Friday, September 26, 2008

Mchungaji Christopher Mtikila alazwa baada ya kupigwa Mawe Tarime


Nimesikitika sana kusikia kuwa Mchungungaji Christopher Mtikila, kapigwa huko Tarime leo. Sisi waTanzania si tulikuwa tunajivunia ni watu wa amani? Sioni sababu ya mtu yeyote hata awe mwanasiasa kutoka chama gani kupigwa.
*******************************************************************

Kutoka Lukwangule Blog (Beda Msimbe):


Mtikila apigwa mawe Tarime

MCHUNGAJI Christopher Mtikila amelazwa katika Zahanati ya Tarime mjini hapa baada ya kupigwa jiwe la kichwani wakati akihutubia kumnadi mgombea wake.

Kwa mujibu wa maelezo ya daktari anayemtibu Mchungaji Mtikila, Philemon Hungiro, kiongozi huyo ameumizwa vibaya na jiwe hilo kisogoni kiasi cha kushonwa nyuzi tatu.

Mtikila alisema alipigwa jiwe hilo na mtu asiyemfahamu wakati akimnadi mgombea ubunge kupitia chama chake cha DP, Denson Makanya, kwenye Uwanja wa Shule ya Sabasaba mjini Tarime.

Jiwe hilo alipigwa majira ya saa 11 jioni leo wakati akitoa ufafanuzi wa taarifa zake kuhusu kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Tarime, Chacha Wangwe.

Wakati akiishambulia Chadema kuhusika na kupanga mauaji hayo, ndipo mtu huyo alipochoropoka kutoka nyuma na kumpiga jiwe la kisogoni.

Hata hivyo, Mchungaji Mtikila alidai kipigo alichokipata ni matokeo ya ahadi ya Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbrod Slaa, kwamba damu itamwagika na kwamba kiongozi huyo akifika Tarime atapigwa mawe.

Awali akihutubia mamia ya wananchi waliofurika katika uwanja huo wa mkutano, Mchungaji aliwataka wananchi kumchagua mbunge anayemnadi kwani yeye hana ufisadi wala mipango ya mauaji.


*****************************************************

Kutoka ippmedia.com

Tarime ni soo!

2008-09-26 16:35:51
Na Mwandishi Wetu, Tarime

Wakati siku za kuelekea uchaguzi mdogo wa kumsaka mbunge wa Jimbo la Tarime zikizidi kukaribia, hali ya kisiasa mjini hapa imeanza kuwa tete baada ya wafuasi wa vyama vinavyoshiriki uchaguzi huo kuendelea kufanyiana visa mfululizo, vikiwemo vile vya kumwagiana pilipili na kuwatwangana mawe mikutanoni.

Uchaguzi huo mdogo, unatarajiwa kufanyika Oktoba 12, ili kujaza nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Marehemu Chacha Wangwe, aliyefariki mjini Dodoma Julai 28 mwaka huu baada ya kupata ajali ya gari.

Jana, muendelezo wa visa vya baadhi ya wafuasi wa vyama hivyo vya CCM, CHADEMA, NCCR-Mageuzi na DP ulifikia pabaya baada ya Mwenyekiti wa UDP, mchungaji Christopher Mtikila kupigwa jiwe la kichwa wakati akiwa kwenye mkutano wa kampeni kwenye viwanja vya Sabasaba.

Mtikila alijeruhiwa vibaya na kukukimbiziwa hospitali mjini hapa ambako inadaiwa alishonwa nyuzi saba.

Kutokana na vibweka vinavyoendelea katika kampeni za kuelekea siku ya uchaguzi huo, , viongozi mbalimbali wa vyama vilivyosimamisha wagombea wamekuwa wakitoa kauli tofauti kuhusiana na yanayojiri.

Dk. Sengondo Mvungi (NCCR-Mageuzi)
Yeye aliripotiwa kuwa kiongozi wa kwanza kufanyiwa vurugu wakati wa kampeni jimboni humo.

Mvungi alikumbana na kadhia ya kutimuliwa kwa mawe wakati akimnadi mgombea wa chama chake cha NCCR.

Baada ya hapo, Dk. Mvungi ambaye pia ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alilaani tukio hilo na kueleza kuwa ni la hatari, kwani hakuna chama chenye hakimiliki ya jimbo hilo.

Pius Msekwa (CCM)
Makamu huyu Mwenyekiti wa CCM, naye alionja ya joto ya jiwe ya kufanyiwa vituko vya kampeni hizo wakati alipokuwa akimnadi mgombea wa chama chake, Bw. Ryoba Kangoba.

Msekwa alifanyiwa fujo na kuzomewa na watu wanaodaiwa kuwa ni wafuasi wa vyama pinzani.

Aidha, wafuasi wawili wa chama chake wameripotiwa kuumizwa baada ya mmoja kupigwa jiwe na mwingine kumwagiwa pilipili.

Kutokana na hali hiyo, bosi huyo namba mbili wa CCM akailalamikia hali hiyo na kuripotiwa akitishia kulifikisha suala hilo kwa Rais Jakaya Kikwete ili hatimaye zifanyike taratibu za kudhibiti hali ya namna hiyo ambayo ni ya hatari.

Christopher Mtikila (DP)
Baada ya kasheshe la jana la kupigwa mawe kwenye uwanja wa Sabasaba, amekaririwa akilalamikia hali hiyo aliyodai kuwa imetokana na njama za wapinzani wake.
Akizungumza na waandishi wa habari, Mtikila amekaririwa leo asubuhi akisema: ``Nilitoa taarifa mapema kwa Msimamizi wa Uchaguzi na OCD.. niliwaeleza juu ya agizo la mimi kupigwa mawe...``

Freeman Mbowe (CHADEMA):Mbowe na chama chake cha CHADEMA wamekuwa nao wakilalama kuonewa na askari polisi walio katika operesheni kali ya kulinda amani katika jimbo hili.

Aidha, kwa nyakati tofauti, yeye, Katibu Mkuu wake Dk. Wilbroad Slaa na Mbunge wa Viti Maalum wa chama hicho, Halima Mdee, wamekuwa wakitoa madai ya kuonewa kwa kunyimwa viwanja vya kufanyia kampeni za mgombea ubunge wa chama chao, Bw. Charles Mwera.
Prof. Ibrahim Lipumba (CUF)

Baada ya kutosimamisha mgombea jimboni humo ili kuwapa fursa wenzao wa upinzani jimboni humo, Prof. Lipumba na chama chake wamekuwa katika wakati mgumu wa kuamua wamuunge mkono mgombea yupi baada ya wenzao kuwasaliti kwa kusimamisha mgombea zaidi ya mmoja, kinyume cha makubaliano.

Mkanganyiko huo unadaiwa kutokea baada ya vyama vinavyoungana nacho katika umoja wao wa vyama vikiwemo vya CHADEMA, TLP na NCCR-Mageuzi kushindwa kumsimamaisha mgombea mmoja, hasa baada ya NCCR na CHADEMA kusimamisha wagombea wawili tofauti.

Hata hivyo, ingawa CUF Tarime wameamua kumuunga mkono Bw. Charles Mwera wa CHADEMA, Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, Bw. Wilfred Lwakatare, amekaririwa asubuhi ya leo akisema kuwa wamemtuma jimboni humo kiongozi wao Mustafa Wandwi ili kuangalia ni mgombea yupi anayeelekea kukubalika zaidi ili hatimaye wamuunge mkono.

Wakati huohuo, Jeshi la Polisi jimboni humo limesema liko makini katika kudhibiti vitendo vyote vinavyoashiria kuvunja amani.

Akizungumza na Alasiri juzi, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mara, Liberatus Barlow, amesema FFU na polisi wengine kibao waliomwagwa jimboni humo wamejipanga vilivyo katika kuhakikisha kuwa uvunjifu wa amani unadhibitiwa ipasavyo.

Wakati huohuo, katika kuthibitisha kuwa Polisi wako makini, tayari wameshawanasa watu wanne wanaotuhumiwa kumvurumishia mawe Mchungahji Mtikila jana na kuwawezesha kuburuzwa kortini.

Walionaswa na polisi katika tukio hilo la jana na ambao leo wamepandishwa kizimbani ili kujibu mashtaka.

Kamanda Barlow amewataja watuhumiwa hao kuwa ni Mussa Peter, Mwita Chacha, Hafidh Stanslaus na Mwita Kilongo.

Amesema watuhumumiwa hao, mmoja alikamatwa wakati wa tukio la kupigwa kwa Bw. Mtikila na wengine watatu walikamatwa jana katika msako wa Polisi uliofuatia kujiri kwa tukio hilo la kupigwa kwa Mtikila.

SOURCE: Alasiri

1 comment:

Anonymous said...

MI NAONA SAWA SAWA YE KUPIGWA.ATAONGELEAJE HABARI ZA KIFO CHA WANGWE KUWA KIMESABABISHWA NA WATU FULANI KWENYE MKUTANO.
HABARI HIZO AKATOE POLIS SIYO KUPANDIKIZA CHUKI UKU JION AKIVUTA MSHIKO WA ELA TOKA KWA ROMSTAN,MUIRAN WAKE.
WANANCH WAMECHOKA NA MAMBO YA MTIKILA LIWE FUNDISHO KWA WENGINE.
TUTEGEMEE KUONA MENGI ZAHID KWA WANAFIK KAMA MTIKILA KUAZIBIWA DUNIAN KABLA YA JEHANAM.
NA SIJUI NI MCHUNGAJ WA WATU AU MIFUGO SABABU SIMUELEW.
jj,boston