Monday, October 24, 2011

‘Rushwa ya Ngono Inatumika Kupata Ubunge’

Ni Kweli rushwa za Ngono zimezidi Tanzania!
***************************************************
Kutoka Gazeti la Habari Leo.


UTAFUTAJI wa vyeo kama ubunge na vingine vya maofisini miongoni mwa wanawake wasiojiamini, ni sababu kubwa ya kuendelea kuwepo kwa rushwa ya ngono nchini.

Aidha, imeelezwa kuwa matumizi mabaya ya madaraka yanayofanywa na baadhi ya wanaume ni kichocheo kingine cha rushwa hiyo, inayochangia nchi kuwa na viongozi wasio na uwezo, maadili mema, kwa asilimia kubwa.

Akizungumza wakati wa mkutano wa Kamati ya Bunge ya masuala ya Ukimwi iliyokutana Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, kujielimisha kuhusu unyanyasaji wa jinsia nchini, Mbunge wa Viti Maalum, Hilda Ngoye (CCM) alisema rushwa hiyo ipo na inarindima hata kwa wabunge.

Huku akiungwa mkono na Waziri Kivuli wa Afya na Ustawi wa Jamii, ambaye pia ni Mbunge wa Biharamulo Magharibi (CHADEMA), Dk.Gervas Mbassa, Ngoye alisema anachokizungumza kinafanyika si tu katika kuutafuta ubunge, bali hata katika kutafuta vyeo maofisini.

Wakati akisema hayo, Mbunge wa Viti Maalu, Margret Mkanga (CCM) alishtuka kwa mshangao ulioashiria kuisikia habari hiyo kwa mara ya kwaza na ndipo Ngoye alipomwambia, “Usishangae! It is a practical example, akimaanisha kuwa alichokizungumza ni mfano hai uliopo.

Kwa upande wake, Mbassa aliliambia gazeti hili kuwa hali hiyo ipo kweli na kwamba inatokana na kukosa utu miongoni mwa wanaoomba na wanaotoa rushwa ya ngono.

Alisema, wengi wanaojihusisha na rushwa hiyo na kushindwa kupata wanachokitaka huishia kuaibika au kupata maambukizi ya VVU huku walioigawa na kuupata uongozi wakiiharibu nchi kwa njia tofauti kutokana na kukosa maadili ya uongozi pamoja na uwezo wa kazi.

“Alichokisema Ngoye ni sahihi kabisa, rushwa ya ngono ipo hata kwa wabunge. Lakini pia ipo katika nyanja zingine ambazo si za siasa. Watu wanataka uongozi wakati wanajua hawana uwezo na matokeo yake wanaamua kutumia miili yao.

“Ufike wakati Watanzania tuikatae na kuthamini utu vinginevyo nchi itajaa viongozi watakaotusababishia matokeo mabaya,” Ndassa alisema.

Wakati huo huo, baadhi ya wabunge wanaounda kamati hiyo wamewataka wanafunzi wanaoombwa rushwa ya ngono kutoa taarifa kwa maofisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ili wahusika wakamatwe na kushitakiwa, kwa sababu kitendo hicho, licha ya kuwa kosa la jinai, kinatumiwa na wengi kusambaza VVU.

Mbunge wa Viti Maalum, Rosweeta Kasikila (CCM) na Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo (CCM), walisema hayo kwa nyakati tofauti wakati wakitoa michango yao, kuhusu unyanyasaji wa kijinsia, unaohusisha ngono nchini.

Kasikila ambaye ni Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, alisema kuwa wanafunzi ni waathirika wakubwa wa rushwa ya ngono na kwamba wanahitaji kupewa elimu zaidi juu ya athari za rushwa hiyo ya ngono kwa watu mbalimbali wanaowarubuni ili waikatae na kuwaripoti wanaowashawishi kuishiriki.

“Wapo wasichana na hata wavulana jasiri wanaowaeleza maofisa wa Takukuru kuhusu kuombwa rushwa ya ngono na hivyo kuandaa mitego inayowezesha kunaswa kwa wengi wao na kushitakiwa.

Hiyo ni njia mojawapo inayoweza kusaidia kupunguza kuenea kwa maambukizi ya VVU ambayo wengi wao huyapata wanaposhiriki kujamiiana huko”, Kasikila alisema.

Naye Shelukindo alisema kuwa wanafunzi wanastahili kujengewa ujasiri wa kuwaeleza wakubwa wao na taasisi zinazoshughulikia masuala ya haki zao ili kukomesha vitendo vya unyanyasaji vinavyofanywa dhidi yao, kama vile kuhisishwa katika masuala ya kujamiiana kwa kurubuniwa kupata wanachokihitaji.

Alisema, rushwa ya ngono haistahili kuwepo mahali popote pale kwa kuwa ni njia mojawapo inayochochea maambukizi kutokana na ukweli kuwa mara nyingi wahusika wanaoishiriki hawapati muda au kukumbuka

CHANZO: Gazeti la Habari Leo

No comments: