Sunday, March 30, 2008

Fomu za Tuzo za Vinara Zatolewa

Fomu za ushiriki katika kinyang'anyiro cha kuwania Tuzo za Vinara wa
filamu Tanzania 2007/8 zimeanza rasmi kutolewa jana katika vituo
mbalimbali nchini ikiwa ni hatua ya kwanza kabla ya kutolewa kwa tuzo
hizo.

Tuzo hizo zitakazotolewa kwa mara ya kwanza nchini, zimeandaliwa na
kampuni ya One Game Promotions na kudhaminiwa na Kampuni ya Bia
Tanzania (TBL) kupitia bia yake ya dovu Power Malt.

Mratibu tuzo hizo, Khadija Khalili, amesema kuwa, kutokana na sababu
zilizo nje ya uwezo wao, fomu hizo zilichelewa kutoka kwa tarehe ya
awali hivyo kusababisha kuongezwa kwa muda wa kurejeshwa fomu na
kupokea filamu zitakazoshiriki katika tuzo hizo hadi Aprili 18 badala
ya Machi 31 kama ilivyotangazwa awali.

Alisema watengenezaji wa filamu nchini wanakaribishwa kutuma nakala za
filamu zilizotengenezwa kati ya Januari 2007 hadi Machi 31, 2008, kwa
ajili ya kuwania tuzo hizo.

Khalili alisema kuwa, jopo la majaji litakutana baada ya Aprili 18
kuchagua watakaowania tuzo za Vinara wa Filamu Tanzania 2008.
Alisema fomu za kushiriki kuwania tuzo hizo zinapatikana katika vituo
vilivyotangazwa awali ambavyo ni ofisi za Baraza la Sanaa la Taifa
(BASATA) kwa Omari Mayanga, pia zinapatikana kwa wasambazaji wa filamu
ambao ni Wananchi Wote, GMC, Kapico na Game First Quality.

"Fomu zilizojazwa na nakala ya filamu iliyopo kwenye mfumo wa VCD na
DVD zitumwe kwenye ofisi za BASATA zilizopo Ilala Bungoni jijini Dar
es Salaam au ofisi ya One Game Promotion," alisema.

Vipengele vitavyoangaliwa na majaji katika filamu hizo kuwa ni Filamu
Bora ya Mwaka, Muigizaji Bora wa Mwaka wa Kiume, Muigizaji Bora wa
Mwaka wa Kike, Muigizaji Bora Chipukizi wa Mwaka wa Kiume, Muigizaji
Bora Chipukizi wa Mwaka wa Kike, Mwongozaji Sinema Bora wa Mwaka,
Mchekeshaji Bora wa Mwaka, Mwandishi Bora wa Filamu, Mtunzi Bora wa
Filamu, Filamu Bora ya kutisha, Muigizaji Mwandamizii Bora wa kike
(supporting actor), Muigizaji Bora Mwandamizi wa Kike, Adui Bora
kwenye Filamu, Wimbo Bora wa Mwaka (Sound Track), Mhariri Bora wa
Filamu ambao wote watapata tuzo na zawadi. Pia itatolewa tuzo ya
heshima kwa wale waliotoa machango wao kukuza sanaa nchini.

No comments: