Thursday, December 01, 2011

TANESCO Kupanda Bei ya Umeme 155%!!! Nchi Imehribika! Mkutano Kesho!

Ujumbe wanaTEHAMA- Kupinga kupanda kwa Gharama za Umeme


Kesho tarehe 2 Disemba 2011 katika Ukumbi wa Makumbusho Dar es salaam (mkabala na IFM) kuanzia saa 4 asubuhi EWURA imeitisha Mkutano wa Wadau kujadili ombi la TANESCO la kupandisha bei ya umeme kwa wastani wa 155% (zaidi ya mara tatu ya bei ya sasa).

Nawaomba wanamtandao wote tuhamasishe umma kwa kutumia TEHAMA (sms, facebook, twitter, email na njia nyingine) ili wananchi waweze kuhudhuria mkutano husika kwa wingi na kutoa maoni.

Mtakumbuka kwamba tarehe 23 Novemba 2011 nilitoa taarifa kwa umma kwamba Serikali inapaswa kusitisha ombi la dharura la kupandisha bei ya umeme kwa kiwango kikubwa ili kuepusha athari katika usalama na uchumi kutokana na mfumuko wa bei na kupanda kwa gharama za maisha. Aidha, serikali inapaswa kuchukua hatua za haraka kulinusuru Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) dhidi ya mzigo mkubwa wa gharama unaotokana na ufisadi wa muda mrefu katika mikataba ya gesi asilia na gharama za mitambo ya kufua umeme wa dharura badala ya kuweka mkazo katika kuongeza bei ya umeme kwa wananchi wa kawaida.

Izingatiwe kuwa tarehe 9 Novemba 2011 Mamlamka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) ilipokea ombi la dharura toka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) la kuidhinisha ongezeko la bei za huduma ya umeme kwa wastani wa asilimia 155 ya bei ya sasa (zaidi ya mara tatu).

Naomba umma wa watanzania uzingatie athari za maombi hayo katika uchumi wa nchi na maisha ya wananchi kwa ujumla hivyo mjadala wa kitaifa unahitajika na natoa mwito kwa wananchi kuweza kutoa maoni yao kuanzia sasa. Aidha ni muhimu kwa wananchi kushiriki kwa wingi katika mkutano wa kukusanya maoni ya wadau ulioitishwa na EWURA tarehe 2 Disemba 2011.

Umma wa watanzania ufahamu kwamba ongezeko hili sio ombi la TANESCO pekee bali ni agizo kutoka kwa serikali kwa kurejea maelezo ya Waziri wa Nishati na Madini William Ngeleja bungeni katika mkutano wa nne wa bunge na kusisitizwa na kauli ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda mwezi Septemba 2011 akihutubia mkutano wa hadhara mkoani Mara.

Namshangaa Rais Jakaya Kikwete katika hotuba yake kwa taifa tarehe 18 Novemba 2011 alipozungumzia utekelezaji wa mpango wa dharura wa umeme hakuwaeleza watanzania kwamba uwasilishaji wa ombi hilo ni sehemu ya mpango huo wa dharura ambao utawaongezea wananchi bei ya umeme na gharama na maisha na hivyo kuathiri utekelezaji wa ahadi ya maisha bora kwa kila mtanzania.

Wananchi wakumbuke kwamba hii ni mara ya pili katika kipindi cha takribani mwaka mmoja kwa TANESCO kupandisha bei ya umeme; mara ya kwanza ikiwa mwezi Januari 2011 ambapo umeme ulipanda kwa asilimia 18.5 na kuchangia katika kupanda kwa gharama za uzalishaji katika nchi na kuongeza ugumu wa maisha kwa wananchi.

Ombi la TANESCO la wakati huo la kupandisha umeme lilikuwa ni asilimia 34 likakataliwa na EWURA na kushushwa mpaka asilimia 18.5, sasa Rais Kikwete, Waziri Mkuu Pinda na Waziri Ngeleja wanapaswa kuwaeleza watanzania sababu za kufanya ombi hilo la dharura kuwa la wastani wa asilimia 155 ili wananchi waweze kutoa maoni kwa kuzingatia mzigo ambao umma unataka kubebeshwa.

Pamoja na matatizo ya kifedha ya TANESCO ambayo serikali inapaswa kuyashughulikia kwa pamoja na mambo mengine kutoa ruzuku katika kipindi hiki cha mpito; gharama kubwa za uzalishaji zinazolikabili shirika zinachangiwa na ufisadi wa muda mrefu katika mikataba ikiwemo ya uzalishaji wa gesi na ukodishaji wa mitambo ya kufua na pia maamuzi ya kukopa kibiashara katika kutekeleza mpango wa dharura wa umeme.

Kabla ya kuongeza bei ya umeme kwa watanzania wa kawaida, Serikali iwaeleze wananchi imewapunguzia mzigo kiasi gani kwa kupitia upya mikataba ya kifisadi inayolinyonya Shirika la Umeme Tanzania kama ilivyopendekezwa kwenye ripoti mbalimbali ikiwemo katika maazimio ya Bunge ya mwaka 2008 juu ya mkataba wa ukodishaji wa mitambo ya kufua umeme ya Kampuni ya Richmond Develepment Company LLC ambapo orodha ya mikataba na makampuni mengine ilitajwa.

Aidha, umma uelezwe pia ukweli iwapo uamuzi wa kuchukua mikopo ya kibiashara yenye riba kubwa umeongeza zaidi gharama za uzalishaji wa umeme na hivyo kuifanya TANESCO iongeze zaidi bei ya umeme kwa wateja ikizingatiwa kuwa tarehe 15 Julai 2011 na 13 Agosti 2011, nilisisitiza bungeni serikali ipunguze bajeti katika maeneo mengine yasiyokuwa ya lazima na kuelekeza rasilimali nyingi zaidi kwenye umeme bila kuongeza mzigo mkubwa wa riba utakaolipwa na wananchi kupitia ongezeko la bei.

Uamuzi huu wa kupandisha kwa kiwango kikubwa bei ya umeme utasababisha ongezeko la ziada la mfumuko wa bei hali ambayo ni tishio wa usalama na uchumi wa nchi na maisha ya wananchi kwa ujumla.

Serikali izingatie kwamba mfumuko wa bei nchini hivi sasa umefikia asilimia 17.9 na bidhaa zinazochangia mfumuko huo kwa kiwango kikubwa ni vyakula, mafuta na umeme. Kupanda kwa bei kwenye sekta ya nishati pekee kumekuwa kwa asilimia 37.4 na kusababisha kupanda kwa gharama za maisha, sasa viongozi wajiulize itakuwaje umeme ukapopanda kwa wastani wa asilimia 155.

Wananchi wakumbuke kwamba katika hotuba yake kwa taifa tarehe 18 Novemba 2011 Rais Kikwete ameelezea kwamba mfumuko wa bei na kuporomoka kwa thamani ya shilingi ya Tanzania dhidi ya dola kwa ujumla kumetokana na uchumi wa nchi mbalimbali duniani hususani za Ukanda wa Sarafu ya Ulaya (Eurozone) kuwa katika kipindi kigumu na cha mashaka na kueleza kwamba suluhisho la matatizo la uchumi wetu litategemea uchumi wao.

Kauli hii imedhihirisha kwamba Serikali haina mpango wa haraka wa kukabiliana na mfumuko wa bei, kuporomoka kwa shilingi na kupanda kwa gharama za maisha. Hali itakuwa mbaya zaidi iwapo tutaruhusu pamoja na sababu za nje ya nchi yetu tukaongeza vyanzo vya ndani vya kuongezeka kwa gharama za uzalishaji na bei za bidhaa kwa kupandisha bei ya nishati ya umeme ambayo chanzo chake ni hapa hapa nchini. Hivyo, mpango huu wa kupandisha bei ya umeme kwa wastani wa asilimia 155 unapaswa kusitishwa ama kubadilishwa kwa kulinda maslahi ya makundi mbalimbali kwa kuzingatia aina za matumizi.

John Mnyika (Mb)

Waziri Kivuli wa Nishati na Madini

1/12/2011

2 comments:

Anonymous said...

Je, wakipandisha bei ya umeme kwa kiasi kikubwa hivyo ina maana itapatikana 24/7 bila kukatika? Au, tutaendelea na hii hali ya unreliable umeme?

Anonymous said...

Kwakusema ukweli tanesco pasua hata kukiwa na janga la umeme tanesco magomeni simu zao zote hazipatikani na ukiangalia watu wanalipa umeme kwa bei kubwa sana kwani sasa sio wakati wakuwanyazia waziri wa nishati na madini aangalie sana hichi kitendo na pia ramadhani inakuja wataanza mitindo yao ya kukata umeme kwani hao walio kuwa wameishikilia serikali wanafanya nini?