Wednesday, April 06, 2011

Wasanii na Wadau wa Filamu Tanzania Wapata Mkombozi wa Kweli

NA JUSTIN KASYOME

www.kasyome.bogspot.com+255 7141696655

Ukizungumzia tasnia ya filamu za Kitanzania kwa kuwataja wanaharakati au wadau wanaooiinua na kuipigania filamu, ni nadra sana kuacha kuwataja waigizaji maarufu, vikundi vyenye majina makubwa, taasisi, vyama au makampuni.

Steven Kanumba "The Great", Vincent Kigosi "The Greatest", Suzan Lewis "Natasha", Charles Magari "Mzee Magari", Blandina Chagula "Johari" na wengine wengi, ni miongoni mwa waigizaji ambao ni lazima uwataje kama ukitakiwa kuwataja waigizaji "wanaipiga tafu" tasnia ya filamu nchini.

Wadau wengine ni kwa mfano, makundi ya Mambo Hayo na The Spendid, yaliyotamba enzi zao na kuibua changamoto ambazo hadi sasa zinaonekana. Mengine ni Kaole Sanaa Group na Jakaya Arts Group.

Taasisi kama kituo cha Utamaduni cha Muungano wa Urusi na Tanzania (Russian - Tanzania Culture Center), taaisisi ya watu wa Ujerumani (Goethe Institute), Game 1st Quality, Steps Entertainment, BASATA, COSOTA na TAF.

Pamoja na wadau na wanaharakati mbalimbali, msanii bado hana mafanikio! bado ni omba omba! Wengi wenye maisha mazuri, si kutokana na filamu! Ni kutokana na background ya familia yake au kipato chake kingine nje ya filamu! wakiwa kwenye vyombo vya habari wanaficha ukweli ili wajikweze kwa kuwa wengi wao wanaingia kwenye taaluma ya filamu "kuuza sura"!

Mzalishaji, anaeumiza kichwa kutafuta mtaji na kuandaa bajeti ya filamu, uandaaji hadi kukamilika, bado hana sauti wala nguvu sokoni! Anafanya kazi kwa shinikizo la woga wa soko! Hana uhakika wa soko lake endapo atakuwa jeuri! kinachobaki ni kuweka mikono nyuma awapo mezeni ili filamu yake isambazwe! Haijalishi atalipwa kiasi gani!
Msambazaji, anatupiwa lawama za unyonyaji, Buguruni na Ubungo, filamu za elfu tano dukani, zinauzwa elfu moja moja! Muigizaji, ndugu jamaa na marafiki wanazinunua kwa wingi!

Mnunuzi wa mwisho bado anafuata mkumbo wa nguvu ya msambazaji bila kujali ubora filamu kuanzia kwa mtunzi wa hadithi, muigizaji, muongozaji, mpiga picha, mbamaji, mazingira na taaluma ya filamu yote! Ananunua filamu kwa mazoea ya majina na hadithi!

Idea For Action Tanzania (IFA Tanzania), mradi uliobuniwa kitaalamu, ni miongoni mwa wadau wa kweli na wa dhati kabisa katika kiwanda cha filamu za kitanzania.
Ni mradi wa kuibua na kuendeleza vipaji vya sanaa kwa kutoa elimu ya sanaa na ujasiriamali, bure, bila ada yoyote! Kila mdau wa sanaa anaalikwa kuhudhuria mafunzo.

Mafunzo haya yatolewayo kwa lugha anayoielewa kila mtanzania (Kiswahili) yanakwenda kwa muda wa miezi mitatu. Mlengwa anatakiwa kujiunga muda wowote na kuanza mafunzo baada ya kujaza fomu ya kujiunga. Hakuna umri, kabila, dini wala kiwango cha elimu kinachofaa kupata mafunzo isipokuwa yeyote mwenye mapenzi mema na sanaa na anayejua kusoma na kuandika, anapaswa kujiunga.

Baada ya kumaliza mafunzo, mwanafunzi anasimamiwa na wataalamu kufanya mafunzo kwa vitendo kwa vitendo ili kuthibitisha uelewa wake na kutunikiwa cheti cha awali cha kuhitimu.

Mwisho, mhitimu akipenda ataunganishwa na makampuni au taasisi wadau kufanya kazi kwa mkataba wa miaka miwili ili kuzidi kuapata uzoefu wa kazi ya sanaa na atabakiwa kuwa mwanachama wa mradi wa IFA Tanzania maisha yake yote kwa kushirikaina na mradi pale atakapohitajika, kuomba ushauri katika kuanzisha na kuendesha miradi mbali mbali ya sanaa na mambo mengine ya kimaendeleo.

Mradi huu ambao ni endelevu, umegawanywa katika vitengo vinne vya filamu, muziki, vichekesho na biashara. Tuzungumzie kitengo cha filamu. Ndani ya kitengo hiki, zinafundioshwa mada nane,saba ni taaluma ya filamu na moja na ujasirimalia wa filamu (Interprenuereship in Film Production)

Mada hizo saba ni Utunzi na Uandishi wa Hadithi (Screenwriting), Uigizaji na Upangaji wasanii (Acting and Casting), Upigaji wa picha (Cinematography), Ubunifu wa Sauti (Sound Designing), Ubunifu wa Uzalishaji (Production Design), Uongozaji/Uzalishaji/Masoko (Directin/Producing/Marketing) na Uhariri(Editing).

Malengo makubwa ya IFA Tanzania, kitengo cha filamu ni matatu. Kutoa taaluma ya filamu ili mnufaika aitambue filamu na kujitambua awapo ndani ya filamu.
Hilo mosi.
Pili, kutoa elimu ya ujasiriamali baada ya taaluma ili kugundua, kutambua na kutumia fursa mbalimbali zilizopo na kupata mafanikio kabla ya kumpelekea msambazaji!
Msambazaji awe mdau wa mwisho kwa mapato ya mzalishaji wa filamu za kitanzania! Tofauti na ilivyo sasa, ambapo mzalishaji ni lazima akampigie magoti msambazaji! Tena kwa kazi iliyomtoa jasho!

Tatu, ambalo ni kubwa zaidi, kuokoa utamaduni wetu. Uzalendo, haki na utaifa uwekwe mbele zaidi wakati elimu na burudani ikiimilishwa kitaalamu kama dhima kuu ya filamu ambayo ni kazi ya sanaa katika jamii.
Malengo ya mradi ni kumzalisha mtaalamu wa filamu mwenye mbinu za ujasiriamali ili atazame, azalishe au kushirikishwa katika filamu zinazozungumzia visa vya vita, magonjwa, upelelezi, tatizo la ukosefu wa ajira, njaa, afya, elimu n.k.
Iweje filamu za kitanzania ziwe na ujumbe wa kisa kimoja cha mapenzi pekee? Je, Je ni makosa kuzungumzia visa vingine? Utamaduni wetu wa sasa kwa vizazi vijavyo, utakuwaje? Tunaijenga Tanzania ijayo au tunaibomoa?

Tunasikitishwa sana na mfumo wa filamu zetu kiutendaji na kibiashara. Tunapoteza utamaduni kwa faida fulani fulani. Nani alaumiwe kati ya muigizaji, mzalishaji, msambazaji au mnunuzi wa mwisho?

Justin Kasyome, anaendelea, IFA Tanzania, ni mradi wa kizalendo, tunapigania utamduni wa mtanzania kwa kutengeneza faida inayokubalika katika mfumo mzuri kimasoko. Watanzania tujikomboe, elimu pekee ndio silaha yetu. Kwa pamoja tutshinda na kumwondoa adui yetu.
IFA Tanzania, inapatikana ndani ya majengo ya Chuo Cha Elimu Kuu Sanaa, eneo la Sinza Legho, barabara ya Shekilango, mkabala na Club ya Sun Cirro. Au kwa mtandao wa www.ifatanzania.blogspot.com

No comments: