Thursday, January 03, 2013

Ujumbe Muhimu Kwa Tanzania Diaspora Kutoka Serikali ya TZ


KUWATUMIA WATAALAMU WA KITANZANIA WALIOKO UGHAIBUNI        (DIASPORA) NA NDANI YA NCHI KUJENGA UWEZO NA UFANISI WA UTEKELEZAJI WA SHUGHULI MUHIMU ZA SERIKALI

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inakusudia kuwatumia wataalamu wa Kitanzania walioko ndani ya nchi na wale walioko ughaibuni (Diaspora) katika kutekeleza mipango yake kadhaa yenye umuhimu kwa Taifa.

Hapo awali, Serikali iliwatumia zaidi wataalamu kutoka nchi nyingine, ambapo kwa sasa lengo ni kuona kwamba wataalamu wa nchi nyingine wanatumika pale tu ambapo wataalamu wa Kitanzania walio ndani na nje ya nchi hawajapatikana kufanya kazi husika.

Katika kutekeleza azma hiyo, Serikali itapenda kupata wataalamu wa Kitanzania kwenye maeneo yafuatayo:-
(i) Mfumo mzima wa utafutaji, uchimbaji, uongezaji thamani na usambazaji wa gesi asilia na mafuta.

(ii) Kuimarisha matumizi salama ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kuboresha utendaji wa Serikali na utoaji wa huduma kwa wananchi.

(iii) Kuboresha utekelezaji wa malengo ya Serikali na kupima matokeo kupitia mfumo unaokusudiwa kuhakikisha tunapata matokeo makubwa na ya haraka katika maeneo ya kipaumbele na kimkakati katika maendeleo ya Taifa.

Wataalamu watakaojitokeza na kukubaliwa kufanya kazi Serikalini katika maeneo haya, watafanya kazi kwa mikataba ya muda mfupi, lakini inayoweza kuongezwa iwapo utendaji utaridhisha.

Mwito unatolewa kwa Wataalamu wa Kitanzania popote walipo, ughaibuni au ndani ya nchi, kujitokeza na kuleta wasifu wao (CV’s) pamoja na maelezo ya kwa nini wanafikiri wao ni aina ya watu tunaowatafuta. Tumia anuani ifuatayo:-


Katibu Mkuu Kiongozi
Ofisi ya Rais, Ikulu
S.L.P. 9120
DAR ES SALAAM

4 comments:

Anonymous said...

Je, nikirudi nitalipwa mshahara unaofaa kipaji changu?

emuthree said...

Habari njema hiyo

Anonymous said...

Unafiki mtupu hao waliopo Nchini hamuwasikilizi Ushauri wao,kutokana Ufisadi wa Watawala.Wasikilizeni na wapeni Nyenzo za kufanyia Kazi na mishahara mizuri waliopo Nchini.

Anonymous said...

Jamani nyie mlioko nje msije huku. Bongo kumejaa unafiki na ufisadi. Kazi zinatolewa kwa kujuana. Watu wanapeana kazi TCRA, Ewura na SSRA kutokana na kujuana au ku-lobby, sio kuwa na sifa. Wanachoangalia watu ni matumbo yao na ndio maana TCRA imelazimisha kubadilisha mfumo wa matangazo ya televisheni kutoka analogue kwenda digital. Wamehongwa na makampuni yanayouza ving'amuzi.