Monday, October 10, 2011

Tanzania Imechaguliwa Kuwa Mjumbe wa Baraza la Utendaji la Shirika la Dunia la Utalii - UN WORLD TOURISM ORGANIZATION

PRESS RELEASE

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

WIZARA YA MALIASILI NA UTALII

TAARIFA KWA UMMA

TANZANIA IMECHAGULIWA KUWA MJUMBE WA BARAZA LA UTENDAJI LA SHIRIKA LA DUNIA LA UTALII

(UN WORLD TOURISM ORGANIZATION)

Tanzania imechaguliwa kuwa mjumbe katika Baraza la Utendaji (Executive Council) la Shirika la Utalii Duniani – United Nations World Tourism Organisation (UNWTO). Nafasi hiyo ilipatikana wakati wa Mkutano Mkuu wa Shirika la Utalii Duniani (UNWTO General Assembly) ambao ulianza za siku ya Jumamosi tarehe 08 Oktoba, na utakamilisha shughuli zake tarehe 14 Oktoba, 2011 nchini Korea.

Katika Mkutano huo, ujumbe wa Tanzania unaongozwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Mheshimiwa Ezekiel M. Maige ambaye ameambatana na viongozi na wataalam waandamizi kutoka wizara hiyo.

UNWTO ni shirika la Umoja wa Mataifa linaloongoza masuala ya Sera, Mafunzo, Uendelezaji na Utangazaji katika sekta ya utalii duniani.

UNWTO inatekeleza majukumu na maamuzi kuhusu maendeleo ya utalii na kutetea maslahi ya nchi zinazoendelea. Aidha, Shirika hili linahimiza utekelezaji wa Maadili katika Utalii kwa kuhakikisha nchi wanachama zinanufaika kiuchumi na wakati huo huo kupunguza athari za kijamii na kimazingira.

Hadi wakati wa Mkutano huu wa Korea, UNWTO ilikuwa na nchi wanachama 154. Idadi hii itaongezeka hadi kufikia 155 baada ya Liberia kukubaliwa ombi lake la kuwa mwanachama.

Kazi kuu ya Baraza la Utendaji la UNWTO, ambalo Tanzania imefanikiwa kuwa mjumbe ni kuchukua hatua zinazostahili, kwa kushirikiana na Katibu Mkuu wa Shirika hilo kutekeleza maamuzi yanayotolewa na Mkutano Mkuu (UNWTO General Assembly). Baraza hukutana mara mbili kwa mwaka. Tanzania itakuwa mjumbe wa Baraza hilo hadi Mwaka 2015.

Akizungumza baada ya uchaguzi huo, Waziri Maige alielezea sababu ya Tanzania kugombea nafasi hiyo muhimu ni kutaka kuwa ndani ya chombo cha maamuzi na hivyo kushawishi maamuzi yatakayoinufaisha Tanzania na kujitangaza zaidi Duniani katika uwanja wa kimataifa wa masuala ya Utalii.

No comments: