Thursday, March 14, 2013

Rais Kikwete Afungua Rasmi Jengo la Kitivo Cha Sayansi MUM

HOTUBA YA MHESHIMIWA RAIS JAKAYA MRISHO KIKWETE KATIKA UFUNGUZI RASMI WA JENGO LA KITIVO CHA SAYANSI KATIKA CHUO KIKUU CHA WAISLAMU CHA MOROGORO (MUM),


TAREHE 14 MACHI, 2013, MOROGORO

Mzee Kitwana Suleiman Kondo, Mwenyekiti wa Taasisi ya Maendeleo ya Waislamu (MDF);
Mheshimiwa Joel Bendera, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro;
Mama Mwantumu Malale, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro;
Profesa Hamza Mustafa Njozi, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro;
Viongozi mbalimbali wa Serikali, vyama vya siasa na Jumuiya mliohudhuria;

Wageni waalikwa;

Mabibi na Mabwana;

Niruhusuni niungane na wenzangu walionitangulia kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma, kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha kukutana hapa. Nakushukuru sana Mama Mwantumu Malale, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro na viongozi wenzako kwa kunialika kuja kujumuika nanyi katika siku hii adhimu ya ufunguzi wa jengo la Kitivo cha Sayansi katika Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro. Mmenipa heshima kubwa ya kuwa sehemu ya historia ya Chuo hiki. Kwa kweli, nimefarijika sana kuona Chuo chetu kinazidi kupata mafanikio ya kutia moyo hasa ukizingatia ukweli kwamba kina muda mfupi tu tangu kuanzishwa kwake.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Natoa pongezi nyingi kwako, Makamu Mkuu wa Chuo na wale wote walioshiriki kubuni wazo la kuwa na jengo la Kitivo cha Sayansi na kufanikisha ujenzi wake. Juhudi zao na moyo wao wa kupenda maendeleo ndio umetufanya sisi kujumuika hapa leo kushuhudia mafanikio haya. Hakika ni jambo la kujivunia. Pia, nawapongeza sana Wajenzi na Mhandisi Mshauri kwa kazi nzuri waliyofanya ya ujenzi wa jengo hili. Sote tunaliona jengo lilivyojengwa vizuri na kwa namna yake linapendezesha mandhari ya Chuo.

Kwa namna ya pekee napenda kwa niaba yenu nitoe shukrani zangu za moyoni kwa taasisi ya Al-Barakah kwa kufadhili ujenzi wa jengo hili. Asanteni sana kwa ukarimu wenu na upendo mkubwa mliouonesha kwa nchi yetu na watu wake. Naomba taasisi nyingine na watu binafsi waige mfano huu mzuri wa kusaidia miradi mbalimbali inayonufaisha jamii. Tukumbuke ule msemo wa wahenga kuwa “kutoa ni moyo, usambe si utajiri”.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Mabibi na Mabwana;

Kwa miaka mingi madhehebu ya dini na mashirika ya dini yamekuwa washirika muhimu sana wa Serikali katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya nchi yetu. Yamekuwa yanajihusisha na kutoa huduma kwa jamii kama vile afya, elimu na nyinginezo. Kwa ajili hiyo watu wengi sana nchini wamenufaika na wanaendelea kunufaika na huduma zinazotolewa na mashirika ya dini.

Kwa miaka mingi mashirika na taasisi za madhehebu ya dini ya Kikristo ndiyo yaliyokuwa yakionekana kutoa huduma hizo. Kwa upande wa Waislamu, ukiacha Mtandao wa Maendeleo wa Aga Khan, mchango umekuwa mdogo sana. Ni jambo la faraja kubwa kuona Taasisi ya Maendeleo ya Waislamu (MDF) ikionyesha njia. Kwa kumiliki na kuendesha Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro kwa ufanisi, MDF inatoa mchango muhimu katika kuendeleza elimu ya juu na maendeleo nchini. Idadi kubwa ya wanafunzi waliofuzu masomo yao na waliopo katika Chuo hiki tangu kilipoanzishwa mwaka 2005 ni ushahidi tosha wa kazi nzuri inayofanywa na MDF. Hongereni sana. Tunawaombea kwa Mola mpate mafanikio makubwa zaidi miaka ya usoni kwa upande wa elimu na huduma nyingine muhimu.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Katika kipindi cha miaka saba sasa, Serikali yetu imeongeza sana uwekezaji katika upanuzi wa elimu tangu ya awali hadi elimu ya juu. Tumeamua kufanya hivyo kwa sababu vijana wengi waliokuwa wanastahili kupata elimu ya awali, msingi, sekondari, ufundi na elimu ya juu walikuwa hawapati. Tanzania ni kubwa kuliko Kenya na Uganda kwa eneo na idadi ya watu lakini ndiyo tuliokuwa na idadi ndogo ya wanafunzi kwa ngazi zote hizo. Kwa mfano, mwaka 2005 idadi ya wanafunzi waliokuwa Chuo Kikuu nchini Kenya ilikuwa 108,407, Uganda 88,360 na kwa baadhi ya nchi za SADC kama vile Afrika Kusini idadi hiyo ilikuwa 717,973. Wakati wenzetu wakiwa na idadi hiyo, sisi tulikuwa na wanafunzi 40,719 tu katika vyuo vikuu nchini. Hali ilikuwa hivyo pia kwa elimu ya sekondari. Kenya ilikuwa na wanafunzi 925,341, Uganda 619,519 na Afrika Kusini 4,186,882 wakati Tanzania ilikuwa na wanafunzi 524,325 tu waliokuwa katika shule za sekondari.

Tuliona hali hii haikubaliki hivyo tukaamua hatuwezi kuiacha iendelee. Tukaamua kudhibiti. Tukachukua hatua tulizochukua za kupanua elimu katika ngazi zote. Matokeo ya uamuzi huo ni kwamba vijana wanaopata fursa ya kupata elimu katika ngazi zote wamekuwa wengi kuliko wakati mwingine wo wote katika historia ya nchi yetu, tumewafikia na kuwapita majirani zetu. Kazi kubwa tunayoendelea nayo sasa ni kuwekeza katika kuimarisha ubora wa elimu waipatayo vijana wetu kwa kuongeza walimu, vifaa vya kufundishia, vitabu na huduma nyinginezo. Inshallah hata kwa dhamira yetu, hii njema Mola atatuwezesha. Mwanzo mgumu lakini hatma itakuwa nzuri.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Kufuatia juhudi hizo, idadi ya wanafunzi waliopo kwenye vyuo vikuu nchini imeongezeka sana, kutoka wanafunzi 40,719 mwaka 2005 hadi wanafunzi 166,484 mwaka 2012. Kwa upande wa sekondari mwaka 2011 tulikuwa na wanafunzi milioni 1.79 na wenzetu wa Kenya walikuwa na wanafunzi milioni 1.77. Haya ni mafanikio makubwa.

Serikali itaendelea kuwekeza kwenye upanuzi wa fursa za elimu na ubora wake. Hata hivyo ushiriki wa wadau wengine kuunga mkono juhudi za serikali ni jambo muhimu sana. Tumeweka mazingira mazuri kwa wadau hao kufanya hivyo na mafanikio yanaonekana wazi. Kama nilivyokwishasema awali, mashirika ya dini yamekuwa wadau wa kutumainiwa na mchango wao uko wazi. Unajieleza wenyewe. Kwa mfano, katika vyuo vikuu 49 vilivyopo nchini, vinavyomilikiwa na umma ni 14 tu. Vyuo vikuu 24 vinamilikiwa na mashirika ya dini na 11 na sekta binafsi.





Ndugu Mkuu wa Chuo;

Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa na muhimu unaotolewa na vyuo vikuu vinavyomilikiwa na mashirika ya dini na sekta binafsi. Ninyi mmekuwa washirika wazuri na wa uhakika katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya elimu katika nchi yetu. Napenda kuwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kuwaunga mkono na kushirikiana nanyi ili kuwawezesha vijana na Watanzania wengi zaidi waweze kupata elimu. Uamuzi wa kufanya utaratibu wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu uhusishe wanafunzi wa vyuo visivyokuwa vya umma ni moja ya mambo mengi muhimu yanayofanywa na Serikali kuthibitisha usemi wangu huo.

Tulipoingia madarakani mwaka 2005 tulifanya mambo mawili muhimu kuhusu mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu. Kwanza uamuzi kwamba, mikopo itolewe kwa wanafunzi wa vyuo vikuu vya umma na vile visivyokuwa vya serikali. Kabla ya hapo ilihusu vyuo vya umma pekee. Pili kwamba, kila mwaka tuongeze fedha zinazotengwa kwa ajili ya Mfuko huo ili idadi ya wanafunzi wanaonufaika iongezeke. Tulikuta Mfuko ukiwa na shillingi billioni 56.1 unanufaisha wanafunzi 16,345 mwaka 2005. Tukaongeza kila mwaka na katika mwaka huu wa fedha (2012/13) tumetenga shillingi bilioni 345 zinazowanufaisha wanafunzi 98,772.

Tutaendelea kuongeza fedha katika Mfuko huo ili wanafunzi wengi zaidi wanufaike na hata ifikie siku moja tuweze kuwakopesha wote bila ya kujali sifa ya uwezo wa wazazi au walezi kulipa ada. Kwa kasi tuliyonayo na kwa jinsi tunavyozidi kufanikiwa katika kukusanya mapato ya serikali, naamini miaka michache ijayo tunaweza kufikia lengo hilo. Nawasihi Bodi ya Mikopo iwekeze katika kuimarisha uwezo wa kuwafuatilia waliokopeshwa kulipa mikopo waliyopewa. Matamanio yangu ni kuwa fedha zilizotolewa zizunguke ili tupunguze kiasi kinachotolewa na bajeti ya serikali kila mwaka.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Mabibi na Mabwana;

Niruhusuni nitumie nafasi hii kukupongeza wewe Mkuu wa Chuo, Makamu Mkuu wa Chuo, Wahadhiri na Jumuiya nzima ya Chuo Kikuu hiki kwa kazi kubwa na nzuri muifanyayo ya kuendeleza na kuboresha Chuo. Tumeshuhudia ujenzi wa jengo nililolifungua leo. Tumeona mafanikio kwa upande wa ongezeko la idadi ya wanafunzi, walimu, wafanyakazi na fani zinazofundishwa katika kipindi hiki kifupi cha uhai wa Chuo hiki.

Nimefurahishwa na kufarijika sana kusikia kuwa ubora wa elimu inayotolewa hapa chuoni ni jambo linalopewa kipaumbele cha kwanza. Jambo hili ni muhimu sana kulisisitiza kwani tunataka wahitimu wa Chuo hiki wafanane na wahitimu wa Chuo chochote kizuri nchini na hata duniani. Ningependa kuona wahitimu wa Chuo hiki wanagombewa katika soko la ajira. Hili ni jambo linalowezekana. Kinachotakiwa ni uamuzi wa Baraza na Seneti kuwa iwe hivyo na kuchukua hatua zipasazo. Sina shaka kuwa mnaweza kufanya hivyo. Hakika mnaweza, na sote kwa umoja wetu tunaweza.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Nimefurahi sana, pia, kusikia kuwa Chuo kinatoa mafunzo ya ualimu. Bila ya shaka mnaelewa kwa nini nafurahi. Tuna uhaba mkubwa wa walimu nchini hivyo Chuo cho chote kinachotoa mafunzo ya ualimu hunifurahisha. Endeleeni kuimarisha mafunzo hayo ili Chuo chenu kitambulike na kukubalika nchini kwa sifa ya kutoa walimu wazuri. Walimu wa kutoka Chuo hiki wawe wale wanaojua vyema masomo wanayofundisha, mahiri kufundisha na waadilifu. Naomba pia mtoe kipaumbele cha juu kwa mafunzo ya ualimu wa masomo ya sayansi na hisabati. Mkifanya hivyo, mtakuwa mnatoa mchango mkubwa katika jitihada za kupunguza uhaba wa walimu wa masomo hayo nchini. Naamini kitendo cha kuzindua Jengo la Kitivo cha Sayansi, kilichofanyika muda mfupi uliopita kinatoa matumaini ya Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro kuchangia katika jitihada za kupunguza pengo la walimu wa sayansi nchini.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Nimewasikia mkieleza kwa ufasaha changamoto kubwa na ndogo ambazo Chuo inakabiliana nazo. Nawapongeza kwa dhati, wewe na viongozi wenzako kwa ubunifu wenu na hatua mnazochukua kuzikabili changamoto hizo. Nawaahidi msaada na ushirikiano wangu na wa serikali kwa yale yaliyoko kwenye uwezo wangu na wa serikali katika kutafuta ufumbuzi kwa changamoto zinazowakabili.

Nawapongeza kwa uamuzi wenu wa kutafuta vyuo vikuu rafiki vilivyoko katika nchi mbalimbali duniani mnavyoweza kushirikiana navyo. Endeleeni kufanya hivyo kwani vyuo vikuu vingi duniani hufanya hivyo. Hamtakuwa wa kwanza na wala hamtakuwa mnafanya jambo la kustaajabisha. Mnaweza, mkipenda, kuwaomba Mabalozi wetu waliopo katika nchi mbalimbali duniani wawasaidie. Ni wajibu wao kufanya hivyo kwani kusaidia kusukuma maendeleo ya hapa nchini kutoka huko waliko ndilo jukumu lao la msingi. Vile vile, nimefurahishwa na mipango yenu ya baadaye ya kuwa na matawi katika mikoa mbalimbali nchini. Hongereni kwa uamuzi wenu wa busara. Lazima Chuo kitanuke kwa maana ya kuwa kikubwa zaidi, makao makuu na kwa kuwa na vyuo vishiriki na shule au vitivo sehemu mbalimbali nchini.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Kazi iliyo mbele yenu ni kubwa, hivyo ni vyema kuweka mikakati mizuri na mipango thabiti ya utekelezaji na ufuatiliaji wa dhamira yenu hiyo njema. Rai yangu kwenu ni kuwaomba muwe wabunifu zaidi hasa katika kutafuta vyanzo vingine vya mapato vitakavyosaidia Chuo kujiendesha bila kutegemea ada peke yake. Chuo kiangalie uwezekano wa kufanya shughuli zitakazowaingizia mapato kama vile kufanya shughuli za kutoa ushauri. Pia muangalie uwezekano wa kuwekeza wenyewe kwenye miradi ya kiuchumi au kwa kushirikiana na wawekezaji katika baadhi ya maeneo.

Kuhusu nafasi mbili za ufadhili nilizopewa na Chuo kikuu cha Tun Abdul Razak cha Malaysia, nitafuatilia kujua kilichoendelea na kinachoendelea. Je, nafasi hizo bado zipo? Zikiwepo, nitawasiliana na wahusika waangalie uwezekano wa kuwapeni. Kama zimeshagawiwa basi tusubiri safari ijayo. Kwa masuala ya ardhi na maombi mengine nimeyasikia, yaleteni tuangalie namna ya kusaidiana.

Ndugu Makamu Mkuu wa Chuo, na

Wafanyakazi wote wa Chuo cha Waislamu cha Morogoro;

Napenda kuwakumbusha kuwa mnayo dhamana kubwa na wajibu mkubwa na wa kihistoria. Ule ukweli kwamba ni mara ya kwanza kwa Taasisi ya Waislamu wazawa kuwa na Chuo Kikuu inawapeni wajibu maalum wa kuhakikisha Chuo kinafanikiwa. Ni mtihani na changamoto ya aina yake kuthibitisha kuwa Waislamu nao wanaweza kuwa na Chuo kizuri na chenye kutoa elimu ya ubora wa hali ya juu. Kwa sababu hiyo hamna budi kuhakikisha kuwa mna mipango mizuri ya kujenga Chuo cha hadhi na ubora wa hali ya juu. Ihakikishwe kuwa mipango hiyo inatekelezwa kwa ukamilifu.

Aidha jumuiya yote inao wajibu wa kufanya kazi kwa bidii, ubunifu, maarifa na weledi ili dhima hiyo ya Chuo iweze kutimizwa kwa ukamilifu. Timizeni wajibu wenu ipasavyo ili jina la Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro likue haraka. Sifa yake isambae na kuvuma kote nchini. Chuo kifanye vizuri ili wanafunzi waone fahari kuwa wahitimu wa Chuo hiki. Chuo ambacho, wazazi wapende kuleta vijana wao kuja kusoma hapa. Kwa jinsi Mkuu wa Chuo alivyoeleza, mimi nina imani mnaweza, fanyeni kweli.





Ndugu Wanafunzi wa Chuo cha Waislamu cha Morogoro;

Naomba wote muone fahari ya kuwa wanafunzi katika Chuo cha kihistoria hapa nchini. Nawasihi mjitume kwa kadri ya uwezo na vipaji mlivyopewa na Mwenyezi Mungu mfanikishe kile kilichowaleta. Jifunzeni kwa bidii mfaulu vizuri ili mkihitimu muwe kielelezo kizuri cha mafanikio na ubora wa Chuo Kikuu Cha Waislamu cha Morogoro. Muwe Mabalozi na kioo cha ufanisi wa Chuo hiki. Nawasihi mjiepushe na mambo yatakayowapunguzia muda au kuwaondoa katika shughuli ya msingi iliyowaleta hapa ya kujifunza mpate digrii katika fani mliyochagua mwenyewe kuisomea. Vishawishi ni vingi na wapo watu wengi wanaopanga kuwashawishi mtumie muda wenu adhimu kufanya wanayoyataka wao ambayo mkishiriki huwatoa kwenye malengo na kutekeleza yao. Mambo ya dunia ya nje ya Chuo ni mengi huna budi kutambua lipi ufanye na lipi usifanye na kwa wakati gani!

Mwanafunzi wa Chuo Kikuu ni mtu mzima, si mtoto. Lazima ujue kuwa unawajibika kwa kila unaloamua na kutenda. Amua kuwajibika vizuri. Fikiri kabla ya kutenda, changanua lipi ni lipi kabla ya kufanya uamuzi wa kile unachotaka kufanya. Wakati wote uongozwe na busara na hekima na siyo jazba na ushabiki wa matakwa ya kundi. Kama ni jema fanya na kama si jema usifanye. Kwanza tambua wewe ni nani na uko hapa kwa ajili gani. Lazima ujue kuwa hatma ya yote uko peke yako. Utafaulu au kufeli wewe. Utapata shahada wewe na si mtu mwingine. Hakuna ubia wa kufaulu au kufeli au kiwango cha kufaulu. It will always remain personal. Katika masomo unanufaika wewe. Shirikiana na wengi lakini usisahau kujali maslahi yako. Maslahi ya wengi yasiyojumuisha yako, yahoji vizuri kabla ya kuamua kushiriki au kufanya. Vinginevyo labda kama umeamua kujitoa muhanga, uwe shujaa. Hata kwa hilo, sijui utakuwa shujaa wa nani.

Mabibi na Mabwana;

Kabla ya kumaliza napenda kutambua na kumshukuru Rais wa Awamu ya Tatu, Mheshimiwa Benjamin Mkapa na viongozi wa MDF kwa juhudi zao za pamoja zilizowezesha Chuo hiki kuwepo. Nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipowashukuru wananchi wanaokizunguka Chuo kwa ujirani mwema na wakazi wa Morogoro kwa ujumla kwa kukipokea vizuri na kuishi na wanajumuiya wa Chuo hiki kwa upendo mkubwa. Naomba muendelee na moyo na ushirikiano huo.

Baada ya kusema hayo, nawashukuru sana kwa kunialika. Nawatakia kila la heri na mafanikio tele.

Asanteni sana kwa kunisikiliza.

No comments: