Thursday, July 31, 2008

Rais Kikwete Aongea na Wananchi Leo!

Rais Jakaya Kikwete



HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO
WA TANZANIA,MHESHIMIWA JAKAYA
MRISHO KIKWETE,KWA WANANCHI,
TAREHE 31 JULAI,2008..

Ndugu Wananchi;Naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uzima na kuniwezesha kuzungumza nanyi leo mwishoni mwa mwezi wa Julai,2008.Nasikitika na nawataka radhi kwamba kwa miezi ya Aprili,Mei na Juni, sikuweza kupata fursa ya kuzungumza nanyi kupitia utaratibu wetu huu mzuri.

Sababu kubwa iliyonifanya nishindwe kuzungumza na Taifa, ni ule ukweli kwamba, tarehe za mwisho wa mwezi katika miezi hiyo zilinikuta nikiwa nje ya nchi kikazi. Safari ambazo nisingeweza kuacha kwenda labda ningekuwa nimepata dharura kubwa.

Huko nyuma katika mazingira ya namna hii nilitumia utaratibu wa kurekodi hotuba yangu kabla ya kuondoka na kuacha itangazwe siku ya mwisho wa mwezi ilipofikia. Utaratibu huo ulikidhi haja, lakini nikaambiwa kuwa haukufurahiwa sana na wengi hasa pale ilipotokea kuwa Rais wao waliyemsikia redioni leo akihutubia,walimsikia jana akiwa nchi ya mbali na wanajua hajarejea.Kwa sababu hiyo basi,nikaona kwamba nizungumze katika utaratibu huu wa mwisho wa mwezi pale tu nitakapokuwa ndani ya nchi.

Hata hivyo, uamuzi huo umezua manung’uniko yake hasa pale ambapo miezi mitatu mfululizo imetokea Rais kutozungumza kwa sababu ya kuwa nje ya nchi kikazi.Maoni ya pande zote nimeyasikia,nipeni muda nitafakari lipi bora tufanye.Ndugu Wananchi;

Ni makusudio yangu leo kuelezea matokeo ya safari zangu hizo.Mwishoni mwa mwezi wa Aprili nilikwenda Ethiopia na Uganda.Kule Addis Ababa,Ethiopia tarehe 28 Aprili,2008 nilitimiza jukumu la kushuhudia makabidhiano ya ofisi ya Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika baina ya Mwenyekiti aliyemaliza muda wake wa uongozi, Mheshimiwa Prof.Alpha Oumar Konare,na Mwenyekiti mpya Mheshimiwa Jean Ping.

Ni utaratibu uliowekwa kuwa shughuli hiyo ya makabidhiano ya ofisi husimamiwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika wa wakati huo.Nilitumia nafasi hiyo kuzungumza na uongozi mpya wa Kamisheni ya Afrika juu ya matarajio yangu na viongozi wenzangu wa Afrika kwao. Aidha,nilizungumza na wafanyakazi wa Umoja wa Afrika pamoja na kuwatambulisha viongozi wapya wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika kwao.

Siku iliyofuata niliitumia kuzungumza na Wajumbe wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika kuhusu hali ya amani na usalama ya Bara letu.Tulitumia muda mwingi kujadili migogoro inayolikabili Bara letu na hatua muafaka za kuchukua kuitafutia ufumbuzi.Tarehe 30 na 31 Aprili,2008 nilikuwa Uganda kwa mazungumzo na Rais Yoweri Museveni wa nchi hiyo.

Pamoja na kuzungumzia masuala yahusuyo nchi zetu za Afrika Mashariki na Afrika tulijadili hali ya usalama na amani ya eneo la Maziwa Makuu.Hususan tulizungumzia Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Jamhuri ya Burundi. Matokeo ya mazungumzo yetu hayo ni mambo mawili muhimu.

Kwanza, ni mkutano uliofanyika Dar es Salaam kati ya Rais Yoweri Museveni wa Uganda na Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo tarehe 11 Mei,2008.Katika mkutano huo nchi hizo mbili jirani zilifanikiwa kuzungumzia tofauti zao na kuafikiana kuhusu namna ya kuzimaliza.

Pili,kuhusu Burundi ni kufanikiwa kumrejesha Burundi Bwana Agathon Rwasa, Kiongozi wa PALIPEHUTU-FNL na viongozi wenzake waandamizi wa chama hicho. Kitendo hicho kimefunga ukurasa wa shughuli za usuluhishi wa mgogoro wa Burundi zilizotuchukua takriban miaka 13 (tangu Disemba, 2005).

Aidha, kitendo hicho sasa kimefungua njia ya kumaliza tatizo la wakimbizi wa Burundi. Wapo waliokuwa wanasita kurejea kwako kwa sababu ya viongozi kuwa nje ya Burundi. Sasa wingu hilo limeondoka. Ni matumaini yangu kuwa kasi ya wakimbizi hao kurudi kwao itaongezeka.
Ndugu Wananchi;

Mwishoni mwa mwezi Mei, 2008 nilikuwa nchini Japan kuongoza ujumbe wa viongozi wa Afrika katika Mkutano wa Nne wa Kimataifa wa Tokyo Kuhusu Maendeleo ya Afrika (TICAD IV) uliofanyika Yokohama kuanzia tarehe 27 hadi 30 Mei, 2008.

Ujumbe wa Afrika niliouongoza nikiwa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, ulikuwa na Wakuu wa Nchi na Serikali wapatao 40.Huu ulikuwa ni moja ya mikusanyiko mikubwa ya viongozi wa Afrika kwa mikutano nje ya Afrika.

Ndugu Wananchi; Mikutano ya TICAD ilianza mwaka 1993 na hufanyika kila baada ya miaka 5. Wazo la kuwa na mikutano hii liliasisiwa na Mheshimiwa Morihiro Hosokawa, aliyekuwa Waziri Mkuu wa Japan wakati ule.Madhumuni ya Mikutano hii ni kusaidia kuongeza kasi ya maendeleo ya Bara la Afrika.

Serikali ya Japan iliamua kutumia mikutano hii kuchangia nguvu zake za kiuchumi na kiteknolojia na zile za nchi rafiki zake pamoja na za mashirika ya kimataifa yanayojihusisha na masuala ya maendeleo kusaidia kukuza uchumi wa Afrika na kuboresha hali ya maisha ya watu wa Bara la Afrika. Katika mkutano uliopita wa TICAD, nchi 34 marafiki wa Japan na Afrika zilishiriki ikiwa ni pamoja na mashirika ya kimataifa 75.

Maamuzi mengi ya msingi yamefanywa na ahadi nyingi za manufaa kwa maendeleo ya nchi za Afrika na watu wake yalifanywa.Kama maamuzi hayo yaliyojumuishwa katika Tamko la Yokohama na Mpango wa Utekelezaji wa Mkutano wa Nne wa TICAD yatatekelezwa, itasaidia sana kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya Afrika kwa kasi zaidi.

Ndugu Wananchi;
Miongoni mwa maamuzi muhimu yenye maslahi kwa Afrika ni haya yafuatayo:(a) Serikali ya Japan itaongeza mara mbili misaada ya maendeleo inayotoa kwa nchi za Afrika.(b) Maeneo ya kipaumbele kwa misaada ya Japan itakuwa ni kuendeleza miundombinu hususan barabara, bandari, reli, usafiri wa anga,maji na umeme.

(c) Japan itasaidia Afrika kuongeza mara mbili uzalishaji wa mpunga.(d) Japan kusaidia Afrika kuendeleza elimu na huduma ya afya.Kwa upande wa huduma ya afya, kipaumbele kimewekwa kwenye kupambana na UKIMWI na kupunguza vifo vya watoto na kina mama kwa matatizo ya uzazi. (e) Japan kuongeza misaada kwa nchi za Afrika kukabili athari za mabadiliko ya hali ya hewa duniani au kwa neno la kitaalam tabia nchi; na(f) Kwa nia ya kukuza uwekezaji wa makampuni ya Kijapani Barani Afrika, serikali ya Japan imetenga dola 2.5 bilioni kwa ajili ya kusaidia wawekezaji wa nchi hiyo watakaowekeza Afrika.Ndugu Wananchi; Hayo ndiyo matokeo ya Mkutano wa Nne wa Tokyo kuhusu Afrika.Ni matokeo yenye matumaini makubwa kwa Afrika kwa maana mbili: Kwanza, tofauti na mikutano iliyopita, safari hii mfumo wa ufuatiliaji umetengenezwa (Follow up mechanism). Hii inatupa imani kuwa yale yaliyokubaliwa yatafuatiliwa kwa dhati.

Pili, kwa maana ya yale yaliyokubaliwa na kuamuliwa kuwa ni mambo yenye maslahi makubwa kwa nchi zetu na watu wake.

Hata hivyo,ndugu wananchi, mambo haya mazuri watayapata wale watakaoyachangamkia. Nchi zitakazopeleka mapendekezo yao ya miradi watanufaika, na wale ambao hawatafanya hivyo watakosa.Kwa kutambua ukweli huo nimeziagiza Wizara husika chini ya uongozi na uratibu wa Wizara ya Fedha na Uchumi watayarishe miradi na kuiwasilisha kwa Serikali ya Japan mapema iwezekanavyo.

Ndugu Wananchi; Wakati wa Mkutano wa TICAD tarehe 29 Mei,2008 kulifanyika mkutano maalum wa kuzungumzia tatizo la bei kubwa za chakula duniani.Nilipewa heshima ya kuwa Mwenyekiti wa mkutano huo ulioitishwa na Benki ya Dunia ikishirikiana na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO),Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo(IFAD)na Shirika la Dunia la Chakula (WFP).

Katika mkutano huo ilibainika kuwa bei za vyakula takriban katika nchi zote duniani imeongezeka mara mbili katika kipindi cha miaka mitano iliyopita na kwamba bei inatarajiwa kuendelea kupanda mwaka huu na hata mwaka ujao.Ilielezwa pia kwamba zipo sababu kadhaa zinazosababisha bei kupanda lakini kubwa zaidi ni:
(a) Chakula kilichopo kuwa kidogo kuliko mahitaji;
(b) Kupanda kwa gharama za uzalishaji kwa sababu ya kupanda sana kwa bei ya mafuta na bei ya mbolea;
(c) Mabadiliko ya hali ya hewa duniani kunakosababisha ukame na mafuriko ya mara kwa mara siku hizi; na
(d) Kupungua kwa kilimo cha nafaka kwa sababu ya kilimo cha mazao ya kuzalisha nishati.
Ndugu Wananchi; Kwa kauli moja mkutano umekubaliana kuwa kwa upande wa Afrika suala la msingi ni kuwasaidia wakulima wa Afrika waongeze tija kwenye kilimo.Hili likifanyika Afrika inao uwezo siyo tu wa kujilisha wenyewe bali pia wa kulisha watu wengi wengine duniani.Mkutano ulipongeza juhudi zinazoendelea kufanywa na mashirika hayo manne ya kimataifa kusaidia nchi za Afrika kuendeleza kilimo.

Aidha, wito ulitolewa kwa nchi zilizoendelea na mashirika ya fedha ya kimataifa kuunga mkono jitihada hizo zikiwemo zile za kuwawezesha wakulima wadogo wadogo kupata mbegu bora, mbolea na mikopo.

Nafurahi kwamba tangu mkutano ule kuna utambuzi mkubwa zaidi na vuguvugu la kuwasaidia wakulima wadogo wa Afrika limeongezeka. Na, sisi kiserikali tumeshaomba Tanzania ijumuishwe katika jitihada hizo.Tunasubiri majibu. Iwapo tutafanikiwa kujumishwa na kupatiwa misaada tuliyoomba, matatizo ya sasa ya upatikanaji wa mbegu, mbolea na mikopo kwa wakulima wadogo yatapungua.

Ndugu Wananchi; Nafurahi pia kwamba tarehe 7 Julai,2008 nchi yetu ilipewa heshima nyingine kubwa ya kuongoza ujumbe wa Marais saba wa Afrika kwenye Mkutano wa Mataifa Manane yenye Viwanda Vingi Duniani (G-8).Mataifa hayo hukutana kila mwaka kujadili hali ya uchumi wa dunia na mwelekeo wake.

Kwa mwaka huu wa 2008, nchi hizo zilikutana huko Hokkaido nchini Japan mwanzoni mwa mwezi huu.Mimi na viongozi wenzangu wa Algeria, Senegal,Ghana,Afrika Kusini,Nigeria na Ethiopia tulitumia fursa hiyo kuelezea matatizo yanayolikabili Bara la Afrika na kusisitiza haja ya wajibu wa nchi zilizoendelea zikiongozwa na Kundi la Nchi Nane zenye viwanda vingi duniani, kuzisaidia nchi za Afrika kuondokana na umaskini uliokithiri na kuwa nyuma kwa kimaendeleo. Tulisisitiza kama tulivyofanya katika mkutano wa Nne wa TICAD haja ya kuongeza misaada ya maendeleo kwa Afrika.

Tuliwakumbusha viongozi wa G-8 kuhusu ahadi yao walioitoa kwenye mkutano wao wa Gleneagles mwaka 2005 kuhusu kuongeza misaada ya maendeleo kwa Afrika. Tumewataka watekeleze.

Aidha, kuhusu vipaumbele,tulisisitiza umuhimu wa kuongeza misaada inayotolewa kuendeleza miundombinu barani Afrika, kwani maendeleo hayatawezekana bila barabara nzuri, bandari, usafiri wa anga,umeme,maji na mawasiliano.Tuliitumia nafasi hiyo kuwasilisha kilio chetu kuhusu matatizo ya kupanda sana kwa bei za chakula na mafuta ya petroli duniani na athari zake kwa watu wa nchi zinazoendelea za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara.Tumeelezea kwa kina athari zake na hasa tishio la kufuta mafanikio kiasi yaliyopatikana na kurudisha nyuma jitihada za kujiletea maendeleo.

Tuliowaomba Wakubwa hao wafanye kila wawezalo kuzuia kupanda holela kwa bei za mafuta na kuzisaidia nchi maskini na zinazoendelea za Afrikakukabili athari za kupanda kwa bei ya mafuta na bei ya chakula. Kama tulivyosema kwenye Mkutano wa TICAD na katika mkutano wa G-8 nako tuliomba kwa upande wa tatizo la upungufu wa chakula,nguvu zielekezwe kwenye kusaidia nchi zetu kufanya mageuzi ya kilimo na siyo kwenye kupewa misaada ya chakula pekee. Ujumbe wetu ulipokelewa vizuri na kuahidiwa kusaidiwa.Tunachosubiri sasa ni kuona vitendo.

Tutaendelea kufuatilia na kukumbushia bila ya kuchoka.Ndugu Wananchi; Mwishoni mwa mwezi wa Sita sikuweza kuzungumza na taifa kwa sababu ya kwenda Misri kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika.Ulikuwa mkutano mgumu kwa kiasi chake, hasa kwa mie niliyekuwa Mwenyekiti.Hata hivyo,nilifurahi kuwa hatimaye mambo yaliisha vizuri hata kuliko tulivyotarajia.

Nilifurahi sana pale rai yangu ya kujipa muda wa kutosha wa kujadili masuala ya maendeleo ya Afrika ilipokubaliwa.Niliomba hivyo kwa sababu tumekuwa na mazoea ya kutumia muda mwingi kujadili masuala ya siasa na migogoro.Watu wan chi zetu hawakuishi kwa siasa pekee. Safari hii tulijipa muda wa kutosha kujadili masuala ya maendeleo ya Afrika. Kuendeleza rasilimali maji na utekelezaji wa malengo ya Milenia barani Afrika yalikuwa ndiyo mambo makubwa yaliyotuchukulia muda mwingi.Kwangu mimi kutoa nafasi stahiki kuzungumzia masuala ya maendeleo ya nchi zetu na watu wake ni hatua kubwa ya maendeleo kwa Umoja wa Afrika. Hili ni jambo la faraja sana na nimeeleza matumaini yangu kuwa utaratibu huu tutaudumisha na kuuendeleza.

Ndugu Wananchi;
Kwa upande wa siasa na migogoro, mambo mawili yalichukua muda mwingi wa mjadala kwenye mkutano wetu. Mambo hayo ni:
(a) Uanzishaji wa Serikali ya Umoja wa Afrika.
(b) Mgogoro wa Zimbabwe. Nafurahi kwamba pamoja na ugumu wa mijadala lakini hatimaye tulielewana vizuri kuhusu nini cha kufanya. Kuhusu Serikali ya Umoja ya Afrika tumekubaliana kuhusu viashiria na vichocheo vya kuwezesha Serikali hiyo kuwepo. Hata hivyo, hatukuweza kuelewana kuhusu lini Serikali hiyo inaweza kuundwa na muundo wake. Bado kuna tofauti kubwa za mawazo miongoni mwetu. Tumekubaliana tuendelee kulizungumza suala hilo kikao kijacho.

Kuhusu Zimbabwe, tulikubaliana kuwa,pamoja na kasoro zilizojitokeza wakati wa mchakato wa uchaguzi na kutia dosari kwa uhalali wake,bado jawabu litapatikana kwa pande husika kukaa chini na kuzungumza.Nafurahi kwamba yale tuliyoamua yafanyike yameanza kutekelezwa. Mchakato huo umeanza.Tuwatakie kila la heri ndugu zetu wa Zimbabwe mazungumzo yakamilike salama na nchi yao irejee katika hali yake ya kawaida na wananchi wa nchi hiyo waanze kazi ngumu ya kujenga upya taifa lao.

Ndugu Wananchi; Katika kipindi cha miezi mitatu hii ambayo sikupata nafasi ya kuzungumza na taifa. Kumekuwepo na matukio kadhaa hapa nchini yaliyogusa maisha,nyoyo na hisia za watu kwa namna mbalimbali.Yalikuwepo mambo mazuri,yalikuwepo mambo magumu na hata ya huzuni na majonzi.
Aidha,yalikuwepo mambo yaliyoleta mtikisiko kwa jamii na hata kwa taifa na utaifa wetu. Kwa vile mambo ni mengi kiasi sitapata nafasi ya kuyazungumzia yote moja baada ya jingine.Napenda kuitumia nafasi hii kuwatoa wasiwasi na kuwahakikishia Watanzania wenzangu kuwa, taifa letu bado ni moja na watu wake bado ni wamoja.

Tofauti za mawazo na fikira miongoni mwetu hazitakosekana.Naomba tuyaone mawazo na fikira hizo kuwa changamoto za kushughulikia katika kuimarisha umoja wa taifa letu na mshikamano wa watu wake.Napenda kuwahakikishia kuwa sisi viongozi wenu tunayatambua hayo na tunayashughulikia. Hakuna kubwa la kutuzidi kimo na kwamba hakuna litakaloharibika. Kwa vile nia yetu ni njema na penye nia pana njia sina shaka mambo yatakuwa sawa.Nawaomba tuwe watulivu kwani utulivu wetu ni sehemu ya jawabu.Ni imani yangu kuwa kila anayeitakia mema nchi yetu atafanya hivyo.

Ndugu Wananchi;

Jambo la mwisho ambalo ningependa kuliongelea leo linahusu msiba uliotukuta wa Mbunge wa Tarime, Marehemu Chacha Wangwe.Kifo chake cha ghafla kimetushtua na kutusikitisha wengi. Marehemu alikuwa mtu muwazi na mkweli.Hakuwa na woga wa kutoa maoni yake kwa jambo analoliamini. Hakika Bunge,Jimbo la Tarime na Taifa limepoteza mwakilishi wa kutumainiwa. Daima atakumbukwa kwa sifa zake hizo na mchango wake huo kwa taifa.

Ndugu Wananchi;
Napenda kuitumia nafasi hii kutoa mkono wa pole na rambirambi kwa familia na ndugu wa marehemu.Naelewa machungu mliyonayo.Mimi na Watanzania wote wenye nia njema tuko pamoja nanyi katika msiba huu mkubwa uliowakuta. Ni msiba wetu sote na ni machungu yetu sote.

Nawapa pole sana Wabunge wote wa Bunge letu tukufu kwa kupoteza mwenzi wenu na rafiki yenu. Nawapa pole viongozi na wanachama wa Chama cha CHADEMA kwa kupoteza kiongozi wenu mahiri.Wananchi wenzangu wa Jimbo la Tarime nao nawapa pole kwa kupoteza mwakilishi na mtetezi wenu shupavu.Tuzidi kumwombea kwa Mwenyezi Mungu ampe mapumziko mema.Hitimisho

Ndugu Wananchi;

Kwa mara nyingine tena nawashukuru tena kwa msaada wenu na ushirikiano wenu. Mimi na wenzangu mliotupa dhamana ya kuliongoza taifa letu tutaendelea kuwatumikia kwa nguvu na uwezo wetu wote ili tufikie kwenye dhamira yetu ya kuharakisha maendeleo ya nchi yetu.
Kwa pamoja tutashinda.Mungu Ibariki TanzaniaMungu Ibariki Afrika.

Asanteni kwa kunisikiliza.

Fujo kwenye Mazishi ya Wangwe - FFU waingilia!

Mdau Jacob Mugini kamletea Kaka Michuzi picha hizi sasa hivi kuonesha hali ilivyokuwa huko tarime kwenye mazishi ya hayti chacha wangwe. Juu ni meza kuu ambapo viongozi wa vyama vya siasa wakiwa wameketi, na chini ni baadhi ya waombolezaji. Duh, naona walikuwa roho juu juu hapo!

Na Mwandishi wa Globu ya Jamii, Tarime

Mazishi ya Mh. Chacha Wangwe, aliyekuwa Mbunge wa Tarime aliyefariki dunia kwa ajali ya gari majuzi huko Dodoma, yameshindwa kufanyika leo kijijini kwake Kamokorere baada ya kufumuka kwa vurugu kubwa ambapo wabunge na viongozi wa serikali na vyama vya siasa walohudhurian ilibidi watoke bomba kusalimisha maisha yao.

Vurugu hiyo ilianza dakika chache baada ya kuwasili kilioni hapo kwa Mwenyekiti wa Taifa wa CHADEMA, Mh. Freeman Mbowe, katika kijiji cha Kemokorere kiasi cha kilomita 20 hivi toka mjini Tarime.

Hali ilipokuwa mbaya, ilibidi Mh. Mbowe na viongozi wote waliohudhuria mazishini waondolewe kilioni chini ya ulinzi mkali wa FFU ukiongozwa na Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Mara Afande Leberatus Barlow ambao walifanya kazi ya ziada kuepusha balaa.
Viongozi wengine waliohudhuria walikuwa ni pamoja na wenyeviti wa vyama vya upinzani Profesa Ibrahim Lipumba (CUF), Augustino Lyatonga Mrema (TLP), John Cheyo (UDP) James Mbatia (NCCR-Mageuzi) na Mbunge wa Karatu Mh. Wilbroad Slaa pamoja na kiongozi wa upinzani bungeni, Mh. Hamad Rashid.

Wote hao walisindikizwa chini ya ulinzi mkali wa FFU kuondoka mahali hapo na kuelekea Musoma. Waziri wa Kilimo na Umwagiliaji, Mh. Steven Wassira, na Manaibu Mawaziri ambao ni wabunge wa Kanda ya Ziwa, Dr. James Wanyacha na Gaudensia Kabaka nao ilibidi waondoke.
Ujumbe toka Kenya ulioongozwa na Dr Wilfred Machage ambaye ni mbunge wa jimbo la Kurya na pia Naibu Waziri katika serikali ya mseto ya Kenya pamoja na wakuu wa wilaya wawili nao walikuwepo na ilibidi waondoke kwa kuruka ukuta.

Tofauti na walivyoingia, itifaki haikuweza kufuata kama walipowasili wabunge 20 wakiongozwa na mbunge wa Bumburi Mh. William Lukindo vurugu hilo lilipoanza na ilibidi kila mmoja aondoke chini ya ulinzi mkali.

Maelfu ya waombolezaji, wengi wao wakiwa vijana waliobeba mabango yenye ujumbe mbalimbali unaohoji kifo cha Mh. Wangwe, walitawala hapo kilioni. Juhudi za Mkuu wa mkoa wa Mara Mh. Issa Machibya kuwatuliza hazikuzaa matunda.

Hata juhudi za kututuliza ghasia hizo za Wah. Zitto Kabwe na mmoja wa wanafamilia waandamizi kama vile Profesa Samwel Wangwe na Mkuu wa zamani wa Halmashauri ya Tarime Mh. Peter Wangwe pia hazikuambulia kitu.

Prof Wangwe aliwaambia waombolezaji hao wenye hasira kwamba familia ya Wangwe imeamua kumtafuta mtaalamu huru kuifanyia upya uchunguzi maiti ya hayati Chacha Wangwe ili kubaini alifariki kwa njia ipi.

Wengi ya waombolezaji wanatuhumu kwamba Mh. Wangwe hakufa kwa ajali ya gari. Mtu moja aliyekuwa na marehemu wakati wa ajali, Bw. Mallya, anahojiwa na polisi na uchunguzi wa kina unaendelea.
****************************************************
VURUGU zilizuka katika maziko ya Mbunge wa Tarime, Chacha Wangwe, pichani,baada ya ndugu wa marehemu kugoma kuzika mwili wake wakidai hawajaridhika na maiti yao ambayo wanadai kuwa ina tundu la risasi.

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, alinusura kujeruhiwa kwa kumrushia mawe na wengine wakitaka kumkata kwa mapanga na aliokolewa kwa juhudi za ziada za polisi. Kabla ya tafrani hiyo kuzuka, ndugu wa marehemu waliigomea Serikali kumzika Mbunge huyo wakisema hadi uchunguzi mpya ufanyike waweze kujiridhisha kuhusu chanzo cha kifo hicho.

Ratiba ya maziko hayo ilikuwa ianze saa 7 mchana, lakini kuanzia saa tatu asubuhi, ukoo wa Wangwe ulikaa chini ya mwenyekiti wake Profesa Samwel Wangwe na kutoa uamuzi wa kutozikwa marehemu hadi daktari wa familia kutoka Dar es Salaam atakapofika na kuufanyia uchunguzi upya.

Mwenyekiti wa Chadema, Mbowe alifika katika msiba huo saa nane mchana akiwa amefuatana na viongozi wengine wa vyama vya siasa ndipo ghafla vijana walipotoa mabango yaliyokuwa yamebeba ujumbe mbalimbali wakipinga kuwa kifo cha Wangwe ni mipango ya Mungu.
“Hatutaki sura ya Mbowe tunataka mbunge wetu,” walisikika wakisema vijana hao ambao walikuwa tayari kutaka kumpiga mwenyekiti huyo wa Chadema, wakidai kuwa chama chake kimehusika katika kifo cha Wangwe,baadaye wengine walitoa mapanga na mikuki, hali iliyowalazimu polisi kumchukua Mbowe na kumwingiza ndani ya nyumba ambako walikuwa wamekaa wabunge wengine 20.

Kuona hivyo vijana wengine walianza kurusha mawe kuwaelekezea viongozi hao. Viongozi hao kuona hivyo walitimua mbio wakihofia maisha yao. Baadhi ya viongozi waliotimua mbio pamoja na Mbowe ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Salehe Ramadhan Feruzi, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbrod Slaa, Zitto Kabwe ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Mwenyekiti wa CCM Mkoani Mara, Makongoro Nyerere na Mjumbe wa NEC wa CCM wa mkoa wa Mara, Christopher Gachuma.

Kipanya Leo


Translation:
On the left Blackboard - Corruption On the right Blackboard - In Zanzibar a country?
Teacher - So...
Kipanya (Rat Character) - Hey Teacher, Tell them that Zanzibar is not just a country it's a continent. ..and they should have have a reggae version of their natonal anthem if they like... but please lets get back to the real troubling issues!

Wednesday, July 30, 2008

Conspiracy Theories - Kifo cha Chacha Wangwe!

Gari aliokuwa anaendesha marehemu Chacha Wangwe katika eneo la ajali (picha za ajali kwa hisani ya Mpoki Bukuku)

Rais Jakaya Kikwete akimwaga marehemu Chacha Wangwe (picha kutoka Lukwangule blog)
**********************************************

Tangu tupate habari ya kifo cha mwana mpinzani, Chacha Wangwe, tumekuwa tukisikia maneno hapa na pale. Mara kajiua, mara kauliwa na Chadema, mara kauliwa na CCM....jamani! Rest in Peace Chacha Wangwe. Politics is a dirty game!

Soma habari zaidi kwa Dr. Faustine:

Spika wa Bunge amlilia Wangwe!

Kutoka ippmedia.com

Spika amlilia Wangwe

2008-07-30

Na Waandishi Wetu Dar es Salaam , Dodoma

Spika wa Bunge, Bw. Samuel Sitta, jana aliangua kilio kwa sauti ya juu wakati akitangaza kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Tarime kupitia CHADEMA, Bw. Chacha Wangwe.

Kilio cha Spika, kilisababisha baadhi ya Mawaziri na Wabunge kuangua vilio huku nyuso za wengine zikiwa zimejaa huzuni. Spika Sitta alilia baada ya kumalizia kutoa matangazo kuhusu kifo hicho. Alisema ajali iliyomuua Mbunge huyo ilitokea juzi saa 2:55 usiku wakati akiendesha gari lake aina ya Toyota Corolla akitokea Dodoma kuelekea Dar es Salaam.

Alisema Bw. Wangwe, alikuwa ameongozana na rafiki yake, Bw. Deus Mallya, ambaye alinusurika na sasa amelazwa katika hospitali ya Mkoa wa Dodoma kwa matibabu. Kwa mujibu wa Spika, ajali hiyo ilitokea katika kijiji cha Pandambili, kilomita 100 kutoka mjini Dodoma.

Alisema gari hilo liliacha njia na kugonga miti kadhaa iliyopo pembeni mwa barabara kabla halijabingirika na kuanguka. Kufuatia kifo hicho, Spika Sitta aliahirisha Bunge jana saa 3:10 asubuhi hadi saa 6:00 mchana ili Kamati ya Uongozi wa Bunge na Tume ya Maadili iweze kuwasiliana na familia na kuweka mipango ya mazishi. Saa 6:00 mchana, Spika alitoa matangazo ya ratiba ya kuaga mwili wa marehemu na mazishi yatakayofanyika kesho huko Tarime mkoani Mara.

Spika aliahirisha Bunge kwa siku nzima ya jana kwa kutumia kanuni ya 149 inayosema kama Mbunge akifariki, Bunge linatakiwa kuahirishwa kwa siku nzima. Rais Jakaya Kikwete alifika mjini Dodoma jana na kuongoza Mawaziri na Wabunge kuaga mwili wa marehemu Wangwe Bungeni kuanzia saa 10:15 jana jioni. Leo asubuhi mwili wa marehemu utasafirishwa kwa ndege maalum kuelekea Tarime ukiwa na familia yake na Wabunge wawili.

Spika Sitta alisema kesho asubuhi (Alhamisi) Wabunge 20 wanaowakilisha Bunge kwenye mazishi hayo wataondoka Dodoma asubuhi kuelekea Tarime kwa ndege maalum ili kuhudhuria mazishi na watarejea Dodoma jioni. Kabla ya kifo hicho, Bw. Wangwe alikuwa awasilishe Bungeni hoja binafsi kuhusu mapigano ya kikabila na wizi wa mifugo lakini alishindwa kufanya hivyo kutokana ratiba kutoruhusu kufanya hivyo.

Nipashe ilipotembelea nyumbani kwa marehemu eneo la Kisasa nje kidogo ya mji wa Dodoma saa 4:00 asubuhi ilikuta Mawaziri, Wabunge na majirani wakiwa wanaomboleza.

Mmoja wa watoto wa marehemu, Zakayo Chacha (18), alisema tangu juzi baba yake alikuwa akisumbuliwa na malaria. Alisema baba yake alilazimika kusafiri kwenda Dar es Salaam ili kuhudhuria mazishi ya mwanasiasa wa zamani, marehemu Bhoke Mnanka aliyefariki dunia mwishoni wa wiki iliyopita.

``Ingawa alisafiri, lakini alikwenda hospitali kupima na kukutwa na malaria, siku moja kabla ya safari hiyo, alimeza dawa mseto za malaria hali iliyosababisha aamke kwa taabu na uchovu kabla ya safari hiyo,`` alisema.

Alisema awali walipoanza safari, gari hilo liliharibika nje kidogo ya mji wa Dodoma na kulazimika kurudi mjini kwa matengenezo. Alisema hali hiyo ilisababisha wachelewe kuanza safari na ilipofika saa 3:00 juzi usiku, ndipo wakapokea taarifa za kifo hicho.

Kwa mujibu wa Bw. Zakayo, marehemu ameacha wake wawili na watoto 10. Wakati huo huo, Rais Jakaya Kikwete, jana aliwaoongoza Mawaziri, Wabunge na viongozi mbalimbali wa serikali kuuaga mwili wa marehemu Chacha Wangwe.

Mwili huo uliwasili katika eneo la Bunge saa 11.00 jioni na kupokewa na Wabunge huku Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA), Bw. Zitto Kabwe akiwa amebeba msalaba. Akitoa salamu za marehemu, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Bw. Hamad Rashid Mohamed alisema tukio hilo ni pigo kubwa mno.

Alisema kambi ya upinzani ina wabunge 45 ambapo wawili kati yao, wamewatoka akiwemo aliyetolewa na Mahakama na mwingine ni marehemu Wangwe. Aliongeza kuwa, enzi za uhai wake wakati akianza Bungeni, Wangwe alikuwa Waziri Kivuli wa Maji na kwamba hadi mwisho wa uhai wake, alikuwa Waziri Kivuli wa Mazingira.

Bw. Hamad alimsifia marehemu kuwa mtetezi mkubwa wa masuala ya wananchi na wapiga kura wake wa Tarime. Hata hivyo, alisema hoja ya Wangwe itashughulikiwa na kambi ya upinzani. Waziri Mkuu, Bw.Mizengo Pinda , akiwasilisha salamu za rambirambi kwa niaba ya serikali alisema hadi sasa Bunge limepoteza wabunge watano tangu kuanza kwa awamu ya nne na kwamba ni dhahiri si jambo ambalo wanalichukulia kwa wepesi.

Alitoa pole kwa ndugu zake akiwemo kaka yake Profesa Samwel Wangwe, familia, Spika na Kamati ya Uongozi ya Bunge . Spika wa Bunge Bw. Samuel Sitta, akiwasilisha salamu za Bunge alimsifu marehemu Wangwe kuwa alikuwa jasiri, aliyetetea hoja zake kwa nguvu kwa kila alichokiamini bila kujali.

Alisema alijiamini na alikuwa hodari wa kusema kwa ujasiri mkubwa kila alichokiamini bila kujali kuwa lile analosema lingeweza kumfanya atofautiane na wenzake. Alisema Bunge limepoteza mtu ambaye anahitajika sana bungeni, jimboni na serikalini na taifa zima.

Kaka yake marehemu, Profesa Samuel Wangwe alitoa salamu za shukurani kwa niaba ya familia na kulishukuru Bunge kwa kugharamia msiba wa ndugu yao. Naye Bw. Deus Malya, ambaye alinusurika, alisema kabla ya ajali hiyo, Wangwe ambaye alikuwa akiendesha gari hilo, alimtaka ahame kiti cha mbele na kukaa cha nyuma.

Akizungumza na PST katika wodi ya wagonjwa daraja la kwanza alikolazwa, Bw. Malya, alisema Wangwe alimwambia asikae kiti cha mbele kwa vile sio salama kwake na kumtaka akae kiti cha nyuma.

Alisema baada ya kuambiwa hivyo, alihamia kiti cha nyuma na baada ya kama kilomita 20, ndipo ajali hiyo ilipotokea na Wangwe kupoteza maisha. Akisimulia mwanzo wa safari hiyo, Bw. Malya, alisema saa 2:00 asubuhi, alimsindikiza Wangwe bungeni lakini alimweleza kwamba, alikuwa akijisikia kuumwa.

Alisema, hata hivyo hakufahamu kama alikunywa dawa yoyote, isipokuwa ilipofika mchana, alirudi naye nyumbani na kupata chakula cha mchana, kisha akapumzika kidogo. Bw. Malya, alisema ilipofika saa 9:00 alasiri, walianza safari ya kuelekea Dar es Salaam, lakini walipofika kama kilomita 20 hivi nati za tairi la kushoto upande wa dereva, zililegea na wakaamua kusimama na kuzikaza.

Alisema baada ya kurudi gereji, walitengeneza gari na ilipofika saa 12:30 jioni, Wangwe alipitia nyumbani kuchukua `chaji` ya simu. Akizungumzia jinsi ajali hiyo ilivyotokea, Bw. Malya alisema, alisikia kishindo kikubwa na baadaye kutimka vumbi nyingi iliyomfanya ashindwe kuona mbele.


Alisema kilichofuatia ni gari hilo kuserereka umbali wa kama mita 50 kutoka barabarani na kisha kubiringika mara kadhaa. ``Baada ya hapo, sikuweza kutambua chochote na niliposhituka nikamkuta Wangwe akiwa amelala pembeni yangu huku kiti chake alichokuwa amekalia kikiwa kimenibana,`` alisema. Bw. Malya, ambaye ameteguka mguu wa kushoto na kuumia kidogo katika paji la uso karibu na jicho la kulia, alisema kila kitu walichokuwa nacho katika gari, yakiwemo mabegi ya nguo, Laptop na vitu vingine, viliibiwa.


Bw. Malya, alisema alifahamiana na marehemu tangu mwaka 2003 walipokutana jijini Dar es Salaam ambapo kuanzia hapo walianza kushirikiana katika mambo mbalimbali. Alisema kwa jinsi gari lilivyopondeka hasa sehemu za mbele alikokuwa amekaa, kama asingehama, bila shaka asingeweza kupona katika ajali hiyo.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk. Godfrey Mtei, alisema hali ya majeruhi huyo inaendelea vizuri na baada ya siku mbili ataruhusiwa. Baadhi ya wabunge ambao walizungumza na marehemu Wangwe juzi kabla ya kufikwa na umauti, walisema alionekana mnyonge wakati wote.

Mbunge wa Muhambwe (CCM), Bw. Felix Kijiko, alisema alimkuta Wangwe katika mgahawa wa Bunge akiwa hana furaha kama siku zote. ``Nilimuuliza mheshimiwa mbona sijakuona siku kadhaa bungeni, akanieleza kuwa, alikuwa na mambo kadhaa yaliyokuwa yakimtatiza, lakini wakati huo, hakuwa anakula chochote,`` alisema.

Alisema baada ya hapo, alimweleza kuwa atamwambia kinachomsumbua muda si mrefu. Kwa upande wake, Mbunge wa Mchinga (CCM) Bw. Mudhihir Mudhihir ambaye alizungumza naye kwa mara ya mwisho kabla ya kuanza safari katika viwanja vya Bunge, alisema alipokutana na Chacha hakuwa na hali ya kawaida ya uchangamfu aliyoizoea siku zote na alipojaribu kumdadisi zaidi, hakuweza kubainisha ni kwa nini yuko katika hali hiyo.


Kwa upande wake mbunge wa Bariadi Mashariki (UDP), Bw. John Cheyo, alisema kambi ya upinzani imempoteza mtu muhimu mno na pengo lake kamwe halitazibika. ``Alikuwa ni mtu mpambanaji, hakuogopa kitu kusema kweli, aliwatetea wananchi wake bila woga...kwa kweli kifo chache sio pigo kwa kambi ya upinzani pekee, bali ni pigo kubwa kwa wananchi wa Tarime,`` alisema.

Mbunge wa Same Mashariki (CCM), alisema Wangwe alikuwa mpiganaji mkubwa wa haki za wananchi wake, pia alikuwa anashirikiana na kila Mbunge bila kujali itikadi za chama.

Naye Waziri Mkuu, Bw. Mizengo Pinda, ambaye alionekana wazi kujawa na simanzi, hakuweza kuzungumza na waandishi wa habari waliokuwa wamemzonga wakitaka kusikia neno kutoka kwake, alizungumza neno moja tu kuwa, ``Chacha alikuwa rafiki yangu.`` Na katika hatua nyingine Rais Kikwete ametuma salamu za rambirambi kwa Spika wa Bunge, kufuatia kifo cha Mbunge wa Tarime (CHADEMA), Bw. Chacha Wangwe, aliyefariki juzi kwa ajali ya gari.

Katika salamu hizo, Rais Kikwete, alisema amepokea habari hizo kwa masikitiko na majonzi makubwa. Aidha, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kimepokea kwa masikitiko makubwa kifo Bw. Wangwe. Taarifa iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam, na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa kituo hicho, Bw. Francis Kiwanga, ilisema inatambua mchango mkubwa uliotolewa na marehemu Wangwe katika kuimarisha demokrasia nchini.

Alisema marehemu Wangwe alikuwa mpigania haki sio tu za wananchi wa jimbo lake bali hata kwa Taifa lote. Alisema marehemu Wangwe alikuwa mstari wa mbele kutetea maslahi ya wananchi bungeni na kuchangia hoja nzito akishirikiana na wabunge wengine na kukifanya chombo hicho cha wananchi kuwa mhimili imara.

Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa CCM, Bw. Yusuf Makamba, amesema chama kimepokea kwa masikitiko makubwa kifo cha mwasisi wa TANU na CCM, Bw. Bhoke Munanka. Taarifa ya Idara ya Itikadi na Uenezi ya CCM, ilisema marehemu Munanka aliyefariki Julai 25 aliwahi kuwa mweka hazina wa TANU pamoja na kushika nyadhifa mbalimbali kama uwaziri katika serikali ya awamu ya kwanza chini ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

SOURCE: Nipashe

Tuesday, July 29, 2008

Ana Miguu Sita!

Maskini sijui huyo deer (aina ya kongoni) anatembeaje. Wiki iliyopita aling'atwa na mbwa wawili, nadhani walikuwa wanashangaa ni mnyama wa aina gani. Alizaliwa na mikia miwili na miguu sita huko Georgia, USA.

Hivi sasa analelewa na wapenzi wa wanyama huko Georgia


***************************************
Six-legged fawn is recovering at West Rome Animal Clinic in Rome, Ga. after sustaining minor injuries this weekend from two dogs in Everett Springs, Goergia. Due to the injuries, one of its two tails had to be amputated. The fawn has two distinct pelvises and uses one leg from each pelvis to walk seen Monday, July 21, 2008. (AP Photo)

Tanzia - Chacha Wangwe (Mbunge Chadema)


Mbunge wa Tarime kupitia chama cha CHADEMA Mh. Chacha Wangwe(Pichani) amefariki dunia usiku huu kwa ajali ya gari ilitotokea sehemu ya Kongwa Mkoani Dodoma. Alikuwa analekea Dar es Salaam kwenye msiba wa Mzee Bhoke Munanka.

Mungu ailaze Roho ya Marehemu Mahala Pema Mbinguni. Amen.
***********************************************************
Kutoka Habari Leo (Daily News)

Wasifu wa Wangwe

MAREHEMU Chacha Zakayo Wangwe alizaliwa Julai 15,1956. Nyumbani kwao ni Kijiji cha Kyamakorere,umbali wa kilomita 20 kutoka Tarime Mjini.

Alipata elimu ya msingi katika shule za Rosana na Magoto kati ya mwaka 1962 na 1968 kabla ya kujiunga na elimu ya sekondari katika Shule ya Nyaroha.Baadaye alihamia Dar es Salaam na kujiunga na Sekondari ya Kinondoni Muslim ambako alimaliza kidato cha nne mwaka 1974. Alisoma kidato cha tano na sita katika Sekondari ya Mkwawa kati ya 1975 na 1976.

Alijiunga na masomo ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1978, lakini hakumaliza. Aliwahi kufanya kazi na Benki ya NBC,Shirika la Kujitolea la Ujerumani,Kampuni ya Lacop na Mgodi wa Dhahabu wa Afrika Mashariki.

Kisiasa amewahi kushika nyadhifa mbalimbali ukiwamo uenyekiti wa tawi la vijana wa Tanu katika sekondari ya Mkwawa,Mwenyekiti wa Wilaya wa Chadema,Tarime,kati ya 1994 na 1998 kabla ya kujiunga na NCCR-Mageuzi ambako alikuwa Mwenyekiti wa Mkoa kati ya 1998 hadi 2000,lakini akarejea tena Chadema mwaka 2002 na kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Mkoa wa Mara wa chama hicho.

****************************************************************************

SALAMU ZA RAMBIRAMBI kutoka kwa Rais Kikwete


Mheshimiwa Spika,Nimepokea taarifa ya kifo cha Mbunge wa Tarime, kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo, (CHADEMA) Mheshimiwa Chacha Zakayo Wangwe kwa masikitiko makubwa.

Kupitia kwako, napenda unifikishie rambirambi zangu za dhati kwa wabunge wa Bunge lako Tukufu kwa kumpoteza mbunge mwenzao katika kipindi hiki ambacho wako katika kutekeleza majukumu yao waliyotumwa na Watanzania, ya uwakilishi.

Kwa masikitiko makubwa napenda kutoa salamu zangu za pole kwa wana familia, ndugu, wananchi wa Jimbo la Tarime, wanachama wa Chama cha Maendeleo na Demokrasia (CHADEMA) na Watanzania wote.

Kifo huleta masikitiko na majonzi mengi katika familia na jamii, naungana nanyi ndugu zanguni katika kipindi hiki kigumu cha majonzi na maombolezo, Mwenyezi Mungu awape imani na subira katika kipindi hiki kigumu na huku tukimuombea ndugu yetu, Chacha Wangwe mapumziko mema peponi. Amina.

Bagamoyo Beach



Picha kutoka Maggid Mjengwa blog

Nimeona hii picha hii kwa kaka Mjengwa. Aliipiga Bagamoyo beach hivi karibuni. Kweli TV na sinema zinasababisha mabadiliko katika jamii. Miaka ya nyuma usingeweza kukuta wapenzi wakiongea hivyo hadharani. Au siyo? Lakini ni jambo la kawaida kuonyesha mapenzi hadharani katika video na sinema. Watu wameiga. Kwenye giza ni mambo mengine lakini.

Hivi mnakumbuka enzi za censorship Bongo? Enzi za Mwalimu na kabla ya TV kuingia 1993. Yaani kabla ya kuona sinema, Tanzania film company wanafuta busu, na mambo mengine ya mapenzi. Scene ya mapenzi inakatwa! Kweli walikuwa tuchunga kweli. Hata magezeti na vitabu vya mapenzi yalikuwa marufuku. Mmewahi kusoma kitabu cha After 4:30? Labda ganda ilitolewa na kuwekwa brown paper!

Lakini watu walikuwa wanapendana na kufanya mapenzi!

Monday, July 28, 2008

Yanga - Rest in Peace

Upinzani kati ya timu za soka, Simba na Yanga ni kali sana huko Bongo. Yaani nakumbuka watu wamepigana na hata ajali za gari na vifo zimesabishwa na upinzani huo. Lakini si mchezo jamani? Kwa nini watu wanachukulia 'serious'?

Hebu cheki washabiki wa Yanga walivyowatania timu ya Yanga leo! Wamebeba jeneza la Yanga! DUH!

*********************************************************
Kutoka Michuzi Blog:



Yanga yafungiwa miaka 3, na faini dola 35,000

KLABU ya Yanga imefungiwa kushiriki michuano inayoandaliwa Shirikisho la vyama vya soka vya nchi za Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) kwa miaka mitatu sambamba na kupigwa faini dola za Kimarekani 35,000 kutokana na kugomea mchezo wa kuwania nafasi ya mshindi wa tatu ya michuano ya kombe la Kagame.

Akitangaza uamuzi huo uliofikiwa na kikao cha kamati ya uendeshaji wa michuano hiyo ya Kagame jana usiku mara baada ya michuano hiyo kukamilika, Katibu Mkuu wa Cecafa, Nicolas Musonye alisema mbali na adhabu hiyo ya kufungiwa pia Yanga imepigwa faini hiyo ambayo inatakiwa kulipwa katika kipindi kifupi iwezekanavyo.

Musonye ambaye alikuwa akizungumza huku akionyeshwa kukerwa mno na kitendo hicho cha Yanga kugomea mchezo huo, alisema jambo walilofanya Yanga ni kitendo cha aibu na ndio maana wameamua kuchukua hatua hiyo ili iwe onyo na fundisho kwa timu nyingine.

"Adhabu hii haina suala la kukata rufaa na adhabu hiyo itakuwa ikitekelezwa pale tu Yanga itakapokuwa imefuzu kucheza michuano ya Cecafa na endapo hatalipa faini yake iliyotozwa haitoshiriki michuano yoyote ile ya Cecafa hadi ilipe faini hiyo" alisema Musonye.

Musonya aliongeza kuwa wao kama Cecafa wameliomba pia Shirikisho la soka Tanzania ambao ndio walikuwa wenyeji wa michuano hiyo ya Kagame kwa mwaka huu kuichukulia hatua Yanga kutokana na utovu huo wa nidhamu iliyoonyesha.

Aidha Musonye alisema pamoja na kuwapa adhabu hizo mbili pia italiandikia Shirikisho la soka la Afrika (CAF) kuielezea juu ya kitendo hicho cha utovu wa nidhamu kilichofanywa na klabu ya Yanga ili kuonyesha ni jinsi gani timu hiyo haina nidhamu.

"Unajua kitendo walichofanya Yanga kinaonyesha upambavu wa viongozi wa klabu hiyo na kwa kweli wana bahati sana mimi si kiongozi wa soka hapa la sivyo ningewafungia maisha" Musonye alisema.

Musonye aliongeza kuwa uongozi wa Yanga mbovu wa Yanga umeiletea hasara Cecafa na TFF kwa sababu ya uamuzi wa viongozi wachache wa klabu hiyo na wasipoangalia klabu hiyo ina hatari ya kuporomoka kabisa katika soka.

Aidha Musonye alikanusha kuwepo makubaliano ya aina yoyote kati ya Cecafa, TFF na klabu za Simba na Yanga za kupeana fedha kama ilivyodaiwa na viongozi wa Yanga na kusema huo ni uongo wa mwaka kwani kanuni za Cecafa zinajulikana wazi kabisa kuwa hakuna suala la timu kupewa mgao wa mechi na timu zote zinatambua hilo.

Neema Mushi Afufuka!

Wadau, hivi huyo binti ni huyo huyo Neema Mushi au ni mwingine? Shangazi yake anadai kuwa alimfia mikononi mwake. Neema mwenyewe anasema hakufa ila alikuwa anakaa Tanga.

***********************************************************
Kutoka ippmedia.com

Mtu adaiwa kufufuka

2008-07-28

Na Patrick Chambo, PST Hai

Mamia ya wananchi katika Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, wameshikwa na butwaa baada ya kumuona msichana aliyedaiwa kufariki dunia takriban miaka mitatu iliyopita akiranda randa mitaani.

Tukio hilo la aina yake, lilitokea katika kijiji cha Machame Mkuu, mkoani Kilimanjaro na msichana huyo anayedaiwa kufa na baadaye kukutwa akitembea mitaani ametajwa kuwa ni Neema Mushi, mkazi wa kijiji hicho.

Aidha, habari zilizopatikana kijijini hapo zilisema kuwa, binti huyo alisema kuwa alikuwa akiishi Tanga. Mchungaji Elimfoo Mushi wa Usharika wa Machame Mkuu, alisema ndiye aliyeendesha ibada ya kumuombea Neema ambaye mwili wake ulifikishwa kanisani hapo.

Akizungumza na PST, Neema alisema kuwa kweli hilo ni jina lake, lakini alikanusha kuwa alikufa na kuzikwa na badala yake alikuwa akiishi Tanga. Alisema eneo alilokuwa akiishi ni siri yake na kwamba akiwa huko alisikia kuwa alikufa na kuzikwa mwaka 2005. ``Mimi sijui kitu, najua nilikuwa naishi Tanga ?na wala siwaambii nilikokuwa naishi. Nimeshangaa narudi watu wanakimbia hadi nilipopelekwa polisi, wakaja ndugu zangu wakanitambua kuwa eti mimi nilikuwa marehemu,`` alisema.

Shangazi wa Neema, Bi. Liliani Mushi, alisema ndiye aliyemuuguza Neema hadi umauti unamfika na kusafirisha mwili wake hadi kijijini hapo na kuzikwa kwenye makaburi ya kanisa. ``Kweli mimi nimeokoka na sali Kanisa la Ephata, huyo mtoto alinifia mikononi huko Namanga nilikokuwa naishi naye nimeshangaa kuambiwa eti njoo umuone Neema, amekuja Machame kutoka Tanga, nilichoka, hakika huu ni muujiza wa Mungu watu wanasema kuwa eti ni msukule, mimi siamini, ninachojua alinifia tukamzika. Huyu hapa muulizeni wenyewe katoka wapi,`` alisema shangazi huyo.

Naye Mchungaji Mushi alisema, ``nasema nijuacho mimi ni kuwa huyu ndiye Neema ambaye msukule, mimi sijui,`` alisema. Polisi wilayani Hai, wamekiri kuchukua maelezo ya Neema, mwili wake uliletwa hapa kanisani na tukauzika makaburini, kwamba ni muujiza wa Mungu au wazazi, Mchungaji na ndugu wengine walioshiriki katika mazishi.

Hata hivyo, Kamanda wa Polisi wa mkoa Bw. Lucas Ng'ohoko, hakuweza kupatikana kuzungumzia sakata hilo. Aidha, ndugu na jamaa wa Neema wako kwenye harakati za kupata kibali cha polisi ili waweze kufukua kaburi hilo.

SOURCE: Nipashe

Sunday, July 27, 2008

Ubatizo Revere Beach - IGC

Leo, waumini wawili wa International Gospel Church walibatizwa na kuazaliwa upya katika jina la Bwana Yesu huko Revere Beach.Iko karibu na uwanja wa ndege wa Logan hapa Boston . Waumini Lillian na Faith, walibatizwa leo mbele ya umati na waumini wa kanisa. Bahati mbaya kulikuwa hakuna jua hivyo picha hazijatoka vizuri.
Waumini Lillian na Faith (Morine) wakiwa na wasimamizi wao kwenye ibada. Walitambulishwa mbele ya kanisa kabla ya kwenda baharini kubatizwa

Waumini wa IGC wakifika Revere Beach Lillian na Faith wakiwa na Pastor Jared, wakiombewa kabla ya kuingia kwenye maji



Baadhi ya waumini wa IGC kwenye ibada ya ubatizo

Pastor Jared ndani ya maji akingojea wanaobatizwa

Lillian akjiandaaa kubatizwa

Lillian alisema maji ni ya baridi

Faith akiomba kabla ya kubatizwa
Faith akibatizwa

Tulivyokuwa tunabatiza wazungu waliangalia kwa mshangao wengine walichangia katika kusema, 'Amen' na Halleluyah!
Baada ya Kubatizwa

Saturday, July 26, 2008

Kipanya Wiki Hii


Kwa kweli hii katuni inasema mengi!

Tupinge Mauji ya maAlbino

Harambee tukusanye signature 100,000 za majina na ujumbe mfupi kwa ajili ya kuziwakilisha kwa vyombo husika kusaidia kampeni ya kupinga na kuachisha kabisa mauaji ya Albino.

Kila kukicha hii habari imekuwa ikiongelewa na kutunyima raha tulioko nje kwani tunashindwa kujibu tuhuma na kejeli hizi ambazo zinatupaka matope.

Kwa kutumia blog hii ya jamii shime wananchi andika jina na maoni mafupi hata kama ni sentesi mbili tupate signature 100,000 tuwakilishe kwa Waziri wa Mambo ya Ndani.

Kwa wanachama wa FaceBook group hii ipo na inakwenda vizuri pia ukiingia kwenye facebook (http://www.facebook.com/) serch kwenye albino utaipata.

Ref: Angalia hii Video ya Al Jazeera
http://youtube.com/watch?v=qKDwIiPw94I
Na hii ya The New York Times
http://youtube.com/watch?v=2iHu4NGDVno

Sikiliza ya BBC Hapa

********************************************************
Wadau, hivi kwa nini watu wanahofia maalbino mpaka wanadiriki kuwaua. Hata wazungu wanakuwa na maalbino lakini hawauliwi. Albino ni bindamu sema kakosa ile 'pigamentation' (rangi) kwenye ngozi yake. Lazima tupinge kuuliwa kwa malbino! Na hao wengi imani potofu waelimishwe!
Hebu someni jinsi maisha ya Mwandishi wa Habari, Vicky Ntetema, ilivyohatarishwa shauri ya kuwaumbua hao wanoaua malbino:
Maisha ya Mtangazaji Vicky NtetemaYapo Hatarini.. Baada ya kuwaumbua Wagaga(Wachawi) wanaotumia au Kuagiza wateja wao kuleta Viungo vya Maalbino nchini Tanzania kwa Tiba au Kupata Utajiri..Mtangazaji wa shirika la habari la uingereza BBC Vicky Ntetema amesema amekua akipokea vitisho kila kukicha juu ya maisha yake...Soma habari hapo chini upate ukweli wa mambo kutoka kwake..am living in hiding after I received threats because of my undercover work exposing the threat from witchdoctors to albinos living in Tanzania.I do not regret it, even if I am very scared.More Click Here.

Friday, July 25, 2008

Hata UKIWMI ni dili!

Habari ya kugeuza UKIMWI mradi, njia ya kujipatia mapesa tumesikia siku nyingi. Nani anaumia? Ni hao waathirika ambao misaada haiwafikii, huko waliopata mapesa wanajenga majumba ya fahari na kuendesha magari ya fahari.
Na mambo mengine. Hata haya hawana!

********************************************************************

Wanaougeuza ugonjwa wa ukimwi kuwa dili...

2008-07-25

Kutoka ippmedia.com

Na Haji Mbaruku, Jijini

Watanzania wametakiwa kutogeuza ugonjwa wa Ukimwi kama mradi wa kujinufaisha na badala yake kuwa na dhamira ya kweli katika kupambana na ugonjwa huo. Wito huo umetolewa na Dk. Thecla Kohi kutoka mtandao wa wanawake wanaoishi na virusi vya ukimwi nchini, TNW + wakati akihojiwa na kituo kimoja cha redio Jijini Dar es Salaam.

Akasema hivi sasa zimeanzishwa taasisi nyingi za ukimwi ambazo baadhi yao ni kwa ajili ya maslahi binafsi. Dk. Kohi akasema hivi sasa kuna baadhi ya watu wanaonufaika kwa kujipatia mamilioni ya shilingi kwa kutumia kigezo cha kusaidia watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi.

Hata hivyo, akasema ukifuatilia mamilioni hayo, utabaini hayatumiki kwa shughuli iliyokusudiwa bali ni kwa ajili ya manufaa ya baadhi ya watu. Akasema Watanzania wengi bado wanahitaji kusaidiwa lakini wanashindwa kutokana na ugonjwa huo kugeuzwa kuwa mradi.

Akawashauri watu wasikae na kusubiri pesa ili kupambana na ugonjwa huo ambao bado unaendelea kupunguza nguvu kazi hapa duniani. Akasema sio vyema kila siku kukaa na kufikiria ni wapi zitapatikana pesa za Ukimwi wakati kuna mambo mengi ya kufanya.

kasisitiza kuwa, endapo taasisi za kupambana na ugonjwa huo zitafanya kazi zake ipasavyo, upo uwezekano wa ugonjwa huo kupungua nchini. Lakini endapo watu wataendeleza maslahi binafsi, hali ya Watanzania itaendelea kuwa mbaya kila kukicha.

Amesema ni lazima kuwa na dhamira ya dhati ya kupambana na ugonjwa huo badala ya kuendeleza maslahi binafsi.

SOURCE: Alasiri

Thursday, July 24, 2008

Bibu Arusi - Ana miaka 84!


Fesheni za karibu Uchi!

Wanaume nao siku hizi!
Fantasia alishinda American idol na sasa anatembea karibu. Nguo ya kuogelea hiyo! Akipiga mbizi huo uzi utafunguka! Wimbi ukikija uzi unafunguka Khaa!
Miaka ya 90 watu walilalamika kwa vile J-Lo alivaa nguo amabayo uliweza kuona matiti yake ukitazama vizuri. Sasa huyo kaamua kufunga mkanda kwenye chuchu zake feki (implants) na kusema kavaa!


Jamani, nilishasema kuwa fesheni za siku zinaonyesha kila kitu, bado kidogo watu watakuwa wanatembea uchi na watu hawatajali. Mambo ya kuvaa ka-uzi (G-string) matakoni na kusema uemvaa ndo mambo gani. Mambo ya Adamu na Hawa ni hapo zamani za kale kweli!

Aibu - Taasisi ya Moyo kufukuzwa kwenye Jengo!



juu mwenyekiti wa nccr-mageuzi mh. james mbatia anaoneshna kukata tamaa na kutojua la kufanya wakati mama martha ndunye akiangua kilio kutokana na hali ya mwanae kelvin katalama ambaye kalazwa katika taasisi ya moyo ambayo leo ndiyo siku ya mwisho wa notisi ya taasisi hiyo kuhama waliyopewa na wenye nyumba nssf kutokana na kutolipia pango. picha ya juu ni sehemu ya mapokezi ya taasisi hiyo.
kwa mujibu wa mahojiano na tbc jana uongozi wa nssf umesema umeshafanya kila liwezekanalo kumaliza na mwendeshaji wa taasisi hiyo pekee binafsi ya moyo lakini ufumbuzi wa kulipwa hilo pango haujapatikana hata pale swala lilipofika kwa waziri husika. akiongea na waandishi muda mfupi kabla ya kutembelea wagonjwa waliolazwa hapo, mh. mbatia alimuomba jk aingilie kati sakata hili kwa kudai kwamba taasisi hiyo ni nyeti kiasi na haifai iachwe inataabika kwa jinsi inavyosaidia wenye kipato cha chini kupata matibabu ya moyo wakiwa nchini.
****************************************************************
Maoni yangu:
Jamani! Hapa nashindwa kuelewa serikali yetu. Navyoona ingekuwa vizuri kama wanageingilia. Hebu fikiria pesa zinazotumika kusafirisha wagonjwa kwenda Nairobi, India na South Africa! Kungekuwa na haja ya kuwasafirisha kama huduma nzuri ingekuwepo TZ? Na aliyeanzisha hiyo Taasisi ni shujaa maana anagweza kupeleka utaalam wake nchi nyingine na wangem-appreciate. ndo maana kuna Tanzanian brain drain!

Kwa kweli sijajua sababu hawajalipa pango. Lakini kufukuza watu wagonjwa si vizuri. Wataenda wapi? Je, Muhimbili watawapokea.

Wednesday, July 23, 2008

Msiba wa Mzee Kizigha

Mwandishi Mwandamizi wa Tanzania Standard Newspapers Ltd (TSN) wachapishaji wa gazeti la Daily News na HabariLeo, Charles Kizigha, akiwa amebeba msalaba baada ya Ibada maalum ya kumuombea Marehemu Baba yake mzazi, Mzee Thomas Marijani Kizigha ambaye anatarajiwa kuzikwa wiki hii nyumbani kwao Usangi mkoani Kilimanjaro. Imepangwa asafirishwe kesho kwa ndege. Kwa picha zaisi tembelea Michuzi Blog.

*************************************************************

Nimeona hii habari ya mziba wa Mzee Kizigha kwenye Michuzi blog. Nilifanya kazi na mwanae Charles Kizigha, miaka mingi Daily News. Kwa kweli lazima nimpe pole Kaka Charles maana ni majuzi tu alifiwa na mama yake mzazi. Msiba ni msiba lakini kufiwa na wazazi wote wawili katika kipindi kifupi duuh. Poleni familia.

Mungu ailaze roho ya marehemu mahala pema mbinguni. AMEN.

Wabongo wachemsha tamasha la filamu la ZIFF?

Maoni ya Kaka Beda Msimbe Lukwangule Entertainment Blog:

Wabongo wachemsha tamasha la filamu la ZIFF?

There is something very seriously wrong with Tanzania artist and this can been seen katika tamasha la filamu la kimataifa linaloishi ndani ya nchi hii ZIFF ambalo hufanyika Zanzibar kila mwaka. What is wrong jamani!!!!!

Nikiandika katika busati la filamu Habari leo Jumapili nilishawahi kusema jamani tutumbukize filamu huku kwani ipo nafasi ya kwenda maeneo mengine, kukosolewa na pia kuna sababu... lakini Roma haikujengwa kwa siku moja, lazima tusonge mbele.. kwa kujionyesha hadharani.. lakini wapi kw amara nyingine tena tamasha la 11 lina upungufu mkubwa wa local component.

Watu wanatoka all the way from Europe,America and Far East to look for nafasi just to shoo his or her film but Watanzania wanaozalisha filamu kwa fujo kwa sasa wamepeleka filamu hizi zifuatazo na moja nadhani ni ya Da Chemi huko Marekani, Bongoland II ambayo katika entry imeelezwa director wake ni Josiah Kibisa.

ZIFF hufanyika Zanzibar kila mwaka na ni tamasha kubwa kama hutaki filamu yako iingie katika mashindano lakini angalau uonyeshe basi kwa watu:Nini majidai kama hatuwezi hata kufanya kweli kwenye tamasha lenye heshima Afrika Mashariki na Kati?

CEO wa ZIFF mtanzania mwenzetu, manake nasikia wakati ule (zamani) watani zetu wakiingiza filamu kama nyuki tulikuwa tunasema ohh Foreigners hawatutakii mema, sasa huyu mswahili wa Tanga mwenye utaalamu wa filamu ambaye ameishi ughaibuni na anafundisha ughaibuni ametoa wito sana toka mwaka jana akililia filamu za nyumbani lakini mwe wamesema waluguru chilanga komo, yaani unayashangilia maji halafu unakuwa kama huna akili nzuri jamaa wanakucheka, tuache hayo kwani tulikuwa tunazungumzia filamu zilizoingia ZIFF kutoka hapa nyumbani nazo ni hizi zifuatazo:Bongoland ll,Mwanahiti l (oloibon na Layoni)na ll Zawadi ya Fisadi;The Trip ya James Gayo; Sasa na Jando.

Can you imagine?

Watu sijui niwasemeje, labda sijui woga? Haya hatukupeleka hizo sineema zetu je tutaenda kuhudhuria kujifunza manake nasikia kuna manguli wa filamu kutoka Amerika ya Kusini, Amerika kaskazini, Nigeria na Asia ya mbali wanakuja kutufunza mambo ya ABC za utengenezaji sinema, tutakwenda?

Mimi yangu macho.CEO wa ZIFF Dr Martiun mhando amesema kwamba hakuwa na chaguo la kutosha kwani hata zile zilizoletwa hizo zitakazoonyeshwa ni nafuu zaidi na yeye anasema I wonder, kweli hata mimi namuunga mkono I wonder.Hatuwezi kukua kisanii kama tusipokubali kuwa tunamapungufu na lazima tuwasikilize watu watusaidie.

Kitabu - The Kitchen Party

BOOK LAUNCH BY SWALEHE MSUYA

Book Title: THE KITCHEN PARTY
Author: SWALLEHE MSUYA

About the book: THIS IS RURAL AFRICA's ROMEO & JULIET LOVE STORY WHERE MARRIAGES AND FAMILY BONDS ARE UNSHAKABLE.

TIME: Friday July 25, 08 at 5:30 pm

LOCATION: 1st CUP CAFE located at 2740 Minnehaha Avenue South Minneapolis, MN 55406

COPIES @ $ 20: Proceeds to support a Child Day Care Center at UGWENO, a village at the foot of Africa's highest mountain, the mesmerizing Kilimanjaro.

COME & ENJOY A CONVERSATION WITH THE AUTHOR ON THE CHANGING AFRICAN STORY TELLING TRADITION THAT HAS EVOLVED FROM ORAL TRADITION TO THE PRINTED ELECTRONIC WORD .........

Tuesday, July 22, 2008

Kenyan Blog - Mwewe

Mdau Kazungu Samuel(Mhimili) kutoka Mombasa, Kenya anawakaribisha mtembelee blogu yake mpate mavitu vya Kenya.

http://mhimili.blogspot.com/

Kuna mambo huko!

Monday, July 21, 2008

Survival Sisters aka. Choka Mbaya Sisters

Kutoka Haki Ngowi Blog:

Walipokuwa wanaingia kwenye‘game’walikuwa wanajiita ‘Choka Mbaya Sisters’,wakafanikiwa kutoka na albamu yao ya kwanza iliyokuwa na jina la ‘Yatima’, lakini kunako mauzo wakala za uso na kuambulia jina kidogo tu, Mariam Mndeme anashuka nayo zaidi.

Sasa wanajiita ‘Survival Sisters’,huku mkononi wakiwa na albamu ya pili waliyoipa jina la ‘Tukiwezeshwa Tunaweza’.Nawazungumzia mabinti watatu, Irene Malekela, Lucy Samsoni na Latifah Abdallah wanaoonekana pichani ambao wamesema na ShowBiz kwamba,sasa wako tayari kwa utambulisho wa albamu hiyo utakaofanyika Agosti 26,ndani ya ukumbi wa Dar West Park,uliyopo Tabata,Dar es Salaam.

Zaidi wasanii hao wenye ulemavu wa viuongo ambao hivi sasa wanafanya vyema kupitia ngoma yao yenye jina la ‘Siyo siri’,iliyomshirikisha Dully Sykes,walisema kwamba mastaa kibao wa Bongo Flava wamejitolea kuwapiga tafu siku hiyo,wakiwemo Profesa Jay,Fid Q,Dully na Mr.Blu na wengine kibao.”Siyo wasanii hao tu, pia makampuni na watu binafsi wamejitolea kutusaidia kama Global Publishers,Morgan Sound,Dotnata Decorations, Screen Masters na Times FM.Habari hii na Mdau Abdallah Mrisho Salawi.

Kwa nini sinema za Tanzania zilifanya vibaya ZIFF

Nimeona watu wanaulizia kwa nini sinema ya Bongoland II haikupata zawadi ZIFF, wala hata mention. Sina jibu. Sikuwepo huko ZIFF.

Ila nimeona hii story kwenye gazeti ya Daily News (TZ) leo iliyoandikwa na kaka Michuzi.

Naona Dr. Martin Mhando anasema kuwa ingawa Bongoland II, ilikuwa sinema pekee ya kiTanzania kwenye mashindano ya 'Feature' ina hadithi mbili, ya familia ya Juma na hadithi ya yeye kurudi Bongo. Alisema ni sinema nzuri kwa ujumla.

Haya, niwaulize wadau walioona sinema ya Bongoland II, mliionaje?

**************************************************************************
ZIFF wants more focus to develop film industry

MUHIDIN ISSA MICHUZI in Zanzibar
Daily News; Tuesday,July 22, 2008

The Zanzibar International Film Festival (ZIFF) believes that developing a funding structure to link up with creative capacity and a local distribution structure is the answer if Tanzania's infant film industry is to grow.

The Chief Executive Officer of ZIFF, Dr Martin Mhando, said this in an exclusive interview with the 'Daily News' here yesterday, adding that one of the key problems with African cinema depended entirely on distribution.

"ZIFF has undertaken research looking into distribution hence the Tanzania Film Chain Study Report that was presented at ZIFF 2008", he said, adding: "We hope we can have time to again discuss it at length with our filmmakers with the view of looking into how to link distribution to production", said Dr Mhando at the climax of the 11th edition of ZIFF on Saturday.

On the poor participation of Tanzanian films at the annual festival, the ZIFF CEO expressed deep concern, saying something should be done to reverse the situation as it makes them feel bad about it.

He said the ZIFF plans to begin serious discussions with local filmmakers so that production efforts on the ground were supported. He, however, pointed out that there a need to encourage local filmmakers to see the use of festivals in marketing or at least promoting their films.

"Festivals generally do not need to chase after filmmakers -- the opposite is the case. However ZIFF needs filmmakers just as filmmakers need ZIFF", he quipped. The ZIFF CEO emphasised that to learn how to distribute films internally was paramount to putting the industry on its feet.

Dr Mhando said until Tanzania reached the point that audiences who clamour for the local product are satisfied one can not say the country has an industry. "Therefore let us deal with what distribution structures exist in the country, know who our audiences are and how to reach them and then start making films for those audiences and their distribution structures" he stressed.

On Bongoland II, which was Tanzania's lone nominated entry in the ZIFF 2008, Dr Mhando said it is a good film but had its setbacks on its story board. He said while the juries did not discuss film by film but one of the things that have been said about Bongoland II is that it went well until it began the story of the family's intrigue.

"The family intrigue needed to be brought in earlier and better fused into the script for the film to work. "Currently it looks like there are two stories - about the young man's problems of resettlement and then the family's", he concluded.

Orodha ya Washindi wa ZIFF

Dr. Martin Mhando, afisa mtendaji mkuu wa ZIFF akiongea kwenye hafla ya kufunga rasmi tamasha la 11 la ZIFF ngome kongwe, Zanzibar (picha kutoka Michuzi Blog)
Watoto wakitazama filamu kwenye ZIFF
Baadhi ya watazamaji kwenye ZIFF

1. THE GOLDEN DHOW -Awarded to a film that exemplifies excellence in film language and one highlighting Dhow culture.Ezra (2007, Dir: Newton I Aduaka, Nigeria/France)


2. THE SILVER DHOW- Awarded to a film that is a runner up to the Golden Dhow awardee.India Untouched (2007, Dir: Stalin K. India)


3. SHORT/ ANIMATION -Awarded to the best short film in the festival reflecting mastery of the short film structure and aesthetics.Subira (2007, Dir: Ravneet Chadha, Kenya/)


4. EAST AFRICA -Awarded to the best film by an East African filmmaker that shows the greatest commercial aptitude and potential marketabilityAfrican Lens (2008, Dir: Shravan Vidyarthi, India/Kenya)


5. SPECIAL JUROR'S CHOICE -Laya Project (2006, Dir: Harold Monfils, India)SEMBENE OUSMANE PRIZEAwarded to a film that takes a particular look at topics of development coperation.INTO THE LIGHT by Peter Glen, 2007, USA


6. SIGNIS JURY AWARD -Awarded to a film that is deemed to to exemplify universal and spiritual values that enhance human dignity, justice and tolerance.TARTINA CITY by Issa Serge Coelo - (Chad)


7.Special Commendations-Behind this Convent By 2007, Gilbert Ndahayo (Rwanda)African Lens 2008, by Shravan Vidyarthi (Kenya)East African TalentSubira (2007, Dir: Ravneet Chadha, Kenya)


8. VERONA JURY AWARD -Awarded to a film deemed the best African feature film in competition.Behind this Convent 2007, By Gilbert Ndahayo (Rwanda)


9.FIPRESCI JURY PRIZE- Awarded to a feature film from the Dhow Countries that combines cultural astuteness and commercial potential.EZRA directed by Newton I. Adauka, Nigeria/France, 2007


10. THE ZIFF CHAIRMAN'S AWARD -The award is given to a film that reveals an acute reflection on contemporary issues in a balanced manner in these times of polarised perspectives.In The Name of God , Shoaib Mansour, Pakistan, 2007


11.THE AIR TANZANIA AWARD FOR THE BEST EAST AFRICAN FILM- African Lens (2008, Dir: Shravan Vidyarthi)


12. THE UNICEF AWARD -For the Best film that encapsulates issues of children and WomenThe Kadogo Brothers, 2007, Ivory Coast, By Joseph Muganga

Sunday, July 20, 2008

Mnao lilia kuja Dar Shauri Lenu! - Father Kidevu

Mnao lilia kuja Dar shauri lenu!

Kutoka Father Kidevu Blog

Na Father Kidevu

YALAAAH! Jamanai mjini sasa hapafai na chonde chonde mlio huko mashambani wala msililie kuja jijini Dar es Salaama maana kuna tabu na karaha siku hizi.Nimelia maana sasa ninaona tunakokwenda kwa hizi nauli za daladala na mabasi ya kwenda huko kwa babu na bibi ni hatari.

Wajameni mimi leo nalia na na nimeamua kuropoka niwezavyo juu ya upandaji huu wa nauli hapa mjini na za kwenda makwetu, walahi ni zambi kabisa. sababu naambiwa eti mafuta na gharama za uendeshaji zimepanda, Haya mi mnyonge sina la kusema pandisheni tu hata misosi nayo hivi sasa sii ipo juu kisa mafuta.

Juzi hapa muuza madafu na machungwa wananiambia sasa dafu ni 300 badala ya 250 kisa eti mafuta. Mafuta haya hadi lini? SUMU ya MATRA nayo hiyo imekubali kutuua kwa kupanda kwa mafuta. haya tuendelee.

Ndio! Hatari sana, eti SUMATRA imeridhia baadhi ya nauli za mikoani kupanda, awali nilipo sikia ni nilihisi sasa maskani huko kwa babu watanisahau zaidi maana huu mwaka wa nne sijatia tumu bado naichanga nauri na leo huyu Izraeli Mwakilasa wa hiyo Mammlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini ameongeza tena.Kha!

Nitaendaje kwetu Kigoma kwa basi maana bila ya kuwa na shilingi 200 elfu/= sijaenda na kurudi kwangu Vingunguti. Nauri tu ya kwenda ni sh 84,elfu nikichanganya na msosi inaweza fika 100 elfu na zaidi.Lakini usishtuke hiyo ni ya ndugu zangu walio soma na wakabahatika kufanya kazi BOT au katika mashirika na taasisi kubwa kama Mabenki na kule TRA ambao hupenda kupanda mabasi yaliyo na raha kamili.

Mimi na mwenzangu hapo ambao hufanya kazi katika NGOs za kuzoa taka hapa mjini na kuropoka ropoka kama huku nauri yetu leo imepanda kutoka sh 40,500 hadi 49,000 hadi huko Kigoma.Nauri hii jamani inatugombanisha na kututenganisha na familia zetu.

Akina Masawe, Mushi, Manka, Kekuu, Mboro, Lymo, Mgonja, Mbaga, Msuya, Nendiwe, Nakiete na hata wewe Naelijwa kwenda kwenu kama mpo hapa Disim mtalipa sh 31,000 kama mmesoma na mnamiliki maduka makubwa pale Kariakoo na mnamabucha ya kule Koregwe ya kuuza Astaghafilula.

Ofkozi nitatumia ka eropleni kwenda kwetu Kyaka na hata kwa my frendi Prof. Rwegoshora wa pale Chuo kikuu cha Univasiti, lakini siwezi lipa 75,000 hadi Bukoba.Kaka Kyaruzi, nawewe Rwebangira mmesoma au ndio akina mimi?

Haya wewe Bishanga hukusoma lipa 44,000 tu hadi kwenu Kanyigo.Hahahahaaa! Yeto Msangi, unastuka nini kwani nani kakuita kuja hapa mjini uache mikahawa yako na makilaume kule kwenu, Masawe unalia sana, kama pato lako la chini panda mabasi yale yaliyo na Chesisi za malori ambazo nauri zake sasa ni 18,000 badala ya 14,900.

Akina Lukwangule, Msimbe, Mloka, Malonga, Chamhene, Mwenda na wewe Chuma mnaotoka hapo Matombo, Mgeta, Mlali na kule Gairo hadi Ifakara nauri hadi pale Msavu kituo Kikubwa Mjomba sasa uwe na buku sita (6,000) na sio 5,000 ya zamani.Be Mwakitosi, Se-Fute, Mwatagalile, kule kwetu Lilinga ah! Iringa, sasa kwenda kusalimia home kupata Ulanzi kidogo na tule tumboga twetu tudogo ni sh 29,000 taslim kama unataka kuangalia na video kama hutaki panda Upendo ulipe 17,000.

Wewe nani anasema kwa Akina Somo kule Ntwara na Lindi ni Mbali? Acha habari hiyo kule ukipanda basi swafi Video na Maliwato humo humo utalipa 25,00 tu hadi Lindi na kama utashukia Ntwara lipa 29,000.Jamani wewe bado unataka kuja bandari ya Salama tu, kwa kazi gani kubwa unayotaka huku, kuuza maji au mambo flani…. Tulia huko huko unaweza kushindwa hjata kurudi bush bure maana wengine kwa kuja na malori ama mabehewa ya Ng’ombe na mbio zamwenge ndio wenyewe halafu kurudi soo.Kuna watu wanacheka hapa!

Eti aende huko sijui Kigoma,Moshi na Iringa kuna nini ilhali babu yake mwenyewe kazaliwa Taasisi ya Saratani Ocean Road, nauri ya kuja kutoka Mwenge au Kimara ni 300 mara mbili hapo 600 umeliwa.Kwataarifa yako sasa nauri zote za hapa town zimepanda. Tobah!

Ndio Sekilasa wa SUMATRA amesema hivi sasa ukitoka Mbezi mwisho hadi Kariakoo au Posta utalipa Sh 600, Mwenge Posta sasa utalipa 500 na nauri ya chini sasa ni 300 hakuna kulia lia.Hapo sasa utajiuliza kwa mshahara gani niupatao nauri 1200 kwa siku?

Ebwana ninawazo sasa akili zikiniruka tu nahamisha watz wote weupe pale NHC za Posta na Kariakoo wakaishi Kimara naTegeta halafu WaTz weusi tuhamie zile nyumba za mjini amabazo hata kodi yake ni nafuu.

Watahama tu wao si, wanavipato vikubwa unafikiri watashindwa kukaa nje ya mji na magari wanayo.Waajiri sasa muangalie upya sakata hili la nauri kupanda na gharama nyinge za maisha, muwahurumie hao wanao wazalishia kwa kuwapa nyongeza kama ya SUMATRA.-------------------------------------------------------------------------------------------------

Wasomaji wa gazeti tando hili kuanzia sasa nitakuwa naweka maneno kama haya hapa chini na yeyote mwenye maoni au ushauri aniandike mrokim@gmail.com au sms +255373999.

Saturday, July 19, 2008

Washindi wa Tamasha la Filamu Zenj Watajwa

Asante Kaka Beda Msimbe (Lukwengule Entertainment) kwa update:


Hotuba tu ya jaji wa ZIFF kuhusu Tamasha:


Good evening ladies and gentlemen:

As the ZIFF festival enters its eleventh year and is now a key festival in African cinema, we – my colleagues Rachel Dwyer, Flavio Florencio and I - are honoured to have been invited to serve on the ZIFF jury.

Since its inception in 1998, ZIFF has strived to reflect the cultures and traditions of the Swahili culture of East Africa, and to celebrate and explore the Dhow culture emanating from the Indian Ocean Basin. And to recognize, appreciate and most importantly, enjoy African film.

Eleven years on and we’ve been privileged to select four films out of a staggering 41 features and documentaries in competition for the coveted prizes of the Golden Dhow, the Silver Dhow, Best Short film and Best East African film.The films in competition have resonated with this year’s theme of ‘Cultural Crossroads’ and have adhered to the proud tradition, established by the founding ZIFF Jury of 1998 to ‘explore and learn from Dhow culture and its importance in global experience.’

In keeping with the history of the iconic Dhow as ‘a symbol of communication, migration and interaction’, many of the films have explored the contestations that arise from migration.Issues that continue to bedevil Africans on the continent and the diaspora, such as indigenous land-rights, identity, genocide and ethnic cleansing, the exploitation of child soldiers and blood diamonds, have been explored from many angles and in different ways.

While films from the Indian Ocean basin have turned the spotlight on the thorny issues of untouchability and religious fundamentalism.

We were delighted with the number of East African productions and the inclusion of Bongowood films such as Bongoland 2, Mwanaihti and The Trip, all from Tanzania.Films from Tanzania, Kenya, Zimbabwe, South Africa, Rwanda, Nigeria, Ivory Coast, Senegal, the Congo, the Sudan, Liberia, Zambia, Egypt, Uganda, Ghana, Chad and Morocco, speak to the growth of the African cinematic canon.

The canon has not only expanded, but African filmmakers are clearly seizing the opportunity to tell their stories, from their perspectives, in ways that are nuanced, textured, beautiful to look at, and most importantly: cinematically exciting and entertaining.

In conclusion, and before announcing the final winners, the ZIFF Jury 2008 would like to make special mention of three films, which left a lasting impression on us:

Awaiting for Men, from Senegal, director Katy Ndiaye, for its sensitive and transgressive portrayal of women.

We are Watching You from Egypt, directors Sherief Elkatsha & Leila Menjou, for its powerful portrayal of three brave women and their determination to keep their government’s feet to the fire in the pursuit of democracy.

The Iron bone from Morocco, director Hisham Lasri for its beautiful cinematography and contemporary exploration of youthful (if misguided) urban camaraderie.And now, without further delay, the winners are:

Golden Dhow for Best Feature: Ezra (2007, Dir: Newton I Aduaka, Nigeria)

Silver Dhow for Best Documentary: India Untouched (2007, Dir: Stalin K, India)

Best Short/Animation film: Subira (2007, Dir Ravneet Chadha, Kenya)

Best East African film: African Lens (2008, Dir: Shravan Vidyarthi,Kenya)

Special Juror’s Choice: Laya Project (2006, Dir: Harold Monfils, India)for the most relevant to the themeof the Dhow countries

Gail SmithChairperson ZIFF Jury 2008


In the picture Ms Gail Smith reading her speech

Portfolio Mpya


Karibuni muone portfolio mpya ya picha. Picha zilipigwa Rhode Island, mwezi uliopita na mpiga picha Debra Gagnon.

http://animoto.com/play/gQ1KkRAFBGb06iR2uKc80w

Open Casting Call - Brotherhood TV Show


Wadau mnaotaka kuwa kwenye TV show.... kesho kuna Open Casting Call mjini, Providence Rhode Island. Ni kwa ajili ya ile show Brotherhood ambayo inaonyeshwa Showtime. Ni kama Sopranos lakini ni waIrish.

**************************************************************
BROTHERHOOD OPEN CASTING CALL

Showtime is back to film the THIRD SEASON of BROTHERHOOD. Set and produced in Providence, Brotherhood tells the story of the Irish-American Caffee brothers. Tommy Caffee (Jason Clarke) is a local politician, while his brother Michael (Jason Isaacs) is involved in the neighborhood's Irish Mob.

We’ll be seeking people to be considered for SPEAKING roles as well as BACKGROUND ACTING.In some cases, no experience is necessary.Filming will start July 28 and the show will continue filming through October.You could be called to work any time during that period.

SEEKING:All Ages – yes, this means all ages…including minors, babies, retired folk, college, teens, uh, all ages.All Types – yup…all types. – self-employed, unemployed, middle-management, all races, both genders, nice people, sad people, mean people, happy people…all types.

But most of all RELIABLE people.

Please bring a recent photo of yourself that we can keep.You will be asked to fill out a form and you’ll be on your way. We look forward to seeing you there!!


BROTHERHOOD OPEN CALL TIME & LOCATION!

The open call will be held THIS SUNDAY, JULY 20th!

TIME: 11a.m.- 3p.m.
LOCATION: ATRIUM Building in Providence - at One Capitol Hill.

Please bring a non-perishable food item for the Rhode Island Food Bank