Friday, June 27, 2008

Kumbukumbu - Amina Chifupa


Wadau, ni mwaka moja tangu Mbunge maarufu na chipukizi, Amina Chifupa, atutoke. Sitasahau nilivyopata habari za kifo chake kutoka kwa kaka Michuzi.

Kaka Fadhili amatunga shairi safi ya kumkumbuka.

*********************************************************************************

Bado Tunakukumbuka

Mwaka sasa umepita, bado tunakukumbuka,
Machozi hatujafuta, bado tunahuzunika,
Jina bado twaliita, kumbe ulishatutoka,
Bado tunakukumbuka, rafiki yetu Amina.

Ni vigumu kuamini, kuwa ilishatokea,
Machungu tele moyoni,vigumu kuyazowea,
Hupo tena duniani, mbali umeelekea,
Bado tunakukumbuka, rafiki yetu Amina.

Ni kama utani vile, ua letu kunyauka,
Nakumbuka siku ile, kichwani haitotoka,
Umekwenda zako kule, mwisho wako ‘lipofika,
Bado tunakukumbuka, rafiki yetu Amina.

Amina mpiganaji, mahiri wetu vijana,
Nasi tulikutaraji, ‘ngetusaidia sana,
Mambo yetu kuyahoji, majibu kupatikana,
Bado tunakukumbuka, rafiki yetu Amina.

Uliacha changamoto, kwenye timu ya taifa,
Sasa imepamba moto, yacheza kwa maarifa,
Na sasa tunayo ndoto, itat’ongezea sifa,
Bado tunakukumbuka, rafiki yetu Amina.

Bunge uliloliacha, sasa kumepambazuka,
Kwa hakika kumekucha, hoja zinajadilika,
Kwa mafisadi kwachacha, kwao moto unawaka,
Bado tunakukumbuka, rafiki yetu Amina.

Ila vita ya madawa, bado inasuasua,
Ingawa wanaelewa, moyoni ‘likusumbua,
Dhati kwao haijawa, bado hawajatatua,
Bado tunakukumbuka, rafiki yetu Amina.

Amina dada Amina,rafiki yetu wa kweli,
Kama ingewezekana, kulitenda jambo hili,
Basi tungeomba sana, uturejee kimwili,
Bado tunakukumbuka, rafiki yetu Amina.

Kimwili haupo nasi, kiroho tupo pamoja,
Ni kweli tunakumiss, tutakwona siku moja,
Familia yakumiss, Mungu aipe faraja,
Bado tunakukumbuka, rafiki yetu Amina.

Naweka kalamu chini, bado sisi twakupenda,
Upumzike kwa amani, mahali ulipokwenda,
Mahala pema peponi, malaika kukulinda,

BADO TUNAKUKUMBUKA, RAFIKI YETU AMINA.

1 comment:

Anonymous said...

Rest in Peace my beautiful sister.