Thursday, January 22, 2015

Viongozi wa South Sudan Wafika Makubaliano

Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Naibu Rais wa Afrika Kusini Cyril
Ramaphosa (kulia) na Bw. Bw. Deng Alor Kuol  wakifurahia wakati  Rais
Salva Kiir Mayardiy wa Sudan ya Kusini (wa pili kushoto) na Makamu wa
Rais wa zamani wa Sudan Dkt Riek Machar Teny (wa pili kulia) wakipeana
mikono na kubadilishana nyaraka baada ya kutia saini mkatana wa
makubaliano ya kukiunganisha upya chama cha SPLM cha Sudani Kusini
katika hoteli ya Ngurdoto jijini Arusha Jumatano Januari 21, 2015
usiku.  PICHA NA IKULU


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

MKATABA wa kujenga tena umoja na kukiunganisha upya Chama Tawala cha Sudan Kusini cha Sudan People’s Liberation Movement (SPLM) ulitiwa saini usiku wa jana, Jumatano, Januari 22, 2015, katika sherehe ya kufana iliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Ngurdoto, Wilaya ya Arumeru, Mkoa wa Arusha.
Mkataba huo unaojulikana kama Agreement on the Re-unification of Sudan People’s Liberation Movement umepongezwa kuwa ni hatua muhimu katika kulitoa taifa changa la Sudan Kusini katika hali ya machafuko, vita vya wenyewe kwa wenyewe, kutoelewana na kutoaminiana, mambo ambayo yameligubika taifa hilo tokea mwishoni mwa 2013 wakati kutokuelewana kulipozuka ndani ya SPLM na hatimaye katika Serikali ya nchi hiyo.
Baada ya siku nzima ya mawasiliano na majadiliano baina ya pande zinazovutana ndani ya chama hicho pamoja na viongozi wa nchi jirani na rafiki na Sudan Kusini, viongozi watatu wa vikundi vinavyopingana ndani ya SPLM walitia saini Mkataba huo muhimu sana.
Viongozi waliotia saini ni Mheshimiwa Salva Kiir Mayardit, Rais wa Sudan Kusini ambaye pia ni Mwenyekiti wa SPLM na anayeongoza kundi linalojulikana kama SPLM in Government (SPLM-IG), Mheshimiwa Dkt. Riek Machar ambaye alikuwa Makamu Mwenyekiti wa SPLM na pia aliyekuwa Makamu wa Rais wa Sudan Kusini anayeongoza kundi la SPLM in Opposition (SPLM-IO) na Dkt. Deng Alor Kuol ambaye anaongoza kundi la SPLM Leaders- Former Detainees (SPLM Leaders – FD).
Sherehe hiyo ilishuhudiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) ambacho ndicho kimesimamia mazungumzo yaliyozaa Mkataba huo. Rais Kikwete pia ndiye mdhamini mkuu wa Mkataba huo.
Wengine walioshuhudia tukio hilo muhimu ni Rais wa Uganda, Mheshimiwa Jenerali Yoweri Kaguta Museveni; Rais Uhuru Muigai Kenyatta wa Kenya; Naibu wa Rais wa Jamhuri ya Afrika Kusini Mheshimiwa Cyril Ramaphosa, Makamu Mwenyekiti wa zamani wa CCM Mheshimiwa John Samwel Malecela ambaye ndiye alikuwa mwenyekiti wa mazungumzo yaliyozaa Mkataba huo na Katibu Mkuu wa CCM Mheshimiwa Abdulrahman Kinana ambaye alikuwa mwezeshaji wa mazungumzo.
Mazungumzo yaliyozaa Mkataba huo yalianza mwishoni mwa mwaka jana baada ya Rais Kikwete na Chama cha CCM kuombwa na Rais Kiir Mayardit kukubali chama hicho tawala cha Tanzania kutumia uzoefu na ujuzi wake wa miaka mingi wa uongozi na siasa kujaribu kuleta suluhu ndani ya SPLM.
Mazungumzo hayo ya kutafuta suluhu ambayo yamefanyika kwa awamu mbili, ya kwanza yakiwa yamefanyika Oktoba mwaka jana na pili yakiwa yameanza mwanzoni mwa mwezi huu, Januari 2015,  yameongeza thamani kwenye mazungumzo mengine yanayofanyika Addis Ababa, Ethiopia chini ya usimamizi wa taasisi ya IGAD na yanayojadili jinsi ya kurejesha amani nchini humo.
Viongozi wa SPLM wanaamini kuwa kwa sababu mgogoro wa kisiasa nchini mwao ulianzia ndani ya chama hicho na kwa sababu SPLM ndicho chombo pekee ambacho kinawaunganisha wananchi wote wa Sudan Kusini, basi busara inaelekeza kuwa suluhu ianze kutafutwa ndani ya chama hicho.
Mkataba wa jana, kimsingi, unalenga kuweka mazingira ya kujenga utulivu, maelewano, amani na umoja wa kudumu ndani ya chama hicho na nchini humo kwa kuhakikisha kuwa utekelezaji wa mambo ya msingi yaliyokubaliwa kuhusu shughuli za siasa, uongozi na oganisheni ya chama hicho yanafanyika bila kukawia.
Mkataba huo pia unalenga kuhakikisha kuwa chama cha SPLM kinabuni na kutekeleza sera za kuondokana na ukabila, makundi yenye mitazamo finyu na mwenendo wa kijeshi katika siasa za Sudan Kusini.
Aidha, Mkataba huo unalenga kuhakikisha kuwa chama cha SPLM kinafanya mageuzi ya kuanza kujenga utamaduni wa kuvumiliana na ujenzi wa misingi ya demokrasia.
Mkataba huo pia unataka watu wote ambao walishiriki katika mauaji na umwagaji damu katika vita vya wenyewe kwa wenyewe wasiruhusiwe kugombea wala kushika nafasi ya uongozi wa umma ndani ya chama hicho.
Pia viongozi wote wa Sudan Kusini wanatakiwa, chini ya Mkataba huo, kuwaomba radhi wananchi wa nchi hiyo ya Sudan Kusini kwa kuruhusu nchi hiyo kuingia katika machafuko ya umwagaji damu mkubwa.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu – Dar es Salaam.
22 Januari,2015

No comments: