Saturday, August 13, 2011

Bibi Arusi Ashikwa na Uchungu Kanisani!

Makubwa. Habari kutoka Muheza, Tanga zinasema Bibi Arusi, Mariam Shabani, kashikwa na uchungu kanisani, na kupelekwa hospitalini na shela yake na kuzaa huko! Pole zake. Mama na mwana wako salama. Wanasema alikuwa na mimba ya mieza saba.

*****************************************************************
Kutoka Gazeti la Mwananchi:


Bibi harusi ashikwa uchungu, ajifungua kanisani Muheza
Thursday, 11 August 2011 21:16

Mwandishi Wetu, Muheza

BIBI harusi aliyefahamika kwa jina la Mariam Shabani, ameshikwa na uchungu wa kujifungua kanisani wakati akifungishwa ndoa na mchumba wake, aliyefahamika kwa jina la Deo Massawe.Tukio hilo lilitokea juzi Kanisa Katoliki lililopo maeneo ya Majengo Shimoni, wilayani Muheza, huku umati wa watu ukiwa umejaa ndani ya kanisa hilo ukiisubiri kufungwa kwa ndoa hiyo.

Mwandishi wa habari hizi alishuhudia tukio hilo ndani ya kanisa hilo, wakati Padri Martin Kihiyo, akiendelea na misa ya kufungisha ndoa hiyo, ghafla bibi harusi akiwa amevaa vazi rasmi la harusi, alianza kupiga kelele akidai anasikia uchungu wa kujifungua.

Hata hivyo, baada ya bibi harusi huyo kupiga kelele, Padri Kihiyo alisitisha misa hiyo na Mariamu kuchukuliwa haraka na kuwekwa kwenye gari huku akiwa hajiwezi hadi Hospitali Teule Muheza.Pia, Mariamu anafahamika kwa jina la Sada Shabani, baada ya kufikishwa hospitali alipelekwa chumba cha kujifungulia huku akiwa na vazi lake la harusi.

Baada ya kuhudumiwa Mariamu, alijifungua mtoto wa kike na kulazwa wodi ya Azimio wanakolazwa wazazi.
Mmoja wa muuguzi hospitalini hapo aliyeomba asitajwe, alisema bibi harusi huyo alijifungua njiti akiwa na miezi saba.Kwa upande mwingine, kwenye ukumbi ambao ulikuwa umeandaliwa kwa sherehe ya harusi hiyo, watu walikuwa wamekaa ndani wakisubiri maharusi bila kufahamu kilichokuwa kikiendelea.

Hata hivyo, kutokana na hali hiyo bwana harusi alilazimika kufunga ndoa na msichana mwingine wa pembeni kwa niaba ya bibi harusi, ili kuhalalisha sherehe hiyo huku bibi harusi mwenyewe akiwa hospitali analea.

Inasemekana Mariamu alianza kusikia uchungu akiwa saluni na aliwaeleza baadhi ya watu, lakini walimjibu kuwa huo ni woga wa harusi.Katika hatua nyingine, mbuzi wa ndafu aliyekuwa ameandaliwa alianguka chini kwenye mchanga.

Baadhi ya Wakristo walisikitishwa na tabia ya viongozi wa dini kuendelea kuwafungisha ndoa watu ambao wake zao wana mimba kwamba, ni aibu.

No comments: