Tuesday, August 12, 2008

'Multi Miss' hatarini kuvuliwa mataji Bongo

pichani Multi Miss (mwenye mataji mengi) Angela Lubala


Na Grace Hoka, Mtanzania


MISS Temeke 2008, Angela Lubala, huenda akavuliwa mataji yote anayoshikilia baada ya kukiuka mkataba wa mashindano ya urembo kutokana na kuvua moja ya taji alilokuwa akilishikilia na Balozi wa Redds Premium Cold.

Habari zilizopatikana jana jijini Dar es Salaam zinasema kuwa Angela ambaye pia anashikilia taji la Miss Temeke 2008 na lile la Chang’ombe 2008 anashutumiwa kukiuka makubaliano baina yake na Kamati ya Miss Tanzania.

Inaelezwa kuwa kabla ya kushiriki shindano la Miss Tanzania, Kamati ya shindano hilo chini ya Mkurugenzi wake Hashim Lundenga, huwa inawakabidhi warembo wote mkataba na kukaa nao kwa siku moja ili wausome na kuuelewa, ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha wazazi au walezi wao na ndipo wausaini.Katika mkataba huo kipengele kinachosema kuwa mrembo yoyote ni lazima akubali kufanya kazi zozote za wadhamini wa shindano hilo, ilimradi tu kamati ya Miss Tanzania iridhie.

Angela, akiwa kama mmoja wa warembo waliowania taji la Miss Tanzania mwaka huu, pia alisaini mkataba huo kabla ya kuanza kambi. Mbali na hilo mrembo huyo alishiriki katika shindano la kumtafuta Balozi waRedd’s lililofanyika mkoani Mwanza.

“Atalazimika kuvua mataji yote, kanuni ni zile zile toka ngazi ya kitongoji, kanda hadi taifa, mtu huwezi kuvua Blauzi ukabaki na sketi, akitaka kuvua nguo, ni lazima avue zote, sio moja,” alisema mmoja wa wajumbe wa Kamati ya Miss tanzania.

Endapo atavuliwa mataji yote, Angela atatakiwa kurudisha zawadi zote alizopata kuanzia ngazi ya kitongoji cha Cha’gombe kanda ya Temeke hadi taifa.

Wakati huo huo, Lundega alisema kuwa anatarajia kukutana na wajumbe wenzake ili kujadili suala hilo na kutoa uamuzi.‘Mimi sikujua lolote, ndio kwanza nimetoka Mwanza hii leo, nilikwenda kushiriki katika hafla ya mapokezi ya Miss Tanzania 2008 jijini Mwanza Nasreem Karim iliyofanyika jana, mara baada ya kuiona barua ambayo ninasikia amekabidhiwa mjumbe mmoja wa kamati yetu, tutakaa na kujadili na kutoa uamuzi’, alisema.

2 comments:

Anonymous said...

Mbona siyo mzuri kiasi hicho. Khaa.

Anonymous said...

Nanukuu
"Katika mkataba huo kipengele kinachosema kuwa mrembo yoyote ni lazima akubali kufanya kazi zozote za wadhamini wa shindano hilo, ilimradi tu kamati ya Miss Tanzania iridhie"

Duh hapa ndo nnapo sema wanaoshiriki Miss Tanzania wote ni mambumbumbu(samahani kwa lugha kali)au wamkata tamaa na maisha wako tayari kwa lolote. Hivi utakubali vipi mkataba unakwambia uridhie kufanya yoyote ya mzamini, ilimradi Hashim lundenga aridhie! Inamaana kwa mkataba huo hata mzamini akikupa kazi ya kucheza movie za ngono au kupiga picha za uchi kama Bwana Hashim akisema sawa huna jinsi?! au ukipewa kazi ya kuuza cocaine, Hashim akisema sawa huna ujanja?!

Hapa kwa mwenyewe uelewa na anaejuwa haki zake hawezi "kusain" mkataba huu hata akiahidiwa kupewa dunia yote iwe yake kama atashinda!