Saturday, March 06, 2010

Mkurugenzi wa TAMWA apata Tuzo Muhimu!

Mkurugenzi wa TAMWA Ananilea Nkya akipiga posi na tuzo nje ya ofisi za TAMWA huko Sinza mara baada ya kuwasili kitoka ubalozi wa Marekani

HOTUBA YA MKURUGENZI MTENDAJI WA CHAMA CHA WANAHABARI WANAWAKE NCHINI (TAMWA), ANANILEA NKYA KATIKA MKUTANO WA WANAHABARI, UBALOZI WA MAREKANI KWA AJILI YA KUKABIDHIWA TUZO YA MWANAMKE JASIRI WA TANZANIA KWA MWAKA 2010


Mheshimiwa Balozi wa Marekani, Alfonso Lenhardt,
Wafanyakazi wa Ubalozi wa Marekani,
Wanahabari na wanaharakati wenzangu,
Wageni waalikwa,
Mabibi na Mabwana.


Ninashukuru kwa kupata heshima hii kubwa ya kusimama mbele yenu kama mteule wa tuzo ya Mwanamke Jasiri wa Tanzania kwa mwaka 2010.

Kwa heshima na taadhima nianze kwa kushukuru Ubalozi wa Marekani hapa nchini na wananchi wa Marekani kwa ujumla kwa kunichagua mimi kama MWANAMKE JASIRI WA TANZANIA KWA MWAKA 2010 kutokana na juhudi na ubunifu wa kutumia vyombo vya habari katika kuimarisha usawa, fursa na haki za wanawake na watoto wa kike wa Tanzania.

Sina shaka kwamba Ubalozi wa Marekani ulifanya utafiti kikamilifu na tena kwa mapana na kupata majina mengi tu, maana kuwa jasiri maana yake ni kuzungumza kwa sauti kile unachokiamini kuhusu uonevu na uvunjifu wa haki hasa za wanyonge ili hatua ziweze kuchukuliwa kurekebisha hali hiyo. Katika mapambano ya kutetea haki za watu wa hali ya chini hasa wanawake, wasichana na watoto hapa nchini, wako watu wengi wanaofanya harakati hizi kwa juhudi kubwa mijini na vijijini. Hivyo mimi kuchaguliwa miongoni mwao, ni ishara kwamba Marekani imetambua mapambano yetu, ambapo mimi ni mwakilishi wa wapambanaji wengi.

Kwa hiyo, nachukua fursa hii kushukuru na kuipongeza serikali ya Marekani kwa kubuni TUZO YA MWANAMKE JASIRI. Kwa kubuni tuzo hii serikali ya Marekani imedhihirisha kuwa inaunga mkono mapambano mbali mbali ya wanawake katika kupigania haki zao.

Wanawake wanapambana kuweza kushiriki katika masuala ya maendeleo; wanapambana ili waweze kunufaika na rasilimali mbali mbali za taifa, wanapambana kupata haki yao kwenye huduma ya afya, elimu, mirathi, uchumi na uongozi wa nchi yao.

Natambua kuwa tuzo hii ilishatolewa kwa wanawake wawili hapa nchini; Helen-Kijo Bisimba (2008) kwa ujasiri wake mkubwa wa kutetea haki za binadamu akiwa Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu na Mheshimiwa Anne Kilango Malecela (Mbunge wa Same Mashariki) kutokana na ujasiri wake katika kupambana na ufisadi.

Nina hakika, baada ya muda, tuzo hii itazaa matunda ya neema hasa kwa wanawake wengi wanaotaabika kwa madhila mbali mbali mijini na vijijini. Wanawake ambao wanapambana ili wapate haki ya kuthaminiwa utu wao. Wanawake wengi hapa nchini hawana amani wala furaha kwa sababu mifumo gandamizi imewapora haki na fursa ya kutoa maamuzi kuhusu mambo yanayohusu maisha yao na familia zao na wameporwa pia fursa ya kushiriki katika vyombo vya kutoa maamuzi kuhusu namna wanavyotaka nchi yao iendeshewe.

Ninaamini kuwa kama taifa letu lingejenga mazingira sahihi ya kuwawezesha wanawake kuwa sehemu ya rasilimali uongozi katika ngazi mbali mbali, hakika wangedhihirishia taifa kuwa wana uwezo mkubwa wa kuongoza, na bila shaka nchi yetu ingenufaika kiuchumi, kisiasa na kijamii kuanzia ngazi ya kitongoji hadi taifa. Kwa hali hiyo tungepiga hatua kubwa katika nyanja ya demokrasia na maendeleo na kuweza kufikia ndoto ya ukombozi siyo Tanzania pekee bali pia ukombozi wa Bara la Afrika.

Wanawake na wasichana na hata wanaume na vijana wengi hapa nchini nao wameonyesha uwezo mkubwa wa kuhimili changamoto zinazotokana na sera mbaya za uchumi. Wengi wao wamekuwa wakitegemea kilimo cha jembe la mkono na biashara ndogo ndogo kuweza kujikimu huku wakiwa na jukumu kubwa la kulea yatima ambao wanaongezeka kila siku na kuwahudumia wagonjwa wa UKIMWI ambao hulazimika kurudishwa majumbani kutokana na mfumo duni wa afya.

Wanaume, Wanawake na vijana hawa wa kike na wa kiume wa taifa hili siyo tu wamedhihirisha kuwa ni ni watu jasiri, bali pia ni watu wenye uwezo wa kuibadilisha Tanzania kuwa ni mahali pazuri pa kuishi watu wa wakundi yote wanaume, wanawake, wazee na vijana, wenye ulemavu na wasio na ulemavu. Ndiyo sababu Tanzania inahitaji kuwa na mipango ya maendeleo yenye malengo mahususi na mikakati madhubuti ya utekelezaji wa mipango hiyo. Mipango hiyo ni muhimu itengenezwe kwa kuzingatia sauti, mitizamo, uwezo na mahitaji ya watu wa ngazi za chini na wanaharakati na wanahabari wana wajibu wa kushinikiza bila woga hatua zichukuliwe kutekeleza mipango hiyo kwa ufanisi.

Ukatili wa kijinsia una athari mbaya kwa wanawake na wasichama kwa kuwa unawaathiri kisaikolojia na hivyo kushindwa kutekeleza wajibu wa kuboresha maisha yao na maisha ya wale wanaowategemea. Sheria zilizopitwa na wakati ambazo zinakoleza ukatili dhidi ya wanawake na watoto wa kike zinahitaji taifa kupata viongozi imara na hasa Wabunge wenye ujasiri wa kuisimamia serikali ili iwajibike kubadilishe sheria hizo. Sheria hizo mbaya ni pamoja na ile ya ndoa ya mwaka 1971 ambayo inaruhusu mtoto wa chini ya miaka 18 kuolewa na hivyo kumkosesha haki yake ya kupata elimu na kuhatarisha maisha yake endapo atapata ujauzito.

Mheshimiwa Balozi,

Mimi ujasiri nilionao kwa kiwango kikubwa umechangiwa na taaluma yangu ya uandishi wa habari na uanaharakati wa masuala ya jinsia, demokrasia, maendeleo na haki za binadamu.

Kunichagua mimi kama mwanamke jasiri mwaka huu 2010, ni motisha kwa wanahabari na wahaharakati; wanawake na wanaume ambao wamekuwa wakijishughulisha kwa namna mbali mbali kuleta mabadiliko katika mila mbaya, mifumo, imani na sera gandamizi ambazo zinabagua na kuwatupa pembezoni wanawake na wasichana.

Kwa hiyo, naipokea tuzo hii kwa niaba ya wanawake wote wa Tanzania na wanaume na wanawake wa umri mbali mbali ambao nimekuwa ninashirikiana nao katika vyombo vya habari, kwenye harakati na Chama cha Wanahabari Wanawake nchini (TAMWA) ambacho tangu kilipoanzishwa miaka 21 iliyopita kimekuwa kikipaza sauti kutetea haki na fursa za wanawake, wasichana na watoto. Tuzo hii niliyoipata leo, sote tuichukulie kama changamoto, mwanzo mpya na kitu cha pekee cha kututia moyo katika kuendeleza jitihada za kutetea usawa, fursa na haki kwa wanawake, wanawake wasichana na watoto wa Tanzania.

Mheshimiwa Balozi,

Kuna msemo wa Kiswahili usemao “Sema Usiogope Sema”. Naichukulia hii tuzo ya ujasiri niliyopewa leo kama ishara kwamba Marekani inatambua kwamba mapambano katika ngazi ya familia, kitaifa, kikanda na kimataifa kwa ajili ya kuimarisha usawa wa jinsia, haki za binadamu na uhusiano mzuri baina ya mataifa ni muhimili muhimu katika kujenga amani duniani.

Sisi wanaharakati wa Tanzania tunashikamana na wanaharakati wengine duniani kote katika mapambano ya kubadilisha dunia ili iwe mahali pazuri pa kuishi watu wote wanaume na wanawake, maskini na matajiri wa rika zote.

Mhusiano usio sawa katika ngazi ya kimataifa unaguza na kuleta amthari mbaya katika mahusiano ya kikanda, kitaifa na hata ngazi ya familia. Mahusiano kama hayo huchangia moja kwa moja kuwepo na mahusiano yasiyo na uwiano sawa baina ya wanaume na wanawake. Mahusiano yasiyo na usawa huchangia kwa kiasi kikubwa vitendo vya kikatili na ukiukwaji wa haki za binadamu siyo tu dhidi ya wanawake na wasichana, bali pia dhidi ya makundi mengine yaliyoko pembezoni. Hali hii iko dhahiri katika Bara letu la Afrika ambalo limekuwa likishuhudia uporaji wa ardhi ya wanyonye, wimbi la rushwa na ufisadi unaohusisha baadhi ya viongozi na wafanya biasharawakubwa.

Ni imani yangu kuwa tuzo hii ya MWANAMKE JASIRI itaendelea kuimarika na kuwa kichocheo kwa wanaharakati wote ili wasichoke na mapambano, hata yatachukue muda mrefu kiasi gani maana dunia iliyo bora na salama kwa wanawake na watoto ndiyo itatengeneza dunia bora, salama na yenye neema na furaha tele kwa watu wote.

Nawashukuru wote kwa kunisikiliza,

Nakushukuru Mheshimiwa balozi na wananchi wa Marekani kwa wazo hili zuri la kutoa tuzo ya mwanamke jasiri.

Ananilea Nkya

Executive Director (TAMWA)

02/03/2010
*****************************************************
Nami nasema HONGERA Dada Nkya! Kweli umetoka mbali na unfanya kazi nzuri mno TAMWA! - Chemi

1 comment:

Paul Mbenna said...

Hongera Mama Ananilea Nkya. Juhudi zako zimewasaidia wengi mijini na vijijini. Paul Mbenna