Wednesday, May 08, 2013

"Taifa Lina Nyufa" - Mh. Mbunge Zitto Kabwe



TAIFA LINA NYUFA

Na Mh. Mbunge Zitto Kabwe

NDUGU KABWE Z. ZITTO, MB – BUNGENI TAREHE 6 MEI, 2013


Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia leo katika mjadala huu muhimu sana.

Hapa Afrika kulikuwa kuna nchi, na bado ipo, inaitwa Ivory Coast. Ilikuwa ni nchi ambayo inasifika sana kwa amani na utulivu; na ilikuwa ni nchi ya kupigiwa mfano. Leo hii Ivory Coast imegawanyika vipande vipande. Ukienda leo Ivory Coast unakuta wanaoitwa Ivorite na wanaoitwa wageni ambao wazazi wao walienda Ivory Coast kufanya kazi miaka mingi sana. Lakini pili katika mgawanyiko huo kuna mgawanyiko mkubwa sana wa kidini kati ya watu wa Ivory Coast wanaotokea Kaskazini na watu wa Ivory Coast wanaotokea Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tuna Sierra Leone nchi ambayo wageni walikuwa wanakirimiwa katika hali ambayo haijawahi kutokea hapa duniani. Lakini leo Sierra Leone ina rekodi kubwa sana ya watu wenye ulemavu kwa sababu ya vita ya wenyewe kwa wenyewe.

Naomba nichukue nafasi hii kufuatia matukio ambayo yametokea hivi karibuni na hasa jana na siku zilizopita ninanukuu hotuba ambayo Rais wa Awamu ya Tatu Mheshimiwa Benjamin Mkapa aliitoa katika Bunge hili tarehe 4 Novemba, 1998. Alisema:

“Mr. Speaker, after three years of my presidency, I can dare to modify the words of famous Zanzibar maestro Siti Binti Saada by saying, Tanzania is a good country, let one who wishes to come do so. God has showered blessings on our country. It is a country of unity, peace, love, rejoicing and exciding generosity. It is a country of people who love equality and justice. Our national unity brings from our firm believe in equality of human beings before God and before the Law. A Unity reinforced by correct policies of national building. Policies based on the principles of social justice, peace, harmony and development for all. A unity which is extra sensitive to policies, statements behavior and actions which may sore seeds discard hatred and suspicious among Tanzanians”

Mheshimiwa Mwenyekiti sitatafsiri. Lakini naomba kila Mbunge ajiulize leo iwapo Rais Mkapa tukimpa fursa ya kuja kuhutubia Bunge hili anaweza akayatumia maneno haya tena? Hakuna mtanzania yoyote anayeweza kuthubutu leo kutumia maneno haya tena kwa sababu nchi yetu ina nyufa. Ina nyufa ambazo kwa kujua au kwa kutokujua sisi kama watu ambao tumepewa wajibi na wananchi wa kuitunza nchi hii na kuipeleka pamoja tumejikuta tukiingia katika kutoa kauli, maneno na vitendo ambavyo ni “irresponsible” vinavyopelekea kugawanya nchi; na yanayotokea sasa ni matumizi ya nyufa hizo.

NDUGU KABWE Z. ZITTO

Asubuhi hapa Mheshimiwa Lissu amesema, ametoa rekodi ya namna ambavyo wanasiasa wa chama kinachoongoza (CCM) wamekuwa wakitoa kauli dhidi ya vyama vya upinzani kuhusiana na masuala haya ya kidini. Wametoa mfano kuhusu chama cha CUF kilipoitwa chama cha waislam, wamekitolea mfano kuhusu CHADEMA kinavyoitwa mpaka sasa chama cha wakristo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana ikawa ni rahisi sana tuka-“point fingers” kwa wenzetu nyie, ni rahisi sana; lakini CUF wakati wanaitwa ni chama cha waislam ambao walikuwa hawaitwi ni chama cha waislam hawakunyoosha mkono kupinga. Wakati CHADEMA kinaitwa cha cha Kikristo ambao hawaitwi hivyo hawakunyoosha mkono. Matokeo yakeni nini? Tumejenga hofu kubwa sana katika Taifa na hii ni lawama kwa wote. Wote kama nchi ili tuseme kwamba hapa tumekosea na tuanze upya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, adui anapokuja kwenye nyumba anaangalia ni wapi ambapo ni rahisi kamba kukatika. Tumeji-“expose”, tumejiweka wazi. Leo mtu anayetaka kuishughulikia Tanzania ata-deal na udini tu. Kwa sababu anajua watanzania hivi sasa wamegawanyika katika misingi hiyo. Jana limetokea tukio Arusha, angalia kwenye mitandao ya kijamii mara moja watanzania wenyewe kwa wenyewe na ukiangalia majina ya watu wanaojadiliana wanaanza kusemana kwa dini zao. Ndiyo hatari ambayo tumeifikia; na ndio anachokitaka adui. Ni hicho. Atakuja, wanaitwa “Agent Provacateur”, watapiga, mtabaki mnagombana ninyi. Tukiruhusu NYUFA hizi ziendelee hatutakuwa taifa. Ni lazima sote kwa pamoja tusimame imara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, waislam na wakristo nchi hii hawana chuki kwa sababu wanaishi pamoja, ni marafiki, ni ndugu na kama ingekuwa kwa mfano waislam wanawachukia wakristo waislam wangevunja makanisa au wangechoma makanisa au wangewalipua wakristo. Wakati wa tukio la Mwembechai ndipo ambapo Polisi waliingia mskitini wakaua watu, wanawake wakateswa kwenye magereza na kadhalika, watu wakakaa miezi mitano gerezani bila kushtakiwa lakini hapakuwa na mtukio yoyote ya namna hii. Waislam na wakristo wa nchi hii ni wamoja. Wananchi wetu ni wa moja lakini sisi viongozi kwa kutoa kauli ambazo ni “very irresponsible” tunawagawa watu wetu na ni lazima tukatae hali hii. Tunafanya nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima twende mbele. Kwanza ni lazima sasa Serikali ijenge utamaduni wa kufuatilia “grievances” zote ambazo wananchi wanazo bila kujali dini zao. Pili turuhusu watu kuwa huru kusema. Nimesikia hapa watu wanasema kwamba maandamano ni tatizo nakadhalika. Maandamano si tatizo, ukimzuia mtu kuandamana akiweka hasira zake kesho atafanya nini? Atatoka na bomu. Turuhusu “honest discussions” miongoni mwetu kama wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu ni lazima sasa tuseme ya kwamba ni marufuku kuwa na kauli za chuki “hate speeches”. Kama hatuna vipengele vya kisheria tutunge sheria kwa sababu kumekuwa na “hate speeches” nyingi sana katika hii nchi na hakuna hatua ambazo zinachukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, state, dola, ihakikishe inajiondoa kwenye shughuli za uendeshaji wa mambo ya kidini. Ijiondoe kabisa. Kwa mfano kuna lawama ya muda mrefu sana ya waislam kuhusu BAKWATA, Waislamu miaka mingi toka mwaka 1969 wakati Serikali imeunda BAKWATA wanalalamika. Leo hii Serikali ikitaka kuzungumza na waislam inafanya nini? Inaenda kuwaita BAKWATA. Hawana legitimacy ya waislam, hamtaweza ku-addres masuala ya waislam lakini ni rahisi sana kuweza kuongea na CCT kwa sababu CCT ni chombo ambacho kina uhuru wake. Kwa hiyo Serikali ijiondoe kwenye uendesheji wa shughuli za kidini. Hapa ndipo tutakapoweza kuhakikisha kwamba tunakuwa na nchi moja nchi ambayo ina amani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namaliza kwa kusema nchi hii si ya waislam peke yake, nchi hii si ya wakristo peke yake. Nchi hii si ya CCM au ya CHADEMA, CUF au ya NCCR-Mageuzi au TLP na kadhalika. Nchi hii ni moja, nchi hii ni ya Jamhuiri ya Muungano wa Tanzania. Lazima wote tusimame kuhakikisha tunailinda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru sana asante.

1 comment:

Anonymous said...

Zito nikukmbushe enzi za juke box anayetumbukiza sarafu ndiye anayechagua wimbo! Vema umeliona hili la BAKWATA sasa ikija Kadhi na mahakama yake iendeshwe na serikali si itakuwa taabu zaidi. Ni budi serikali ijitoe katika kuendesha mambo ya dini na isikubali kuingizwa.