Monday, September 06, 2010

MFUMO WETU WA ELIMU NA CHANGAMOTO ZAKE!

Ubungo mwaka 1980. Mwanafunzi wa Chuo Kikuu alienda kunywa pombe kwenye baa fulani. Wakati ule wanafunzi wa UDSM walikuwa na hela shauri ya posho zao kutoka serikalini. Jamaa alilewa. Akaanza kuongea kimombo/kiingereza. Alipigwa na wananchi wenye hasira kwa vile jamaa eti alikuwa na KASUMBA!

Wadau waliosoma Tanzania tangu miaka ya sabini katikati waliposema kuwa eti Shule za msingi zifundishwe kwa kiswahili halafu sekondari na kuendelea ziwe English wtakubaliana na mada huu.

Na mimi siku zote nasema maana ya shule ya msingi ni nini? Si ndo msingi? Sasa kama huna msingi mzuri si utapata shida baadaye. Katika jumuiya ya Afrika Mashariki sisi waTanzania ndo tuna matatizo ya kuongea na kuandika kiingereza shauri ya kukosa msingi mzuri wa Kiingereza shuleni.

Fikiria watoto wanafundishwa kiingerea na watu ambao hawana msingi wa lugha, yaani lugha yao ni broken. Kuna dada moja ambaye nilisoma naye Tabora Girls alikuwa ancheka akisema, "Chemi, si unakumbuka English ilivyokuwa taabu kwangu, basi mimi ndio mwalimu wa English katika shule ya sekondari fulani! Si maajabu hayo" Maajabu ndo yeye eti alijua kiingerza kuliko wengine.

Hata hapa USA unakuta mTanzania ana Masters/Ph.D lakikni anakosa kazi ya maana kwa vile hajui kuongea kiingereza vizuri. WaKenya na WaGanda hawana shida hiyo. Naukumbuka miaka ya 90 mwanzo nilienda kwenye kijiji fulani huko Uganda. Wau masjini watoto wamevaa nguo zilizochanika hlafu mavumbi matupu lakini walikuwa wanajua kiingereza kizuri.

Nashukuru kuwa sasa Tanzania wameruhusu shule za msingi za kiingereza kwa muda, lakini ni za kulipia (private). Lakini ni wakina nana wanafaidi? Ndo matokeo ya KASUMBA.

Mwaka 1993 (?)...mara baada ya kuruhusu vyama vingi, Chifu Abdallah Fundikira alihubiria umati mkubwa wa wananchi huko Jangwani. Chama chake ilikuwa UMD. Alisema, "Mwalimu Nyerere alikuwa anaongea Kiingera kizuri sana...The Queen's English, halafui alitaka nyie msiongee!" (Nilikuwa mwandishi wa habari Daily News wakati huu, na iliandika hiyo kwatika original copy, lakini ilifutwa kabla ya kuchapishwa!)



***********************************************************************



Imeandikwa na Malkiory William Matiya

Waswahili walisema, mkunje samaki angali mbichi. Wataalamu na watafiti katika fani mbali mbali wanatuambia kuwa hali/tabia ya mtu mzima kwa kiwango kikubwa ni matokeo ya mazingira ya makuzi/malezi yake ya utotoni. Mfano tabia kama vile ukatili, ukimya, woga, wasiwasi, hasira, okorofi, furaha, upendo, kujiamini n.k. ukubwani ni baadhi tu ya matokeo hayo.

Kama hivyo ndivyo basi, nadhani utakubaliana nami kuwa tunahitaji mfumo dhabiti na bora wa kujifunza/ufundishaji katika ngazi ya elimu ya awali/kindergarten na msingi. Ni dhahiri kuwa tendo la kijifunza linakuwa limekamilika pale ambapo mabadiliko ya kudumu ya kitabia yanapoanza kujitokeza kwa walengwa ambao ni wanafunzi. Hivyo basi, inatubidi tukubali ukweli kuwa mabadiliko chanya ya kitabia yatatokana na ufundishaji/uelimishaji chanya pia.

Mtoto wa kitanzania anapoanza elimu ya msingi hufundishwa masomo yote kwa lugha ya kiswahili isipokuwa somo moja tu la kiingereza kwa miaka yote saba ya elimu yake ya msingi. Baada ya hapo mambo hubadilika ghafla pale mwanafunzi anapoanza elimu ya sekondari, kwani masomo yote huwafundishwa kwa kiengereza isipokuwa somo la kiswahili.

Tatizo hili huchangia kwa kiwango kikubwa kupunguza kasi, ari na uwezo wa mwanafunzi kujifunza, kwasababu mwanafunzi hujifunza mambo mageni kwa lugha ya kigeni kwa maana ya kiingereza. Hali hii kwa mtizamo wangu inachangia kuzorotesha na kupunguza ufanisi wa wanafunzi wetu kilugha katika ngazi zote.

Zaidi ya yote, mfumo wetu wa elimu katika ngazi zote haujaandaliwa katika misingi ya kumwezesha mwanafunzi kujifunza kwa vitendo. Pamoja na shule zetu kuwa na ukosefu wa vifaa vya kufundishia kwa vitendo, lakini pia ubunifu miongoni mwa walimu ni jambo jingine.

Mfano, wakati wa kufundisha somo la umeme kwa wanafunzi washule ya msingi, hapa si lazima kuwa na umeme, maana shule nyingi za vijijini hazina umeme, badala yake walimu wanaweza kutumia betri ya gari kuzalisha umeme na mwanga.


Madhalani, wakati wa kufundisha somo la uzazi wa mimea, hapa walimu wanapaswa kuandaa bustani ya majaribio, ambapo wanafunzi watapata fursa ya kuona jinsi mimea inavyoweza kuzaliana kwa vitendo.

Na kama kama ni wakati wa kufundisha somo linalohusiana na mifumo mbali mbali kama vile mfumo wa chakula, mfumo wa hewa, mfumo wa uzazi, mfumo wa neva, mfumo wa fahamu n.k hapa walimu wahusika wanaweza kumchinja chura au panya ili waweza kuonyesha kwa vitendo.

Ili kukabiliana na changomoto hizi ningependa kuishauri serikali kupitia wizara ya elimu na mafunzo kama ifutatavyo. Kwanza, kubadili mfumo wa mitaala yetu ambayo tumeirithi toka enzi za mkoloni. Jambo la msingi hapa ni kubadilisha lugha ya ufundishaji toka ngazi ya chini ya elimu hadi elimu ya juu, yaani kutoka shule ya vidudu hadi chuo kikuu.

Kama ni kiswahili basi iwe ni kiswahili toka mwanzo hadi mwisho na kama ni kiingereza basi iwe ni kiingereza toka mwanzo mpaka mwisho. Pili mitaala ibuniwe kwa lengo la kumwezesha mwanafunzi kujifunza kwa vitendo zaidi tofauti na hali ya ufundishaji wa sasa uliojikita zaidi kwenye nadharia.

Hakika kama serikali inakusudia kuwekeza kwenye ubora wa elimu basi ni lazima walimu wa stashahada/diploma na wale wa shahada/degree nao wapewe jukumu la kufundisha katika shule za msingi.

Jambo hili linaweza kuwa na ugumu wake katika utekelezaji endapo mazingira ya kufanyia kazi kwa walimu hayataboreshwa, hii ikiwa ni pamoja nyumba nzuri za kuishi walimu, huduma kama vile umeme, maji, internet, minara ya simu na TV. Upatikanaji wa huduma hizi unaweza kuwafanya walimu kudumu katika mazingira yao ya kufanyia kazi.

Iwapo jambo hili litazingatiwa basi ubora wa elimu yetu utaongezeka, na hata uwezekano wa kubadili mitaala yetu kuwa katika lugha ya kiingereza toka shule ya vidudu/ kindergarten hadi chuo kikuu utafanikiwa.

Mwisho, tukumbuke kwamba uimara wa nyumba kwa kiasi kubwa hutegemea MSINGI! Bila kusahau usemi kuwa, utavuna ulichopanda.


--
Malkiory William Matiya

Mnaweza kutembelea blogu yake: http://www.malkiory-matiya.blogspot.com/

7 comments:

Anonymous said...

Dada Chemi leo umetuchokoza! Ni kweli, kuna kipindi ilikuwa ukiongea Englishi hadharani uunamabiwa eti una kasumba! Watu walikuwa na nguo nzuri lakini wanavaa viraka, eti ndo wajamaa! Ukiwa na friji nyumbani kwako eti bepari! Tumeumia! Heko Chifu Fundikira, alisema ukweli!

Anonymous said...

Ni kweli mfumo wetu wa elimu huna kasoro nyingi sana, pamoja matatizo ambayo mdau ametaja pia kuna matatizo ya mfumo mzima unasaidia watu wachache na vijana wengi (au nguvu kazi) tukiziacha nyuma kila mwaka kitu ambacho ni hasara kwa taifa, mfano ukiangalia watoto wanaoanza darasa la kwanza na kujiunga na Sec. school ni wachache sana yaani karibia nusu ya watoto tunawaacha wakishamaliza darasa la saba, hivyo hivyo kwa O´level kwenda Vacational training au kwenda A´Level, tunawaacha vijana wengi sana wakibaki mtaani wakiranda randa,

Mimi nafikiri pamoja na mawazo mazuri ya mwanzisha mada pia tuwe na utaratibu watoto wote wanaoanza darasa la kwanza twende nao mpaka Sec. School baada hapa ndio tuanze mchanganua wale ambao hana marks za kutosha basi waanza kujifunza kazi ndogo kama vile Salon, Mfundi ujezi,kufanya usafi, ufundi selemala na nk. na wale wenye marks nzuri waote wanakwenda High School, na hao wakimaliza baadhi wataingia vyuo vikuu, wengi watakwenda Ualimu, Nursing,Secretarials, Police, Askari magereza na nk. hapo ndipo tutajenga taifa lenye nguvu, taifa la wabunifu na taifa ambalo at least percent kubwa ya vijana wake watakuwa na kazi!

Anonymous said...

Wewe Dada Acha zako za kuleta ingawa kuna mambo nakubaliana na mwandishi lakini hili la lugha kwamba ndio maendeleo katika nchi like umecompare wakenya na wagana mimi naona mfumo wa wa kufundisha Kiswahili baadae kiingereza at Sec sio mbaya. tatizo ni mfumo na ufundishaji darasani. ngoj nichanganue hapo mimi naishi America mfumo wa hapa wa ufundishaji tangu elementary unaendana na real life hii ina maana kwamba ukimchukua mwanafunzi wa high schoo hapa USA ukawapa project lets say Namna ya kuboresha miundo mbinu e.g IT pale NASAKO kuweza kucompete na bandari kama Dubai, result ya project kwa hao wahusika itakushangaza maana TZ-student watakuwa very short katika kutatua tatizo hilo hii ina maana kwamba USA-student imply b'se wanafundishwa nadharia darasani na vitendo pia Critical thinking. also kujua lugha ya kiingereza sio tija ya maendeleo kwa nchi yoyote unaweza kuwa hujui kiingereza lakini ukafanikiwa kibiahara hata nchi kwa ujumla. Hebu checki China wanafunzi wake shuleni wanafundishwa na lugha yao SIO ENGLISH" lakini unaona wao wanongoza kibiashara, kifedha mambo mengi yanyozunguka Dunia soo,, kwahiyo mimi binafsi nashauri mfumo wa ufundishaji ndio ubadilishwe i mean curicullum nzima ibadilishwe bati l;ugha yetu ibaki pale, pale ya kiswahili kwa watoto wa msingi

Anonymous said...

Mimi sikatae kuwa wabongo tuna shida na lugha ya English. Lakini lazima tujivunie kuwa tuna UMOJA! Je, Kenya na uganda kuna Umoja? Kuna ukabila tele huko. Kiswahili kimesaidia kuondoa ukabila.

Bennet said...

Tuna kazi sana tuliosoma enzi hakuna English medium school wakati huo zilikuwepo swahili medium school au St goverment school, maana tunakuwa tunakariri bila kuelewa masomo

joji said...

Dada,

Ingawa mimi mzungu kila mara mpaka sasa nilikubaliana nawe.

Lakini sasa lazima nikupinge. Kiswahili kiwe lugha ya kufundishia toka shule ya msingi mpaka chuo kikuu.

Kwenye karibu nchi zote lugha ya kufundishia ni lugha ya mama. Angalia Ujerumani na China kwa mfano.

Kiingereza kiwe lugha ya kigeni. Muhimu sana, nakubali. Lakini kifundishwe kama lugha ya kigeni.

Nani ana kasumba? Si yule ambaye anazifuata utamaduni, desturi pia lugha ambazo si zake.

Tujivunie Kiswahili chetu!

Anonymous said...

Nawaombeni wote kwanza msome maoni yote halafu muangalie Kiswahili kilivyoandikwa hapo. Mtagundua mara moja kwamba Kiswahili chenyewe hakijaandikwa vema. Nadiriki kusema hayo ni matokeo ya mfumo mbaya wa elimu na si kwa sababu tulikikataa Kiingereza.
Katika matokeo ya kidato cha nne mwaka huu, shule fulani ambayo wanafunzi wake wanaporomosha Kimombo kizuri, wanafunzi wengi waliishia Divisheni III.
Tusirahisishe mambo na kukitangaza Kiswahili kama chanzo cha matatizo. Tunahitaji mfumo mzuri wa elimu ambapo lugha kadha zinafundishwa VIZURI siyo kiubabaishaji, na wala siyo kwa kukifanya Kiingereza ndiyo elimu.
Na kwa taarifa yenu Wakenya wameshakuja juu sana na Kiswahili duniani sasa hivi. Soon, we will be playing catch up again.