Tuesday, April 25, 2006

Miaka baada ya Tukio kaniomba Msamaha!

Nilipokuwa Jeshi ya Kujenga Taifa (JKT) karibu nibakwe na afande Fulani (jina nahifadhi). Lazima niseme kuwa katika kipindi hicho wanaume wengi waliona makambi ya JKT kama ‘buffet’ ya wasichana. Si maafande wa jeshi tu, bali hata viongozi wa serikali walikuwa wanapitia makambi ya JKT kula tani yao!

Mimi nilikuwa Masange JKT, Tabora. Wakati huo huyo jamaa alikuwa ni Kepiteni wa JKT. Nadhani alidhania kwa vile yeye ni kepiteni basi alikuwa na haki ya kutembea na yeyote aliyemtaka. Kwangu aligonga ukuta! Bila shaka alikuwa hajawahi ‘kunyimwa’ mpaka siku hiyo alipokutana na mimi.

Miaka baada ya tukio nikiwa nafanya kazi Daily News mara nyingi nilikuwa napishana naye Posta Mpya. Basi ananisemesha, na mimi namnunia halafu napita zangu kimya bila kumjibu kwa hasira. Siku moja kanisimamisha kaniambia, "Chemi, naomba msamaha, nisemahe tafadhali, kweli nilikukosea!” Aliongeza kuwa miaka mingi imepita hivyo sina sababu ya kuwa na hasira naye! Na mimi nilimjibu, “Mshenzi sana wewe!” nikaenda zangu.

Ikapita kama mwaka nyingine. Jamaa anaendelea kunisalimia kila nikimpita njiani na mimi kwa uchungu bado nikashindwa kusema kitu. Basi nikafikiria alichoniambia Posta Mpya. Lakini nilona kama jambo hilo linamsumbua. Na nikasema kama Bwana Yesu aliweza kusamehe watu kwa madhambi yao kwa nini mimi nisimsamehe. Basi baada ya hapo ikiwa nikimwona na akinisalimia naitika na naendelea zangu na nikaona kidogo hata yeye alikuwa na raha. Lakini bado najiuliza kama kitendo chake kilimsumbua miaka na miaka kama ilivyonisumbua mimi.

Unauliza ilikuaje mpaka nikajikuta kwenye situation ya kubakwa. Au mnasema nilitaka mwenyewe. Ngoja niwaelezee ilivyokuwa. Nilikuwa mhudumu Officer’s Mess, mpishi na msafishaji. Huyo jamaa alikuwa ni mgeni kutoka Makao Makuu ya JKT Dar es Salaam. Kwa kweli sikutaka kufanya kazi pale Mess lakini tulichaguliwa special na Matron, mimi kwa vile niijua kupika vyakula mbalimbali hasa za kizungu. Lakini uzuri wa hiyo kazi ni kuwa uanambulia mabaki ya vyakula (leftovers), na mara nyingine kulikuwa hakuna.

Basi huyo Afande alikaa kambini wiki kadhaa. Katika kumhudumia tukawa tunaongea na mimi nikawa namheshimu kama kaka vile. Wala sikusikia mapenzi yoyote kwake. Basi jioni fulani, kanialika chumbani kwake kunywa soda na biskuti na kwa Maongezi zaidi. Sasa kama ulienda jeshi unajua njaa kali unayokuwa nayo. Nikaenda, kanikaribisha vizuri, nilipewa soda na tukawa tunaongea. Basi nikaona mwenzangu anabadilika ghafla! Mara ananikumbatia kwa nguvu, na kunibusu na mengine. Nikajaribu kuaga lakini jamaa hakuniachia. Baada ya ku-plead naye aniachie, kaniachia. Kaomba msamaha na kaniomba niendelee kukaa nimalize hizo soda alizoninulia. Kama mjinga nikamwamini, nikakaa nakunywa hizo soda. Tukaendelea na Maongezi, kukaa kidogo huyo kanirukia, najaribu kusimama huyo, kanivuta na kuniangusha kitandani! Mimi saa hizo nikawa naogopa kabisa nia yake!

Kaniambia eti, “ukipiga makelele najua nitasema nini! Nyamaza! Huna sababu ya kunikatalia!” LOH! Kanizaba na kibao! Nikamwuliza kwa nini anaifanyia hivyo, na mimi nilikuwa namwona kama kaka yangu!

Hapo sasa ikaniingia. Nabakwa! Loh! Nilimpiga mangumi na mateke lakini jamaa alikuwa na nguvu huyo kachana chupi yangu! Baada ya hapo, jamaa kashika miguu yangu huko anafoka kwa sauti kama vile anatoa amri “panua miguu! PANUA MIGUU!” Huko katoa ume wake uliyosimama kwenye suruali! Basi kuona sipanui jamaa kaongeza makofi na kafanikiwa kupanua miguu yangu! Kuona kafanikiwa kupanua huyo kajaribu kupenya. Ilipogusa kwangu nilipiga kelele cha kufa! Nikasema, “Nakuufaaaa!” Heh! Ghafla jamaa kaniachia kaniambia niende. Alisema, “Nimeigusa na ume wangu, unatosha!” Nenda zako! Na ukimwambia mtu najua nitasema nini!”

Loh nilikimbia bwenini na giza lile la Masange huko nalia. Wenzangu wananiuliza vipi, nikashindwa niseme nini! Kwanza niliona haya! Fikiria, niliona haya (shame)!

Kesho yake nikaenda dispensary na kujiandikisha mgonjwa. Sikwenda kazini Officer's Mess bali nililala bwenini. Siku iliyofuatia huyo Afande mshenzi kapita bwenini kwetu kaulizia hali yangu, na mimi huko natetemeka kwa woga nikashindwa niseme nini. Alininunulia Orange squash na biskuti na kuzileta bwenini. Sitasahau alivyonitazama! Ilikuwa kama vile anapanga jinsi gani atanipata.

Baada ya hapo alimwopoa msichana mwingine na huyo alimkubali kabisa. Akawa analala kabisa huko Officer’s Mess. Hakuna anayemsumbua wakijua ni bibi wa Afisa. Basi, siku za yule jamaa kukaa kambini zikaisha, na yule binti alienda naye Tabora mjini kwa siku kadhaa. Halafu jamaa karudi zake DSM. Yule binti karudi zake kambini! Kumbe alienda bila pass. Alidhania kwa vile yuko na mkubwa hana haja ya pass. Na yule Afande ndo kaondoka kimoja! Maafande waliobakia wacha wamtese huyo binti alivyorudi kambini! Walimtesa kwa Extra drill na mengine mpaka ikabidi Military Police waombe wakuu wamsamehe la sivyo atakufa. Raha yake iliishia kwa suluba! Sijui yule binti alidhania jamaa atamwoa! Kwa nini alimkubali yule mshenzi. Anyway, kila mtu na vyake. Alivyotoka kwenye suluba tulimwuguza! Siku haizkupita na mimi nilitolewa kazi Officer’s Mess na kupelekwa kwenye kikosi cha Ujenzi na lazima nisema hapo nilifurahi sana.

Basi miaka ilipita. Mimi nilikuwa mwandishi wa habari Daily News, tena nilijenga jina. Sasa nikawa napishana na yule jamaa huko kapandishwa cheo na yuko JWTZ. Jamaa anajaribu kunisalimia na mimi napita zangu kimya, namnunia kabisa. Nilimwona mshenzi, mnyama, na kila kitu kibaya ndo ilikuwa yeye! Angefanikiwa kuingiza na kunimwagia uchafu wake ningejiona mchafu mpaka leo! Miaka kama 20 imepita sasa na bado nina uchungu naye.

Jamani nyie wanaume nawaambia kubaka kinaathari zake kwa wanawake. Unataka raha ya dakika na unamwachia mwenzio na uchungu wa maisha! Wengine mpaka wanakuwa wagonjwa wa akili.

Kwa nini nimeamua kuzungumzia kubakwa kwangu hapa, ni kwa sababu naona wasichana wengi wanabakwa, halafu wanaamua kunyamaza kimya. Kisa wakienda polisi na hospitali wanahofia kuambiwa ni Malaya au walitaka wenyewe! Hata mwamanke mwenzako anaweza kukufokea kuwa ulitaka mwenyewe.

Tanzania, wanaume walikuwa na usemi wao kuhusu wanawake na ngono. Walisema eti ukimwomba mwanamke halafu akijibu ndiyo, manake ndiyo atafanya. Akisema labda, manake atafanya, akisema hapana, manake hapana. Lakini jamani tendo si inakuwa tamu kama wote mmekubali? Na kama angefanikiwa kuingiza si angeniumiza sana!

Wengine wanasema ningemshitaki. Je, ningemshitaki ingekuaje? Kwanza jeshini mimi ningepewa Extra Drill mpaka niumie au kufungwa jela ya jeshi iliyojaa maji na mbu kusudi niteswe. Kumbuka ilikuwa Tanzania na yule alikuwa ni Kepiteni wakati huo na mimi nilikuwa Private. Hakuna ambaye angekuwa tayari kunisikia zaidi ya wenzangu maPrivate, na yeye alijua hivyo. SHENZI TAIPU!

21 comments:

mwandani said...

Doh! pole sana. Uonevu kama huo ulikuwa ukiendelea sana wakati ule, ilikuwa ikisikitisha sana haswa pale matendo kama hayo yalipokuwa hayachukuliwi hatua yoyote - hata kuripotiwa tu.
Mara nyingine maafande walikuwa wakikokota watoto kwa biskuti tu kama unavyosema.

Chemi Che-Mponda said...

Yaani acha tu, wasichana walikuwa wanonewa kweli hasa wale walionekana wazuri wazuri. Halafu kulikuwa na wanawake special kwa ajili ya Viongozi wa serikali na wakuu wa jeshi. Tulikuwa na mama moja alipewa Usajini kwa ajili ya kazi ya kumbudurisha mkubwa fulani!

boniphace said...

Chemi matukio haya bado yapo. Kuna makundi ambayo hayazungumziwi kabisa na ninashukuru kwa ujasiri wa wewe kuzungumza hapa. Katika Barua kwa Mama, nina chapters zinazozungumzia akina kaka na dada wanaofanya biashara ya ngono katika Tanzania, na pia kazi ya baameid. Hawa walimkosea nani? Kwa nini hatuwajadili matatizo yao? Je ukimya huu unasaidia au unaongeza wanaowadhalilisha kudhani kuwa ni haki yao kufanya hivyo?

Chemi Che-Mponda said...

Hi Kaka Boniface,

Habari za siku? Hapa nimeamua kufungua mlango kwa waliobakwa. Wasichana wanaolazimishwa kufanya tendo na si ajabu wengine bikra. Lakini mijitu inasema, ina cheo kwa hiyo basi ni haki yao kula! Na najua wapo waliopenda kutembea na maafande kwa ajili ya kupata 'privileges'. Lakini kama hukutaka kufanya tendo na umelazimishwa umebakwa. Fikiria msichana anachunga ubikra wake kwa ajili ya mchumba wake halafu afande anauiba! Ni haki hiyo! Pia kubakwa unaathiri 'sexual performance' ya aliyebakwa, maana atakuwa na woga kila mara, inakuwa vigumu kusikia raha inayotakiwa. Psychological effects.

Kwa kweli lazima niseme kuwa hao wanaofanya biashara ya ngono wanajua kazi yao ni nini, na wamejiamulia wenyewe. Labda hawakutaka kufanya hivyo lakini wanajua 'job description'. Ni kweli hao mabaamedi na maCD wana matatizo yao lakini lazima tutenge matatizo yao na wasichana waliobakwa. Si uwongo maCD wanabakwa pia Lakini huwezi kuwalundika na wasichana wa shule au JKT ambao wamebakwa.

Na nilivyokuwa Bongo nilifuatilia kesi kadhaa za mabamedi, CD's waliodai kuwa walibakwa. Hakimu alisema eti ilikuwa kazi yao kwa hiyo wamezoea, case dismissed. DUH! Haki iko wapi? Na kulikuwa na kesi ya Mwanamke aliyeolewa alibakwa, kamshitaki jamaa, Hakimu kasema eti wka vile alikuwa ameolewa amezoea kufanya tendo! Case Dismissed!

Jamani kwa kweli ni lazima tubadilishe fikra za jamii. Bora hapa USA sheria zinalinda kweli waliobakwa hata hao MaCD unayowasema. Na kama unavyosema Ukimya umezidi.

Sema usiogope sema!

John Mwaipopo said...

Pole sana Chemi kwa masaibu yaliyokupata-ga miaka hiyo 20 nyuma. Ni wazi kubakwa kuna athari kama ulivyoziainisha kwa ustadi mkuu. Masaibu mangapi yamekukuta katika kipindi cha miaka hiyo 20 lakini bado umeweza kukumbuka na kusimulia kama vile limetokea jana tu. Ni athari hiyo. Vile vile nikupongeze kwa kulitoa hili ili mwanga sasa uangaze kizazi hiki na kujua nini la kufanya. Hats off!

Jeff Msangi said...

Chemi,
Nikupe pole kwa mkasa mzima kwanza.Pole sana.Pili naomba nikuambie kwamba umefanya mambo mawili ya busara sana.Kwanza umeandika ili wengine wote waliopatwa au watakaopatwa na mkasa kama wako wasione haya kuyazungumzia na hata kuwapeleka wahusika mbele ya sheria.
Lakini pia umefanya busara muhimu mno ya kusamehe.Mtu akikutendea jambo,ukaudhika na ukabakia na hasira,chuki na kinyongo moyoni mwako unakuwa victim mara ya pili na kimsingi unakuwa mtumwa wake.Umeweza kuandika kwa sababu umevuka kikwazo cha kutosamehe.Najua huwezi kusahau na wala sitaki kukudanganya kwamba unaweza sahau.Cha muhimu ni kusamehe kama ulivyofanya ili uwe mtu huru daima.Natumaini wengine wataiga mfano wako.

Anonymous said...

Pole Chemi, habari kama hizi lazima zisemwe. Sio jeshini tu hata majumbani. Yako mengi, na blogu ni kati ya milango ya kusemea.

Jeshi lile la "kubomoa" taifa nililichukia sana. Nkya wa blogu ya Pambazuko shahidi. Na nilijenga ukaidi wa hali ya juu. Nakumbuka siku mimi na Nkya na Malisa tuliponyanyua mawe na kumwambia afande kama ni dume asogee. Kipindi chote cha jeshi ninavyoona kwangu ilikuwa ni kupoteza muda katika maisha. Dhana ya jeshi lile ni nzuri ila muundo na utekelezaji ovyo kabisa. Na ndio unaona jeshi likawa kama ni mahali pa maafande kudhalilisha wanawake (na wanawake wengine kujidhalilisha wenyewe). Toboa yote Chemi!

Anonymous said...

Pole sana dada yetu mpenzi.Mwanzo wa kisa hiki nilianza kwa mtizamo hasi dhidi yako nikidani labda wewe ni katika kundi la wanawake wanaojiona aghali.Lakini kwa namna ulivyo kielezea kisa hiki kinasikitisa sana kabisa.Pole sana dadangu.Ila nashauri kwa mila zetu pamoja na malezi ya dini zetu usingefikia kuelezia mpaka wapi alikugusa(baada ya kkukupanua miguu).Ni kweli unayosema lakini ni mazito jamani.Pole sana.

Chemi Che-Mponda said...

anonymous,

Asante sana kwa feedback yako. Ni kweli unavyosema kuwa kwa mila na desturi za Tanzania nisingesema jamaa kanigusa wapi. Sikatai. Lakini niliona ni bora ni vunje na kusema maana mengi tunaficha au hatutilii manani kwa kusingizia mila na desturi. Matokeo yake mambo yanaendelea.

Navyoona ni bora kuweka wazi. Na kwa kweli kipindi hicho ningeona aibu sana hata kuandika mkasa huo, lakini baada ya kuona mengi duniani na hasa uonenevu wa wanawake mpaka wanawake kuoza huko chini shauri ya kubakwa naona ni bora tuweke kila kitu wazi.

Anonymous said...

Kwanza nikupe pole lakini uliyapenda mwenyewe. Wewe mwanamke unaalikwa kwenye nyumba ya AFANDE WA JESHI unakubali kwenda peke yako ulitegemea nini? Tena usiku ulitegemea yeye akuelewi vipi? Mazingira ya kubakwa mnayatengeneza wenyewe halafu mnaanza kulalamika.

Anonymous said...

pole sana, leo ni mara yangu ya kwanza kutemblea hapa na nimesikitishwa sana na tukio hilo. Mambo kama hayo bado yapo yanaendelea Tanzania na hata kote duniani. Talking is the best remedy na utakuwa umewasaidia wengi ambao walikumbwa na janga kama hilo kujitikeza na kusema yalitiwapata. Swali ni moja watu kama hawa bado sheria ya Tanzania inawalinda they need to be locked away. Pole sana.

Innocent Kasyate said...

Oh!Pole Bibie,
Wewe mwanamama jasiri kweli.Sio rahisi watu kuhadithia kama wewe.Nafikiri unajua ni wanawake wengi tu wanabakwa hasa sehemu za kazi na wanamezea tu. Si unajua tena 'priveledge.
Hata leo maofisini hali bado ni mbaya sana.Nakwambia wako hata viongozi waheshimiwa wanatumia vyeo vyao kuendeleza hili.
Dada Chemi naomba ufuatilie huko Kenya yuko mwanamama mmoja mbunge kapeleka muswaada bungeni ili kuwaadhibu wabakaji. Lakini wabunge wanaume wameupinga kabisa.
Nakwambia ubakaji utaendelea kwa mwendo huu.

mwandani said...

Bado nafikiria, unajua weye jasiri sana kusema yote namna hii. Niliwahi kukutana na mtanzania mmoja ulaya, akanisimulia kwa kirefu jinsi alivyomgaragaza dada mmoja kule kimara saa za jioni migombani.

Nikamwambia "unajua hilo ni kosa la kubaka?"
hata asielewe, na huyu alikuwa ni msomi, anayeonekana kuerevuka...

Ati akanijibu: Demu akikutokea kizalizali, wawili tu kizani hata we Tunga ungefanyaje? Si inabidi tu ufanye kweli...

Kwa kifupi bado wengi tunawaza hivyo.

Tunahitaji kusikia haya ili tuujue upande wa pili - kutoka kwa akina mama - vilivyo.

Anonymous said...

Hi Chemi,

My boyfriend is Tanzanian and he translated this to me. I do know some Swahili. This is terrible what happened and my boyfriend says this is a normal occurence in Tanzania and that in most cases the woman gives willingly. So I thnak you for fighting this wicked man.

If you were here in the States you could have him charged with Sexual Assault and Assault and Battery. What are the Statute of Limitations. Here Priests are charged for sex crime of fifty years ago. I am glad that you spoke out! I am sure that this wicked man did the same to many others and sadly away with it.

mzee wa mshitu said...

Hehhh Chemi umepataje ushujaaa huu! Pole saana ndugu yangu mimi ingawa sijapata bahati ya kulikuta JKT, lakini hivi majuzi katika kuhangaika nilibahatika siijui niseme hivyo kuingia JWTZ hakina nilikimbia kwasababu ya niliyoyaona huko.
Wapo wasichana wengi tu wanabakwa wengine kutokana na umri mdogo kutokujua nani ni mwajiri na yupi siyo na zipi ni haki zao zipi siyo wanataabika. Lakini hatimaye wanabahatika kumaliza na je Ukimwi si ndiyo balaa. Pole sana haya unayoyasema yanatusikitisha sote sijui kama kuna mwenye akili timamu anayefurahia hili. Pole saaaana

Anonymous said...

kwa hiyo dada Chemi baada ya kutukanwa na hao wahuni ndiyo umeamuaje? Maana naona kimya wakati sie mawazo na ushauri wako bado tunauhitaji.
Tafakari tafadhali.

Chemi Che-Mponda said...

Hi anonymous,

Nipo, ilikuwa kuwa busy na shughuli zingine. Karibu (East Coast) mtaniona kwenye TV commerical ya TD BankNorth.

Mija Shija Sayi said...

Dada Chemi, baada ya kusoma kisa hiki nikapata wazo kwamba maadamu suala la jeshini lilistopishwa lakini kuna haja ya maisha yale kuwekwa katika kumbukumbu. Sasa wewe si huwa ni mtu wa mafilamu? unaonaje ukafikiria juu ya kutengeneza filamu moja kabambe ya maisha ya jeshini?

Indya Nkya said...

Kwanza Pole. Nilikuwa sijatembelea uwanja wako siku nyingi. Ushenzi wa JKT tunaujua. Macha ameeleza mimi na yeye tulivyokuwa tukipambana na maafande wapuuzi. La maana umefanya kuyaweka wazi. Yapo mengi ya namna hii. Da Mija katoa ushauri mzuri kweli. Kuyaweka kwenye kumbukumbu. Historia hujirudia kwa sababu matatizo hayatatuliwi yakaisha au historia iliyopo hupotoshwa. Kama si filamu basi kitabu. Tunaweza kusaidia tukaweka case kama zako hata kama hatutataja majina ya wahusika. Ni muhimu kumbukumbu kama hizi zikawepo.

Anonymous said...

Dah! Nilikuwa napita tu hapa, ila macho yakawa glued kwenye screen. Pole sana dada yangu, na hongera pia kwa kuwa na moyo wa namna hii. Nafahamu unavyojisikia. Mambo haya yanatokea zaidi ya watu wanavyoamua kuyazungumzia na jamii imeyaacha yafikie hali mbaya kutokana na kuwapachika majina na aibu watu wenye kukutwa na hayo mambo.
Mungu akubariki.

Anonymous said...

hi chemi,
mie ni mara ya kwanza kutembelea hii blog.
ahsante kwa kutelezea hiki kisa cha kubakwa wakati ukiwa JKT. kama ma-blogger wengine walisema, unasatahili pongezi kwa kutupa hadithi yote bila kuacha kitu. Nafikiri wakina Mama wakisoma juu ya hivi visa , wataweza kusimama na kujitetea mara wakikumbwa na matatitio kama hayo. By the way hata mie nilikuwa Msange lakini miaka minne (1990) baada yako, nilisikia sana hivyo visa vya ubakaji.
Hivi bado wewe ni mwandishi wa habari? Nafikiri Vitabu,filamu/documentary za haya matukio zinaweza kusadia akina dada wenzetu walioko nyumbani ili wawe 'aware' na haya masuala.
Ahsante sana, keep up the good work
Anonymous,Canada