumu sana. Wengi wamemshambulia Kikwete kwa majibu yake kiasi wengine wamediriki kuandika; kuwa hatuna Rais.

Tunafanya makosa sana kutoa hukumu zenye kusukumwa na hisia hasi. Nimesikiliza mara mbili majibu ya Rais. Sikuona mahala pa kumshutumu Rais isipokuwa nimesikitishwa na maswali ya mwandishi wa BBC ambayo kwa Kikwete ilikuwa kama penalti alizokuwa akipigiwa mikononi na yeye kuzidaka huku akitabasamu.

Tusisahau, kuwa Kikwete ni mwanasiasa mahiri. Mwandishi anayekutana na Kikwete ni vema akajiandaa vilivyo juu ya namna ya kumbana Kikwete ndani ya majibu yake. Afanye hivyo ili kupata maswali mapya na hivyo basi habari mpya kutokana na majibu ya Rais.

Niseme tu, mahojiano yale ya Kikwete na BBC hayakutoa maswali mapya wala kuja na habari mpya. Na huo si udhaifu wa Kikwete bali mwandishi wa BBC aliyemhoji Kikwete.

Si tumemwona? Kikwete aliweza kucheza anavyotaka kwenye mahojiano yale. Na umahiri wake ulijidhihirisha pale alipogeuza sura ya mahojiano yale na Kikwete kuchukua nafasi ya mwandishi kwa kumbana mwandishi na husuan juu ya maarifa ya mwandishi katika eneo husika;

Wakati mwingine na nyinyi mjifunze hayo mambo ya kitaalamu kulikoni kuuliza tu hivi hivi. Unajua ungekuwa na wewe unauliza kwa hoja - unajua kwamba hiki kitu hiki ingekuwa umeme wa jua miezi miwili tu upo - tungeweza kufanya hivyo. Kikwete anamwambia mwandishi wa BBC.

Katika mahojiano yale Kikwete alikwenda na takwimu zake mfukoni. Kama moja ya mbinu katika sanaa ya mawasiliano ili kufikisha ujumbe, mara tatu ndani ya mahojiano yale Kikwete alizungumzia MW 600 zilizozalishwa tangu uhuru na MW 145 zilizozalishwa tangu 2009, na MW 160 zitakazozalishwa ifikapo Desemba mwaka huu. Jumla zitakuwa MW 305 tangu 2009. Na hapo ndipo kwenye hoja ya msingi ya Kikwete. Ana haki kuwashangaa wasioona jitihada zake.

Na Kikwete hakosi majibu ukimwuliza juu ya umeme wa jua, upepo na mvuke. Ana hoja anaposema kuwa umeme huo pia unahitaji mipango na kuwa huwezi kupata umeme wa jua kesho kwa vile jua linawaka.

Kama msikilizaji ningependa mwandishi ambane Kikwete kwenye maeneo ya ufisadi kwenye mikataba ikiwamo yenye kuhusiana na nishati ya umeme. Hakika, kama tungedhibiti ufisadi kwenye mikataba, basi, ni imani ya wengi kuwa tungejenga uwezo wa kuzalisha MW nyingi zaidi za umeme na kwa kasi kabisa, kulifanya tatizo la umeme kuwa ni historia. Tungeweza pia kupunguza gharama za mtumiaji wa umeme.

Tuna tatizo pia la baadhi ya wanasiasa kujiingiza katika kuwekeza kwenye eneo la nishati ya umeme. Wachague kati ya uongozi na uwekezaji. Kiongozi huwezi kuwa na hisa kwenye kampuni binafsi ya kuzalisha umeme na wakati huo huo ukalinda maslahi ya umma badala ya kampuni yako.

Vinginevyo, kwa waliokuwa na utayari wa kuelewa, mahojiano yale ya BBC na Kikwete yamempa nafasi Kikwete ya kujenga hoja ya msingi juu ya nini alichofanikiwa kufanya tangu aingie madarakani katika jitihada za kutatua tatizo la umeme nchini.

Nawasilisha.

Maggid,
Sweden, Jumanne, Julai 26,2011
http://mjengwa.blogspot.com/

1 comment:

Anonymous said...

Watanzania bwana! Unamsifia mtu kwa maneno matupu