Monday, November 14, 2011

FFU Watumia Mabomu Iringa, Waandishi wa Habari Wajeruhiwa Vibaya!


Wananchi wakiishambulia nyumba inayotuhumiwa kuwa na misukule kwa mawe


kamera ya mwandishi wa ITV ikiwa imevunjwa




Mwandishi wa ITV Iringa Laulian Mkumbata akionyesha kamera iliyovunjwa



Wananchi wakiwa wameizunguka nyumba inayodaiwa kuwa na misukule ndani ,huku ndani ya nyumba hiyo kukiwa na wanahabari pia

Askari wa kikosi cha askari wa kutuliza Ghasia (FFU) Iringa watumia mabomu ya machozi na risasi za moto kuwatawanya wananchi waliovamia nyumba ya mtumishi wa Mungu kwa madai kuwa kuna watu 15 wanaodaiwa kufa na kuonekana katika nyumba hiyo ( misukule).


Wananchi hao wenye hasira kali zaidi ya 200 walitumia mawe kuwashambulia FFU huku wao FFU wakitumia mabomu ya machozi kupambana Huku wanahabari wa vyombo mbali mbali na askari polisi na mchungaji mmoja wakinusurika kuuwawa wakishambuliwa kwa mawe na wengine kuvunjiwa kamera zao na wananchi hao ambao walionyesha kuwachukia askari polisi pamoja na wanahabari ambao waliteuliwa na wananchi wenyewe kuwawakilisha katika kukagua nyumba hiyo bila mafanikio .


Tukio hilo lilitokea eneo la Frelimo katika Manispaa ya Iringa na kudumu zaidi ya masaa manne baada ya kuanza majira ya saa 8 mchana na kuendelea hadi saa 12.50 jioni .


Wakielezea juu ya tukio hilo wananchi hao walisema kuwa walipata taarifa kutoka kwa mmoja kati ya wananchi wa eneo hilo kuwa katika nyumba hiyo ya mfanyabiashara wa maji kumeonekana misukule 15 ambayo ilionekana ndani ya uzio wa nyumba hiyo.


Kutokana na uvumi huo wananchi kutoka pande mbali mbali za mji wa Iringa walifika katika nyumba hiyo na kuizingira kwa lengo la kutaka kuichoma moto kabla ya askari polisi kufika na kuwaomba wananchi kutofanya hivyo na badala yake kuteuwa wawakilishi ili kuingia ndani ya nyumba hiyo kujikagua misukule hiyo bila mafanikio .


Hata hivyo baada ya askari hao walioambatana na wanahabari zaidi ya sita kutoka vyombo mbali mbali akiwemo mwandishi wa habari hizi kushindwa kuona misukule hao baadhi ya wanahabari akiwemo mwandishi wa habari hizi waliamua kuruka ukuta baada ya kuona wananchi wakionyesha jazba zaidi .


Huku baadhi ya waandishi wakiongozwa na katibu wa klabu ya waandishi wa habari mkoa wa Iringa (IPC) Frank Leonard ambaye ni mwandishi wa gazeti la Habari leo wakilazimika kujifungia ndani ya nyumba hiyo baada ya wananchi kuanza kuishambulia kwa mawe .


Hali hiyo iliwalazimu askari polisi zaidi ya 10 walikuwepo kuanza kutumia mabumu ya machozi kuwatawanya wananchi hao ambao walikuwa wakiimba kuwa mmekela rushwa wote wanahabari,wachungaji na polisi hivyo lazima mchomwe moto .


Katika tukio hilo mabomu ya machozi zaidi ya 30 yalipigwa hewani huku wananchi wakizidi kuongezeka na kupelekea askari hao kuomba msaada zaidi wa askari wa FFU ambao walifika wakiongozwa na mkuu wa FFU mkoa wa Iringa Mnunka na kufanikiwa kuwatawanya wananchi hao .

Zaidi ya watu 10 walikamatwa na jeshi la polisi kwa kujihusisha na vurugu hizo huku watu wengine zaidi ya 20 wakiwemo wanahabari familia ya mfanyabiashara huyo ,mchungaji aliyefahamika kwa jina la Mang’uliso walijeruhiwa kwa mawe .


Kamanda wa polisi wa mkoa wa Iringa Evarist Mangalla hakuweza kupatikana kuzungumzia madhara yaliyojitokeza katika tukio hilo japo mwandishi wa habari hizi alishuhudia magari matatu likiwemo la polisi yakiwa yameharibiwa vibaya kwa mawe.


ZAIDI SOMA HAPA

No comments: