Wednesday, March 11, 2009

Mzee Ruksa Apigwa Kofi Jukwaani!


Hivi kama Rais Mstaafu, Mzee Mwinyi si ana kuwa na wanausalama wake? Halafu ajabu wanakataa kuwa jambo hiyo ilitokea...wakati waandishi wa haabri wengi walishuhudia!

********************************************************************
Kutoka Ippmedia.com

Rais Mwinyi apigwa kofi jukwaani

2009-03-11
Na Muhibu Said

Rais Mstaafu Rais Ali Hassan Mwinyi jana alipigwa kofi la shavuni na muumini wa dini ya Kiislamu katika Baraza la Maulidi mara baada ya kuwataka Waislamu kujikinga na Ukimwi kwa kutumia kondomu kuliko kuwaambukiza watu gonjwa hilo hatari kwa jamii.

Rais Mwinyi ambaye pamoja na mambo mengine, alizungumzia masuala ya uchumi yanayoikumba nchi, alianza kuzungumzia vita dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi, kwa kusema kuwa zinaa katika Uislamu ni jambo haramu moja kwa moja.

Mwinyi aliendelea kudai kuwa mtu akifanya zinaa, kwa kutumia mpira (kondomu), atakuwa amefanya dhambi moja, lakini akifanya bila kutumia mpira, mtu huyo ni dalali wa kutembeza zinaa na Ukimwi.

Baada ya hapo akauliza mashekhe, kwamba kufanya dhambi Mungu anaweza akasamehe, lakini yule ambaye atafanya dhambi bila kondomu, bora ni vipi?

Mwinyi akaendelea kusema: ``Dharura ya mtu asiyeweza kujizuia na kufanya zinaa, mashekh na maulamaa tufanyeje hapo?``

Baada ya kusema hivyo, akatoka muumini mmoja akapanda jukwaani na kumpiga Rais Mwinyi kofi upande wa shavu la kuume, akapepesuka almanusra aanguke na kuokolewa na maafisa usalama.

Hali hiyo ilisababisha Mwinyi asitishe hotuba yake baada ya maafisa wa usalama na polisi kuvamia jukwaa na kumkamata mtuhumiwa aliyefanya kitendo kisicho cha kiuungwana.

Katika harakati za kumkamata, askari hao walianza kumpiga na ukumbi ukapatwa na taharuki kubwa.

Baada ya kumdhibiti mtu huyo ambaye alitia dosari sherehe hizo zilizokuwa zimeandaliwa vizuri, wanausalama hao walimpakia kwenye gari na kuondoka naye.

Baadhi ya waumini walitaka kukimbia, wengine wakaenda kuwasaidia maafisa usalama kumkabili mtu huyo aliyempiga Rais Mwinyi maarufu kama Mzee Ruksa.

Miongoni mwa watu waliomkabili kijana huyo ni pamoja na viongozi wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata) na waumini wengine.

Taharuki hiyo ilisababisha waandishi ambao walikuwa wakifuatilia shughuli nzima ya Baraza la Maulidi, baadhi kutaka kukimbia na wengine kujua kulikoni.

Hali hiyo ilidumu kwa muda wa dakika mbili, huku viongozi wa Bakwata wakiwatuliza watu kutulia ili shughuli iendeleee.

Nipashe jana iliwasiliana na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, juu ya tukio hilo lakini akasema kwamba amewasiliana na Kamanda wa Polisi Ilala, na tukio hilo halijatokea.

Nipashe ilipomuuliza kwamba mbona waandishi wa habari wameshuhudia tukio hilo, na pia Kaimu Mufti, Sheikh Suleiman Gorogosi, amewaomba waumini radhi kwa rabsha iliyotokea, Kamanda Kova alisema`` ``Wasiliana na Kamanda wa Ilala kwa habari zaidi.``

Akiomba radhi, Sheikh Gorogosi alisema mtu aliyefanya kitendo hicho cha aibu ni kichaa. Hadi tunakwenda mitamboni jina la mtu huyo lilikuwa halijajilikana.
Baada ya hapo, Mwinyi aliendelea kuhutubia.

Baada ya hapo, Nipashe iliwasiliana na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Faustine Shilogile, ambaye alisema kwamba alikuwa hana taarifa kamili kwa kuwa alikuwa katika viwanja vya Ikulu jijini Dar es Salaam.

``Ndio naelekea huko sasa hivi baada ya kuambiwa na askari waliokuwa huko Diamond Jubilee kupata habari kamili,`` alisema Shilogile.

Rais Mwinyi ni rais mstaafu anayependwa na wananchi kwa kiwango kikubwa, na kila anapohudhuria hafla mbalimbali amekuwa akishangiliwa kwa nguvu kutokana na mchango wake katika kubadili hali ya mambo nchini.

Ilikuwa ni chini utawala wake, akiwa Rais wa awamu ya tatu mageuzi makubwa ya kiuchumi na kisiasa yalianza kutekelezwa nchini ikiwa ni pamoja na kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi vya kisiasa.

Jina la Mzee Ruksa alipachikwa baada ya kuwa mkali kutokana na vitendo vya baadhi ya watu kuvamia na kuvunja mabucha ya nyama ya nguruwe, akiwakanya na kusema kwamba kila mtu ana ruksa ya kula atakacho.

Kutokana na utaratibu wa utawala wa kuachia wananchi uhuru wa kufanya watakalo ilimradi hawavunji sheria, alijiziolea umaarufu mkubwa na kupachikwa jina la Mzee Ruksa.

SOURCE: Nipashe

7 comments:

Anonymous said...

Aisee nimesikitika sana... Nampenda sana Ali Hassan Mwinyi. Ana mawaidha poa, kweli ukimwi unatumaliza... sio siri, na sio mara ya kwanza Mwinyi kuongelea janga la ukimwi alishasema haka kagonjwa kamekaa pabaya sana tangu enzi zileeee, tujikinge wananchi sio swala la uislamu wala ukristo hapa ni facts and reality. Alamsiki.

Anonymous said...

Nimelia kusikia habari hizi. Mimi ni Mkristo lakini nilimpenda sana Mzee Ruksa. Tulikuwa tunashinda njaa, Mzee Ruksa aliruhusu vyakula viagizwe nje ya nchi. Mafuta ya kupikia mchele na mengineo. Tulikuwa tunavaa viraka, Mzee Ruksa katuletea Mitumba. Friji enzi za Mwalimu ilikuwa anasa! Walioishi enzi zile wanajua Mzee Ruksa alivyotusaidia. POLE SANA MZEE WETU!

Anonymous said...

Tanzania inaelekea wapi jamani? Mzee Ruksa anaendekeza amani halafu muone! Pole sana Mzee wetu.

Anonymous said...

Piga ua!

Anonymous said...

Jamaa apigwe lakini sioni sababu ya kumwua. Usalama watamdhabiti!

Anonymous said...

"Mimi ni Mkristo lakini nilimpenda sana Mzee Ruksa"

Sijui kuna uhusiano gani hapa wa "dini" na kumpenda mzee ruksa.

Anonymous said...

Pole sana Mzee Ruksa. Unapendwa na waislamu na wakristo. Hukustahili kutendewa hivyo Mzee wetu.