Sunday, May 15, 2016

Shukurani Kutoka Kwa Familia ya Michuzi - Msiba wa Maggid Muhidin

Familia ya Ankal Muhidin Issa Michuzi inapenda kutoa shukrani nyingi sana sana kwa ndugu, jamaa, majirani, marafiki na wafanyakazi wenzie kwa kujitoa kwa hali na mali katika wakati huu mgumu wa msiba wa mawanae Maggid (pichani) aliyefariki huko Durban, Afrika Kusini Jumapili ya wiki iliyopita na kuzikwa katika makaburi ya Kisutu jijini Dar es salaam juzi Jumamosi.
Ni vigumu mno kumshukuru mtu mmoja mmoja kutokana na wingi wenu na kwa jinsi kila mmoja wenu alivyojitoa na kuonesha upendo wa dhati kabla na baada ya mazishi. Tunaweza kujaza kurasa 200 kama hizi na tusiwe tumehitimisha robo tu ya shukrani zetu kwa kila mmoja wenu. Hivyo tunaomba radhi kwa yoyote ambaye hatutomtaja, kwani wafadhili wetu nyie mko wengi mno.
Pamoja na hayo shukrani za kipekee ziwaendee Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Mama Janeth Magufuli na familia yao yote, Rais Mstaafu wa awamu ya Nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete na Mama Salma Kikwete na familia yao yote, Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili Alhaj Ali Hassan Mwinyi na familia yake yote, Rais Mstafu wa awamu ya Tatu Mzee Benjamin William Mkapa na Mama Anna Mkapa na familia yao yote, Waziri Mkuu Mstaafu Jaji Joseph Sinde Warioba na Familia yake yote, Katibu Mkuu Kiongozi Mhandisi Allan Kijazi, Katibu Mkuu Ikulu Mhe. Peter Ilomo, Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu Mhe. Ombeni Sefue pamoja na wafanyakazi wenzie wote wa baba mfiwa kwa kuwa karibu naye katika wakati wote, na kuhakikisha kuwa kila kitu katika msiba huu kinaenda sawasawa. TUNAWAOMBEA KWA MOLA AWAPE BARAKA ZAKE ZOTE...

Salamu zingine za kipekee ziwaendee watumishi wote wa Ubalozi wetu Afrika kusini mjini Pretoria ambao wakiwa chini ya Brigedia Jenerali Kimaryo na Afisa wa Ubalozi kaka Awesi walisimamia maswala yote ya kuusafirisha mwili kutoka Durban kuja Dar es salaam. MOLA AWAONGEZEE PALE MTAPOPUNGUKIWA...

Vile vile shukrani za kipeke ziwaendee Viongozi na wanachama wa Jumuiya ya Watanzania waishio Durban pamoja na Muslim Burial Society ya hapo hapo Durban ambao walihakikisha mwili wa marehemu unahifadhiwa, unakafiniwa na unasafirishwa kwa heshima zote. ALLAH AWAJAALIE KATIKA KILA JAMBO...

Kwa Uongozi wa msikiti wa Maamur uliopo Upanga Dar es salaam pia familia inatoa shukurani za kipekee kwa yote mliotutendea ikiwa ni pamoja na mwongozo wa kidini katika wakati wote wa msiba na mazishi.
Tutakuwa watovu wa fadhila endapo kama hatutatoa shukurani za kipekee kwa magrupu ya WhatsApp yote ambayo baba mfiwa Ankal ni mwanachama. Shukurani hizi maalum ziwaendee Ma-Admin na wanachama wa Kariakoo Family Group (KFG), Dar es salaam Old Friends (DOF), Ma Best Group (MBG), Wanahabari, Tasnia ya Habari, Uongozi, Siasa na Matukio Mix, The New Team, TSJ Alumni, Zama Zile, The Brain Team, Jazz Fans, The Kop in Tanzania, LFC Bongo, Uswazi Academia, Tanzania Bloggers Network (TBN), The Legends Family, SID Tanzania Chapter, Mawasiliano, Team Michuzi, Amani Kwanza Group, Photojournalists TZ, PPAT Members, P Mamas, RUBY 15, Warembo wa KA, Mambachoz Group, Ndanshau Group, Empress Group kwa Fundi Mussa na wengi wengine wote katika Social media wakiongozwa na Jamii Forum na VIJIMAMBO BLOG ya Marekani. TUMEHEMEWA MNO NA KUFARIJIKA SANA KWA MICHANGO YENU YA HALI NA MALI. WE ARE HUMBLED. MBARIKIWE SANA, SANA, SANA...
Mwisho, lakini sio kwa umuhimu bali kwa nafasi na mpangilio, tunatoa shukrani za kipekee kwa shirikia la ndege la Emirates kwa kufanikisha usafiri wa mwili wa marehemu, hali kadhalika kampuni mahiri ya SWISSPORT kwa kusaidia logostics zote katika Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es salaam.

HATUNA CHA KUWALIPA ZAIDI YA KUTOA SHUKURANI NA KUSEMA ASANTE SANA NA KUWAOMBEA KWA MOLA KILA MMOJA WENU AWABARIKI KATIKA SHUGHULI ZENU ZOTE...

Inna Lillahi wa inna ilaihi raji'un

AMIN!




1 comment:

Anonymous said...

Pole sana familia ya Michuzi.