Tuesday, August 18, 2009

Libeneke la Kulizwa Airport Dar

Mdau amenitumia maoni yake:

Kuhusu libeneke la kulizwa airport na ufisadi unaoendelea Tanzania kwa ujuma; Mtazamo wangu nini kifanyike!

Kwanza nawashukuru kwa pongezi mlionipa katika ile makala ya libeneke la tathmini ya bei za nyumba nilipost kwa kaka Michuzi, nimepata moyo kuwa nimeandika kitu ambacho kitawasaidia wengine. Asanteni sana kwa maoni mazuri. Sasa nikija kwenye kadhia ya airport na ufisadi tanzania. Nakubaliana na baadhi ya maoni yoliyosema na wadau mbali mbali kuhusu huyo mtasha aliekutwa na mkasa airport. Binafsi, nadhani huyo mzungu alitia chumvi katika hizo allegations zake, kwa mfano polisi kumuomba dola 500, polisi wetu kwanza wanaogopa sana wazungu na wageni wengine matokeo yake wanaishia kutuumiza wenyeji! sijui ni tatizo la lugha ama vipi ila huo ni ukweli, istoshe wanapoa kwa kitu kidogo hata ukiwatoa kwa buku tano tu wanafurahi! Nawapa pole waliobiwa, ila nina shaka na baadhi ya hizo complaints, wanaosema wameibiwa laptop kwa posta ni sawa inakubalika ila airport, jamani laptop ilikuwa inafanya nini kwenye checked luggage, tusidanganyane hapa! Natoa tahadhari, hii makala kidogo iko inclined kwenye kuonesha the negative side of our society, ni kutokana na nature ya mada yenyewe sikusudii kukashifu au kuashiria hakuna jema huko kwetu naomba mniwe radhi kama nitaudhi ieleweke sio lengo langu, makala nimekusudia iwe constructive analysis ya jamii yetu na sio kuonesha udhaifu wetu. Siku hizi watu wamekuwa sensitive sana ndio maana najihami na ninachokiandika sio kwa woga bali sitaki kuudhi kundi lolote.

Mimi naamini chimbuko la matatizo haya na mengine ya aina hii ni hali mbaya ya uchumi huko nyumbani, ajira chache, mishahara midogo sana na dukani wafanyabiashara wanapanga bei wanavyopenda wenyewe. Hali ya kiuchumi na kipato kidogo kinachangia moja kwa moja kwenye migogoro mingi ya kijamii kuanzia kuibiwa simu mtaa wakongo, kuchomolewa wallet kwenye daladala hadi wizi kama ule wa NMB, ila hili la wizi kama huu wa airport, vifurushi vya posta, na kadhalika linaendekezwa na usimamizi mbovu katika hizo idara husika. Haya mambo yaashiria serikali yetu inabeza majukumu yake sana, sio kama inashindwa kutatua matatizo makubwa tu bali hata kero ndogo ndogo. Huo wizi wa mizigo kama wahusika wangekuwa makini kidogo tu usingekuwepo, ila ndio hivo kubwa ni changa la macho wanaweka CCTV halafu hata ikitokea wizi hakuna kumbukumbu yeyote inayoweza kupatikana! Halafu mwisho wa siku mkurugenzi ana kuja kujikosha tuandikie utueleze uliwasili siku gani na ndege gani, sasa nauliza, nikishatuma hiyo barua na ukanijibu mikanda ya hizo CCTVs ambazo nyingi huwa ni dummies haioneshi tukio la uhalifu itakuwaje? Si ndio mwanzo wa kusutana tu mimi nasema nimeibiwa na wewe kumbukumbu zako hazioneshi! Jambo la muhimu hapo kama mkuu wa idara unaskia malalamiko kama haya unaweka mikakati kuhakikisha hayo malalamiko na kasoro zinashughulikiwa, usikae sana ofisini unakula kiyoyozi jaribu kupita pita bila kutoa taarifa ujionee mwenyewe watendaji wako wanafanya nini (Hiyo itakusaidia hata kupunguza hicho kitambi). Any way, hii mada si juu ya unene, muhumu ujitahidi kufanya kazi yako vizuri, naamini juhudui zako hazitakuwa in vain, waswahili wanasema wema hauozi. Hapa nazungumzia kinadharia wala sikusudii kukashifu mtu yeyote, ila mara nyengine utakuta baadhi ya hao wasomba mizigo bosi anawaonea aibu kuwajibisha kwa vile ni watoto wa dada yake aliwasaidia kupata hicho kibarua au mbaya zaidi ni ndugu zake mkewe.

Ukiachana na udhaifu wa hizo mamlaka husika, jengine nadhani inatokana na jinsi tunavolitizama hili swala la maisha bora kwa kila mtanzania, yani lazima tuelewe jamani jamii yeyote haitafikia kuwa utopian, na Tanzania ndio tuko mbali zaidi, sasa basi watu inabidi tukubali katika jamii kutakuwa na watu wenye uwezo na wasio kuwa, iliobaki tuzungumze na roho zetu ukishapata ya lazima basi tupunguzeni tamaa. Hii tamaa ndio inatufikisha pabaya, ndio maana viongozi, wafanyabiashara na wengi wetu bado tu wanaendelea na ufasadi kila kukicha yani hawatosheki, sijui ni kutokana na ushandani au nini. Wengi tunaangalia alie juu yetu ana nini na mimi nile dili wapi nikipate, badala kuangalia wa chini ukashkuru, hii ndo hatima yake inapelekea mauwaji ya maalibino. Cha ajabu kuna baadhi yetu hata hawakubahatika kupata watoto, lakini bado unakuta mtu huyo huyo ana majumba zaidi ya moja na bado tu anaendelea kukomba ulaji, sijui anategemea kumuachia nani manake wengi wetu tunajustify our struggle kwa ajili ya watoto wetu. Yani tumekuwa consumed na ulafi enough is not enough! Wenzetu mtu wanapigania apate uongozi ili waache legacy, sisi zaidi tuko materialistic kwenye kila kitu, kuanzia mahusiano, ndoa na kadhaika, achievements za mtu tunaziangalia kwa nyumba na gari analoendesha. Mitazamo kama hii ndio inayobreed mafisadi na wahalifu kwenye jamii zetu, sasa kama kipimo cha mafanikio kwenye jamii ni utajiri matokeo yake ni nini, na njia za halali za kupata utajiri huko nyumbani ni finyu na chace. Yani mtu kamaliza chuo mwaka huu kabahatika ajira anakwera na nyumba ya kupanga, anataka awe amejenga baada ya miaka miwili wakati mshahara wenyewe haueleweki, hube niambie atafanyaje kama hajahujumu.

Kwa kuongezea juu ya kubadilisha tabia na mitizamo, inabidi tupunguze tabia tegemezi kutoka kwa ndugu zetu hasa hawa wenye nyadhifa serikalini, pia akina mama nyumbani wawe na huruma kwa baba sio kila kukicha anadai vitu vipya baada ya kumuona navyo mke wa jirani. Jengine tupunguzeni wivu, kule kwetu zanzibar tuna msemo bahari hailindwi(unfortunately ndio wa mwanzo kuwazuia wake zetu wasitoke nje wakati hatuwezi kuwatimizia mahitaji yao) akina mama ambao hawana watoto wadogo tusiwaache nyumbani wakawa "goal keepers", nao watoke wakatafute rizki mradi iwe ya halali tukiwaacha nyumbani hawa tunapunguza labour force kwa kiwango kikubwa sana katika jamii na kuzidisha uzito wa mzigo. Nahimiza kubadili tabia kwani lazima tukumbuke sio wafanyakazi wote maofisini na katika sector nyengine nyeti wanaingia kwenye corruption kwa kupenda, yani wengine wanakuwa ni victims of circumstances, kama mlibahatika kusoma kitabu cha mwandishi wa kinaijeria Chinua Achebe kinaitwa "No Longer at Ease" mtaelewa zaidi naongelea nini hapa.(nilipokuwa secondary ilikuwa lazima usome hiyo novel). Muhusika mkuu Bwana Obi, alisoma ulaya na aliporudi kwao initially he was determined to fight corruption, but to his dismay mwisho wa mambo akatumbukia humo humo nae akawa fisadi kutokana na ugumu wa mazingira alikuwa nayo na high expactions za jamii yake, tena ikumbukwe hiyo ni settings ya 1960s sembuse leo.

Hebu fikiria wewe ni afisa wa kawaida tu, nyumbani kuna mahitaji ya kawaida ya lazima, mama ana ng'ang'ania hili na nile unaogopa usipompatia haraka atakukimbia, watoto wanaenda shule wanahitaji kulipiwa ada, umefanya kosa la kuwapeleka shule mjini na wewe unakaa tegeta kama vile huko hakuna secondary, sasa inabidi uwape nauli ya kutosha wasinyanyaswe na makonda kwenye mabasi, pia pocket money ya kula chips mayai wakati wa mapumziko, unahofia usipofanya hivo binti yako wa miaka 16 ataharibika, mtoto mdogo yupo nyumbani mgonjwa anahitaji hela ya matibabu, kuna ndugu na jamaa zako na ndugu zake mkeo wametoka kijijini wapo nyumbani wote wanakutegemea, huwezi kulisha wote unaamua waondoke, huruma inakujia huwezi kuwatimua mikono mitupu, unasubiri kimshahara kije uwape nauli warudi mkoa, ulitaka kujirahisishia usafiri (au sijui kushindana na class mate ulisoma nae mlimani), ukajiroga na kununua kicorolla cha mwaka 91 ambacho baada ya kusota sana kama taxi ndio uliuziwa wewe kwa milioni tatu baada ya kumshinda huyo mmiliki wa mwanzo, hicho nacho hakikuonei huruma, kila jumamosi lazima ukipeleke garage na huko kuna kigongo chake mara inatakiwa hili mara lile! kuna mchango wa harusi ya rafiki yako mara sijui mwengine kapata maafa na majambazi na wewe alikusaidia sana, kumetembezwa bakuli kwenye mtandao unahisi unawajibika kuchangia, mshahara wenyewe mkia wa mbuzi! Sasa hebu niambie bosi wako corrupt anafanya mambo yake kupitia idara yako, kweli hutakula nae ukizingatia hali yako ya kimaisha? besides huwezi hata kumripoti ukizingatia yeye ana udugu na waziri wenu ukileta longo longo unapigwa transfer kigoma, bye bye dari salama, the only logical thing ni kula nae sahani moja tu. Na kwenye hili wadau wala tusianze kujiona tofauti, ndio maana wengi wetu hasa wanasiasa, wanapiga kelele sana wakati wakiomba kura na kuahidi watasimamia hayo maswala, na inawezekana kipindi hicho walikuwa na nia hiyo safi ya kufanya mema, ila siku akiingia na kujionea mambo yanavyokwenda mwenyewe wananywea, manake ni aidha ushirikiane nao kufisidi au ukubali kupigwa vita. Kule kwetu Zanzibar, wafanya kazi serikalini wamebuni kirefu chao cha CCM, yani wanasema Chukua Chako Mapema na hiyo ndio hali halisi hata bara.(huu ni mfano tu, naomba nisieleweke vibaya sipigii kampeni chama chochote sina uhusiano wala uwanachama na chama cha siasa, na wala sikusudii kuponda au kukashifu CCM kama chama nazungumiza jamii, Infact sijawahi hata kupiga kura na nina miaka 27 ila hiyo ni mada nyengine). Hapa sio kama najaribu kujustify hiyo tabia ila lazima tuelewe hili tatizo linachangiwa na jamii yetu wenyewe.

Niliwahi kuandika paper ya economics of crime kwenye darasa langu la ECON243 nilichukuwa kama elective, humo nilijaribu kuonesha uhusiano wa kiuchumi na tabia ya uhalifu, nilitumia refferences kutoka makala mbali mbali na moja wapo ni maarufu kutoka kwa mchumi mmarekani alieshinda tunzo ya nobel, Gary Becker juu ya Crime and punishment. Hadithi inasema aliandika hiyo paper baada ya siku mmoja kuwa katika haraka, akapima faida na hasara ya kuegesha gari lake katika sehemu inayoruhusiwa ila ingebidi atembee masafa hivo angechelewa zaidi, au aegeshe karibu pasiporuhusiwa ili awahi! Baada ya kupima na kuona uwezekano wa kukamatwa kuwa mdogo na pia hata angekamatwa angetozwa fine ndogo basi akaamua kuvunja sheria na kuegesha sehemu isiyoruhusiwa. Cha kuzingatia hapo ni kwamba, kinadharia, mhalifu sio mtu wa aina ya peke yake sana kwenye jamii, yani hakuna anaezaliwa mhalifu. Katika kutenda uhalifu mara nyingi kanuni za uchumi zinafanya kazi katika kupelekea uamuzi wa kutenda kosa au ku refrain. Mtu wa kawaida mwenye kazi nzuri inayomuwezesha kupata mahitaji yake ya lazima ni vigumu kwenda kuvunja nyumba na kuiba baada ya kutathmini "Opportunity cost" ukizingatia kuiba kunaweza kupelekea kukamatwa na kufungwa au hata kuchomwa moto na raia wema, ila sasa kwa kijana asie na kazi au mwenye kazi ya kipato cha chini sana ni rahisi kwake kutenda kosa kama hilo manake what else is there for him? Ndio maana huko nyumbani karibu nyumba zote kasoro ikulu madirishani zimewekewa vyuma na huku ughaibuni hawaweki vyuma ukizingatia ni wachache sana wanaweza ku opt kuvunja na kuiba. Hapa naamini Bw. John Mashaka anaweza kutuandikia akatuelewesha zaidi huo uhusiano na nini kina hitajika kufanyika huko kwetu, tafadhali bwana mashaka! (Again, sina affiliation yeyote na Mashaka au mtu mwengine anaetoa makala humu, personally I dont know him na wala yeye hanijui, hapa najihami na wapinzani wa Mashaka kama akina US Blogger).

Kwa kutumia kanuni hizo hizo za uchumi tunaona ni jinsi gani hawa vibaka, wizi wa airport na kadhika tunavowalea wenyewe, wengi wao wakichukua hivi vitu wanategemea kwenda kuuza mtaani au kwa pawnshop, sasa hapa kuna tatizo jengine sisi wa mtaani tunaonunua hivi vitu ndio tunapromote hii tabia kuendelea, manake kusingekuwa na hiyo demand ya hizo bidhaa za wizi au magendo wizi na uhalifu ungepungua. Hapa nimekumbuka, huko nyumbani sasa kumekuwa na fesheni ya kuwa na laptops simu sio dili tena, rafiki yangu aliibiwa laptop april mwaka huu, kwenye bus akitokea Morogoro na ilikuwa na kazi zake muhimu sana! Hizi ndio zinaibiwa sana zinaenda kuuzwa laki 4 na watu tunanunua, jamani kuna ulazima gani wa kuwa na laptop kama hatumiliki milioni mmoja ya laptop kwanini mtu usinunue desktop na unapata nzuri tu kwa huyo laki 4, istoshe hakuna ulazima wakuwa na computer kama humiliki tujifunze kujikuna tunapojipata, kuna njia mbadala kama kwenda internet cafe tena huko nyumbani zimejaa kama uyoga! besides wanaojua mambo computer wala hawabodhi na laptop, mi binafsi hapa nilishaachana na laptop na siwezi kabisa kutrade desktop yangu kwa laptop uchwara!

Kwa uolewo wangu mdogo, nadhani ili kupambana na uhalifu na ufisadi kwa ujumla inabidi tuwe makini na kuwashughulikia wakorofi wote ipasavyo, tuwajengee hofu au hata nidhamu ya woga ili kabla mtu hajafanya hiyo hujuma afikirie mara mbili madhara yatakayomkuta akishikwa, pia tuongeze msako wa watu hao wakiona uwezekano wa kushikwa mkubwa watasita. Naamini sheria za adhabu tanzania ni kali za kutosha ila tatizo hazitumiki! Haitoshi kwa mfano akishikwa huyo mwizi wa airport baada ya kurudisha alichoiba kusamehewa, na wale wa EPA waliopewa sharti warudishe hela au watakamatwa, au kiongozi kufanya urichmond na kumwambia ajiuzulu kwisha habari, kwa utamaduni huo bado wataendelea na ufasaidi. Nahisi kuna haja sehemu nyeti kuweka maasifa wa kipelelezi, au kutoka PCB, ofcoz baada ya kufanya housekeeping huko manake nako kumeoza kinyama, hii itaongeza hofu na woga wa kukamatwa hivo makosa yatapungua. Hapo airport si waweke angalau wawili au ndio na wawao watakula pamoja! noma kweli. Jengine muhimu zaidi, serikali na sekta binafsi tujitahidi kuongeza ajirai, vijana wengi tunamaliza kusoma, na wengine wana vipaji vingi sana vya ufundi ila wanakosa vibarua, hapa sina hakika sana kama kubuni mashindano ya urembo ya msindi wa mwanzo anajinyakulia laki 5 kunastahili much praise, mwisho wa mambo wengine wanazirai jukwani na kwa ukatili au sijui kuogopa kukosa taji wenzake wanampita kama mzoga, hatari! Serikali yetu pia ijikite kuimarisha kilimo ili kupunguza ongezeko la vijana mijini. Wito kwa viongozi wetu wazee nadhani muda wa kung'atuka umewadiwa hata kama ni brain kiasi gani you have played your cards baki pembeni bado ungali na heshima toa nafasi kwa damu mpya ivuruge! naamini bado mtaweza kutoa mchango wa taifa na kusikilizwa sio lazima muwe serikalini au ndio tumekuwa nzi hadi tufie kwenye kidonda? Nashauri jamii tuzingatie uzazi wa mpango ili tupunguze ukali wa maisha, tukubali mambo yanakuwa magumu zaidi ukiwa na watoto 6 wa rika moja badala ya 3. Jengine, mwisho wa mwezi, siku tukipata mishahara jamani tusijisahau, huto tuhela ni tudogo mno na nyumbani ndio mwezi mzima walikuwa wanasubiria baba yao upokee, kwa hiyo tusikimbilie kwenye kiti moto na bia, au nyumba ndogoz. Nadhan kama utajitahidi kumtunza vizuri mamaa na mtanzaa kwa mpango, basi haja ya nyumba ndogoz naamini haitakuwepo. Hapa najaribu kujenga hoja tuwe makini na matumizi ili hicho kidogo tunachopata kitutosheleze na hivo tuweze kushinda vishawishi vya kufanya ufisadi na uhalifu kwa ujumla. Nimekumbuka ile hutuba ya baba wa taifa katika mchakato wa kumpata raisi wa awamu ya 3, alitoa hadithi ya yule mgiriki aliyejitapa serikali yake iko mfukoni, mwalimu akasema enzi zake ukithibitika umekula rushwa viboko 12 siku unaenda ndani na 12 siku ukitoka ukamuoneshe mkeo!, sijui hiyo sheria ilishafutwa, nahisi yafaa irudishwe hiyo na hao wa airport na wengine aina hiyo au hata wale wakubwa wanaojitapa shs. bilioni moja vijisenti kamateni japo mmoja mtembeze fimbo japo nusu ya hizo 12 angalau muoneshe mfano.

Hapa najaribu ku tackle morals zetu in general, hii ni hadithi ya kweli kabisa imenitokea mimi binafsi, mwaka 2003 mimi na rafiki yangu wa kike tuliokota simu ya mkononi maeneo ya posta karibu na british council, enzi hizo simu za coloured screen ilikuwa ndio zinaingia, bado ilikuwa on sikuizima niliitia mfukoni na baadae ilipigwa nikaipokea nikamuelekeza mwenyewe nilipo akaja kuifata, alikuwa ni mama mmoja balozi wa tanzania kama sijasahau alisema india. Alitueleza sijui alitoka foreign akaidondosha! akatuombea dua ya mafanikio na alishangaa sana Tanzania bado kuna vijana kama sisi, akaomba contacts zetu mimi nikasita kumpa nikamwabia haina haja, ila ng'ang'ania nikampa namba ya mwezangu akatuahidi atatutafuta atushukuru zaidi ukweli sikumskia tena ila yawezekana alitutafuta hakutupata. Honestly, sikukusudia kuichukua hiyo simu ila awali nilikuwa naomba mwenyewe asitokee, tulipokuwa wadogo tulikuwa na msemo cha kuokota si cha kuiba. Rafiki yangu ni kutoka bara yeye alisema hii ni simu ghali sana aliomba tu mwenyewe atokee, huwezi jua ningekuwa peke yake yangu pengine nisingeirudisha kutokana na madhila nilifanyiwa. Nilisomea A level dar katika kipindi cha miaka 2, niliibiwa simu mbili shuleni na ya tatu nilitupa kwenye daladala mpya kabisa nimechaji mara mmoja, nikaja kupiga siku mbili baadae ikapokewa na dada mmoja, akanieleza aliokota hiyo simu card tu na sio simu, nikamsihi tukutane anipatie hiyo chip angalau nipate contacts zangu akakubali, maskini kijana nilikuwa so naive, nikajitoa kwenda posta mpya kumsubiri nikaishia kuachwa solemba! Ila kuna siku mimi binafsi pia nilishangazwa, nilikuwa naelekea Zanzibar mwaka 2002, tulipelekwa bandarini kwa taxi na dereva nisie mfahamu, nilikaa nae mbele tukawa tunaongea kawaida tu na nilikuwa nimeshikilia discman (ilikuwa ya sony nilinunua mwaka 2000 kwa pound 100 na tanzania enzi hizo bado ilikuwa ni kitu tunu hasa kwa vijana) tulishuka kwenye taxi na nikaidondosha bila kujua, huwezi kuaamini tulikaribia kuingia kwenye geti la kuelekea kupanda boat yule dereva alitukimbilia huku anashout, bila kujua ataka nini nilishangaa, kumuona ameshika ile discman sikuamini kabisa kama dar ningeona dereva wa taxi wa aina ile, sasa kwa kuogopa kuibiwa sikurudi nayo tena badala yake nikamuomba dada yangu aniazime walkman yake zile za kuweka tape Mungu wangu shahidi nayo nilienda kuiponza ikaibiwa. Hizi hadithi zote ni za ukweli sijatia chumvi inawezekana na mimi mwenyewe nilizidi uzembe ndio wakaniibia. (Natoa tahadhari hapa nisije nikaeleweka vibaya nawaaccuse wabara wezi kwa vile niliibiwa, hata zanzibar kuna wizi vile vile ila nashkuru kule sijawahi kuibiwa simu, ila niliibiwa mountain bike mwaka 1999 na nyumbani kwetu tushalizwa mara kadhaa). In fact hata huku ughaibuni wizi upo, kama mchangiaji mmoja aliesema Heathrow nako kunasifika inawezekana ni kweli ila sina ushahidi nishapita hapo mara 3 na sikuibiwa! binafsi huku shuleni kwetu niliibiwa flash drive ya 2 Gb mwaka 2007, yani niliisahau computer lab kama nusu saa tu, kurudi wapi, nilipita lost n found mwezi mzima manake kulikuwa na kazi zangu za shule humo sikuipata hadi leo hii.

Samahanini sana kwa kuwachosha na makala ndefu, sina skills za uandishi najaribu tu kutoa mchango wangu, hii ni makala ya kwanza kutuma hapa swahili time. Ukiangalia kwa makini unaweza kuona sehemu nyingi nimeandika kama naaddress wanaume tu, hapana ni mfumo dume tu katika makala yangu, ila sijakusudia kubagua wala kudhalilisha wanawake au kuashiria wanaume tu ndio mafisadi! Naombeni msome na mtoe maoni yenu, tafadhali nieleweke kwa nilichoandika sitatufi uongozi, bara wala Zanzibar kwanza nasoma science na haina uhusiano na uongozi in fact I'm too timid hadi nashindwa kuweka jina langu hapa! Labda kwa kumalizia nitoe ushauri wa bure, tukiona post kama hizi kwenye blog au kwengineko tujaribu kusoma na ku dig zuri lolote ambalo muandishi kaandika na tusiwe tunaangalia wapi kumekosewa grammar ya kiswahili au kiengereza bila hivo hatutofika. Kwa mfano kumuandama mdau kama US Blogger na Phd yake ya Oxford, alikosea aliandika "hungry"badala ya "hunger" nadhani is being shallow, sijui huko Oxford ila huku Canada, shuleni kwetu kuna professors wageni kutoka poland, india na asia, english inawapiga chenga balaa, matumizi ya tense wabovu kabisa na mwalimu ana lack vocabularies inafika hadi anauliza class kitu gani kinaitwaje, yet akifundisha unamskiliza kwa makini uelewe anachofundisha na wala wanafunzi hawacheki! Hiyo ni kasumba mbovu, kweli duniani leo english ni lugha muhimu sana, personally I admire hao akina Mashaka na wenzake kwa elimu zao na umahiri wa kujieleza ila sijioni nikifanya bidii yeyote ya kuwa kama wao, naomba hii isiwe chanzo cha kudharau mtu. Kwanza sisi watanzania tuna advantage tunaweza angalau kuomba maji kwa kizungu na wengine wanaongea lugha za makabila yao in addition to kiswahili. Huku Canada, wanatumia english na french kuna jimbo la Quebec wanaongea french zaidi, hawa wengine wengi tu hawawezi hata kuomba maji kwa kifaransa sembuse lugha nyengine kama kispanish. Natoa wito kwa akina Mashaka, US Blogger na wengine jamani bora tutumie kiswahili kwenye haya makala, besides nyote mkofluent kwenye kimombo manake akina mimi angalau naweza kusema wacha niandike in english ili ni practice ila nyinyi mko super na naamin audience yenu kubwa wanapendelea na wataelewa vizuri kwa kiswahili, kutumia english mwisho wake ndio huo mshindwa kueleweka watu wanaishia kukosoa grammar badala ya kuzingatia mlichoandika, mnajua tena siku zote kazi ya critic nyepesi, ngoja ni nyamaze na mimi nisije kuoneka critic!

Nawasilisha

4 comments:

Anonymous said...

chemi hizi hotuba za mwisho wa mwezi kama hizi uwe unaziedit na kuweka point wise. nani atasoma yote haya?

LaMbegu said...

Watu wana muda wa mchezo sana. Tangu lini Da Chemi umeanza kuweka mashindano ya insha?
blah blah blah blah x100000^100000.
Utumbo mtupu.

Anonymous said...

mimi naomba umtumie hizo keki dada shamim aziweke kwenye blog yake ya fashion tujadili kwa uzuri ili usikie wanawake watasemaje hapa kijiwe hiki sio kwa sana wanawake hawa ingii humu maranyingi kule

Anonymous said...

hooo blah blaa ooo blah blah maneno meeeeeengi mpaka tunasahau unaandika kuhusu topic gani,Babu acha longolongo tushachoka na maneno sie ah.get a job.