Friday, December 17, 2010

Tido Mhando Atemwa TBC

DUH! Mbona watu walisema alifanya kazi nzuri sana pale TBC. Hii habari ya kutisha!


17 December 2010

Tido Mhando atemwa TBC

Sadick Mtulya na Patricia Kimelemeta

BAADA ya kufanya kazi nzuri ya kuboresha matangazo na uendeshaji wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC), serikali imeamua kuachana na mkurugenzi wa chombo hicho, Tido Mhando baada ya mkataba wake kuisha, lakini mtangazaji huyo maarufu ameielezea uamuzi huo kuwa kuwa ni wa utata.

Kuenguliwa kwake kumefanyika takriban miezi miwili baada ya kumalizika kwa uchaguzi mkuu ambao TBC iliripoti kwa kina na bila kupendelea chama chochote na hivyo kujivunia sifa kemkem kutoka kwa watazamaji wa TBC1 na wasikilizaji wa redio hiyo ya umma.

“Hatua hii imenishtua kidogo na hata hivi ninapoongea na wewe wafanyakazi wengi wamepata mshtuko na wengine wanalia," alisema Tido alipoongea na Mwananchi jana. "Ni juzi (Jumatatu) ndio niliandikiwa barua na serikali ya kutakiwa kuondoka.... ilikuwa kinyume kabisa na uratatibu wa serikali.

“Barua ya kutakiwa kuondoka niliipata mara baada ya kukutana na kuzungumza na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Michezo, Utamaduni na Vijana , Seti Kamwanda.’’

Tido, ambaye kabla ya kujiunga na TBC alikuwa mkuu wa Idhaa ya Kiswahili ya Shirika la Habari la Uingereza (BBC), alisema kwa mujibu wa taratibu mfanyakazi anayemaliza mkataba wake anatakiwa kujulishwa suala hilo miezi sita kabla.

"Kimsingi (barua) hukumbusha kwamba mkataba unamalizika na kama serikali inakusudia kuuendeleza au la. Sasa hilo halikufanyika kwangu," alisema.

Kwa mujibu wa Tido, hatua hiyo inaweza kutafsiriwa tofauti na wananchi hasa ikizingatiwa kwamba imefikiwa miezi miwili tu tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu.

Wafanyakazi walipata taarifa ya kuondolewa kwa Mhando jana baada ya mkurugenzi huyo kubandika tangazo la kuwataarifu kuwa anaondoka na kwamba ametakiwa akabidhi ofisi kwa Joe Rugabaramu.

"Tangazo linasema kuwa amefanya kazi na sisi kwa miaka minne na sasa mktaba wake umeisha na kwamba ametakiwa akabidhi ofisi kwa Rugarabamu," alisema mmoja wa wafanyakazi wa TBC.
"Baadaye alitushukuru kwa ushirikiano wetu kazini na akatuambia tusubiri hadi hapo mkurugenzi mpya atakapotangazwa."

Mfanyakazi mwingine alisema kuwa walitarajia kuwa Mhando angetimuliwa mapema kabla ya uchaguzi kwa kuwa wanadai kuja kwake nchini kulitokana na uhusiano wake na kigogo mmoja wa CCM ambaye kwa sasa hayuko madarakani.

"Angetimuliwa hata kabla ya Desemba 15, lakini ikaonekana kuwa isingekuwa sahihi," alisema mfanyakazi huyo ambaye alieleza kuwa Mhando aliwasiliana pia kwa simu na mfanyakazi mmoja mmoja kumuelezea uamuzi huo wa serikali.

Habari za Tido kuondoka TBC zilianza kuvuma wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wakati iliposemekana kuwa alikuwa akipigana vijembe vya chinichini na vigogo wa CCM kutokana na vyombo hivyo vya umma kutangaza habari bila ya upendeleo.

Baadhi ya mambo yaliyoibua hisia kuwa mtendaji huyo wa shirika la umma angeondolewa ni msimamo wake wa kuendelea kurusha hewani kipindi cha "Jimbo kwa Jimbo" ambacho kilikutanisha wagombea ubunge wa vyama mbalimbali vya siasa kwenye mdahalo kuhusu maendeleo ya eneo lao.

Kipindi hicho kilichorushwa kwa wakati mmoja na vituo vya televisheni na redio kilianza kwa kushirikisha wagombea wote wa ubunge kwenye jimbo, lakini katibu mkuu wa CCM, Yusuf Makamba akaandika waraka wa kuzuia wagombea wa CCM kushiriki kwenye mdahalo huo akidai kuwa chama hicho tawala kina njia zake za kufanya kampeni.

Pamoja na CCM kujitoa, TBC iliendelea kurusha vipindi hivyo hadi kumalizika kwa uchaguzi ambao uliisha kwa CCM kupoteza viti vingi Tanzania Bara, ikiwa ni mara ya kwanza tangu serikali iruhusu mfumo wa vyama vingi.

"Ilikuwa aondoke kabla kampeni hazijaanza ingawa mkataba wake ulikuwa umalizike Desemba 15. Lakini serikali ilikuwa inarekebisha mambo yake na kumtafuta mtu anayeweza kurithi nafasi yake," chanzo cha habari cha ndani serikalini kilidokeza.

Chanzo kingine alisema: "Kuna watu wanaajiriwa pale TBC ambao malipo yao yanayotokana na Saccos ya shirika hilo, kitu ambacho ni kinyume na taratibu za serikali zinazotaka mwajiriwa alipwe na Hazina."
Jitihada za gazeti hili kumpata katibu mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, Seti Kamhanda hazikuzaa matunda.

Alipoulizwa endapo atakubali kurejee kwenye wadhifa huo ikitokea serikali ikamwita tena, Mhando alijibu: "Nitalazimika kuchukua muda zaidi kutafakari hilo kwa kina.

“Nitafanya maamuzi ya kazi ya kufanya kulingana na wakati utakavyokuwa, lakini itanichukua muda kidogo kutafakari hilo kwa kuwa nimefanya kazi mfululizo.’

Kuhusu utendaji wa shirika hilo, Tido alisema amefarijika kwa kiasi kikubwa na mafanikio ya kiutendaji yaliyofikiwa.
“Nilikuwa na mipango mikakati mingi ya kuendeleza shirika hili hususani kulifanya lijiendeshe kwa kujitegemea bila ya kuhitaji ruzuku serikalini," alisema na kuendelea:

“Lakini nimefarijika vya kutosha na utendaji wangu na mafanikio yaliyofikiwa na TBC hadi wananchi kukiamini chombo hiki na ‘reaction’ imekuwa nzuri kutoka kwao na kwa vyama vya siasa.’’

Mbali na kurusha taarifa za kampeni katika njia iliyoonekana kuwa si ya upendeleo hata kwa chama tawala, TBC ilifanikiwa sana katika urushaji wa moja kwa moja wa matangazo ya mechi za mpira wa miguu na matukio makubwa ya kisiasa na kijamii.

Mechi za michuano mbalimbali ya kimataifa na ya ndani, urushaji wa matangazo ya moja kwa moja ya vikao vya Bunge, urushaji wa moja kwa moja wa matukio makubwa na staili ya utangazaji ulilifanya shirika hilo kuwa na mvuto mpya na hivyo kuweza kupambana na vituo vingine vya redio na televisheni vya kampuni binafsi.

1 comment:

Anonymous said...

Nakubaliana na Tido kwamba alitakiwa apewe notice ya miezi sita inayomjulisha kuwa mkataba wake unamalizika—jambo ambalo halikufanyika. Mkataba ni wa pande mbili—mwajiri na mwajiriwa—na kila upande una majukumu yake.


Kwa mujibu wa Tido, mojawapo ya majukumu ya mwanjiri ni kumpa notice hiyo, lakini hajatuambia kama naye alitakiwa kutoa notice ya miezi sita kabla mkataba wake haujamalizika. Kama ndivyo, je, alifanya? Na kama alifanya, majibu yalikuwa nini? Au ni ile tunayoiita ‘business as usual’? Kwamba unaendelea tu na kazi bila kujua mwajiri anafikiria nini kuhusu mkataba wako unaomalizika? Kinachomuuma sana Tido—na Watanzania wengi—ni kwa sababu walimshtukiza.


In life, there's nothing as worse a being taken by surprise. That's what happened to Tido. May GOD bless this country and its politics.